Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 10/1 kur. 447-450
  • Imara Ingawa Mataifa Yanatikisika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Imara Ingawa Mataifa Yanatikisika
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MATAIFA ‘YANATIKISWA’ KWA SABABU YA ULIZO LA ENZI
  • MATAIFA YATATIKISWA KWELI KWELI
  • UZITO WA HALI YA MKRISTO MWENYEWE
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Habari Njema kwa Wanadamu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • “Ufalme wa Bwana Wetu na wa Kristo Wake” Waanza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Ni Mambo Gani Unayotaka Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 10/1 kur. 447-450

Imara Ingawa Mataifa Yanatikisika

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1, 2. Kumetukia nini katika karne hii kwa habari ya serikali zilizo kuu za kikoloni?

KARNE hii imekuwa ya ajabu kwa kuwa ndipo serikali kubwa za kikoloni zimemalizika. Kwa sababu ya watu kuwa na tamaa yenye nguvu ya kutaka kujitawala wenyewe, na kwa sababu ya kumalizika kwa nguvu za mamlaka za kikoloni, yaliyokuwa makoloni yamejitenga yajitawale yenyewe bila kutegemea serikali zilizokuwa zikiyasimamia. Leo serikali zenye nguvu sana kama United States na Urusi zinatumia njia tofauti. Badala ya kutawala kwa kufanya nchi nyingine ziwe makoloni, zinajaribu kufanya nchi ndogo ndogo ziwategemee kwa njia za kiuchumi na za kisiasa.

2 Mazoea haya yameleta magumu. Na ingawa kwa kawaida zile nchi ndogo zina uhuru zaidi wa kisiasa, mara nyingi hali za maisha ya watu walio chini ya serikali zao zilizo huru ni kama sawa na zilivyokuwa hapo kwanza. Hata mataifa haya yanatikisika.

MATAIFA ‘YANATIKISWA’ KWA SABABU YA ULIZO LA ENZI

3, 4. Ulizo kubwa ambalo mataifa yanatetea sana ni nini?

3 Ulizo kubwa linalohusu mataifa ni enzi: Ni nani atakayetawala nchi yao au sehemu kubwa ya dunia, hata dunia yote?

4 Kwa hiyo, mataifa yanatikisika sana sana enzi yao inapopingwa. Wanailinda sana bila kutaka wanadamu wengine na mataifa mengine yaichukue, na hata hawataki Mungu aichukue. Hawataki kuikubali haki ya enzi kuu ya Mungu ya kuitawala dunia, kwa sababu wao hawataki kujipatanisha na kanuni zilizoandikwa katika Biblia.

5, 6. Ni tangazo gani ‘linalotikisa’ mataifa kweli kweli, na kwa sababu gani?

5 Kwa hiyo, inapotangazwa kwamba huu ni wakati wa ufalme wa Mungu kutawala, mataifa yanatikisika. Pengine haya yanaweza kusikika kama maneno yasiyo na msingi. Lakini angalia ulinganifu mbalimbali wa unabii wa Biblia na matukio ya kweli ya ulimwengu.

6 Mwaka wa 1914 “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilikwisha. Yaani, wakati wa serikali zilizofanyizwa na mwanadamu wa kutawala bila kupingwa au kukatizwa na serikali ya Mungu ulikwisha. Mungu hakuwa na serikali yo yote yenye kumwakilisha ikitawala kwa jina lake kutoka wakati mfalme wa mwisho wa ukoo wa Daudi aliposhushwa kutoka kiti cha enzi katika Yerusalemu mwaka wa 607 B.C.E. (Luka 21:24, NW; Eze. 21:26, 27) Lakini alikuwa amekwisha sema mapema kwa unabii kwamba ungetokea ufalme utawale kutoka mbinguni mfalme akiwa mrithi wa Daudi, Yesu Kristo. (Isa. 11:1, 2; Dan. 7:13, 14) Mwaka wa 1914 wakati ulifika wa Kristo kukubali mamlaka isiyoonekana ya Ufalme juu ya ulimwengu. (Dan. 4:32)a Uhakika huu ulitangazwa pote na Wakristo wakati huo. Habari hii ya kukatizwa kwa utawala wa wanadamu wa dunia na ufalme wa Mungu wa kimbinguni ‘ilitikisa’ mataifa.​—Hag. 2:6.

7. Tunajuaje kwamba tangazo la kuzaliwa kwa Ufalme lilishtua mataifa kweli kweli?

7 Pengine mtu atasema, Tangazo kama hilo tu lingewezaje ‘kutikisa’ mataifa, ingawa wakati huo lilitangazwa na lingali likitangazwa kote kote? Basi, tunaufahamu uhakika wa kwamba Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilianza katikati ya hari ya mwaka huo, vita iliyopigwa kwa ajili ya utawala wa ulimwengu. Hatuwezi kuona mambo yote yanayofanywa katika serikali zilizo kuu za kilimwengu, lakini Biblia inatupa ufahamu wa mengine ya mambo haya. Inatueleza juu ya tangazo lililopaswa kufanywa wakati “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilipokwisha. Kwa unabii inaonyesha kwamba walioko mbinguni waliona yaliyokuwa yakifanyika, wakaona mataifa yalivyohusika, wakasema: “Tunakushukuru wewe, Bwana Mungu Mwenyezi, uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu umeutwaa uweza wako ulio mkuu, na kumiliki.” Sauti hizo za kimbinguni zinasema Mungu alipochukua hatua hii mbinguni matokeo yalikuwa nini duniani? “Na mataifa walikasirika.” Walionyesha hasira hii kwa kugandamiza wale wenye kuutangaza ufalme wa Mungu kwa kutumia hali za wakati wa vita. (Ufu. 11:17, 18) Katika mataifa mengi, watangaza Ufalme walishtakiwa kwa uongo kuwa wachochea fitina ya kuasi serikali, wenye kujaribu kupindua serikali zilizokuwako.

8, 9. (a) Sababu hasa ya mataifa kutikiswa na tangazo la Ufalme ni nini? (b) Kwa sababu gani Shetani alichochea hasira ya mataifa wakati wa kuzaliwa kwa Ufalme?

8 Lakini iko sababu hasa ya mataifa kutikisika. Mataifa yenyewe hayaioni. Njozi iliyo katika Ufunuo inaendelea kueleza. Inaeleza ‘kuzaliwa’ kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi ukiwa mikononi mwa Mwanawe Yesu Kristo. Inaonyesha kwamba baada ya hapo vita ilitokea mbinguni na kwamba Ibilisi, ambaye kwa muda mrefu amekuwa ndiye mpinzani mkuu wa enzi kuu ya Mungu, alitupwa nje. Kwa sababu hiyo, masimulizi yanasema hivi: “Ole kwao wanaoikala ku dunia na bahari! Kwani yule Diabolo ameshuka kwenu mwenye gazabu nyingi kwa sababu anayua ana wakati muchache tu.”​—Ufu. 12:5-12, Swahili Congo Bible.

9 Ibilisi (Diabolo), ambaye anaitwa ‘mtawala wa ulimwengu’ na “mungu wa dunia hii,” alichochea mataifa yaingie katika vita ya dunia yote. (Yohana 12:31; 2 Kor. 4:4) Kama angeweza kutupilia mbali tangazo lililokuwa likifanywa duniani pamoja na wenye kulitangaza, utawala wake usingepingwa (kama yeye alivyodhani) na tangazo lo lote la kidunia. Na kama Shetani angefaulu katika jitihada ya kufanya hivyo, basi, wakati ufalme wa Mungu ungetawala kabisa mwishoni mwa ‘wakati mchache’ wa Shetani akiwa duniani, usingekuwa na raia za kidunia, kusingekuwa na watu wa kutetea enzi kuu ya Mungu.

MATAIFA YATATIKISWA KWELI KWELI

10, 11. Mataifa yamechukua hatua gani huku ‘yakitikitiswa’ vibaya zaidi, na je! wanafaulu katika kutimiza kusudi lao?

10 Kwa hiyo Yehova Mungu ‘anayatikisa’ mataifa, naye ataendelea ‘kuwatikisa’ kwa nguvu hata zaidi. Tangazo juu ya Ufalme linazidi kufanywa wakati wote na kufikia maeneo ya mbali zaidi. Ndivyo na mataifa yenye kutawala kwa nguvu yanavyozidi kuonyesha chuki kwa sababu ya ‘kutikiswa’ kwa kuchukua hatua kali kunyamazisha wenye kutangaza Ufalme.

11 ‘Kutikiswa’ kwa mataifa kutaendelea mpaka wakati gani? Na kwa sasa, je! wenye kupinga kutangazwa kwa Ufalme watakomesha watangazaji? Huenda ikaelekea kuwa mataifa yanaweza kufanya hivyo wakiwa na uwezo wao wote na njia zao za kisiasa. Lakini habari njema za Ufalme zingali zinasikiwa hata katika serikali za Kikomunisti zenye kutumia ukatili. Matokeo yatakuwa nini?

UZITO WA HALI YA MKRISTO MWENYEWE

12, 13. Mwandikaji wa barua kwa Waebrania anaelezaje hali nzito ya Wakristo?

12 Mwandikaji wa barua kwa Wakristo Waebrania, anayefikiriwa kwa kawaida kuwa mtume Paulo, anatujibia ulizo hilo akionyesha kwamba mataifa hawataacha kutikiswa na tangazo linaloendelea kufanywa juu ya Ufalme halitakoma. Lakini kwanza anaonyesha Wakristo uzito wa hali yao, akisema hivi:

13 “Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi, mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika, na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili.”​—Ebr. 12:22-24.

14. Hali ya Wakristo leo inalinganaje na ile ya Waisraeli wakati wa kufanywa kwa agano la Torati?

14 Paulo alikuwa ndio amemaliza kueleza juu ya mambo ya kuogofya waliyoyaona Waisraeli katika Mlima Sinai wakati agano la Torati lilipofanywa. (Ebr. 12:18-21) Mlima ulitikisika ukatoa moshi, ukamfanya hata Musa ateteme. Lakini sasa Wakristo hawasimami mbele ya kusanyiko la makumi ya maelfu ya malaika tu, bali pia mbele za Yehova Mungu na Yesu Kristo aliye katika mkono wake wa kuume, ambaye dhabihu yake ilifanya agano jipya lifae. Kwa kuwa yeye alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyetoa uhai wake uwe dhabihu ya kupatanisha, damu yake ni yenye thamani zaidi kuliko ya mwanadamu ye yote asiyekamilika, kutia na wanadamu wenye haki kama vile Habili. Zaidi ya hilo, ndugu za kiroho wa Yesu Kristo walio duniani si watenda dhambi waliolaaniwa, kama walivyokuwa wale Waebrania wa kale waliokuwa katika Mlima Sinai, bali wao wamesafishwa wakatangazwa kuwa wenye haki. Kweli hiyo ni hali na daraka lenye kuogofya. Je! Wakristo hawa wataweza kuendelea kusimama mbele za Mungu? (Luka 21:36) Mtume anaendelea kuwaambia hivi:

15. Mtume anatoa onyo gani?

15 “Angalieni msimkatae yeye anenaye. . . . Sauti yake iliitetemesha nchi wakati ule; lakini sasa ameahidi akisema, Mara moja tena nitatetemesha si nchi tu, bali na mbingu pia. Lakini neno lile, Mara moja tena, ladhihirisha kuhamishwa vile viwezavyo kutetemeshwa, kama vitu vilivyoumbwa, ili vitu visivyoweza kutetemeshwa vikae. Basi kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho; maana Mungu wetu ni moto ulao.”​—Ebr. 12:25-29.

16, 17. Ni nini kitakachotikiswa kitowekee mbali, na ni nini kitakachobaki?

16 “Vitu vilivyoumbwa [“ambavyo vimetengenezwa,” NW],” na mikono isiyo ya Mungu, yaani, taratibu hii ya mambo pamoja na dini yake ya uongo ambayo imepotosha mamilioni ya watu, pamoja na biashara yake ya kichoyo na serikali zake, zinazofananishwa na wanyama-mwitu katika Biblia, havitaweza kuvumilia kutikiswa huko. Hata “mbingu” zilizo mbovu zitatoweka. Ni nini kitakachobaki? Mtume anatuambia: Ni ufalme wa Mungu.​—Dan. 8:20-25.

17 Kwa kuwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi utabaki, wafuasi wake na wenye kuutangaza watabaki, nalo tangazo lake halitakomeshwa kamwe kabla taratibu hii ya mambo haijatikishwa kabisa itowekee mbali.​—Dan. 2:44.

18. Kwa sababu ya mambo haya, mtume alisema imewapasa Wakristo wafuate mwendo gani?

18 Kwa kuwa ni wale tu wanaoshikamana na Ufalme wakati huu wote wa kutikiswa watakaoendelea kuwa hai, mtume alionya Wakristo juu ya mwendo wanaopaswa kufuata, akisema hivi: “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo. Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu [“wala mtu ye yote asiyethamini mambo matakatifu,” NW].”​—Ebr. 12:14-16.

19. Daraka la Mkristo ni nini, na matokeo ya uaminifu wake au ya kutokuaminika kwake ni nini?

19 Kwa hiyo, lazima Wakristo wa kweli wawakilishe kweli kweli jina la Yehova mbele ya watu wote. Si kwamba tu lazima wautangaze Ufalme, bali pia lazima waishi kulingana na kanuni zake bora. Watapokea upendeleo na baraka, utawa wao ukiwatolea mambo mazuri katika ‘uzima wa sasa’ na ahadi ya “ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Tim. 4:8) Lo! ingekuwa vibaya namna gani kufanya jambo lo lote lililo chafu, la aibu, na kuanguka katika hukumu ya laana ya Mungu aliye hai, ambaye anateketeza uchafu wote kama kwamba kwa moto’

20. Kwa sababu gani wale ambao si Wakristo wa kweli wamepaswa wamsikilize “yeye atuonyaye kutoka mbinguni”?

20 Kwa hiyo bila shaka Wakristo hawataki ‘kumkataa’ “yeye atuonyaye kutoka mbinguni.” (Ebr. 12:25) Na wale ambao sasa si Wakristo wa kweli wenye kumwabudu Mungu, imewapasa wazisikilize habari njema, kwa maana zinaweza kuwapa watu waaminifu furaha nyingi katika maisha ya sasa na yale yatakayokuja.

​—Kutoka Kitabu Paradise Restored to Mankind​—By Theocracy!

[Maelezo ya Chini]

a Tazama kitabu Amani ya Kweli na Usalama wa Kweli​—Kutoka Chanzo Gani?, kur. 72-85 (1974), vile vile “Your Will Be Done on Earth,” kur. 94-103 (1958), vilivyochapwa na Watch Tower Bible and Tract Society, Brooklyn, New York.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki