Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 12/15 kur. 558-564
  • Iweni na Akili Mambo Yote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Iweni na Akili Mambo Yote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSITAWISHA MAONI YA AKILI TIMAMU JUU YA MADARAKA
  • KUTENGENEZA UPYA WENYE KUKOSA
  • KUTOEPUKA MADARAKA WAKATI WA KUFANYA MAAMUZI
  • FANYA MAAMUZI YAKO KULINGANA NA BIBLIA
  • Uangalizi Wenye Upendo Hujenga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Wakumbukeni Wale Wanaoongoza Kati Yenu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Wazee Wanaosimamia Vema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Wanaume Wenye Hekima, Akili na Ujuzi wa Kuongoza Watu wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 12/15 kur. 558-564

Iweni na Akili Mambo Yote

“Iweni na akili, iweni macho.”​—1 Pet. 5:8, NW.

1. Watu wengi wanageukia nini waepuke magumu ya maisha, na matokeo ni nini?

INABURUDISHA sana kushirikiana na watu wanaokuwa na akili na kuendelea kuwa katika hali yao ya kawaida wanapokuwa katika hali zenye kuleta wasiwasi na mkazo. Ndivyo ilivyo hasa leo, hali zikiwa kama zilivyo katika ulimwengu wote. Hata katika sehemu za mbali watu wanapatwa na magumu yenye kulemea sana hata viongozi wa ulimwengu wanakata tamaa ya kutafuta njia za kupambana nayo, licha ya kuyaondoa. Wanapokabiliwa na hali hizo, watu wengi wamejaribu kuzisahau kwa kutumia vileo au dawa za kulevya ili akili zao zipumbazike kutoweza kuyafikiria magumu hayo ya maisha. Lakini kwa kufanya hivyo wanajiletea wenyewe magumu zaidi tu.​—Mit. 23:29-35.

2. Ni hali gani zilizokuwa zinawajia Wakristo wa karne ya kwanza zilizowataka wawe na akili, naye Paulo alielezaje jambo hili?

2 Katika karne ya kwanza, Wakristo walipatwa pia na hali za kila namna zilizowajaribu kweli kweli. Je! walishauriwa wapumbaze akili zao ili waweze kuzivumilia zaidi hali hizo? Badala yake, walio imara walipaswa kujua yaliyokuwako mbele ili waweze kuyashinda, ingawa pengine ilichukiza kuwa na matumaini ya kupatwa na mateso na kuona wengi wakiiasi imani. Kwa hiyo, mwangalizi Timotheo alionywa waziwazi juu ya uasi huo ambao ulikuwa unakuja na mtume Paulo, ambaye alisema hivi: “Maana wakati utakuya na watu hawatavumilia mafundisho ya kweli; lakini kwa kufuata tamaa zao wenyewe watayipatia walimu wingi kwa kuwa wana masikio ya kuwasha; na watageuza masikio yao toka kweli.” Kwa sababu hatari hiyo ilikuwa inakaribia sana, mtume aliendelea kusema hivi: “Lakini wewe, [“uwe timamu katika akili”​—Kingdom Interlinear] katika maneno yote.” (2 Tim. 4:3-5, Swahili Congo Bible) Akiwa amejitayarisha hivyo, Timotheo angeweza kupinga hila hizo.

3. (a) Kwa sababu gani ni jambo la haraka kwa mtu kuwa na akili leo? (b) Kama ilivyoelezwa na Petro kwa sababu gani lazima wazee wawe macho, na kwa sababu gani Paulo anatia moyo tukeshe?

3 Katika miaka zaidi ya mia kumi na tisa iliyofuata kuandikwa kwa maneno hayo na Paulo, uasi huo umetokea waziwazi kabisa nao unaonekana katika Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) ya kisasa. Ingawa Yehova Mungu amelitenganisha kundi lake la kweli la Kikristo na jumuiya hiyo, bado kuna umuhimu ule ule wa kuwa na akili kwa maana uasi wake unakaribia kufikia kilele chake nao unaienea dunia yote. Zaidi ya hayo, kwa sababu jumuiya hiyo ina ukatili kwa wafuasi wa kweli wa Kristo, huenda wakati wo wote ikawatesa vikali, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Kwa hiyo, je! wazee wa makundi wanatia washirika wao wa Kikristo nguvu za kustahimili mikazo hiyo inayoongezeka na kuendelea kuwa waaminifu? Mtume Petro alikuwa na sababu nzuri ya kusihi wazee ‘walichunge kundi la Mungu lililo katika uangalizi wao,’ na kuongeza onyo hili: “Iweni na akili, iweni macho. Adui yenu, Ibilisi, anatembea hapa na pale kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Pet. 5:2, 8, NW) Hatari inayotokana na adui huyo imeongezeka nyakati hizi ambapo hali za ulimwengu zinazidi kuwa mbaya nayo lazima ifikiriwe kwa utimamu ili nyakati zenye kupita kasi kasi na tamasha ya ulimwengu yenye kubadilika mbio mbio isije ikatuvuruga akili. Uwezo wa wazee kulinda kundi la Kikristo kwa uongozi wenye busara na utimamu unajaribiwa. Huu si wakati wa kupumbazika akili. Paulo alionya kwamba “siku ya Yehova itakuja sawasawa na mwizi usiku” kisha akasihi ‘tusilale kama wengine wafanyavyo, bali tukeshe na kuwa na akili.’ (1 The. 5:2, 6-9, NW) Basi, lazima wewe kama mzee ufanye nini kuonyesha kwamba umesikia unavyosihiwa ‘kuwa na akili katika maneno yote’?

KUSITAWISHA MAONI YA AKILI TIMAMU JUU YA MADARAKA

4. Ni kwa njia gani lazima mzee ‘atimilize huduma yake’?

4 Onyo hilo linalorudiwa-rudiwa mara nyingi ‘kuwa na akili’ limepaswa liamshe wazee wakumbuke madaraka yao mengi ikiwa ‘watatimiliza huduma yao’ kama Timotheo. Mapendezi ya mzee mwenyewe yanaweza kumfanya asukumie kando mambo mengine na kukaza fikira zake zaidi juu ya upande mmoja au pande mbili tu za uangalizi wake. Walakini, hayo yasingekuwa maoni timamu. Badala ya kufanya hivyo, anapofikiria ana wakati kadiri gani, kusudi lake limepaswa kuwa kuona vile anavyoweza kuugawanya ili aweze kuangalia madaraka ya jamaa, ya kuchunga, ya kufundisha, na ya kuhubiri na kufanya wanafunzi.Ili kuangalia madaraka hayo yote vizuri kuwaza safi kunatakiwa, usawa na akili zinahitajiwa ili kila moja la mambo hayo liangaliwe bila kuachiliwa mbali.

5. Mzee mwenye jamaa amepaswa atumie wakati wake wote akiwa na jamaa yake? Kwa sababu gani?

5 Kwa mfano, chukua mzee mwenye jamaa. Bila shaka imempasa sana awe mwenye akili timamu anapofikiria majaribu na mikazo mikali inayokabili jamaa yake. Ili aendelee kuwa mzee lazima aonyeshe anapendezwa kweli na jamaa yake mwenyewe na kuwekea kundi mfano mwema kama baba. Paulo alieleza sifa ambazo imempasa mzee atimize, akataja kwamba amepaswa kuwa “mwanamume mwenye kusimamia nyumba yake mwenyewe katika adabu nzuri, mwenye kutiisha watoto kwa uzito wote.” (1 Tim. 3:4, 5, NW) Hata hivyo, kama angetumia wakati wake wote akiwa na jamaa yake asingekuwa akiwawekea hata wao mfano mwema. Kwa sababu gani? Kwa sababu kufanya hivyo kungewatia moyo wawe wenye kujifikiria wao peke yao, wajitenge na watu wengine. Lakini, wamepaswa watiwe moyo kupendezwa na wengine, wale waliomo katika kundi na wale walio katika ulimwengu pia. Wamepaswa waombwe washiriki kulitangaza tumaini zuri sana la uzima wa milele walilopewa. Ndipo maoni hayo yaliyopanuka yatakapowafanya wahurumie wengine kwa ufahamu na kuwafanya wathamini zaidi kusudi la Muumba.

6. Imempasa mzee aoneje uhitaji wa kupata ujuzi?

6 Vivyo hivyo, wazee wamepaswa wawe ‘wenye kustahili kufundisha’; kwa hiyo imewapasa wawe wanafunzi wa Neno la Mungu wenye bidii. (1 Tim. 3:2, NW) Huenda wengine wakaona lazima watumie muda mwingi wakijifunza, wakichunguza Maandiko na kutayarisha hotuba, ikitegemea elimu yao, kadiri ya miaka ambayo wamekuwa wakijifunza Biblia na kwa sababu nyinginezo. Walakini, hapa tena huenda mzee akapita kadiri asipokuwa mwangalifu kukaza fikira juu ya madaraka yake mengine. Paulo anaonyesha hatari isiyoonekana wazi inayoweza kuwapata wale wanaotafuta ujuzi kupita kadiri, akisema, “Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga.” (1 Kor. 8:1; 13:2) Huko si kusema kwamba ujuzi si wa maana, bali kwamba umepaswa uwe pamoja na upendo ndio utimize jambo lenye mafaa. Upendo unatofautiana na ujuzi kwa sababu unaonyeshwa kwa matendo wala si mambo yaliyowekwa akilini tu. Kwa hiyo, mzee ‘mwenye kuwa na akili’ atajifunza lakini pia ahudumie ndugu zake na walio katika ulimwengu; hivyo atatumia vizuri ujuzi wake.​—1 Yohana 3:18.

7. (a) Kazi ya uchungaji ni ya haraka kadiri gani? (b) Mzee anawezaje kuhakikisha kwamba upendo wake ni kamili?

7 Paulo alitia mkazo mwingi juu ya uchungaji, akasihi waangalizi wa Efeso “kulilisha [kundi] lake Mungu, alilolinunua kwa damu [ya Mwana wake] mwenyewe.” (Matendo 20:28) Bila shaka hiyo ni kazi ya haraka, kwa sababu ya nyakati hizi za hatari ambapo maisha zenyewe za Wakristo huenda zikawa hatarini. (2 Tim. 4:2) Tena, uchungaji wenye matokeo mazuri unahitaji wakati. Lazima saa nyingi zitumiwe kutayarisha mikutano na hotuba, kutembelea na kutia moyo wale wanaohitaji msaada au wagonjwa. Na hali kazi hii ya maana pia imepaswa ionwe kwa kuhusiana na pande nyingine za madaraka ya mzee. Yesu alionyesha kwamba, ingawa upendo kwa ndugu za mtu za Kikristo ni ishara kuu ya uanafunzi wa kweli, hauwapi wafuasi wake sababu ya kutoonyesha upendo wale walio katika ulimwengu. Kwa kweli, upendo wao usingekuwa kamili kama usingetia ndani hata wapinzani, kama vile anavyosema Yesu: “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi.” (Mt. 5:43-48) Kwa hiyo, ingawa uchungaji ni wa maana sana, nao pia lazima ulinganishwe na madaraka yale mengine ya mzee.

8. (a) Ni kazi gani inayofunua upendo na huruma ya Yehova, na watu wanafahamuje hilo? (b) Ni kwa njia gani peke yake ‘matendo yetu mema’ yanavyoweza kumtukuza Mungu?

8 Daraka moja ambalo ushirika mzima wa Wakristo unaweza kushiriki ni lile daraka la haraka la kuzihubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kazi hiyo inafahamisha watu upendo na huruma ambayo Yehova Mungu anayo kwa wanadamu, upendo ulio mwingi “hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Wanaweza kupata nuru ya kweli kwa watumishi wa Mungu tu, kwa maana Yesu alisema: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu.” Wamepaswa wafanye nini na nuru hiyo? Si kuificha, bali alisema, “nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:14-16) ‘Matendo mema’ yanajulisha watu kuwa ni wazuri​—matendo kama yale yanayofanya jamaa ziwe nzuri na zenye utaratibu, yanayofanya wafanya kazi wawe waaminifu na makundi ya Wakristo kupendana. Lakini, je! watu wengi wanaweza kuiona maana halisi ya ‘matendo mema’ hayo tusipotangaza kweli, tukizihubiri habari njema nyumba kwa nyumba? Inaelekea watatuona kuwa ‘watu wema’ tu. Walakini, tukisema waziwazi, watafahamu sababu gani sisi ni tofauti, watafahamu kinachotufanya tuzae matendo mema, halafu, badala ya kutusifu sisi, ‘watamtukuza Baba yetu aliye mbinguni.’ Wazee hasa wamepaswa wajitahidi kushiriki kabisa kutangaza habari njema wakiwa na akili timamu na ‘kuwa vielelezo kwa kundi’ kwa njia hiyo, wakitia ndugu zao moyo wajiunge nao kufanya kazi hiyo ya maana, kama vile mitume walivyoshiriki katika kazi ya kuhubiri.​—Mt. 4:19, 20.

KUTENGENEZA UPYA WENYE KUKOSA

9. Ni maoni gani yaliyosawazika yanayoamua vile wazee watakavyotendea wenye kukosa?

9 Zaidi ya madaraka ya wazee yaliyotajwa kwanza, ziko nyakati ambapo lazima wajaribu kutengeneza upya ndugu zao wa Kikristo wanaofanya makosa na kuingia dhambini. Hapa tena, lazima wajitahidi ‘kuwa na akili’ na kuwa na maoni yaliyosawazika. Kwa mfano, si juu yao kujaribu kuonyesha wengine namna watakavyokuwa wakiishi. Wala hawapaswi kufanya jambo dogo liwe mgogoro mkubwa wala kutwika wengine maoni yao au kanuni yao wenyewe. Badala yake, Petro alishauri hivi: “Mtu wa kwenu asiteswe . . . kama mtu ajishughulishaye na mambo ya watu wengine.” (1 Pet. 4:15) Hata hivyo, wamepaswa wawe macho kuona mahitaji ya ndugu zao na kuwa tayari kuwapa msaada ukihitajiwa.

10. (a) Wakati mzee anaposhughulika na wenye kukosa, kwa sababu gani nia yake ni ya maana? (b) Mwenye kukosa anayetendewa kwa upole anatofautianaje na anayestahili kukemewa vikali?

10 Zaidi ya hayo, nia yao juu ya wenye kukosa ni ya maana sana. Haiwapasi kuwa wakali na wenye kuteta. Nia hiyo inaweza kufukuzia mbali tu mtu mwenye kutubu kweli kweli, hali fadhili zinaweza kusaidia hata wale wanaoelekea kuwa wenye vichwa vikubwa kidogo. Angalieni, tafadhalini, vile Paulo alivyoshauri tutendee wenye kukosa: “Ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani ya uongo kabla ya yeye kuijua, ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumtengeneza upya mtu huyo katika roho ya upole.” (Gal. 6:1, NW) Kwa hiyo Paulo anaonyesha kwamba ikiwa kweli mzee anataka asaidie mtu huyo, imempasa awe na “roho ya upole” anapojaribu kwa upendo kumtengeneza upya ndugu yake na kuupata moyo wake tena. Anayesemwa na Paulo hastahili kukemewa vikali kama wale aliowaita “wasiotii, wenye maneno yasiyo na maana, wadanganyaji.” (Tito 1:10, 13) Mwenye kusikiliza si mzoelevu wa dhambi, bali ni mtu ‘aliyechukua hatua ya uongo kabla ya yeye kuijua.’ Kwa hiyo hastahili kutendewa kama adui. Kwa kweli, yeye na mzee pia wana adui, Shetani; kwa hiyo lingekuwa kosa kwa mzee kuongeza mzigo wenye kulemea juu ya mtu aliyekwisha huzunikia dhambi yake. Kinachopaswa kuchukiwa si mwenye kufanya kosa, bali ni lile tendo baya alilofanya.​—Yuda 22, 23.

11. Paulo anatoaje mfano juu ya mwenye kukosa, na ni nini kinachohitajiwa kumwonyesha wazi mwendo wake mbaya?

11 Akitupa mfano wa mwenye kukosa, Paulo anamfananisha na mnyama maskini aliyenaswa katika mtego wa mwindaji. Walakini, huyo si mwindaji wa kawaida; hao wananaswa katika “mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye, hata kuyafanya mapenzi yake.” (2 Tim. 2:24-26) Ni kweli kwamba unaweza kuondoa mnyama aliyenaswa mtegoni kwa kumvuta-vuta vyo vyote tu, lakini hiyo itamwumiza. Je! isingekuwa afadhali kutumia uanana na upole ili akiisha kufunguliwa aweze kupona majeraha aliyojiletea? Vivyo hivyo, wenye kukosa lazima watendewe kwa huruma; lakini wamepaswa pia watendewe kwa imara ili kuwaonyesha waziwazi hatari ya mwendo wao mbaya. Wamepaswa wajifunze kuchukia kabisa ubaya walioutenda na kuona namna ulivyo mbaya. Ni lazima wafahamu sababu maoni ya Yehova juu ya jambo hilo yanafaa na kwamba ni kwa faida na furaha yao, hata washikamane na Neno lake, kama ilivyoandikwa: “Maana maagizo hayo ni taa, na sheria hiyo ni nuru, na maonyo ya kumwadilisha mtu ni njia ya uzima.”​—Mit. 6:23.

12. Woga katika kukaripia au kutengeneza upya watenda makosa unawezaje kuleta hatia ya damu juu ya wazee?

12 Wazee wanaopenda wenye kukosa kweli kweli hawataogopa kutoa karipio linalohitajiwa wala kutengeneza upya wenye kukosa. Badala yake, watatenda kupatana na Mithali 27:5, 6, inayosema hivi: “Lawama ya wazi ni heri, kuliko upendo uliositirika. Jeraha utiwazo na rafiki ni amini; bali kubusu kwa adui ni kwingi sana.” Kwa kweli, mzee akikosa kutoa onyo au sahihisho linalofaa wakati imeonekana kwamba mwendo mbaya unafuatwa, hiyo inaweza kumfanya awe mwenye hatia ya damu. Paulo alihakikisha kwamba asingerukiwa na tone lo lote, kwa hiyo akatimiza agizo lake bila woga, akisema hivi: “Nawashuhudia wote siku hii ya leo, ya kuwa mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu.” (Matendo 20:26, 27) Wazee wakiwa na akili kama Paulo na kutimiza madaraka yao kwa ushujaa, wataona wale waliowasaidia watoke katika mwendo wa upotovu wakipata faida ya milele.

KUTOEPUKA MADARAKA WAKATI WA KUFANYA MAAMUZI

13. Ni nani aliyewapa wazee daraka walilo nalo, na kwa sababu gani wanastahili kufanya maamuzi yanayofaa?

13 Kutokana na tuliyozungumza sasa hivi ni wazi kwamba huenda nyakati nyingine wazee wakaona ni lazima kufanya maamuzi mazito, pengine hata mengine yayo yakihusu maisha za ndugu zao. Daraka hili zito la kutenda kama waangalizi na wachungaji halitoki kwa chanzo cha kidunia bali wanapewa na roho takatifu ya Mungu, kuwafanya mawakili wake. Paulo aliwaeleza wazee wa kundi la Efeso jambo hilo kwa njia hii: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwake roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi, kuchunga kundi la Mungu.” (Matendo 20:28, NW) Kwa hiyo imewapasa wajione kama Timotheo kuwa wana wajibu kwa Mungu na Kristo kutimiza kazi waliyogawiwa. (2 Tim. 4:1, 2) Katika hali nyingi wazee wanastahili sana kufanya maamuzi yanayofaa, kwa sababu Yehova Mungu amewapa roho ya “nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi [“ya utimamu wa akili,” NW]” (2 Tim. 1:7) Wanapewa “nguvu,” au uwezo, ili waweze kuzitumia karama za kiroho walizo nazo. Wanayo ‘roho ya upendo’ ili wasaidie wengine kwa kusudi linalofaa, na kwa “utimamu wa akili” wanaongozwa upande ufaao wanapojitahidi kutimiza madaraka yao.

14. (a) Eleza sababu gani inakuwa lazima mambo mengi yarudishwe kwa wazee wajifanyie maamuzi. (b) Wazee wanawezaje kujitayarisha kushughulika na mambo katika makundi yao wenyewe, na wanaweza kuendea nani wapate msaada?

14 Ingawa wanapata msaada kutoka kwa Mungu na Neno lake lililoandikwa, mara kwa mara wazee wanaomba afisi ya tawi ya Watch Tower Society au baraza inayoongoza iwafanyie maamuzi, kama yale yanayohusu kupendekeza wazee wawekwe na mambo kama hayo. Ingawa afisi ya tawi ina nia na tamaa ya unyofu kusaidia, mara nyingi inakuwa lazima jambo hilo lirudishwe kwa wazee walio na mambo ya hakika, wafanye pendekezo wenyewe. Wazee wanaweza kuuliza maulizo, kupata majibu, kupata mambo zaidi ya hakika juu ya shauri linalohusika ikiwa lazima, kabla ya kufanya uamuzi wa mwisho. Wala hawapati hasara ya kiroho. Zaidi ya hayo, wao wamepewa daraka na Mungu kufanya maamuzi hayo na si kuwaachia wengine bila sababu wayafanye. Kwa hiyo imewapasa wajitayarishe kwa funzo na sala kufanya maamuzi yanayofaa kupatana na mapenzi ya Mungu. Paulo alitia mkazo kwa Timotheo juu ya uhitaji wa kuyategemea Maandiko kwa moyo wote, kwa maana ‘yaliongozwa na Mungu na ni yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kutengeneza mambo, kwa kuadibisha katika haki.’ Mzee akifanya maamuzi yake kulingana nayo, atajihakikisha kuwa mtu wa Mungu ‘mwenye uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.’ (2 Tim. 3:16, 17, NW) Msaada wa wazee wengine pia huenda ukafaa. Biblia inasema kwamba “pasipo mashauri makusudi hubatilika; bali kwa wingi wa washauri huthibitika.” (Mit. 15:22) Ikiwa mwangalizi wa mzunguko au wa wilaya anatembelea kundi, yeye pia anaweza kuendewa.

15. Ni wakati gani mambo yamepaswa yapelekwe kwa afisi ya tawi ya Sosaiti na wazee?

15 Walakini, ikiwa baada ya kujifunza na kuchunguza sana Maandiko jibu la shauri fulani au ugumu fulani halipatikani, wazee wamepaswa wafanye nini? Kwa hakika ungekuwa upumbavu mwingi sana wakisonga mbele peke yao kuliamua shauri lenyewe, pengine wakikisia jibu au kufanya uamuzi wa kuchukuliwa tu na fikira. Badala yake, ingekuwa vizuri zaidi wakiipasha habari afisi ya tawi ya Sosaiti inayoangalia nchi yao na kuiomba msaada.

16. Ni kanuni gani imepaswa ifuatwe wakati inapokuwa lazima wazee washughulike na wanaopendwa sana, wanaoheshimiwa na walio mashuhuri?

16 Wazee wasikose kamwe kuchukua hatua kwa sababu ya kuogopa mwanadamu. Huenda ikawa kwamba nyakati nyingine watashughulika na wengine wanaopendwa sana au wenye kuheshimiwa au walio mashuhuri. Lakini, maamuzi yao hayapaswi kuwa yenye kupendelea watu hao. Kanuni ya Neno la Mungu inasema wazi juu ya jambo hilo. Inasema hivi: “Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki.” (Law. 19:15; Yak. 2:1-9) Kutokana na hayo ni wazi sana kwamba kuonyesha upendeleo ni udhalimu nako kunavunja sheria ya Mungu.

FANYA MAAMUZI YAKO KULINGANA NA BIBLIA

17. Wazee wanawezaje kuonyesha heshima nyingi sana kwa Maandiko?

17 Zaidi ya mambo yote, imewapasa wazee waonyeshe heshima nyingi sana kwa Neno la Mungu kwa kutoa mashauri yao yote kulingana nalo. (2 Tim. 2:15) Hiyo yamaanisha wataepuka kwa bidii kutoa maoni yao wenyewe kama msingi wa mambo, badala yake watoe kwa uaminifu mafundisho waliyopokea kwa Maandiko na jamii ya mtumishi wa Yehova, “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45; 1 Tim. 4:6, 16) Ndugu zao wa Kikristo wamepaswa waweze kuona pia kwamba wazee hawasemi tu juu ya Biblia, bali wao wenyewe wanaonyesha Neno la Mungu lina uwezo kwa kutumia kanuni za kimungu katika maisha zao. Hii itasaidia ushirika mzima wa Wakristo wathamini uongozi wa wazee na kufuata mfano wao wa imani.​—Ebr. 13:7.

18. Zaidi ya wazee, ni nani ambao lazima wawe na akili, wakiwa na taraja gani lililohakikishwa?

18 Mwishowe, lazima ikumbukwe kwamba watumishi wote wa Mungu wamepaswa ‘wawe na akili,’ si wazee peke yao, kwa maana kila mmoja wetu lazima apatwe na hatari zile zile zinazotoka ulimwenguni. Hali zenye hatari za leo zinaleta majaribu makali ya imani juu ya kila Mkristo. Kwa hakika huu ni wakati wa kuwaza kwa utimamu, ni wakati wa kukuza maoni yanayofaa juu ya mambo kwa msaada wa Neno la Mungu, ili kila mmoja wetu aweze kufanya maamuzi ya hekima. Ni kwa njia hiyo tu tunavyoweza sote kusaidiana ‘tukeshe na kuwa na akili’ ili siku ya Yehova ya hukumu isitutokee kama mwizi. Halafu, tukiwa “wana wa nuru na wana wa mchana,” tutaokolewa tupite uharibifu wa ulimwengu unaokuja tuingie katika taratibu mpya iliyotayarishwa na Mungu hata Yeye apate sifa ya milele nasi tupate wokovu wa milele!​—1 The. 5:5, 6, NW.

[Picha katika ukurasa wa 559]

Imempasa mzee agawe wakati wake kuweza kuangalia madaraka ya jamaa . . .

. . . kutayarisha hotuba na funzo la kipekee

[Picha katika ukurasa wa 560]

Ziara za uchungaji ni sehemu ya daraka la mzee . . .

. . . na pia kushiriki katika utumishi wa shambani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki