Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 12/15 kur. 568-572
  • Kuonyesha Imani Tushambuliwapo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuonyesha Imani Tushambuliwapo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IMANI YAHITAJIWA WAKATI NJIA YA KUTOKEA HAIFAHAMIKI
  • HAKUNA KUSHINDWA
  • UWE MWAMINIFU KATIKA MAMBO MADOGO SASA
  • Ubora Uliojaribiwa wa Imani Waleta Uvumilivu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • “Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Je, Kweli Una Imani Katika Habari Njema?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Onyesha Imani Yako Katika Ahadi za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 12/15 kur. 568-572

Kuonyesha Imani Tushambuliwapo

“Jaribu Halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”​—1 Kor. 10:13.

1. Twaweza kujiuliza maulizo gani juu ya imani?

WEWE una imani kadiri gani? Je! unayo ya kutosha kukustahimilisha mambo yawapo magumu sana? Je! ungeweza kuendelea kuwa imara na bado umtumaini Yehova, huku ukinyimwa chakula ukipendacho zaidi, mavazi upendayo, nyumba uipendayo sana? Je! ungeweza kuvumilia kutiwa gerezani, kuharibikiwa na afya, na hata kupoteza maisha yako na bado usiache kuziamini ahadi za Mungu kwa wakati ujao? “Si wote walio na imani” hiyo. Bila shaka, mashahidi waaminifu wa Yehova wa Kikristo wanaona kama mitume waliomwambia Yesu hivi: “Tuongezee imani.”​—2 The. 3:2; Luka 17:5.

2. Twaweza kuwa na hakika gani juu ya upinzani wa Shetani?

2 Huenda wengine wakawaza, ‘Mimi sitapatwa na hilo kamwe.’ Yesu alitangulia kuonya Wakristo wa kweli hivi: “Lakini, kabla hayo yote hayajatokea, watawakamata na kuwaudhi; watawapeleka mbele ya masinagogi, na kuwatia magerezani, mkipelekwa mbele ya wafalme na maliwali kwa ajili ya jina langu. Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu. Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.” (Luka 21:12, 16, 17) Mitume walioyasikia maneno hayo walijua kwamba kama vile ilivyokuwa hakika jua lingechomoza kesho yake, ndivyo ilivyokuwa hakika unabii huu ungetimizwa juu yao na juu ya wafuasi wote wa Kristo. Bila shaka, Yesu hakusema kwamba kila Mkristo angepatwa na kila namna ya mateso. Mambo hayo yangepata kikundi cha watu wa Mungu. Lakini bila kujali njia atakayotumia kushambulia, twaweza kuwa na hakika kwamba Shetani atahakikisha “wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu watateswa.”​—2 Tim. 3:12.

3. Kwa sababu gani imani bado yahitajiwa leo?

3 Leo si maneno ya unabii tu tunayoona; tunalo kumbukumbu la kweli linaloonyesha mateso yaliyowapata mashahidi wa Kikristo wa Yehova tangu karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida mpaka mwaka huu wa 1976. Wajifunzao historia ya Kirumi wanafahamu sana kumbukumbu la kuogofya sana linaloonyesha Wakristo walikuwa wakiraruliwa na wanyama-mwitu huku maelfu ya raia za Rumi wenye hamu ya kuona damu ikitiririka wakishangilia katika vibanda vya watazamaji. Katika kame hii ya 20, watu wa Mungu wanakazwa bado. Hata leo kazi ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova imepigwa marufuku katika nchi kadha. Wakristo wengi wa kweli wamo gerezani, na wengine wamepoteza maisha zao. Kwa namna nyingi watu wote wa Mungu wanakazwa na nguvu fulani ili wavunje ukamilifu wao. Twahitaji imani ndio tusimame imara.

4. Ni kwa njia gani watu wa Mungu wa nyakati za kisasa wameonyesha imani kuu?

4 Hakuna haja ya kutia shaka kwamba watu wa Mungu siku zetu hawana imani ya kupambana na jaribu. Je! wanaume na wanawake wachache hawakutumia imani mwishoni mwa karne ya kumi na tisa ndipo wakaweza kujitenga na mawazo ya mapokeo ya kidini na kupinga hadharani mafundisho ya uongo yaliyokuwa yamefuatwa karne nyingi yakionekana kama ya kweli? Na je! maelfu machache kati yao hawakupaswa kuwa na imani ndipo wakaweza kuitikia mwito uliotolewa katika Kusanyiko la Cedar Point mwaka wa 1922: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake”? Hakuna mtu wakati huo angeweza kujua kungekuwa na maongezeko makubwa ya mamilioni ya watu wanaoshirikiana na tengenezo la Mungu leo. Na wakati wa miaka ya Vita ya Ulimwengu ya Pili utukuzo wa taifa ulipokuwa umeenea sana, wakati ambapo mtu asiyeunga siasa mkono alionwa kuwa mchukia wanadamu, ni akina nani walioshikamana kwa uaminifu na Neno la Mungu wasiwemo siasani? Ni mashahidi wa Yehova wa Kikristo! Tangu huko nyuma walipokuwa wakianza kidogo kidogo karne ya kwanza mpaka historia yao ya kisasa wao wamekuwa ‘wakienenda kwa imani, si kwa kuona.’ (2 Kor. 5:7) Imani iliwaaminisha yanayosemwa na Neno la Mungu, wakati kila mtu mwingineyo alipodhihaki ujumbe wake. Imani hiyo ya waaminifu hao imethawabishwa. Matumaini yao hakika hayakuwa ya bure, na mamilioni ya watu leo wanatambua hivyo.

5. Ni nini litakalotukia wakati ujao litakalotuhitaji tuwe na imani?

5 Lakini wakati ujao bado kutakuwa na matatizo yatakayofanya imani ihitajiwe ili Mashahidi wa Yehova wawe washindi watakaposhambuliwa na Shetani. Leo tu karibu sana na uharibifu wa taratibu hii ya mambo. Kwa sasa haifahamiki ni kwa kadiri gani Yehova ataruhusu adui wajaribu kuvunja imani ya watu Wake. Wala haifahamiki njia yenyewe atakayotumia kutuokoa sisi mmoja mmoja.​—⁠Mt. 24; Marko 13; Luka 21.

IMANI YAHITAJIWA WAKATI NJIA YA KUTOKEA HAIFAHAMIKI

6. Huenda hali gani zikatokea kujaribu imani yetu?

6 Huu “wakati wa mwisho” uelekeapo haraka kwenye upeo wake, huenda watu wa Mungu wakatiwa katika hali ambamo njia ya kutokea haifahamiki. Kwa kweli, matukio ya ghafula huenda yakatokea maishani mwetu hata kwa maoni ya kibinadamu ikaonekana hatuwezi kuokoka. Wengine leo wanahangaikia sana hali yao itakavyokuwa mwezi ujao na mwaka ujao, lakini huenda mambo yakachacha sana hata ikawa vigumu kujua kama tutapata chakula, mavazi na mahali pa kukaa, au kama tutakuwa huru na hai kesho. Tutafanyaje itakapoelekea kuwa hakuna njia ya kutokea? Tutategemea nani atuonyeshe njia? Huenda imani yetu ikajaribiwa kikweli.

7. Paulo alijifunza “siri” gani iliyomtia nguvu?

7 Paulo aliandikia kundi la waamini wenzake barua akiwa katika gereza la Kirumi Filipi. Katika barua hiyo anaeleza “siri” aliyojifunza kutokana na miaka 25 ya kuwa Mkristo. Alisema: “Si kwamba nasema habari ya kuwa na shida, kwa maana mimi nimejifunza, katika hali zo zote nilimo, kuridhika. Najua kweli jinsi ya kupungukiwa na vifaa, najua kweli jinsi ya kuwa na wingi. Katika kila kitu na katika hali zote mimi nimejifunza siri ya jinsi ya kuwa na shibe na jinsi ya kuwa na njaa pia, jinsi ya kuwa na wingi na jinsi ya kuwa na shida pia. Kwa mambo yote ninakuwa na uwezo kwa sababu yake anitiaye nguvu.”​—⁠Flp. 4:11-13, NW.

8. Ni kwa kupatwa na mambo gani Paulo alijifunza masomo yenye faida?

8 Wengi wa watu wa Yehova hawajaona bado jinsi Yeye anavyowaruzuku wanapokuwa na shida. Maisha ya mtume Paulo yatufahamisha siri hiyo. Kwa mfano, soma Wakorintho wa Pili 4:8-11 ambapo mtume asema huenda tukaonewa, tukatatanishwa, tukateswa na kutupwa chini, lakini “hatuachwi . . . hatuangamizwi” kamwe. Soma pia Wakorintho wa Pili 11:24-27: “Kwa Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi; kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; katika kusafiri mara nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang’anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi.” Kwa hakika, huyu alikuwa mwanamume aliyekuwa na sababu za kutosha kumfanya ashangae atakavyoweza kuwa hai kesho yake. Lakini alijifunza masomo katika maono yake ya Kikristo ambayo kwayo sisi pia twaweza kufaidi.

9. Sisi twawezaje kujifunza “siri” ile ile aliyojifunza Paulo?

9 Mtu alegeaye mambo yachachapo au njia ya kutokea isipofahamika huenda akakosa kujionea mwenyewe jinsi hasa Mungu hutia watu nguvu na kuwaruzuku wakati wa shida na kuwaonyesha njia ya kutokea katika hali yenye kuonekana bila matumaini. Kawaida ya wanadamu ni kutia mashaka tusipoona jambo lenyewe litakalotukia. Hapa ndipo imani yahusika. Imani ni kusadiki sana sana hivi kwamba katika akili ya mtu mwenye imani kitu kisichoonwa na milango ya maarifa ya mwanadamu kinakuwa kimekwisha kutokea. Yeye huwa na uhakika kamili, na uhakika huo ndiyo imani yake. Paulo alieleza maana ya imani kwa njia hii: “Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.”​—⁠Ebr. 11:1.

10. (a) Waisraeli walipatwa na kipingamizi gani mwaka wa 1473 K.W.K.? (b) Hata hivyo Mungu aliwaamuru wafanye nini?

10 Mfano mwema wa vile Yehova Mungu hutazamia imani yetu ifanye kazi wapatikana katika habari inayohusu kuingia kwa Waisraeli katika Nchi ya Ahadi, kama ilivyoandikwa katika Yoshua sura 3 na 4. Ni masika ya mwaka wa 1473 K.W.K. Waisraeli wamepiga kambi upande wa mashariki wa Mto Yordani kaskazini ya karibu ya Bahari ya Chumvi. Kwa miaka 40 wamekuwa wakitanga-tanga jangwani na sasa mwishowe ni wakati wa Mungu kwao waingie na kuteka kutoka kwa adui zao nchi iliyo mali yao kwa haki. Lakini wanaume, wanawake na watoto karibu milioni tatu pamoja na wanyama na vifaa, watavukaje Yordani wakati theluji yenye kuyeyuka na mvua ya masika ifanyapo Yordani uwe bubujiko kuu la maji? Hata hivyo agizo la Yehova ni kwamba wasonge mbele moja kwa moja waingie mtoni wakiongozwa na makuhani. Amri yatolewa pamoja na uhakikisho huu: “Itakuwa, wakati nyayo za makuhani walichukuao sanduku la [Yehova], Bwana wa dunia yote, zitakaposimama katika maji ya Yordani, hayo maji ya Yordani yatatindika, maji yale yashukayo kutoka juu; nayo yatasimama kama chuguu.”​—⁠Yos. 3:13.

11. (a) Waisraeli wangaliweza kuwa na maoni gani? (b) Walionyesha imani kwa njia gani?

11 Waisraeli watafanyaje? Je! watakuwa na maoni haya: ‘Haiwezekani kulivuka bubujiko lile la maji yenye mawimbi kwa miguu sasa. Tutangoja juma kadha mpaka maji yashuke. Hatutaki kuona baadhi ya hema, wanyama wala watoto wetu wakikumbwa na maji wanapojaribu kuvuka katika hali ‘zisizowezekana.’ Kwa sasa, Yehova akifungua kijia ndani ya maji kama alivyofanya Bahari ya Shamu, ndipo tutafurahi kuvuka’? Na tusome yaliyotukia: “Hata ikawa, hao watu walipotoka katika hema zao, ili kuvuka Yordani, makuhani waliolichukua hilo sanduku walipofika Yordani, na nyayo za makuhani waliolichukua sanduku zilipotiwa katika maji ya ukingoni, (maana Yordani hujaa hata kingo zake na kufurika wakati wote wa mavuno,) ndipo hayo maji yaliyoshuka kutoka juu yakasimama, yakainuka, yakawa chuguu, mbali sana, huko Adamu, mji ule ulio karibu na Sarethani, na maji yale yaliyotelemkia bahari ya Araba, yaani Bahari ya Chumvi, yakatindika kabisa; watu wakavuka kukabili Yeriko. Na hao makuhani waliolichukua sanduku la agano la [Yehova] wakasimama imara mahali pakavu katikati ya Yordani; Israeli wote wakavuka katika nchi kavu, hata taifa lile lote likaisha kuvuka Yordani.”​—⁠Yos. 3:14-17.

12. Mfano wa Waisraeli watufundisha somo gani?

12 Lo! jinsi huo ulivyokuwa wonyesho mzuri wa imani na somo zuri pia kwa watu wote wa Mungu kwa maana huenda wakapatwa na mashaka wakati ujao! Kama Yehova angetueleza mambo yote atakayofanya na jinsi atakavyoyafanya, kungekuwa na uhitaji gani wa kuwa na imani? Imani maana yake ni kuelekea upande anaoongoza Mungu hata ikiwa inaonekana haiwezekani kabisa kwa maoni ya kibinadamu. Yehova Mungu ataka kuona kama tuna imani ya kutosha ‘kukanyaga maji kwa miguu yetu.’ Halafu, tukitenda kwa imani, tutaona jinsi awezavyo kutupitisha. Basi si ajabu Biblia inataja “ubora uliojaribiwa wa imani yenu.”​—⁠Yak. 1:3; 1 Pet. 1:7, NW.

HAKUNA KUSHINDWA

13. Huenda tukajiuliza maulizo gani juu ya majaribu?

13 Wengine wanashangaa wakisema hivi: ‘Mimi nina hakika kwamba Yehova atakuwa mwaminifu na kusaidia watu wake, lakini nyakati nyingine najihangaikia na kufikiria nitafanyaje nipatwapo na majaribu na mikazo fulani. Je! nitakuwa na nguvu za kuvumilia? Je! uko upande wangu ulio dhaifu unaoweza kutumiwa kunifanya nishindwe?’ Huenda wengine wakawaza, ‘Mimi mwenyewe naweza kuvumilia cho chote, lakini mimi ni mzazi na siwezi kuvumilia kuona watoto wangu wakipatwa na jambo lo lote. Sidhani naweza kuvumilia wakitaka kuumizwa.’

14. (a) Je! tutapatwa na majaribu ambayo hayakupata watu wa Mungu zamani? Twajuaje? (b) Biblia inatoa uhakikisho gani juu ya majaribu?

14 Tukiwa na maulizo hayo akilini twapata jibu lenye kututia moyo sana kutoka kwa mtume Paulo! Yeye alirudia kutaja mambo yaliyoangusha Waisraeli wengi alipokuwa akiandikia kundi la waamini wenzake. Katika Wakorintho wa Kwanza 10:7-10 twasoma hivi: “Wala msiwe waabudu sanamu, kama wengine wao walivyokuwa; kama ilivyoandikwa, Watu waliketi kula na kunywa, kisha wakasimama wacheze. Wala tusifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu. Wala tusimjaribu Bwana, kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka. Wala msinung’unike, kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.” Alisema mambo hayo yalitukia kama mfano kwa Wakristo, na akaonya juu ya upumbavu wa kuwaza kwamba ‘hayo hayawezi kunipata mimi.’ Halafu akasema maneno ambayo yalipata kuwa kati ya mawazo yenye kutia moyo na nguvu zaidi ya yote katika Biblia. Alisema: “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”​—1 Kor. 10:13.

15. (a) Je! ukamilifu wa Kikristo unaweza kuvunjika? (b) Yehova hufanyaje “mlango wa kutokea”?

15 Je! wajua mstari huo wamaanisha nini kwa Wakristo waaminifu wanaojaribu kufanya mapenzi ya Mungu kwa unyofu? Ikiwa wewe u mtu wa namna hiyo kwa habari ya ukamilifu wako kwa Mungu, huna upande dhaifu unapoweza kushindiwa. Hakuna mamlaka, nguvu, hila, wala ‘silaha ya siri’ inayoonekana au isiyoonekana inayoweza kutumiwa ikulemee kwa uhakika wa kwamba utavunja ukamilifu wako kwa Mungu. Huna upande dhaifu ambao adui zako wanaweza kutumia wakushinde. Ukijitahidi kadiri mwili wako wa kibinadamu uwezavyo ili uwe mwaminifu kwa Mungu, unaweza kujua kwa hakika kwamba, Yehova Mungu atakuja kukusaidia na “atafanya mlango wa kutokea” unapodhani nguvu zako mwenyewe zimekuishia usiweze kuendelea kuvumilia. Hiyo haionyeshi kwamba bila shaka ataondoa kishawishi nyakati zote. Bali, kusudi la kujiingiza kwake ni “ili mweze kustahimili.”

16. Imani inahusikaje katika uvumilivu? Toa mfano.

16 Ufahamu huu wa Maandiko unaofaa utatusaidia tuwe na maoni yanayofaa juu ya mambo hata yawe magumu namna gani. Kwa mfano, wazazi ambao huenda wakanyang’anywa mtoto wao na watesi wataweza kuvumilia, lakini kwa msaada wa Mungu tu. Watajua wamejitahidi walivyoweza na kwamba, Yehova akiruhusu jambo hilo litokee, wanaweza kuliacha mikononi mwake wakiwa na matumaini hakika. Ni nani mwenye uwezo zaidi wa kuangalia mtoto wako? Ni wewe au ni Yehova na jeshi lake la malaika? Huenda hali ikaelekea kuwa bila matumaini kabisa, na huenda tusione wakati uo huo jinsi Yehova atakavyofanya mambo, lakini hapa ndipo imani na matumaini kama ya mtoto yapaswa kuonyeshwa katika Yehova. Hatuwezi kuvumilia bila kufanya hivyo.​—⁠Ebr. 11:6.

UWE MWAMINIFU KATIKA MAMBO MADOGO SASA

17. Kuwa na hakika katika kanuni gani kutatusaidia kukabili majaribu yaliyoko mbele?

17 Watu wa Mungu hawana hakika ni majaribu gani yatakayowapata wakati ujao, lakini hata yawe ya namna gani, sisi tuna hakika kwamba kanuni aliyotaja Yesu bado itakuwa ya kweli: “Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia.”​—⁠Luka 16:10.

18. Kuwa waaminifu “katika lililo dogo sana” sasa kutatusaidiaje siku zijazo?

18 Kwa kuwa ndivyo ilivyo, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanajaribu kila siku kuyashinda majaribu ya imani yanayowapata. Yako mambo mengi yanayoweza kuzuka yakawa kipingamizi katika maisha yetu ya kila siku na katika utumishi wetu kwa Yehova, lakini tukiyashinda majaribu hayo katika mambo mepesi ya Ukristo, tutatiwa nguvu tukutane na jambo lo lote linaloweza kutokea wakati ujao. Basi mwacheni Ibilisi afanye mabaya yote yake. Mwacheni aendeshe mipango yo yote anayofikiria. Si mipango mipya hata kidogo. Imepata kushindwa na itashindwa na wenye kuonyesha imani washambuliwapo na Shetani.​—⁠Kutoka The Watchtower, Aug. 1, 1976.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki