Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 12/15 kur. 555-558
  • Ukristo wa Kweli—Unaweza Kupatikana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukristo wa Kweli—Unaweza Kupatikana?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MSINGI WA KUTAMBUA
  • KUMI WANAKUJA KUJIUNGA NA MMOJA
  • “TUMESIKIA KWAMBA MUNGU YU PAMOJA NANYI”
  • “Tumesikia Kwamba Mungu Yu Pamoja na Ninyi Watu”
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • “Roho ya Uhai Itokayo kwa Mungu Ikawaingia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Tutakuwa Upande wa Nani Taabu ya Ulimwengu Ifikiapo Upeo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Utendaji wa Roho Iliyomwagwa Kutoka Juu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 12/15 kur. 555-558

Ukristo wa Kweli​—Unaweza Kupatikana?

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1. Watu wengi katika nchi zisizo za Kikristo wana maoni gani juu ya Ukristo?

WATU wengi katika mataifa yasiyo ya Kikristo wanachukia Ukristo. Sababu moja ni kwamba wamisionari wa dini za Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) mara nyingi ndio wameongoza mataifa haya yanyang’anywe vitu vyao kwa njia ya kisiasa. Katika kisiwa kimoja kunao usemi huu: ‘Wamisionari walitufundisha kusali, nasi tulipokuwa tumeinama vichwa vyetu wakaiba nchi.’

2, 3. Watu wengi katika nchi ‘za Kikristo’ wanauonaje Ukristo na Biblia, nao wanauliza ulizo gani?

2 Hata katika yanayoitwa mataifa ya Kikristo watu wengi wameacha kuheshimu Ukristo kwa sababu viongozi wa dini kama jamii wameleta suto juu ya Mungu na Biblia kwa kukosa kufanya mambo wanayohubiri. Pia, watu wameona kwamba mara nyingi yanayofundishwa na viongozi wa dini si ya akili, adili wala haki.

3 Kwa hiyo, watu wengi wanaona mashaka sana kama kunao Ukristo wa kweli. Wanauliza hivi, Je! Ukristo wa kweli unaweza kupatikana? Ikiwa ndivyo, wapi na namna gani?

MSINGI WA KUTAMBUA

4-6. Yesu Kristo alitoa uongozi gani wa kutambulisha Ukristo wa kweli?

4 Yesu Kristo alizoea haki alipokuwa duniani na kuelekeza watu kwenye ibada safi ya Mungu. (Yohana 4:23, 24) Alionyesha namna ibada safi inavyoweza kutambuliwa. Alisema hivi alipokuwa akizungumza juu ya waalimu wa uongo ambao wangetokea:

5 “Mtawatambua kwa matunda yao. Je! watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.”​—Mt. 7:15-20.

6 Kwa kweli hukumu ya Mungu itawajilia waalimu wanafiki wenye kusingizia jina lake. Lakini tukiona matunda mazuri, tunajua kwamba chanzo chake ni kizuri. Tunaweza kutambua ibada ya kweli.

7, 8. Ni unabii gani uliotolewa mamia ya miaka iliyopita unaoonyesha kwamba leo watu wengi wangejiunga na watu wa Yehova katika ibada ya kweli?

7 Unabii wa Biblia uliotolewa miaka mingi zamani unaonyesha kwamba katika wakati uu huu tunamoishi maelfu ya watu wangetambua Ukristo wa kweli nao wangeingia katika uhusiano wenye kukubaliwa pamoja na Mungu. Wangekuwa watu wake wa kweli, wakiwa na tumaini la kuishi duniani chini ya serikali yenye haki, ufalme wa Mungu. Unabii huo ulitolewa karibu na mji wa kale wa Yerusalemu baada ya mabaki madogo ya karibu Wayahudi 50,000 kurudishwa makwao kutoka uhamishoni Babeli. Kwa miaka 70 kabla ya wakati huo, Yerusalemu ulikuwa umekaa ukiwa. Sasa idadi yao ilikuwa ndogo ikilinganishwa na ilivyokuwa wakati mmoja, lakini Mungu alisema hivi akiwatia moyo:

8 “[Yehova] wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za [Yehova], na kumtafuta [Yehova] wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta [Yehova] wa majeshi, na kuomba fadhili za [Yehova].”​—Zek. 8:20-22.

9. Tunajuaje kwamba unabii wa Zekaria unahusu matukio ya siku zetu?

9 Ni kweli kwamba Yerusalemu ulifanya maendeleo na bado ulikuwa mji mashuhuri kwa zaidi ya miaka mia tano iliyofuata. Lakini utimizo ulio wa maana zaidi wa unabii huo unatukia wakati wetu, kwa sababu kama mtume Paulo anavyosema, mambo yaliyowapata Israeli yalikuwa mifano kwetu “sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani [“miisho ya taratibu za mambo,” NW].” (1 Kor. 10:11) Na mtume uyo huyo anatuambia hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”​—Rum. 15:4.

10. Kitabu cha mwisho cha Biblia kinaungaje mkono yale ambayo tumesema juu ya utimizo wa unabii wa Zekaria?

10 Tena, kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kinasimulia “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” ambao ungeonekana katika wakati huu wa mwisho wa ulimwengu, na ambao wangemwabudu Mungu kwa unyofu wakiwa waamini wa “Mwana-kondoo wa Mungu,” Yesu Kristo.​—Ufu. 7:9, 10; Yohana 1:29.

KUMI WANAKUJA KUJIUNGA NA MMOJA

11, 12. (a) Zekaria anaendelea kusema nini, akionyesha vile wenye kujiunga na watu wa Yehova wangefanya hasa? (b) “Myahudi” ambaye “watu kumi” wanashika upindo wa nguo yake ni nani?

11 Kwa hiyo, sisi leo twaweza kutazamia kupata watu wanaoishi kulingana na Ukristo wa kweli, wakizaa matunda mema ya haki, adili, upendo na amani. Nabii Zekaria anaendelea kusema hivi: “Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”​—Zek. 8:23.

12 “Yeye aliye Myahudi” ndiye nani? Katika habari hii, maneno ya mtume Paulo yamepaswa yaangaliwe: “Yeye si Myahudi aliye Myahudi kwa nje tu, wala tohara siyo ile ya nje tu katika mwili; bali yeye ni Myahudi aliye Myahudi kwa ndani; na tohara ni ya moyo, katika roho.”​—Rum. 2:28, 29.

13. Tunapotazama hapa na pale tuone ni akina nani wametuatana na “watu kumi” wa mfano, tunaweza kuuliza maulizo gani, na je! tunalipata jibu katika dini za Jumuiya ya Wakristo?

13 Sasa, tunapotazama hapa na pale leo, ni akina nani hasa wanaojitahidi kuhubiri kweli ya Biblia na kuzoea maisha ya Ukristo wa kweli? Ni akina nani wanaotia bidii kama kikundi wasaidie wengine wafahamu mpango wa Mungu wa maisha safi zaidi na yenye furaha zaidi sasa, na uzima wa milele katika dunia itakayokuwa chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo? Ni akina nani wameungwa na “watu kumi” wa mfano, yaani, ni akina nani hata wamepata ongezeko halisi la mara kumi katika idadi za wenye kufuatana nao kwa maana ‘wanaona kwamba Mungu yu pamoja nao’? Bila shaka dini za Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) zilizopangiwa utaratibu hazipati ongezeko hilo la mara kumi. Sasa wako zaidi ya watu milioni 900 wanaojidai kwa uongo kuwa Wakristo wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Kama ongezeko hilo la mara kumi lingeingia katika idadi zao, wangekuwa mara mbili ya idadi ya watu duniani.

14. Ni jambo gani juu ya “watu kumi” wa mfano lililo la maana zaidi kuliko idadi tu?

14 Hapana, madhehebu za kidini za Jumuiya ya Wakristo hazipati ufanisi wa kiroho. Lakini fikiria mabaki yaliyotiwa mafuta ya Wayahudi wa kiroho. Wao wanatia kila jitihada wasaidie watu wengi kama iwezekanavyo wajifunze kweli ya Biblia. Wa maana zaidi kuliko hesabu ya watu wanaoshirikiana nao ni uhakika wa kwamba watu hao wamesafisha maisha zao wakafanya mabadiliko makubwa waishi kupatana na kanuni za Kikristo. Uhakika huo unakubaliwa na watu wengi sana. Katika miaka ya majuzi, mabaki wamepata pia ongezeko la zaidi ya mara kumi katika idadi zao.

15. (a) Sababu hasa ya “watu kumi” kufuatana na “Myahudi” wa kiroho ni nini? (b) Ni tunda gani la maana ambalo ni alama kuu ya Wakristo wa kweli?

15 Wale wanaoyaambia mabaki yaliyotiwa mafuta ya Wayahudi wa kiroho, “Tutakwenda pamoja nanyi,” wanafanya hivyo kwa sababu gani? Kwa sababu, kama vile wao wanavyoyaambia mabaki: “Tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zek. 8:23) Wamesikia​—kwa marafiki, majirani, wafanya kazi wenzao​—juu ya furaha ya jamii ya “Myahudi” wa kiroho, juu ya jamaa zenye umoja za wale wanaofuatana na jamii hiyo na juu ya maarifa yao ya Biblia pamoja na majibu yake kwa magumu ya maisha. Tena, wameona hasa mojawapo la “matunda” aliyosema Yesu yangeonyesha walio wafuasi wake. Aliwaambia wafuasi hao: “Kwa hili wote watajua kwamba ninyi m wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”​—Yohana 13:35, NW.

16. Je! wale ambao sasa ni Wakristo waliotiwa mafuta na wale wanaojiunga nao waliurithi upendo huo? Eleza.

16 Wale ambao wametumikia kama mashahidi wa Yehova wa Kikristo kwa muda mrefu hawakurithi upendo. Wayahudi wa kiroho na pia “watu kumi” wanaoshirikiana nao sasa walihitaji msaada kwanza kwa Wayahudi wa kiroho wa zamani zaidi, sawa na vile Wakristo waliogeuzwa karibuni wa karne ya kwanza katika Yerusalemu ‘walivyoendelea kujitoa wafundishwe na mitume.’ (Matendo 2:42, NW) Wakristo hao wa karne ya kwanza waliotiwa mafuta walijua iliwapasa kujifunza Biblia ndio wamkaribie Mungu zaidi, ndio waanzishe uhusiano naye. Iliwapasa ‘kubadili nia zao’ na ‘kuuvaa utu mpya’ unaoelezwa na Biblia.​—Rum. 12:2; Efe. 4:22-24.

17. Je! hesabu mara kumi halisi imejiunga kutumikia pamoja na mabaki yaliyotiwa mafuta ya Yehova katika siku hizi za mwisho?

17 Kwa hiyo leo “watu kumi, wa lugha zote za mataifa” ambao ni wa mfano sasa ‘wanakwenda pamoja’ na ‘Wayahudi’ wa kiroho wa Mungu kwa sababu wanataka kuingia katika uhusiano wenye upendeleo na Mungu. ‘Wanakwenda pamoja’ na watiwa mafuta hao kwa kuwaunga mkono kwa moyo wote. Je! hesabu mara kumi ya hao imeongezwa kwa mabaki ya kiroho kutimiza unabii? Ndiyo. Mwaka wa 1918 yalikuwako maelfu kadha ya Wanafunzi wa Biblia waliojiweka wakf waliokuwa wenye bidii wakitangaza habari njema za Ufalme, ulimwenguni pote. Mwaka wa 1947, mashahidi wa Yehova 207,552 waliripoti utendaji​—hiyo ilikuwa mara nyingi sana za idadi ya miaka iliyotangulia. Na mwaka wa 1974 walikuwako zaidi ya watu milioni mbili wa jamii ya “watu kumi” ya mataifa yote waliokuwa wakisema: “Tutakwenda nanyi.” Ongezeko hilo la mwisho la mara kumi limetokea baada ya miaka 27 tu.

“TUMESIKIA KWAMBA MUNGU YU PAMOJA NANYI”

18-20. (a) Mambo yaliyoonwa kabisa na mashahidi wa Yehova yanaonyesha nini juu ya vile watu wenye mioyo minyofu wamesaidiwa kutambua Wakristo wa kweli na ‘kwenda pamoja’ nao? (b) Ni mambo gani ambayo yameonwa na wale wanaohudhuria funzo letu hapa la kitabu juu ya mambo haya?

18 Mfano wa hali ya “watu kumi” hao wa mfano na kinachowavutia ‘washike upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi wa kiroho’ unaonekana katika yaliyoonwa na mwanamke kijana katika mkoa wa Virginia, United States ya Amerika.

19 Mwanamke huyo kijana alivutwa na mazungumzo ya Biblia aliyokuwa nayo na mmoja wa mashahidi wa Yehova. Ingawa alijiona mwenye hatia ya njia mbaya ya maisha aliyokuwa akifuatia wakati huo, mambo aliyojifunza na saburi ya Shahidi mwenye kumsaidia ilimvuta aendelee na mazungumzo yao. Alijulishwa kwa mashahidi wa Yehova wengine waliokuwa wamekuwa na mashaka kama yake na kujiona wenye hatia hapo kwanza. Upendo wao na saburi yao katika kumsaidia ilimsadikisha kwamba Mungu kweli alikuwa na watu hao. Mabadiliko aliyofanya katika maisha yake yalivutia wengine, kama anavyosimulia:

20 Mwanamume ninayefanyia kazi amelemaa. Alikuwa mtu mgumu kwa kuwa alikuwa amesitawisha nia ya kujitegemea alipokuwa mdogo. Alikuwa ameona dini yake kuwa ya unafiki. Aliliona badiliko la utu wangu kwa wazi sana hata akaanza kusikiliza niliyokuwa nikimwambia msichana mwenye kufanya kazi nami juu ya Biblia. Nikamjibu maulizo mengi. Mwishowe akafika kwenye mkutano wa Mashahidi. Alipata ujuzi wa kutosha na ufahamu hata akajaribu kubadili mambo aliyoona kuwa makosa, pamoja na tabia ya kuvuta sigara. Akawa mwanamume mpole asiyekasirika upesi. Sasa yeye na mkewe wanajifunza Biblia, wanahudhuria mikutano ya Mashahidi na wanajaribu kurudisha mapatano ya jamaa.

21. Kupatana na funzo letu juu ya unabii wa Zekaria, wenye kutafuta uzima bora wanaweza kufanya nini sasa?

21 Watu hao wamepata na wakatambua Ukristo wa kweli katika ulimwengu ambamo ulizo hili linaulizwa mara nyingi, Je! Ukristo wa kweli unaweza kupatikana? Ikiwa wewe u mtafutaji wa kanuni za haki na “ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye”​—yaani uzima bora katika dunia ya paradiso yenye amani​—tafuta alama zenye kuwatambulisha wanafunzi wa Kristo na, ukiisha wapata, useme, “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”​—1 Tim. 4:8; Zek. 8:23.

​—Kutoka Kitabu Paradise Restored to Mankind​—⁠by Theocracy!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki