Mabadiliko Katika Baraza Inayoongoza
YEHOVA amekuwa akibariki watu kwa ongezeko kubwa la wahubiri wa Ufalme ulimwenguni mwote. Hasa ndivyo imekuwa baada ya kubadilishwa kwa mpango wa tengenezo uliopangwa katika kitabu Tengenezo kwa Kuhubiri Ufalme na Kufanya Wanafunzi, ambao ulianza kufanya kazi mwaka wa 1972.—Isa. 60:17.
Ni wazi pia kwamba tunakaribia kipeo katika historia ya wanadamu. Kwa hiyo mashahidi wa Yehova wanaweza kutazamia kwamba upinzani utaendelea kutokea mahali pengi. (Mt. 24:9) ‘Tunapotazamia hata ije siku ile ya Yehova, na kuihimiza,’ inatazamiwa kwamba watu wengi zaidi watajiunga upande wa ufalme wa Mungu chini ya Kristo, hayo yakiwa ni mapenzi ya Yehova.—2 Pet. 3:12.
Kwa sababu hiyo, inaonekana wakati huu inafaa kufanya mabadiliko zaidi ili watu wa Mungu wawe katika hali bora ya kutunza wapya wengi ambao sasa wamo katikati yao na kuangalia ongezeko zaidi wanalotumaini Yehova atawapa wakati ujao ulio karibu. (Isa. 60:8, 22) Hayo ni mambo ambayo Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova imefikiria kwa sala.
Ili kupunguza kazi yao, halmashauri sita za Baraza Inayoongoza sasa zimeanzishwa. Kila moja itakuwa na mwenyekiti wake, ambaye atatumikia kwa mwaka mmoja. Halmashauri hizi ni za usimamizi na haikusudiwi kwamba zitafanya mambo yote na kazi ya kawaida. Bila shaka yale mashirika mbalimbali ambayo yamekuwa yakitumikia faida za Ufalme vizuri sana mpaka sasa yataendelea kutimiza madaraka yao ya maana kama mashirika ya kisheria ya Mashahidi wa Yehova, ya Baraza Inayoongoza yao na halmashauri zake.
Halmashauri hizi sita, ambazo zilianza kufanya kazi Januari 1, 1976, ni kama ifuatavyo: Halmashauri ya Utumishi; Halmashauri ya Uandikaji; Halmashauri ya Uchapaji; Halmashauri ya Kufundisha; Halmashauri ya Utumishi wa Betheli; Halmashauri ya Mwenyekiti.
Katika matawi yetu ulimwenguni mwote, Halmashauri ya Tawi yenye washiriki watatu au zaidi wenye kuwekwa na Baraza Inayoongoza itasimamia mipango ya tengenezo ya kila tawi. Halmashauri hizi pia zitakuwa na mwenyekiti atakayetumikia kwa mwaka mmoja.
Inaonekana wazi kwamba uongozi wa Yehova umo katika kuanzishwa kwa mabadiliko haya ya karibuni. Bila shaka roho yake pia itatuongoza sote tuunge mkono kabisa na kufanya kazi kwa kushirikiana na mipango hii. Kwa hakika huu ndio wakati wa kuendelea kusonga mbele pamoja na mpanuko wa kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Katika jambo hili tunamtegemea Yehova aendelee kubariki yote ambayo yangali yatafanywa chini ya uongozi wa Kristo Yesu.—Mt. 28:19, 20.