Maanguko Makubwa Zaidi
“KIBURI hutangulia uangamivu,” yasema mithali ya kale ya Biblia. (Mit. 16:18) Kweli ya maneno hayo imetimia kuhusu hata malaika. Naam, siku hizi viumbe vya kiroho vilivyokuwa na cheo cha kutumainiwa na kupendelewa mbele za Mungu viko katika hali ya kushushwa, navyo ni vibaya sana. Maanguko yavyo yamekuwa makubwa sana yakilinganishwa na ya viumbe vyenye akili vilivyoshushwa.
Sababu ya Maandiko inayozuia wapya wasiwekwe wawe waangalizi katika kundi la Kikristo yaonyesha wazi kwamba mkuu wa mashetani hao aliangushwa na kiburi. Sababu hiyo yasema hivi: “Asije [mtu huyo aliyeongolewa majuzi] akajivuna akaanguka katika hukumu ya Ibilisi.” (1 Tim. 3:6) Bila shaka Shetani hakuwa mpya. Basi, jinsi kulivyo na hatari kubwa zaidi kufanya mtu aliyeongolewa majuzi azidi kuwa mwenye kiburi kwa kumkabidhi daraka kubwa!
Kabla hajaanguka, mtu wa kiroho aliyejifanya mpinzani (Shetani) na mchongezi (Ibilisi) wa Mungu alikuwa na pendeleo la kuwa pale pale mbele za Mpaji-Uzima wake. Alikuwa na nafasi ya kupata kumjua sana, sana, Muumba wake na kumpenda zaidi sana. Alikuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo, kwa maana vyote alivyofurahia alivipokea kwa Mfanyi wake mwenye upendo.
Lakini Shetani aliacha kiburi kimtawale maisha yake. Alitenda sana kama “mfalme wa Tiro.” “Mfalme” huyo au nasaba ya ufalme ya Tiro ilikuwa na mapatano mazuri sana na ufalme wa Israeli, siku za Daudi na mwanawe Sulemani. Lakini baadaye watawala wa Tiro wakawa wasaliti. Jambo hilo laelezwa na wimbo wa maombolezo ulioandikwa katika kitabu cha Ezekieli unaposema hivi: “Wewe wakitia muhuri kipimo, umejaa hekima, na ukamilifu wa uzuri. . . . Ulikuwa mkamilifu katika njia zako tangu siku ile ulipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yako. . . . Moyo wako uliinuka [ulitakabari, NW] kwa sababu ya uzuri wako.”—Eze. 28:12-17.
Kama vile ilivyokuwa habari ya ‘mfalme msaliti wa Tiro,’ Shetani alianza kujifikiria kuwa bora kupita kiasi. Inaelekea alijidhania kuwa bwana ya wanadamu wa kwanza na mwishowe akajidhania kuwa bwana ya taifa lote la kibinadamu. Ili kutimiza makusudi yake, aliacha hali yake ya kuwa mwana safi na mkamilifu wa Mungu, akawa mwongo na mchongezi.
Adui huyo alificha choyo yake ya kujitakia makuu juu ya taifa la kibinadamu kwa kumtokea Hawa akijifanya kuwa mfadhili. Alitumia nyoka akaonyesha kwamba Hawa angepata faida kwa kutomtii Mungu. Badala ya kuzungumza jambo hilo na mumewe kwa unyenyekevu, Hawa akawa mwenye kiburi akajitakia uhuru wake mwenyewe na kuvunja sheria ya Mungu. Baadaye alimshawishi Adamu ajiunge naye kumwasi Yehova Mungu. (Mwa. 3:1-6) Kwa hiyo Adamu na Hawa wakahukumiwa kufa, na hivyo kifo kikaenea kwa wazao wao wote. Kwa kuwa Adamu alikuwa amepoteza uzima mkamilifu wa kibinadamu, asingeweza kupitishia watoto wake uzima wa namna hiyo.—Rum. 5:12.
Kwa kuwa Shetani ndiye aliyeanza mfululizo huo wa matukio, hilo lilimfanya awe mwuaji pia. Yesu Kristo, aliyeona matukio hayo kabla hajawa mwanadamu, angeweza basi kusema hivi juu ya Ibilisi: “Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo.”—Yohana 8:44.
Ingawa Adamu na Hawa walianguka vibaya sana, na hivyo jamaa nzima ya kibinadamu ikaanguka pia, Shetani hakuacha kufanya hila yake. Kiburi chake kingi sana kilimfanya aharibu wana wa Mungu wa kimalaika pia, Wengine wao, walijiacha wawe na tamaa isiyo ya asili kama Shetani, wakaruka kwa makusudi mipaka waliyokuwa wamewekewa na Muumba wao. Waliacha vyeo vyao mbinguni, wakavaa miili ya kibinadamu na kuoa wanawake duniani. Gharika ya siku za Nuhu ilikomesha vibaya sana ndoa hizo, ikalazamisha malaika hao waasi wavue miili waliyokuwa nayo.—Mwa. 6:1-7.
Mwanafunzi Mkristo Yuda aeleza yaliyotukia baada ya hapo: “Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, [Mungu] amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu.” (Yuda 6) Walifukuzwa pamoja na Shetani Ibilisi watoke katika jamaa ya Mungu ya wana waaminifu wakaacha kuwa na vyeo vyao vya kutumainiwa mbinguni. Kwa kuwa wametupwa nje, wamo katika hali ya kushushwa na katika giza, kuwekwa mbali na nuru yote ya kimungu. Wanangojea kuhukumiwa na Mungu nao ‘wanatetemeka’ wakitarajia kuangamizwa.—Yak. 2:19.
Mtume Petro aliwataja malaika hao waasi kuwa “roho waliokaa kifungoni,” kuonyesha kwamba waliingia katika kizuizi cha namna fulani. (1 Pet. 3:19) Kwa kuwa hakuna Maandiko wala kumbukumbu la namna nyingine linaloonyesha waliishi tena duniani wakiwa wanadamu, ni wazi kwamba kizuizi walimoingia kiliwazuia wasiweze tena kuvaa miili ya kibinadamu na kuoa wanawake.
Mashetani hawajapunguza uovu wao wakiwa katika hali yao ya kushushwa. Bali, wameendelea kujishushia heshima kwa kutenda wanadamu ukatili mwingi.
Hilo laonyeshwa vizuri katika kisa cha watu waliopagawa na mashetani siku za huduma ya Yesu ya duniani. Kwa mfano, kulikuwa na mwanamume mmoja aliyekuwa ameingizwa wazimu na mashetani. Alitembea-tembea makaburini akiwa uchi, akilia-lia mchana na usiku na kujikata-kata kwa mawe. Mtu huyo mwenye kupagawa na mashetani, pamoja na mwenzake, walikuwa watu wakali sana hata wengine waliogopa kupita katika eneo walilokaa watu hao. Walijaribu kuwafunga kwa minyororo na pingu, lakini wapi. Ni wazi kwamba mashetani walifurahia sana kumwona mtu huyo akitaabika hivyo.—Mt. 8:28; Marko 5:2-5; Luka 8:27.
Halafu, wakati Yesu alipoamuru mashetani wawaache watu hao wawili, mashetani walimwomba ruhusa waliingie kundi la nguruwe, pengine wakikusudia kujipatia raha isiyo ya asili kwa kutenda wanyama hao ukatili. Mashetani waliliingia kundi hilo la nguruwe karibu 2,000, wakawaua kwa kuwaelekeza katika Bahari ya Galilaya.—Mt. 8:30-32; Marko 5:11-13.
Kweli kisa cha Shetani na mashetani wake chaonyesha sana kwamba kuwa na kiburi kunaleta maanguko makubwa sana. Linakuwa jambo la kushangaza sana tunapofikiria kwamba viumbe hivyo viovu vya kiroho, vyenye kusema uongo, vilikuwa kati ya wana wakamilifu wa Mungu wakati mmoja. Jambo hilo lituonyeshe wazi sisi wanadamu tusioamilika uhitaji wa kuzuia kiburi tusije sisi wenyewe tukaanguka barabara, tuangamie milele.