Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 5/1 kur. 205-210
  • Wakati wa Kumchagua Mungu Awe Mwenye Enzi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati wa Kumchagua Mungu Awe Mwenye Enzi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA BWANA MWENYE ENZI KUU
  • BADILIKO LA ENZI KUU YA ULIMWENGU
  • MWENYE ENZI KUU WA WATU WALIOTENGENEZWA
  • Kumwacha Mungu Awe Mwenye Enzi Kuu wa Maisha Zetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Ulimwengu Mmoja, Serikali Moja, Chini ya Enzi Kuu ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Serikali Moja Ile ya Ulimwengu Mmoja Chini ya Enzi Kuu ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Yehova Ni Bwana Wetu Mwenye Enzi Kuu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 5/1 kur. 205-210

Wakati wa Kumchagua Mungu Awe Mwenye Enzi

1. Baada ya karne kumi na sita za kuwako kwa Jumuiya ya Wakristo, ulimwengu wa “kipagani” waona nini juu ya hali ya kidini ya mambo?

KWA zaidi ya miaka mia kumi na sita sasa, au tangu siku za Mtawala Konstantino Mkuu, ulimwengu umeona matendo ya Jumuiya ya Wakristo. Baada ya muda wote huo, ulimwengu uitwao wa “kipagani” waona nini juu ya hali ya kidini ya mambo? Mvurugo na mtengano wa kidini ulio mkubwa kuliko wote katika historia ya kibinadamu! Giza la kidini lenye kuenea dunia yote! Hali hii yapatana na unabii wa Biblia uliosema hivi: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.”​—⁠Isa. 60:2.

2. Giza hilo lilikuwa la kumpinga nani, naye alifanya nini kama ilivyotabiriwa katika Mathayo 24:14?

2 Giza lenye kuenea dunia yote limekuwa la kumpinga Mungu, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Mungu huyu, ambaye mwanzoni mwa juma ya uumbaji aliamuru hivi, “Iwe nuru”​—⁠alikuwa akikusudia kufanya nini? Alitenda kwa kupatana; alitenda kama alivyotenda karne kumi na tisa zilizopita, naye mtume Paulo ataja habari hiyo hivi: “Mungu yule yule aliyesema, ‘Katika giza acha nuru ing’ae amefanya nuru yake ing’ae ndani yetu, kutoa nuru ya ufunuo​—⁠ufunuo wa utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo.” (2 Kor. 4:6, The New English Bible; The Jerusalem Bible) Kwa hiyo, tangu mwisho wa siku zenye giza za Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Mungu uyu huyu ameagiza shughuli ya kutoa nuru iliyo kubwa kuliko shughuli zote katika historia yote ya kibinadamu iendelezwe. Aliitabiri katika maneno haya ya Mwana wake Yesu Kristo: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—⁠Mt. 24:14.

3, 4. Nuru hii imepokewaje, na ni nini kimezuia watu zaidi wasiangaziwe nuru?

3 Walakini, tusidhani kwamba shughuli hii ya ulimwenguni pote imepokewa zaidi kuliko ilivyopokewa karne kumi na tisa zilizopita. Kwa habari ya jinsi jitihada ya kutoa nuru wakati huo ilivyopokewa, twasoma hivi: “Kulikuwako Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu, akija katika ulimwengu. Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea.” (Yohana 1:9-11) Wakati huo, wale walioikubali nuru hiyo walijaribu kuwaangazia nuru wengine; hawakuificha nuru. Sababu kwa nini wengi zaidi hawakuangaziwa nuru ni kwamba kulikuwako upinzani mwingi wa kazi ya kutoa nuru. Yule mkubwa aliyesababisha upinzani huo wa nuru anaonyeshwa kwetu na mtume Paulo anapoandika hivi:

4 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa [taratibu hii ya mambo] amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”​—2 Kor. 4:3, 4.

5. Ni nani mwenye kusababisha upinzani kwa utangazaji wa Ufalme, naye ni mwenye enzi kuu wa nani zaidi ya “majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho”?

5 Vilevile, shughuli ya kutoa nuru inayoendelezwa kupitia kwa tangazo la habari njema juu ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi uliosimamishwa katika mbingu inapingwa ulimwenguni pote. Aliyesababisha upinzani wa habari njema juu ya Masihi (Kristo) karne kumi na tisa zilizopita ndiye yule yule anayeongoza upinzani wa tangazo la ujumbe wa Ufalme tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Huyo ndiye mwenye kupofusha fikira za watu, ambaye mtume Paulo aliita “mungu wa taratibu hii ya mambo.” (NW) “Mungu” huyu anao washiriki wake katika shughuli hii ya kutia giza​—⁠“wakuu wa giza hili,” “majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.” (Efe. 6:12) Kama alivyo mwenye enzi kuu wa haya “majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho,” ndivyo anavyojitahidi kuendelea kuwa mwenye enzi kuu wa maisha za watu duniani. Ndiyo sababu kama iwezekanavyo, anaizuia nuru ya kweli ya Ufalme ising’ae katika akili za watu waliopofushwa.

6, 7. Wakristo wa kweli hushindanaje mweleka na majeshi hayo ya kiroho, kulingana na kanuni gani zilizotajwa na Yesu na Yakobo?

6 Haya “majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho” chini ya mwenye enzi kuu wao, Shetani, Ibilisi, ndio inawapasa Wakristo wa kweli washindane mweleka nao wanapofanya shughuli yao ya kutoa nuru. Wakristo hao hufanyaje hili? Si kwa kufunua chanzo cha Kiibilisi cha imani ya mashetani, unajimu, uchawi, mambo ya kisiri, mambo ya kutumia hirizi na ushirikina wa kuabudu wazee wa ukoo waliokufa tu. Kushindana mweleka kwa Wakristo juu ya majeshi hayo yenye uovu yasiyoonekana, yenye kupita uwezo wa kibinadamu hufanywa pia kwa kukataa kwa imara kulazimishwa kuwa sehemu ya hii “taratibu ya mambo,” ambayo Shetani ndiye “mungu” wake. Wanafuata kanuni ya maisha ya kweli ya Kikristo ambayo Yesu Kristo alisema: “Wao [wafuasi wangu] si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:16) Mwanafunzi Yakobo aliwaambia hivi wale Wakristo wa kujidai wasiokuwa wakiishi kupatana na kanuni hiyo:

7 “Hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”​—⁠Yak. 4:4.

8, 9. (a) Sababu ya kujitenga na ulimwengu ni nini, na matokeo yake ni nini? (b) Kwa hiyo Wakristo wanapewa amri gani na Amri-jeshi Mkuu wao, kupitia kwa mtume Paulo?

8 Sababu ya kujitenga kwa Wakristo na ulimwengu ni kwamba ulimwengu uko upande wa mwenye enzi kuu wake asiyeonekana mwenye uwezo kupita ule wa kibinadamu, yeye aliye Shetani na Ibilisi kwa Mungu wa kweli na aliye hai, Yehova. Hivyo, hakuna matokeo ya jambo hilo kuliko haya, kwamba kushindana mweleka kwa Kikristo na “majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho” kutaendelea maadamu ulimwengu huu wadumu na mpaka Shetani Ibilisi na malaika zake wa kishetani watakapofungwa minyororo na kutupwa katika shimo lisilo na mwisho kwa muda wa miaka elfu ya utawala wa Kristo. (Ufu. 13:1-8; 16:13-16; 19:19 mpaka 20:3) Rafiki za Yehova Mungu wanajitayarisha kwa sehemu mbalimbali za “silaha zote za Mungu” kwa kusudi la kukanusha na kusimama imara katika siku hii yenye uovu. (Efe. 6:11) Huku hakutii ndani silaha zo zote za mwili.​—2 Kor. 10:4.

9 Amri kutoka kwa Amri-jeshi Mkuu wa kimbinguni, kupitia kwa mtume Paulo, kwa askari zake ni hii: “Basi simameni [imara], hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa [roho] ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika [roho].”​—⁠Efe. 6:14-18.

YEHOVA BWANA MWENYE ENZI KUU

10. Wale wanaomfanya Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wa maisha zao wanasimama na nani?

10 Hakuna shaka juu ya anayeachwa na wale wote wanaotii amri hii ya kimungu awe mwenye enzi kuu wa maisha zao. Ni Yehova Mungu, ambaye neno lake ni kama upanga mkononi mwao, “upanga wa [roho].” Katika kumchagua kama Mwenye Enzi Kuu wao, wanasimama, si na ulimwengu na taratibu yake ya mambo, bali na Yesu Kristo na mitume wake, pia pamoja na Mfalme Daudi wa Yerusalemu wa kale, na mzee Ibrahimu babu wa kidunia wa Masihi, naam, pamoja na wanaume na wanawake wote wenye imani ya Kimungu ambao habari yao imo katika Biblia.

11. Ibrahimu alionyesha uhusiano aliokuwa nao na Mungu kwa kumwita Yeye nani, na watafsiri wengine hutafsirije maneno yaliyotumiwa na Ibrahimu?

11 Ibrahimu alimkubali Mungu Aliye Juu Zaidi Sana kama Bwana Mwenye Enzi Kuu wake. Alipokwisha kurudi kwa ushindi kutoka vitani kupigana na wafalme wanne wenye kushambulia akawa amebarikiwa na Melkizedeki kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi Sana, neno la kimungu lilimjia Ibrahimu, likisema hivi: “Usiogope, Abramu. Mimi ngao yako. Thawabu yako itakuwa kubwa sana.” Katika kuitikia hili, Ibrahimu alionyesha nani aliyekuwa Bwana Mkuu kwa jinsi alivyomtaja Mungu, akisema: “Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, utanipa nini?” Mungu alipomwahidi kumpa nchi ambayo kwa hiyo Alikuwa amemwongoza, Ibrahimu alionyesha uhusiano ambao katika huo alijiona yumo kwa kusema: “Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, ni kwa njia gani nitajua kwamba mimi nitaimiliki?” (Mwa. 15:1, 2, 8, NW) Katika lugha yake mwenyewe, Kiebrania, mzee Ibrahimu alitumia hapa maneno haya, katika kumtaja Mungu A·do·nayʹ Yeho·wihʹ. Ili kuepuka kutumia jina la Mungu, watafsiri wengine hutafsiri usemi huu kama “Bwana Mungu.” Mtungaji wa Concordance ya Biblia Young huutafsiri “Bwana Yehova.” Lakini The Jerusalem Bible huutafsiri “Bwana wangu Yahweh.” Ndivyo na The Emphasised Bible ya Rotherham.

12. Ni nini maana ya neno la Kiebrania A·do·nayʹ, kama inavyoonyeshwa katika New World Translation?

12 Walakini, neno la Kiebrania A·do·nayʹ halimaanishi “Bwana wangu.” Lafahamika kuwa aina ya zamani ya A·do·nimʹ, maana yake halisi “mabwana.” Hivyo wakati neno hilo linapotumiwa kuhusu mtu mmoja huwa na maana ya utukufu au fahari; humaanisha bwana katika njia yenye utukufu, bwana wa fahari. Neno hili la zamani la Kiebrania latumiwa katika Biblia kuhusu Yehova au Yahweh peke yake. Kwa sababu hiyo New World Translation hufasiri jina la cheo la Kiebrania A·do·nayʹ kama “Bwana Mwenye Enzi Kuu.”a Kupatana na hili, tafsiri za Kiebrania za Matendo 4:24 hutumia neno A·do·nayʹ kumaanisha “Bwana Mwenye Enzi Kuu.”​—⁠Matendo 4:24, New World Translation.

13. Kwa sababu gani kwa kufaa Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, na kwa hiyo aweza kutoa mwito wa kushindana?

13 Kweli kweli Mungu huyu Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, maana Yeye yu juu ya vitu vyote naye hakumpa ye yote kati ya viumbe vyake uwezo wa kulingana na Wake. Kwa njia hiyo hudumu kuwa Mwenye Nguvu Zote, Mweza Yote. Kwa kufaa, kama Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, Yehova alimwambia Ibrahimu hivi: “Mimi Mungu Mwenye Nguvu Zote. Utembee mbele zangu ujionyeshe asiye na kosa.” (Mwa. 17:1, NW) Na kwa nabii Musa, Yehova alisema hivi: “Mimi Yehova. Nami nilikuwa nikionekana kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo kama Mungu Mwenye Nguvu Zote.” (Kut. 6:2, 3, NW) Kwa ujasiri mwingi yeye aweza kutoa mwito huu wa kushindana: “Mtanifananisha na nani, basi, nipate kuwa sawa naye?” (Isa. 40:25) Je! sisi leo, kama Ibrahimu, tutamfanya Mungu huyu Mwenye Enzi Kuu wa maisha zetu?

14. Kwa sababu gani sasa ndio wakati wetu wa kutenda kwa hekima juu ya enzi kuu ya Yehova?

14 Hakuna mwenye enzi kuu wa kweli anayeweza kungojea raia zake, mmoja mmoja wajiamulie mambo. Mwenye enzi kuu anao utawala wake wa kuendeleza na wajibu wote wa uliwali wake, naye yampasa atimize kazi zake katika wakati wake uliowekwa. Sisi viumbe duni vya kibinadamu hapa duniani tunajitakia makuu mno ikiwa twadhani ni lazima Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, Yehova Mungu, angojee mpaka tuamue awe Mwenye Enzi Kuu wetu kabla Yeye hajatimiza kusudi lake halisi lililowekewa wakati barabara. Yeye hutenda wakati wake uliowekwa ujapo kupatana na haki yake ya enzi kuu! Kwa sababu hii sasa ndio wakati wa haraka kwa kila mmoja wetu kutenda kwa hekima juu ya enzi kuu Yake!

BADILIKO LA ENZI KUU YA ULIMWENGU

15. Ni tangu wakati gani tangazo la kimbinguni juu ya enzi kuu ya kimungu limepelekwa kwa wanadamu, na kwa sababu gani halikupelekwa kabla ya wakati huo?

15 Tangazo lenye maana kuliko yote kuhusu dunia yetu limekwisha kutolewa katika mbingu, nalo lapelekwa kwenye ulimwengu wa wanadamu kuzunguka dunia yote: “Enzi kuu ya ulimwengu imepelekwa kwa Bwana wetu na Kristo wake, naye atatawala milele na milele!” (Ufu. 11:15, The New English Bible; An American Translation) “Sasa enzi kuu ya ulimwengu ni ya Bwana wetu na Kristo Wake; na Yeye atakuwa Mfalme mpaka Vizazi vya Vizazi.” (Weymouth, 3rd ed.) Uhakika huu wa maana sana kwa ulimwengu wote umetimia tangu mwaka wa 1914 W.K. Katika mwaka huo “majira ya Mataifa,” au, “nyakati zilizowekwa za mataifa,” zilimalizika karibu na Oktoba 4/5, zinapohesabiwa tangu kuharibiwa kwa Yerusalemu na nchi ya Yuda na Wababeli katika mwaka wa 607 K.W.K. Kwa miaka 2,520 tangu wakati huo Mataifa (yasiyo ya Kiyahudi) wametawala mambo ya kibinadamu bila kizuizi cho chote upande wa ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Katika wakati huo wote Wayahudi wamekuwa bila ufalme katika Yerusalemu mikononi mwa ukoo wa kifalme wa Mfalme Daudi.​—⁠Luka 21:24, UV, NW.

16. Kwa hiyo, kwa sababu gani tangu mwaka wa 1914 W. K. tangazo juu ya enzi kuu ya kimungu lingeweza kufanywa?

16 Wakati huo, katika mwaka wa 607 K.W.K., mfalme wa ukoo wa Daudi wa mwisho kutawala aliondolewa katika ufalme, na Mataifa wakaruhusiwa kuwa na utawala kamili na kutumia enzi kuu yao juu ya wanadamu, Wayahudi na Mataifa pia. Lakini mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 W.K. ulimalizika wakati wa Yesu Kristo kuendelea kungojea katika mkono wa kuume wa Baba yake wa kimbinguni. Wakati huo Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu alimweka Mwanawe Yesu Kristo katika kiti cha enzi katika “Yerusalemu wa mbinguni,” katika Mlima Sayuni wa kimbinguni. Katika njia hii ukoo ule wa kifalme wa Daudi ulikwezwa tena kwenye kiti cha enzi, na ufalme wa Kimasihi ukazaliwa. Wakati ule ule Mfalme-Kuhani mkuu kama Melkizedeki wa kale, yaani, Yesu Masihi, alitawazwa katika ufalme wa kimbinguni. (Ebr. 10:12, 14; Zab. 110:1-4) Tangu wakati huo ingeweza kutangazwa kwa ulimwengu wa wanadamu hivi: “Enzi kuu ya ulimwengu imepelekwa kwa Bwana wetu na Kristo wake, naye atatawala milele na milele.”​—⁠Ufu. 11:15, AT.

17. Wanadamu na mataifa waliombwa maoni yao kwanza kabla Mungu hajachukua hatua, na itikio linalofaa lilionyeshwaje na wazee wale 24?

17 Ulimwengu wa wanadamu haukuombwa kwanza maoni juu ya hili. Pia mataifa ya kidunia, pamoja na enzi zao za kitaifa, hayakuombwa kwanza maoni juu ya hatua hii ya Mungu. Mungu Aliye Juu Zaidi Sana aliendelea katika wakati wake uliowekwa akausimamisha ufalme wa mbinguni wa Kimasihi, kupatana na haki yake mwenyewe ya enzi kuu ya ulimwengu wote. (Dan. 4:35) Kuitikia kuzuri kwa watu wonyesho wa haki wa Mungu wa enzi kuu kulionyeshwa katika tendo la wazee 24 waliosujudu mbele Zake wakasema: “Tunakushukuru wewe, [Yehova] Mungu Mwenyezi, uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu umeutwaa uweza wako ulio mkuu, na kumiliki.”​—⁠Ufu. 11:16, 17.

18. Hata hivyo, mataifa yaliitikiaje, na hii ilitabiriwaje na wazee wale 24?

18 Namna gani mataifa ya kilimwengu? Ah, wao walipendezwa mno kufanya vita yao ya ulimwengu ya kwanza wakaimalize kwa ajili ya utawala wa ulimwengu. Kwa sababu ya kujaribu kuwashurutisha watu wote wawasaidie katika vita ya kutumia vifaa vyote, waliwatesa vikali wale Wakristo wa kweli waliounga mkono enzi kuu ya Bwana Mungu na Kristo wake. Hii ilikuwa kama ilivyokuwa imetabiriwa na wale wazee 24, walioendelea kusema: “Na mataifa walikasirika, hasira yako nayo ikaja, na wakati ukaja wa kuhukumiwa waliokufa, na wa kuwapa thawabu yao watumwa wako manabii na watakatifu, na hao walichao jina lako, wadogo kwa wakubwa, na wa kuwaharibu hao waiharibuo nchi.”​—⁠Ufu. 11:18.

19. (a) Wakati huu ndio unaotufaa tujiulize maulizo gani juu ya enzi kuu? (b) Tukifuata mfano wa mataifa itakuwaje kwetu?

19 Mpaka leo hii mataifa wanaendelea kuwakasirikia “watakatifu, na hao walichao jina [Lake], wadogo kwa wakubwa” wa Yehova. Hivyo ni wakati unaomfaa kila mmoja wetu ajiulize hivi, ‘Namna gani mimi? Je! mimi nitauacha mwendo wa mataifa ya kilimwengu uniongoze kama mfano? Au, nitakuwa kama wazee wale 24 wa Ufunuo 11:16, 17 nimshukuru Mungu kwa kuonyesha enzi kuu yake na kuutwaa uwezo wake ulio mkuu ili kutawala? Je! mimi nakubali kwamba enzi kuu ya ulimwengu imepelekwa kwa Yehova Mungu? Je! mimi, kwa kukubali uhakika huu, namchagua Yeye kama Mwenye Enzi Kuu wangu wa kimbinguni? Je! ninamwacha Yeye awe mwenye enzi kuu wa maisha yangu?’ Hata iweje, hatuwezi kuepuka sasa kuwa na uhusiano mpya na Mungu Bwana Mwenye Enzi Kuu, ama uhusiano mzuri ama uhusiano mbaya. Ye yote anayejipanga upande wa mataifa yenye hasira anajiweka katika uhusiano mbaya na Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Huo wamaanisha uharibifu wa ye yote anayefanya hivyo, maana mataifa ndio “hao waiharibuo nchi,” nao wataharibiwa katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–​Magedoni.​—⁠Ufu. 16:14, 16.

20, 21. (a) Katika kujibu ulizo la kuwa shahidi wa Yeye tunayefanya kuwa Mwenye Enzi Kuu wetu, tunataja maneno gani ya mtunga zaburi? (b) Kama vile katika habari ya Mfano wetu mkubwa zaidi, hakuwezi kuwa na heshima kuu kuliko ipi duniani?

20 Hili latokeza ulizo, ‘Nikimwacha Mungu awe Mwenye Enzi Kuu wa maisha yangu, je! huko kwamaanisha kuwa shahidi wa Yehova?’ Katika kujibu ulizo hilo, twaweza kuelekeza kwa mtunga Zaburi aliyeongozwa na Mungu, aliyemwacha Mungu awe Mwenye Enzi Kuu wa maisha yake. Yeye aliandika hivi: “Lakini mimi, kumkaribia Mungu ni kuzuri kwangu. Katika Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu nimeweka kimbilio langu, nizitangaze kazi zako kote.” (Zab. 73:28, NW) Pia: “Ee Mungu wangu, uniokoe na mkono wa mwovu, na kiganja cha yeye anayetenda isivyo haki na kwa kuonea. Kwa maana wewe ndiwe tumaini langu, Ee Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, tumaini langu tangu ujana. Nitaingia katika uweza mkuu, Ee Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu; nitaitaja haki yako, yako peke yako.”​—⁠Zab. 71:4, 5, 16. NW.

21 Hivyo twauliza, Je! mtu wa leo anayeweka kimbilio lake katika Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu atafanya tofauti na alivyofanya mtunga Zaburi wa kale, yaani, ‘kutangaza kazi zote za Mungu’? Je! mtu wa leo ambaye ameokolewa “na mkono wa mwovu” na ambaye amemfanya Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu kuwa tumaini lake atafanya tofauti na alivyofanya mtunga Zaburi, yaani, ‘kuingia katika uweza mkuu’ na ‘kuitaja haki ya Mungu’? Bila shaka hatamwonea haya Mwenye Enzi Kuu wa maisha yake. Yesu Kristo, Mfano wetu mkubwa zaidi, hakumwonea haya Mwenye Enzi Kuu wake, Yehova Mungu. Hivyo, akawa shahidi wa Yehova, na kwa sababu hii anaitwa “Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu.” Hujisema kuwa “shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.” (Ufu. 1:5; 3:14) Wale wanaokuwa wafuasi wake kweli kweli yawapasa vilevile wawe mashahidi wa Baba yake Yehova. Hakuna heshima kubwa zaidi ambayo ye yote angeweza kuwa nayo duniani kuliko kuwa shahidi wa Yehova.

22. Tukimfanya Yehova Mwenye Enzi kuu wa maisha zetu tutapatwa na nini, lakini tunaweza kusali namna gani kama mtunga zaburi?

22 Tukimfanya Yehova Mungu Mwenye Enzi Kuu wa maisha zetu tutapatwa na mateso kutokana na wale wanaomfanya Shetani Ibilisi mwenye enzi kuu wao kwa kujifanya wenyewe “wa ulimwengu,” ambao mwovu huyo ndiye “mungu” na “mkuu” na mwenye enzi kuu wake. (2 Kor. 4:4; Yohana 14:30; 15:19) Lakini, wakati wa kuteswa, anayeteswa aweza kusali kama Mfalme Daudi hivi: “Wewe ni Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu. Unitende kwa ajili ya jina lako. Kwa sababu fadhili zako za upendo ni njema, uniokoe.” (Zab. 109:21, NW) “Ee Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, nguvu ya wokovu wangu, umefunika kichwa changu katika siku ya jeshi lenye silaha. Ee Yehova, usiziruhusu tamaa za mwovu. Usiendeleze hila yake, wasije wakakwezwa.” (Zab. 140:7, 8, NW) “Macho yangu yakuelekea wewe, Ee Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu. Nimekukimbilia wewe. Usiimwage nafsi yangu. Uniepushe nisishikwe na mtego ambao wamenitega na mitego ya wale wanaozoea madhara.”​—⁠Zab. 141:8, 9, NW.

MWENYE ENZI KUU WA WATU WALIOTENGENEZWA

23. Kwa kumfanya Yehova Mwenye Enzi Kuu wake, kwa sababu gani mtu hatakuwa peke yake, kama inavyoonyeshwa na Ezekieli 36:37, 38?

23 Ikiwa sasa wamchagua Yehova Mungu kama Mwenye Enzi Kuu wako, hutakuwa peke yako. Utakuwa mmoja wa watu wake. Yeye si Mwenye Enzi Kuu wa mtu mmoja tu duniani, bali ni Mwenye Enzi Kuu wa watu waliotengenezwa. Akitumia taifa la kale la Israeli kama mfano wa Waisraeli wa kiroho ambao anakusanya kutoka katika Babeli Mkuu wa kidini katika huu “wakati wa mwisho,” asema hivi: “Hivi ndivyo amesema Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, ‘Hivi ndivyo bado nitakavyojiacha mwenyewe nitafutwe na nyumba ya Israeli niwatendee: Nitawazidisha kama kundi pamoja na wanadamu. Kama kundi la watu, watakatifu, kama kundi la Yerusalemu katika majira yake ya sikukuu, ndivyo miji iliyokuwa imekuwa ukiwa itakavyojaa kundi la wanadamu; na itawapasa watu wajue kwamba mimi ndimi Yehova.”​—⁠Eze. 36:37, 38, NW; Ufu. 18:1-4; Dan. 12:4.

24. Wale wanaomfanya Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wa maisha zao wanabarikiwaje, na ni uchaguzi gani utakaoamua kama tutaokoka tuishangilie Taratibu Mpya?

24 Wenye baraka ni wale leo wanaomchagua Yehova kama Mungu wao na kumwacha Yeye awe Mwenye Enzi wa maisha zao. Yeye hutawala juu yao kama Mfalme wa kimbinguni kupitia kwa Mwana wake aliyetawazwa, Yesu Masihi. Katika “dhiki kubwa” inayokaribia sana, wakati enzi kuu za kitaifa zenye kugawanyika leo zitakapoharibiwa kisha Shetani Ibilisi, mwenye enzi kuu asiyeonekana wa mataifa afungwe na kutiwa katika shimo lisilo na mwisho, Mungu Mwenye Nguvu Zote atawalinda na kuwasalimisha wale ambao kwa upendo wanaitegemeza enzi kuu yake. (Mt. 24:21, 22; Ufu. 7:14, 15) Je! tutakuwa miongoni mwa waokokaji hao wenye baraka watakaoishangilia taratibu mpya yenye haki chini ya ‘enzi kuu moja ya Bwana wetu na Kristo wake’? Kumchagua kwetu Yehova kama Mwenye Enzi Kuu wa maisha zetu na kuamue hili kwa ajili yetu.​—⁠Ufu. 11:15, AT.

—⁠Kutoka The Watchtower, November 1, 1975.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama maelezo ya chini juu ya Mwanzo 15:2, 8 katika chapa ya 1971 ya New World Translation of the Holy Scriptures.

[Picha katika ukurasa wa 208]

Wale wanaomchagua Yehova kama Mwenye Enzi Kuu wao wanajitia katika jamii moja na watu wenye imani ya Kimungu kama Yesu, Ibrahimu na Daudi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki