Dunia Isiyo na Maumivu
“Wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena. Na yeye [Mungu] aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya.”—Ufu. 21:4, 5.
JE! WEWE unafikiria kuishi katika dunia ambayo hakuna mtu atakayepatwa na maumivu moyoni au mwilini? Huenda ukasema, ‘Hilo haliaminiki.’ Lakini hivyo ndivyo Yehova Mungu, Mfanyi wa wanadamu, ameahidi. Neno lake, Biblia, linataja wakati ambao wala “kilio, wala maumivu” hayatakuwapo tena. (Ufu. 21:4) Itakuwaje ahadi hiyo itakapotimizwa?
Maumivu yote ya mwili hayatakwisha. Kwa sababu gani? Kwa sababu kuna faida za kuwa na maumivu. Kwa mfano, msichana anayemenya viazi aweza kujikata kidogo. Asipoweza kuona maumivu, huenda akajikata sana bila kujua amejiumiza mpaka damu ianzapo kutoka. Kwa hiyo uwezo wa kuona maumivu ni wenye maana kwa sababu unawezesha mtu kuepuka haraka kinachomletea maumivu, na kuyapunguza.
Kisa cha Yesu Kristo kinaonyesha vizuri kwamba mwili mkamilifu unakuwa na maumivu pia. Yesu aliona maumivu moyoni kwa sababu ya ukatili wa wananchi wenzake. Tunasoma katika Maandiko kwamba ‘aliona huzuni kwa ajili ya ugumu wa mioyo yao.’ (Marko 3:5) Kwa habari ya alivyojisikia kabla tu hajasalitiwa, Biblia inasema hivi: “Naye kwa vile alivyokuwa katika dhiki, akazidi sana kuomba; hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchi.”—Luka 22:44.
Linalotakiwa si kumaliza uwezo wa kuona maumivu, bali ni kuondoa mambo yanayoletea wanadamu taabu—uonezi, uvunjaji wa sheria, ugonjwa, kifo na mambo mengineyo. Mambo hayo yatamalizwaje?
Hatua ya kwanza ya kuondoa maumivu ni kuharibu taratibu hii ambayo imefanya maisha yachukize sana mamilioni ya wakaaji wa dunia. Basi watu wote wenye kuiharibu dunia na mali zake watamalizwa. Biblia inaonyesha ndivyo itakavyokuwa. Tunasoma juu ya wakati ambamo Mungu ‘atawaharibu hao waiharibuo nchi.’ (Ufu. 11:18) Hiyo itatimiza Mithali 2:21, 22: “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”
Baada ya waovu wote kuharibiwa, watawala wenye haki wataanza kusimamia mambo yote ya dunia. Unabii wa Danieli unataja habari hiyo na kusema: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Dan. 2:44.
Ufalme huo wa Mungu utatumiwa kumaliza taabu zote. Hakuna mtu atakayetaabishwa na udhalimu, uonezi au uvunjaji sheria wa namna yo yote. Mtawala mkuu, Yesu Kristo, atahakikisha kwamba taabu hazitakuwako. Kwa habari ya vile atakavyosimamia mambo, Biblia inasema hivi: “Hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili.”—Isa. 11:3, 4.
Yesu Kristo atashirikiana na watawala wenzake kuondoa maumivu yanayoletwa na ugonjwa na kifo pia. Mpango watakaotumia kufanya hivyo unaelezwa katika Biblia kwa njia ya mfano kama mto wenye miti izaayo matunda kando kando. Tunaambiwa hivi: “Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni ya kuwaponya mataifa.” (Ufu. 22:2) Kupitia kwa mpango huo wanadamu watawekwa huru na udhaifu na kutokamilika. Mpango huo utawaponya kabisa wasipatwe tena na maumivu ya ugonjwa, uzee na kifo. Mungu anatoa ahadi hii: “Amemeza mauti hata milele; na Bwana [Yehova] atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isa. 25:8.
Wakati ugonjwa, uzee na kifo kitakapoondolewa, maumivu mengine hayatatokea kwa sababu ya dunia kusongamana na watu wenye kumaliza mazao yake. Muumba, ambaye ni mwenye hekima nyingi kuweza kuondoa ugonjwa, uzee na kifo kwa kutumia ufalme wake unaosimamiwa na Yesu Kristo, ana hekima na uwezo wa kuangalia mambo hayo pia kwa faida ya wanadamu. Kusudi lake hapo mwanzo lilikuwa kwamba dunia ‘ijazwe na kutiishwa,’ si kuwa na watu wengi kupita kiasi na kuharibiwa. (Mwa. 1:28) Kusudi hilo litatimizwa.
Namna gani mabilioni ya watu ambao ni wafu sasa, na wengine ambao huenda wakafa kabla ya taratibu hii kuharibiwa? Je! watapata nafasi ya kufurahia baraka katika ulimwengu usio na maumivu.? Kabisa! Yesu Kristo alisema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.
Kwa kuwa Mungu anakusudia kuleta dunia isiyo na maumivu, inatupasa tuwe na matendo yanayoonyesha tunaitaka kikweli. Mtume Petro alihimiza waamini wenzake hivi: “Kwa kuwa mnayangojea mambo hayo, fanyeni yote mwezavyo ili mwishowe mpatikane naye bila doa na bila waa na katika amani.”—2 Pet. 3:14, NW.
Ikiwa kweli tunataka dunia isiyo na maumivu, lazima tuonyeshe hivyo kwa kujitahidi tusiletee wenzetu maumivu ya bure tu, moyoni au mwilini. Inatupasa tutii mapenzi ya Mungu aliyowafunulia wanadamu katika Neno lake, Biblia. Tukifanya hivyo, tunaweza kutazamia dunia isiyo na maumivu makali sana ambayo yamehuzunisha wanadamu karne nyingi. Naam, tunaweza kuwa kati ya wale watakaopata faida ahadi ya Mungu itimizwapo, kwa kuuokoka mwisho wa taratibu hii isiyomcha Mungu, au kufufuliwa kwa wafu ikiwa tutakufa kabla ya wakati huo.