Mawakili wa Uovu
ELEZO la Biblia kuhusu fungu la roho waovu katika mambo ya mwanadamu lajibu maswali ya msingi juu ya uovu ambayo yasingeweza kujibiwa vingine. Kwa kielelezo, fikiria taarifa hii kutoka katika International Herald Tribune kuhusu vita inayoendelea katika mabara ya Balkan: “Kikundi kimoja cha wachunguzi cha Jumuiya ya Ulaya kimeona kwamba [askari-jeshi] wamenajisi wanawake na wasichana Waislamu kufikia 20,000 . . . ikiwa sehemu ya utaratibu wa sera ya kutisha unaokusudiwa kuwaogofya, kuwavunja moyo, na kuwasukuma waondoke makao yao.”
Insha moja katika gazeti Time ilijaribu kueleza hali kwa njia isiyosadikisha: “Nyakati nyingine, vijana vitani huenda wakanajisi ili kuwapendeza wale wenye umri mkubwa zaidi, maofisa wao, na kujishindia upendeleo kama ule ulio kati ya baba na mwana. Unajisi ni uthibitisho wa kujikabidhi kwa ukatili wa kikosi hicho. Kijana aliye tayari kufanya mambo yenye kuchukiza ametiisha dhamiri yake binafsi ili kujiunga na makusudi ya kikosi yasiyoridhiana. Mtu huthibitisha utii wake kwa kufanya ukatili.”
Lakini kwa nini “makusudi ya kikosi yasiyoridhiana” ni mabaya sana kuliko dhamiri moja-moja za washiriki wacho? Akiwa mtu mmoja-mmoja, kila mtu hutamani kuishi kwa amani pamoja na jirani yake. Kwa hiyo ni kwa nini, katika nyakati za vita, watu hunajisi, hutesa, na kuuana? Sababu kuu ni kwamba kani za kishetani zinafanya kazi.
Kuelewa fungu la roho waovu kwaandaa pia suluhisho kwa lile ambalo wengine huita “tatizo la mwanatheolojia.” Tatizo hilo ni jinsi ya kupatanisha mambo matatu: (1) Mungu ni mwenye nguvu zote; (2) Mungu ni mwenye upendo na ni mwema; na (3) mambo mabaya hutukia. Wengine huona kwamba yawezekana kupatanisha mambo mawili yoyote kati ya hayo, lakini yote matatu hayawezi kupatanishwa kamwe. Neno la Mungu lenyewe latoa jibu, na jibu hilo lahusisha roho wasioonekana, mawakili wa uovu.
Mwasi wa Kwanza
Biblia hutuambia kwamba Mungu mwenyewe ni roho. (Yohana 4:24) Hatimaye alikuwa Muumba wa mamilioni ya viumbe vingine vya kiroho, wana wa kimalaika. Katika njozi, mtumishi wa Mungu Danieli aliona malaika milioni mia moja. Watu wote wa kiroho ambao Yehova aliumba walikuwa waadilifu na walipatana na mapenzi yake.—Danieli 7:10; Waebrania 1:7.
Baadaye, Mungu ‘alipoiweka misingi ya nchi,’ wana hao wa Mungu wa kimalaika ‘waliimba pamoja’ na ‘kupiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:4-7) Lakini mmoja wao alisitawisha tamaa ya kujitwalia ibada iliyokuwa haki ya Muumba. Kwa kuasi dhidi ya Mungu, malaika huyo alijifanya mwenyewe shetani (ikimaanisha “mpingaji”) na ibilisi (ikimaanisha “mchongezi”).—Linganisha Ezekieli 28:13-15.
Akitumia nyoka katika Edeni kuzungumza na mwanamke wa kwanza, Hawa, Shetani alimshawishi asitii amri ya Mungu ya moja kwa moja ya kutokula tunda kutoka mti fulani katika bustani. Baadaye, mume wake alijiunga naye. Hivyo, mume na mke wa kwanza wa kibinadamu walijiunga na malaika huyo katika uasi dhidi ya Yehova.—Mwanzo 2:17; 3:1-6.
Ingawa matukio katika Edeni huenda yakaonekana kuwa somo la wazi la utii, masuala mawili ya maana kuhusiana na adili yalitokezwa huko na Shetani. Kwanza Shetani alibisha kama utawala wa Yehova juu ya viumbe vyake ulitekelezwa kwa uadilifu na kwa faida yao. Labda wanadamu wangeweza kujiongoza wenyewe vema zaidi. Pili, Shetani alitia shaka kama viumbe vyovyote vyenye akili vingebaki vikiwa vyenye uaminifu na uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu wakati ilipoonekana kwamba utii hauleti manufaa za kimwili.a
Uelewevu wa wazi kuhusu masuala hayo yaliyotokezwa katika Edeni, pamoja na ujuzi juu ya sifa za Yehova, watusaidia tuelewe suluhisho la lile “tatizo la mwanatheolojia,” yaani kupatanisha kuwako kwa uovu na sifa za Mungu za nguvu na upendo. Ingawa ni kweli kwamba Yehova ana nguvu isiyo na mpaka naye ndiye tashihishi ya (umbo la) upendo, yeye pia ni mwenye hekima na mwenye haki. Yeye hutumia sifa hizo nne kwa usawaziko mkamilifu. Hivyo, hakutumia nguvu zake zisizoweza kuzuiwa ili kuharibu wale waasi watatu mara iyo hiyo. Hilo lingalikuwa jambo la haki lakini halingalikuwa kwa lazima lenye hekima au lenye upendo. Zaidi ya hayo, yeye hakusamehe na kusahau tu, mwendo ambao huenda wengine wakahisi ungalikuwa chaguo lenye upendo. Kufanya hivyo kusingalikuwa jambo lenye hekima wala la haki.
Wakati ulihitajiwa ili kusuluhisha masuala ambayo Shetani alikuwa ametokeza. Ingechukua wakati kuthibitisha kama wanadamu wangeweza kujitawala wenyewe ifaavyo bila kumtegemea Mungu. Kwa kuruhusu wale waasi watatu waendelee kuishi, Yehova alifanya pia iwezekane kwa viumbe kushiriki katika kuthibitisha dai la Shetani kuwa la uwongo kwa kumtumikia Mungu kwa uaminifu chini ya hali ngumu.b
Yehova alikuwa amewaambia Adamu na Hawa kwa wazi kwamba ikiwa wangekula lile tunda lililokatazwa, wangekufa. Nao walikufa, ingawa Shetani alikuwa amemhakikishia Hawa kwamba yeye asingekufa. Shetani pia yuko chini ya hukumu ya kifo; kwa sasa aendelea kuiongoza vibaya ainakibinadamu. Kwa kweli, Biblia husema hivi: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.”—1 Yohana 5:19; Mwanzo 2:16, 17; 3:4; 5:5.
Malaika Wengine Waasi
Muda mfupi baada ya matukio katika Edeni, malaika wengine walijiunga katika uasi dhidi ya enzi kuu ya Yehova. Biblia husema hivi: “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.” Yaani, malaika hao “wa[li]yaacha makao yao yaliyowahusu [mbinguni]” na kuja duniani, wakajivika miili ya kibinadamu, na kufurahia raha za kingono pamoja na wanawake.—Mwanzo 6:1, 2; Yuda 6.
Simulizi hilo laendelea kwenye Mwanzo 6:4: “Wanefili walikuwako duniani siku zile; tena, baada ya hayo, wana wa Mungu walipoingia kwa binti za wanadamu, wakazaa nao wana; hao ndio waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa.” Wana hao mivyauso waliozaliwa kwa wanawake na ambao baba zao walikuwa malaika walikuwa na nguvu zisizo za kawaida, “watu hodari.” Walikuwa watu wenye jeuri, au Nephi·limʹ, neno la Kiebrania limaanishalo “wale wasababishao wengine waanguke.”
Inastahili kuonwa kwamba matukio hayo yalielezwa baadaye katika hekaya za staarabu za kale. Kwa kielelezo, utenzi mmoja wa Kibabuloni wenye umri wa miaka 4,000 husimulia juu ya utendaji mbalimbali wenye kuzidi uwezo wa kibinadamu wa Gilgameshi, mungu-nusu ambaye “ashiki [yake haikumwachia] bikira mpenzi wake.” Kielelezo kingine, kutoka hekaya ya Kigiriki, ni yule Hercules (au Heracles) mwenye nguvu zinazozidi za kibinadamu. Hercules aliyezaliwa na Alcmene, aliyekuwa binadamu, na mungu Zeus akiwa baba yake, alianza mfululizo wa safari hatari zenye jeuri baada ya kuua mke na watoto wake kwa kichaa cha ghafula. Ingawa hadithi hizo zilipotoshwa sana ziliposimuliwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine, zinapatana na yale ambayo Biblia husema juu ya Wanefili na baba zao waasi wa kimalaika.
Kwa sababu ya uvutano wa malaika waovu na wana wao wenye uwezo uliozidi ule wa kibinadamu, dunia ilijawa na jeuri sana hivi kwamba Yehova aliamua kuharibu ulimwengu kwa furiko kubwa. Wanefili waliangamia pamoja na wanadamu wote wasiomcha Mungu; waokokaji pekee wa kibinadamu walikuwa Noa mwadilifu pamoja na familia yake.—Mwanzo 6:11; 7:23.
Hata hivyo, malaika waovu hawakufa. Badala ya hivyo, walivua miili yao ya kibinadamu wakarudi makao ya kiroho. Kwa sababu ya kutokutii kwao, hawakuruhusiwa warudie familia ya Mungu ya malaika waadilifu; wala hawakuruhusiwa tena wajivike miili ya kibinadamu kama walivyofanya katika siku za Noa. Bado, waliendelea kutumia uvutano wenye uharibifu katika shughuli za ainakibinadamu, chini ya mamlaka ya “mkuu wa pepo,” Shetani Ibilisi.—Mathayo 9:34; 2 Petro 2:4; Yuda 6.
Maadui wa Ainabinadamu
Shetani na roho waovu wamekuwa wauaji wa kimakusudi na wenye ukatili sikuzote. Kwa kutumia njia mbalimbali, Shetani aliondolea mbali mifugo ya Ayubu na kuua wengi wa watumishi wake. Halafu, aliwaua watoto kumi wa Ayubu kwa kusababisha “upepo wenye nguvu” ubomoe nyumba walimokuwa ndani. Baadaye, Shetani alimpiga Ayubu kwa “majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.”—Ayubu 1:7-19; 2:3, 7.
Roho waovu huonyesha nia iyo hiyo yenye uovu. Katika siku za Yesu, waliwanyang’anya watu uwezo wao wa kusema na wa kuona. Walimfanya mtu mmoja ajikate-kate kwa mawe. Walimbwaga chini mvulana mmoja na ‘kumtia kifafa.’—Luka 9:42; Mathayo 9:32, 33; 12:22; Marko 5:5.
Ripoti nyingi kutoka kotekote ulimwenguni huonyesha kwamba Shetani na roho waovu ni wenye nia mbaya vivyo hivyo. Wao huwapiga watu fulani kwa maradhi. Wao huwasumbua wengine kwa kuwanyang’anya usingizi au kwa kuwapa ndoto zenye kuogopesha au kwa kuwatenda vibaya kingono. Wamewasukuma wengine bado hadi hatua ya kuwa wenye kichaa, kuua kimakusudi, au kujiua wenyewe.
Watavumiliwa kwa Muda Mrefu Kadiri Gani?
Shetani na roho waovu wake hawatavumiliwa milele. Yehova amewaruhusu waendelee kuwako hadi siku zetu kwa sababu nzuri, lakini sasa wakati wao ni mfupi. Mapema katika karne hii, hatua kubwa ilichukuliwa ya kuzuia kizio chao cha utendaji. Kitabu cha Ufunuo chaeleza hivi: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli [Yesu Kristo aliyefufuliwa] na malaika zake wakapigana na yule joka [Shetani], yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.
Tokeo lilikuwa nini? Simulizi laendelea hivi: “Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo.” Malaika waadilifu wangeweza kushangilia kwa sababu Shetani na roho waovu wake hawakuwako mbinguni tena. Lakini namna gani watu duniani? Biblia husema hivi: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufunuo 12:12.
Wakiwa na hasira Shetani na wale walio chini yake wana nia ya kusababisha ole mwingi iwezekanavyo kabla ya mwisho wao ulio karibu sana. Katika karne hii kumekuwa na vita vya ulimwengu viwili na vita vidogo zaidi 150 tangu mwisho wa vita ya ulimwengu ya pili. Msamiati wetu umeongezewa mafungu ya maneno yanayoonyesha jeuri ya kizazi hiki: “vita vya vijidudu (ambavyo silaha zinazotumiwa zinaeneza vijidudu vinavyosababisha maradhi mabaya sana),” “yale Maangamizo,” “viwanja vya kuua,” “kambi za unajisi” “wauaji wa mfululizo, na “lile bomu (la atomu).” Habari zimejaa masimulizi kuhusu dawa za kulevya, uuaji wa kimakusudi, kulipuka kwa mabomu, watu wenye kichaa wanaokula miili ya kibinadamu, michinjo ya ovyoovyo, njaa kali, na mateso.
Habari njema ni kwamba mambo hayo ni ya muda tu. Katika wakati ujao ulio karibu, Mungu atatenda tena dhidi ya Shetani na mashetani wake. Akifafanua njozi kutoka kwa Mungu, mtume Yohana alisema hivi: “Na mimi nikaona malaika mmoja akija chini kutoka katika mbingu mwenye ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa katika mkono wake. Na yeye akakamata drakoni, nyoka wa awali kabisa, ambaye ndiye Ibilisi na Shetani, na akamboba yeye kwa miaka elfu moja. Na yeye alimvurumisha ndani ya abiso na akaifunga na akatia kalafati juu yake, ili asipate kuongoza vibaya mataifa tena mpaka miaka elfu ilipokuwa imekwisha.”—Ufunuo 20:1-3, New World Translation.
Baadaye, Ibilisi na roho waovu wake ‘watafunguliwa muda mchache,’ kisha wataharibiwa milele. (Ufunuo 20:3, 10, NW) Huo utakuwa wakati mzuri ajabu kama nini! Shetani na roho waovu wake wakiwa wameondolewa mbali milele, Yehova atakuwa “yote katika wote.” Na kila mtu ‘atajifurahisha kwa wingi wa amani.’—1 Wakorintho 15:28; Zaburi 37:11.
[Maelezo ya Chini]
a Hilo lilieleweshwa wazi baadaye wakati Shetani aliposema hivi juu ya Ayubu mtumishi wa Mungu: “Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake. Lakini sasa nyosha mkono wako, uuguse mfupa wake na nyama yake, naye atakukufuru mbele za uso wako.”—Ayubu 2:4, 5.
b Kwa mazungumzo zaidi kuhusu kwa nini Mungu huruhusu uovu, ona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Je! mwanadamu pekee ndiye husababisha mambo haya, au kani mbaya, isiyoonekana hushiriki lawama?
[Hisani]
Visima vya mafuta vikiwaka moto katika Kuwait, 1991: Chamussy/Sipa Press
[Picha katika ukurasa wa 7]
Utakuwa wakati mzuri ajabu kama nini wakati ambapo roho waovu hawataisumbua ainabinadamu tena!