Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 5/15 kur. 239-240
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Habari Zinazolingana
  • Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Mume Anayejipatia Heshima Nyingi
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Ukichwa Katika Ndoa Unamaanisha Nini?
    Amkeni!—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 5/15 kur. 239-240

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Je! Mkristo aliyetiwa mafuta akitengwa na ushirika anaweza kurudishwa baadaye na bado awe na tumaini la kimbinguni?

Naam, hiyo inawezekana. Bila shaka, katika kila kisa Yehova Mungu ndiye atakayeamua kama atatoa msamaha.

Kwamba inawezekana inaonyeshwa na yale tunayosoma katika barua za mtume Paulo kwa kundi la Korintho. Aliandikia Wakristo waliokuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu na Waliopewa tumaini la uzima wa kimbinguni. Paulo alisema nao kama “wale waliotakaswa katika Kristo Yesu, walioitwa wawe watakatifu.”​—1 Kor. 1:2; 15:49.

Mmoja wa Wakristo hawa waliotiwa mafuta alianza kuzoea uasherati. Ilipokuwa wazi kwamba hakutubu na kuacha ufisadi wake, Paulo aliliamuru kundi limtenge na ushirika. (1 Kor. 5:1-5, 9-13) Lakini, inaonekana kwamba mtu huyo aliyetengwa na ushirika alitubu baadaye kwa unyofu. Anafahamika kuwa ndiye ambaye Paulo alitaja katika barua yake ya pili wakati alipowashauri Wakorintho wamsamehe na kumkubali arudi mtu huyo aliyekuwa mtenda dhambi.​—2 Kor. 2:6-11; 7:8-13.

Mtu huyo aliporudishwa katika kundi, tumaini lake lilikuwa nini? Je! alikuwa ameupoteza mwito wa kimbinguni, sasa tumaini lake likabadilishwa likawa la kupata uzima wa milele duniani? Sivyo, kwa maana tumaini la kidunia silo la kuwapa watu nafasi ya pili wanaposhindwa na lile la kwanza. Habili, Henoko, Nuhu, Ibrahimu na watu wengine wengi wenye imani nyingi walikuwa na tumaini la kupata uzima wa milele duniani, lakini hiyo haikuwa kwa sababu walishindwa kufaa katika mwito wa kimbinguni. Sababu tu ni kwamba hawakuishi katika wakati ambao mwito wa kimbinguni ulikuwa ukitolewa kulingana na mapenzi ya Yehova. (Ebr. 10:19, 20) Wote watakaopata uzima wa milele wanatakiwa kuwa na imani na ukamilifu juu ya dunia ya paradiso. Lazima Mkristo aliyetiwa mafuta kwa roho takatifu na aliyefanywa mshirika mwenzi wa Kristo awe mwaminifu kwa mwito huo ikiwa atapokea uzima wa milele wenyewe.​—Ufu. 2:10, 11; Flp. 3:8-14; Rum. 8;14-17.

Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba wakati Wakristo waliotiwa mafuta wanapokuwa duniani hawatendi dhambi kamwe. Wakiwa na mwili, bado wao hawajakamilika na kwa hiyo hutenda dhambi kama wanadamu wote, na huenda hata wakatenda dhambi nzito. Mwanafunzi wa Kikristo aliyekuwa pia mwandikaji wa Biblia na Mkristo mtiwa mafuta bila shaka, aliandika hivi: “Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa, katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yak. 3:2; 2:5) Inaelekea kuwa dhambi kama hiyo isiyo ya kukusudia inayotokana na kutokamilika ndiyo aliyomaanisha mtume Yohana kwa kusema “dhambi isiyo ya mauti.” (1 Yohana 5:16) Mungu aweza kusamehe dhambi kama hizo. Yohana alisema hivi: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”​—1 Yohana 1:9.

Lakini toba ni ya lazima. Mkristo aliyetiwa mafuta leo akizoea dhambi nzito asionyeshe toba, kundi litamtenga na ushirika kwa sababu ya kutii shauri la Mungu. Hata hivyo, akitubu baadaye, anaweza kusamehewa na kurudishwa, kama alivyorudishwa yule mtu katika Korintho.

Walakini, Mungu hasamehei dhambi zote. Kulingana na yale ambayo Yesu alisema katika Marko 3:28, 29, wale wanaokufuru roho ya Mungu kwa makusudi na kwa kujua hawawezi kusamehewa kamwe. Naye Paulo aliandika hivi; “Kama [tukizoea, NW] dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; bali kuna kuitazamia hukumu kwenye kutisha.” (Ebr. 10:26, 27) Dhambi hiyo isiyosameheka kwa wazi ndiyo ile ambayo Yohana alisema ni “dhambi iliyo ya mauti.”​—1 Yohana 5:16.

Mkristo aliyetiwa mafuta akitenda dhambi juu ya roho, akizoea dhambi kwa makusudi bila kutubu na ‘kumtundika mtini Mwana wa Mungu mara ya pili,’ Mungu atamkataa kabisa na milele. (Ebr. 6:4-6) Kwa kuwa hatubu, asingerudishwa katika ushirika. Ingekuwa lazima Yehova achague na kutia mafuta Mkristo mwingine awe badala yake ili hesabu ya 144,000 iendelee kuwa kamili. Hii inaweza kulinganishwa na uchaguzi wa mbingu wa Mathiya awe badala ya Yuda Iskariote asiye mwaminifu ili kuwe na mitume kumi na wawili waaminifu wa Yesu ambao juu yao kundi la Kikristo lingejengwa.​—Matendo 1:23-26; Efe. 2:20.

Je! hiyo ni kusema kwamba Mkristo aliyetiwa mafuta akitengwa na ushirika, pale pale Yehova huchagua mwingine wa kuwa badala yake? Hakuna mwanadamu anayeweza kusema hivyo, kwa maana hatuwezi kujua kama mtu huyo mwenye kutengwa na ushirika ameitenda dhambi isiyosameheka. Yehova ajua, kwa hiyo jambo hilo laweza kuachwa mikononi mwake. Ni juu yake kuamua ni jinsi gani hasa na wakati gani atataka kuchagua mtu wa kuwa badala ya huyo mwingine. Yeye hakutoa maelezo mengi juu ya jambo hilo katika Biblia. Kwa hiyo badala ya kufikiri-fikiri hivi na vile juu ya atakalofanya Yeye au kujaribu kukisia kama mtu aliyetengwa na ushirika hawezi kutubu, tunaweza kumwachia Yehova jambo hilo, yeye ambaye ndiye Mwamuzi mwenye haki,​—Ebr. 12:23.

Ikiwa kundi limelazimika kutenga mtu na ushirika lakini baadaye atubu na kurudishwa katika ushirika, tunaweza kufurahia rehema na msamaha wa Yehova. (Luka 15:7) Tunaweza kufanya hivyo mtu huyo awe alidai kuwa na tumaini la kimbinguni na aendelea kufanya hivyo au alikuwa na tumaini la kupata uzima wa milele na aendelea kuwa nalo. Imetupasa sote tuyafikirie sana masomo tunayojifunza kutokana na hili​—kwamba sisi wenyewe tumepaswa kupigana sikuzote na kutokamilika na dhambi, tumepaswa kufikiria ubora wa kuomba msamaha tunapotenda dhambi na umuhimu wa kuvumilia mpaka mwisho ili tuokolewe.​—Mt. 10:22.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki