Matukio Ambayo Yangali Mbele
KARIBUNI kutakuwa na dunia isiyo na msukosuko, uvunjaji wa sheria, magonjwa na maumivu. Karibuni magereza, mahospitali na wafanya kazi wa mahospitali hawatahitajiwa tena.-—2 Pet. 3:13; Ufu. 21:3-5.
Kuwako kwa hali ya mambo katika siku zetu si ndoto tu. Kunategemea ahadi yenye kutegemeka ya Yeye mwenye uwezo kamili wa kutimiza hayo. Huyo ndiye Muumba wa mwanadamu, Yehova Mungu.
Walakini, kabla hajachukua hatua ya kutokeza dunia yenye kujawa na haki, matukio mengine ya kustaajabisha lazima kwanza yatukie. Yatakapokuwa yakitukia, watu wenye kumcha Mungu watapata uhakikisho zaidi kwamba, ijapokuwa wasiwasi na taabu zinaongezeka duniani, taratibu mpya yenye haki inakaribia. Badala ya kupatwa na hangaiko kubwa na woga mwingi, wao watatii onyo la upole la Bwana Yesu Kristo: “Changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.”—Luka 21:28.
Lakini ni matukio gani yenye kutikisa ulimwengu yatakayotangulia kukombolewa kwa wanadamu na taabu ambazo zimewasumbua muda mrefu?
KUHUBIRIWA KWA “HABARI NJEMA”
Mojawapo la matukio haya sasa linaelekea kufikia upeo. Ni kuhubiriwa kwa “habari njema” za ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo wake. (Mt. 24:14) Wewe mwenyewe umeona ushuhuda nyakati nyingi kwamba “habari njema” hizo zinatangazwa. Je! hajapata mtu fulani kutumia wakati aseme nawe juu ya ufalme wa Mungu? Na je! hukuona kwamba mashahidi wa Yehova ndicho kikundi cha pekee cha Wakristo wanaofikiria kufikia watu kwa faragha na hadharani ili waweze kuusikia ujumbe huo? Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo katika nchi 210. Ingawa wanateswa, kusingiziwa na kufanyiwa dhihaka katika sehemu mbalimbali za dunia, wao hawakuacha utendaji wao. Hata wapigwapo marufuku na serikali, wao huendelea kuhubiri, wakimtii “Mungu kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.
Matokeo ya utendaji huo yamekuwa nini? Kwanza, wanafunzi waliochaguliwa na Mungu wakaungane na Mwanawe katika utawala wamekusanywa kati ya wakaaji wa dunia. (Mt. 24:31) Lakini si hayo tu. Kila mwaka makumi ya maelfu ya waamini wengine huweka wakf maisha zao kwa Yehova Mungu na, kwa kujipatanisha na amri za Biblia, wameanza kuishi kwa njia yenye kuonyesha wanamnyenyekea Yesu Kristo kama Mfalme. Leo zaidi ya wanaume, wanawake na watoto milioni mbili duniani pote wanafanya hivyo. Hatua yao ya kutubu na kumkubali Yesu Kristo kuwa ndiye Bwana wao kwa utukufu wa Baba yake, Yehova, ilisimuliwa kwa mtume Yohana katika njozi ya unabii. Njozi hiyo inawaonyesha kuwa “mkutano mkubwa” wa watu wa mataifa yote ambao “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.”—Ufu. 7:9, 14.
“Mkutano mkubwa” huo wanatazamia kwa shauku nyingi kuokoka mwisho wa taratibu iliyopo ya mambo isiyomcha Mungu. Wanajua kwamba ‘siku ya Yehova’ ya uharibifu itakuja mara tu baada ya watu na mataifa kufikia hatua ya kutangaza “Kuna amani na salama!” (1 The. 5:3) Tayari zimekwisha tokea dalili za kuelekea kufanya tangazo hili. Si kwamba viongozi wa ulimwengu wanatumia-tumia zaidi tu maneno “amani” na “salama,” bali pia wanasitawisha uhusiano mzuri wa kuvumilia zaidi mataifa yaliyo na mawazo tofauti na mipango ya kijamii.
UHARIBIFU WA ‘BABELI MKUU’
Lakini ni nini kitakachokuwa cha kwanza kuharibiwa wakati watu watakapokuwa wakisema, “Kuna amani na salama!”? Kupatana na Kitabu cha Biblia cha Ufunuo twajifunza kwamba “mwanamke,” kahaba aitwaye ‘Babeli Mkuu’ ndiye atakayekuwa wa kwanza. Lakini yeye ni nani?
Maandiko Matakatifu yanasema kwamba kahaba huyu anafananisha “mji ule mkubwa, wenye ufalme juu ya wafalme wa nchi.” (Ufu. 17:18) Hiyo inamfanya kuwa milki. Kwa kuwa Biblia inataja watawala wengine na wafanya biashara wakiomboleza juu ya uharibifu wake, bila shaka ‘Babeli Mkuu’ ni milki ya kidini. (Ufu. 18:9-19) Hii inapatana na uhakika wa kwamba dini imejaribu kutawala siasa. Pia, mji wa kale wa Babeli ulijulikana hasa kwa kuwa mahali pakuu pa kidini. Kwa hiyo basi, kwa kufaa ‘Babeli Mkuu’ inafananisha milki ya ulimwengu ya dini ya uongo.
Ingawa serikali za kisiasa zimetumia pia dini kwa makusudi ya kichoyo, karibuni yatachokeshwa na kusumbuliwa na kuongozwa na dini wanapoendesha kazi zao. Watachukizwa sana na ‘Babeli Mkuu’ na kumwinukia wakiwa na hasira nyingi sana ya kumharibu.—Ufu. 17:16.
VITA KUU YA MUNGU
Kwa sababu ya kutotosheka na kufutilia mbali dini ya uongo, wanasiasa ndipo watakapojaribu kumwaga hasira yao juu ya wale wanaounga mkono ibada ya kweli—“wateule” na “mkutano mkubwa,” wanafunzi wote wenye kushikamana na Yesu Kristo kwa uaminifu. Shetani Ibilisi na mashetani wake atachochea wanasiasa wafanye hivyo na kwa njia hiyo wataongozwa kwa werevu wakapigane na Yehova Mungu na Mfalme wake aliyewekwa, Yesu Kristo.—Ufu. 16:14.
Walakini, Yehova Mungu hatayaruhusu mataifa ya dunia yaharibu watu wake. Kupitia kwa Mwanawe na majeshi hodari ya malaika, atakuja kulinda watumishi wake wa kibinadamu. Biblia inasimulia kwa njia ya mfano litakalotukia:
“Tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda, aitwaye Mwaminifu na Wa-kweli, naye kwa haki ahukumu na kufanya vita. . . . Na majeshi yaliyo mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe, safi. Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi. Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA.
“Kisha nikaona malaika mmoja amesimama katika jua; akalia kwa sauti kuu, akiwaambia ndege wote warukao katikati ya mbingu, Njoni mkutane kwa karamu ya Mungu iliyo kuu; mpate kula nyama ya wafalme, na nyama ya majemadari, na nyama ya watu hodari.”—Ufu. 19:11-18.
WATAWALA WASIOONEKANA WAONDOLEWA
Hata hivyo, uharibifu wa wanadamu wasiomcha Mungu usingetosha kuondokea hali zenye haki duniani. Karne nyingi zilizopita Yehova Mungu aliuharibu ulimwengu mwovu wa wanadamu kwa gharika ya dunia yote. Lakini hiyo haikuzuia uovu usitokee tena kati ya wazao wa waokokaji wa Gharika. Mojawapo ya sababu kubwa za hilo kutukia ni kwamba Gharika haikuondolea dunia maongozi ya Kishetani.
Walakini, baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni, maongozi ya Kishetani yataondolewa kabisa. Shetani na mashetani wake watazuiwa katika shimo refu lisilopimika, yaani, hali kama ya kufa ya kutokutenda. Kwa habari hiyo twasoma hivi katika Ufunuo 20:1-3:
“Nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena.”
BARAKA HUKO MBELE
Kuondolewa kwa masumbuo yote yenye kuletwa na wanadamu wasiomcha Mungu na majeshi ya viumbe vibaya vya kiroho kutaleta hali yenye kufanyiza mapenzi ya Mungu. Tena, wakati huo faida za dhabihu ya Yesu Kristo yenye kulipia dhambi zitatumiwa kwa ajili ya “mkutano mkubwa” wa watu watakaookoka uharibifu wa uovu wote, kwa kusudi la kuwakamilisha. “Mkutano mkubwa” huo wataanza kuelekea kwenye ukamilifu wakati wao mmoja mmoja wanapoitikia msaada watakaopatiwa kwa matumizi ya dhabihu yenye kulipia dhambi ya Yesu.
Chini ya uongozi wa ufalme wa Mungu, dunia hii itageuzwa iwe na hali yenye kupendeza sana ya kiparadiso. Kwa vyepesi Yehova Mungu anaweza kufanya kwa kadiri kubwa zaidi vile alivyofanyia Israeli wa kale apate kutimiza agizo alilompa mwanadamu katika Mwanzo 1:28:
“Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. Litachanua maua mengi, na kufurahi, naam, kwa shangwe . . . maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji.”—Isa. 35:1-7.
Si kwamba waokokaji wa vita kuu ya Mungu wataweza kufurahia baraka hizi tu, bali pia mamia ya mamilioni ya watu waliokufa yatafufuliwa wawe na nafasi ya kufurahia hali zenye haki kwa umilele wote. Kristo Yesu alisema, “saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Kutakuwa na furaha iliyoje wakati waokokaji wa Har–Magedoni watakapokuwa wakikaribisha wafu kutoka makaburini!
MATUKIO YALIYOKO MBELE YAMEPASWA YATUCHOCHEE TUCHUKUE HATUA
Lakini matukio yaliyoko mbele yamepaswa yakuchochee ufanye nini? Kwa kuwa unafahamu kwamba taratibu hii ya mambo isiyomcha Mungu inaelekea kukoma kabisa, je! isingekuwa vizuri ujiunge na kundi la watu wenye kuongezeka wanaosaidia wengine kujitayarisha kupata kibali ya Mungu na uzima? Je! isingefaa zaidi kujitahidi kuendelea kuwa na hali safi mbele za Yehova Mungu? Kabisa! Ndivyo mtume Petro alivyosihi waamini wenzake wafanye kwa sababu ya kuangamizwa kunakokuja kwa wote wasiomcha Mungu. Twasoma hivi:
“Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu [si mbingu halisi, bali “mamlaka zilizo kuu” ambazo zimetawala wanadamu] zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? Lakini, kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake. Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake.”—2 Pet. 3:11-14.
Je! hilo ndilo unalotamani? Ikiwa ndivyo, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanaoishi katika mtaa wako wangependezwa kukusaidia upate maarifa sahihi ya mapenzi ya Mungu sasa. Sababu gani usijipatie nafasi ya kuwa na funzo la Biblia bila malipo nyumbani mwako mwenyewe?