Yehova, Msaidiaji Asiye na Kifani
“Msaada wangu utatoka wapi? Msaada wangu u katika [Yehova], aliyezifanya mbingu na nchi.”—Zab. 121:1, 2.
1. Ni nani aliye msaidiaji mkuu zaidi, na kwa sababu gani?
MSAIDIAJI mkuu zaidi tunayeweza kupata ni Muumba, Yehova Mungu. Vitu vyote vilivyo hai duniani vinaendelea kufaidika kutokana na mfululizo wa matukio ya asili aliyoanzisha vizazi vingi vilivyopita, ambayo ni ya lazima kwa uhai. Kama mwanadamu asingalikuwa na pupa na kama asingalitumia vibaya mali za asili za dunia, sayari hii ingeweza kuchukua kwa starehe idadi kubwa zaidi ya wanadamu bila kuumiza mimea, wanyama na wadudu. Kwa kufaa mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu aliweza kusema juu ya Yehova Mungu hivi: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zab. 145:16.
2. Kwa kawaida Yehova ametendeaje wanadamu wasio na shukrani?
2 Ni mara chache sana Yehova Mungu ametumia uwezo wake kunyima waliotenda kinyume cha mapenzi yake mwanga wa jua na mvua. (Kut. 10:21; Amosi 4:7) Kwa ujumla, hata watu wasio na shukrani wamefaidika kutokana na misaada yake tele. Yesu Kristo alikazia uhakika huo, akisema: “Huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”—Mt. 5:45.
3. Watumishi wa Mungu wanawezaje kutiwa moyo na jinsi Yehova ametendea wanadamu kwa ujumla?
3 Ikiwa Mwenye Nguvu Zote huonyesha fadhili hizo hata kwa wanadamu wasio na shukrani, twaweza kuwa na hakika sana kwamba hataacha kamwe wale wanaompenda sana sana! Yeye ni ‘mpenda haki na hukumu.’ (Zab. 33:5) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba hataachilia kamwe mahitaji ya watu wake bila kuyaangalia wala hatakosa kujibu vilio vyao vya kuomba msaada. Mtumishi mwaminifu wa Mungu, Daudi, alisema hivi: “[Yehova] yu karibu na wote wamwitao, wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.”—Zab. 145:18, 19.
UWEZO WA KUSAIDIA USIO NA KIFANI
4. Kama inavyoonekana wazi katika Zaburi 148:2-6, uwezo wa Yehova ni wa kadiri gani?
4 Hakuna linaloweza kuzuia Yehova Mungu asisaidie watu wake. Yeye ana uwezo wa kusaidia chini ya hali zote. Uwezo wake ni mwingi sana hata unaweza kufanya ulimwengu wote (mbingu na dunia na vyote vilivyomo) uendelee kuwako milele. Hiyo yaonekana wazi katika Zaburi 148:2-6, tunapoambiwa kwamba Yehova Mungu hufanya jua, mwezi na nyota ‘zithibitike hata milele na milele.’
5. Yehova ana uwezo gani juu ya nguvu za asili?
5 Naam, Yehova huongoza nguvu za asili ambazo ni za ajabu sana na aweza kuzitumia kutimiza mapenzi yake. Akimweleza hilo mtumishi wake Ayubu mwenye kushikamana naye, Mungu alisema: “Je! umeziingia ghala za theluji, au umeziona ghala za mvua ya mawe, nilizoziweka akiba kwa wakati wa misiba, kwa siku ya mapigano na vita?” (Ayubu 38:22, 23) Yehova aweza hata kuleta na kuzuia matetemeko ya ardhi, kuamuru umeme na kukausha bahari na mito kwa kutumia roho yake, akikusudia.—1 Sam. 14:15; 2 Sam. 22:15; Zab. 66:6; 74:15.
6. Roho ya Mungu inawezaje kusaidia Wakristo wa kweli wakiwa na shida?
6 Roho takatifu au nguvu ya utendaji ni kama chombo chenye uwezo mwingi anachotumia Yehova sikuzote. Wakati mmoja wa watumishi wake anapokabiliwa na jaribu, Mwenye Nguvu Zote aweza kutumia roho yake kukumbusha mtu huyo kanuni za Maandiko na kumsaidia aone jinsi anavyoweza kuzitumia katika hali yake. (Yohana 14:26) Kwa njia hiyo anatiwa nguvu avumilie na kuendeleza mwenendo mwema. Kwa kutumia roho yake, Yehova Mungu aweza kuchochea mioyo na akili za watumishi wake watimize mahitaji ya waamini wenzao, wawasaidie. (Marko 10:29, 30) Kwa kutumia roho yake, Yehova aweza kuongoza hata watawala wafanye anayotaka, mara kwa mara. Ni kama vile Mithali 21:1 isemavyo: “Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa [Yehova]; kama mifereji ya maji huugeuza po pote apendapo.”
7. Kulingana na Zaburi 34:7, Yehova aweza kutumia nani asaidie watu wake?
7 Aliye Juu Zaidi ni mwenye amri pia juu ya mamilioni ya malaika wenye nguvu. (Dan. 7:10) Katika Zaburi 34:7 inaonyeshwa kwamba yeye huwatumia kusaidia watumishi wake walio duniani, na hapo twasoma hivi: “Malaika wa [Yehova] hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.”
KUMBUKUMBU LA AJABU
8. Kumbukumbu la Biblia linaloonyesha matendo ya Yehova ya kuokoa lawezaje kutusaidia?
8 Yehova Mungu ametoa kumbukumbu lenye kutegemeka linalohusu mengi ya matendo yake ya kuokoa, ili awape watumishi wake msingi imara wa kuamini uwezo wake usio na kifani wa kuwa Msaidiaji. Kumbukumbu hilo, lililo katika Biblia, linaweza kutusaidia kama vile njozi ya mwujiza ilivyosaidia mtumishi wa nabii Mwebrania Elisha. Ilikuwa hivi: Jeshi lenye nguvu la Shamu lilizingira Dothani, mji wa Kiisraeli, likitaka sana kumkamata nabii Elisha. Mtumishi wa Elisha alijawa na woga akapaza sauti akisema: “Ole wetu! bwana wangu, tufanyeje?” “Usiogope,” Elisha akajibu, “maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” Kisha “Elisha akaomba, akasema, Ee [Yehova], nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona. [Yehova] akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona; na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote.” (2 Fal. 6:15-17) Njozi hiyo ya mwujiza haikuwa ya uongo. Yehova Mungu alijitia ndani, akapiga jeshi la Shamu kwa namna ya upofu wa muda na kwa njia hiyo akachafua mipango yao ya kumteka Elisha.—2 Fal. 6:18-23.
9. Yehova alitumiaje nguvu za asili kwa ajili ya Waisraeli wakati wa Baraka?
9 Masimulizi mengi yenye kutia imani nguvu ya vile Yehova alikomboa watu wake yanasisimua sana. Kisa kimoja cha ukombozi huo wa kusifika sana, unaohusu kutumiwa kwa nguvu za asili, kilitukia wakati Waisraeli walipokuwa wakionewa na Mfalme Yabini Mkanaani. Yehova Mungu aliinua Baraka awakomboe Waisraeli. Baraka akakusanya jeshi la wanaume elfu kumi wakajipanga juu ya Mlima Tabori. Mara hiyo mkuu wa jeshi la Yabini, Sisera, akashuka uwandani ambamo mto Kishoni huenda kasi, akiwa na jeshi lenye nguvu zaidi la askari wenye vifaa vingi na magari 900 ya vita. Halafu, Yehova Mungu akaja kuokoa Baraka na watu wake. Yehova akaleta gharika ya mvua nyingi sana ikakwamisha jeshi la Sisera. Maji ya mto uliofurika yakafanyiza matope. Farasi na magari ya vita wakazama matopeni. Askari za Sisera wakawakimbia watu wa Baraka kwa hofu. “Hilo jeshi lote la Sisera likaanguka kwa makali ya upanga; hakusalia hata mtu mmoja.” Mto Kishoni wenye kufurika ukaongeza vijito vyake, ukafagilia mbali maiti zao. Naye mkuu wa jeshi, Sisera, akakimbia kwa miguu akauawa kwa njia ya aibu na mwanamke, Yaeli mke wa Heberi Mkeni.—Amu. 4:12-21; 5:20, 21.
10. Tuna mifano gani katika Maandiko kuonyesha Yehova alitumia malaika asaidie Waisraeli wa kale?
10 Ziko nyakati ambazo malaika walitumiwa sana katika matendo makuu ya Mwenye Nguvu Zote. “Kundi la malaika” lilishiriki kuleta mapigo yenye uharibifu juu ya Misri wakati Farao alipokataa kuwafungua Waisraeli wenye kutumikishwa. (Zab. 78:43-51) Karne nyingi baadaye, jeshi la Ashuru likiongozwa na Senakeribu lilitisha kuuteka Yerusalemu, mji mkuu wa ufalme wa Yuda. Kwa kuwa Mfalme Hezekia mwaminifu ndiye aliyekuwa katika kiti cha ufalme, Yehova Mungu hakuruhusu hilo litukie. Kwa usiku mmoja, malaika wa Yehova aliangusha askari 185,000 wa jeshi la Ashuru—“mashujaa wote, na majemadari, na maakida.” (2 Fal. 19:35; 2 Nya. 32:21) Baada ya kupoteza sehemu ya jeshi lake iliyo ya maana zaidi, Senakeribu alilazimika kuacha mipango yake ya kuuzingira Yerusalemu.
11. Malaika wanapendezwaje na washiriki wa kundi la Kikristo?
11 Je! malaika za Yehova wenye nguvu nyingi bado wana nia na hamu ya kutumikia kwa ajili ya watu wake walio duniani? Kabisa! Wakati Yesu alipokuwa akionya wanafunzi wake juu ya uzito wa kukwaza wengine, alikazia vile malaika wanavyohangaikia jambo hilo: “Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni.” (Mt. 18:10) Tusidhani maneno ya Yesu yana maana ya kwamba bila shaka kila Mkristo aliyejitoa ana malaika wa pekee aliyepewa mgawo wa kumlinda. Lakini inaelekea kuwa kwamba malaika wanaangalia waone Wakristo wa kweli kwa ujumla wana hali njema kiroho Hiyo inahakikishwa na ulizo lililo katika Waebrania 1:14: “Je! hao wote si roho watumikao [hadharani], wakitumwa kuwahudumu wale watakaourithi wokovu?” Lo! twaweza kupata msaada kweli kweli kupitia kwa malaika!
12. Kisa cha Yesu Kristo kinaonyeshaje msaada wa ajabu unaopatikana kupitia kwa roho ya Mungu?
12 Kisa cha Yesu Kristo kinaonyesha vizuri msaada wa ajabu ambao Yehova hutoa kupitia kwa roho yake. Mwana wa Mungu alikuwa na madaraka mazito sana. Alijua kwamba Baba yake alimtumaini kabisa na hata alikuwa ametabiri kwamba angeendelea kuwa mkamilifu. Hata hivyo, Yesu alipaswa kutumia akili yake ya uhuru wa hiari. Kama angalishindwa kwa njia yo yote angalikufa milele, na hiyo ingalitia shaka juu ya ukweli wa Baba yake na ingaliharibia wanadamu wasiokamilika nafasi ya kukombolewa na dhambi na mauti. Yesu alihitaji kweli kweli uwezo wenye kutia nguvu wa roho ya Baba yake. Biblia yasema kwamba, kwa kuwa alijua mambo aliyotakiwa kufanya, Kristo “alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.” (Ebr. 5:7) Uhakika wa kwamba Yesu aliendeleza ukamilifu wake mpaka kufa wahakikisha kwamba Baba yake alijibu vilio vyake vya kuomba msaada, akamtia Mwanawe nguvu kwa kutumia roho Yake.
13. Tunatakiwa tufanye nini ndipo tusaidiwe na roho ya Mungu?
13 Wakati wanafunzi wa Yesu Kristo wenye kushikamana naye wanapokabiliwa na majaribu, wanaweza kuwa na hakika watapokea msaada kama huo. (Yak. 1:2-5) Walakini, kama vile katika habari ya Yesu, hiyo hainyimi mtu uhuru wa kuchagua atakavyo. Roho ya Mungu haitalazimisha yeyote afuate mwendo fulani. Lazima mtu mwenyewe atake sana msaada wa roho. Kwa mfano, mtu anayesali akiomba msaada wa kushinda kishawishi lazima awe na nia ya kutii kanuni za Maandiko ambazo roho ya Mungu yamkumbusha na lazima atende kupatana nazo.
14. Roho ya Mungu yahusikaje wakati mtu asaidiwapo na waamini wenzake?
14 Huenda Mungu akatoa msaada kupitia kwa waamini wenzetu. Walakini, tena, roho ya Mungu yahusika, kwa maana roho hiyo hufanya kazi juu ya Wakristo wote wa kweli. Kwa mfano, wanapoona mmoja wa ndugu zao wa Kikristo akiwa na shida ya kimwili au ya kiroho, roho ya Mungu yenye kufanya kazi juu ya akili na mioyo yao huwajulisha kwamba lazima wamtimizie uhitaji wake nayo huwaharakisha kuchukua hatua inayofaa.
15, 16. (a) Kwa sababu gani Wakristo wengine huitikia vyepesi zaidi wasaidie waamini wenzao? (b) Kwa sababu gani waamini wenzetu ni njia bora ambayo kwayo twapata msaada, lakini hata hivyo tusitazamie nini?
15 Bila shaka, kama mtu mwenye uwezo wa kusaidia ataitikia asaidie yategemea kama yeye anakubali maombi ya roho ya Mungu. Nyakati nyingine huenda watu mmoja mmoja wakakosa kutaka kutimiza uhitaji fulani kwa sababu wameruhusu mapendezi yao wenyewe yazuie uwezo wenye kuchochea wa roho. Hiyo yaonyesha sababu gani hata katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza wengine walikuwa na nia zaidi na hamu ya kusaidia ndugu zao kuliko wengine, Angalia vile mtume Paulo alivyoandikia Wafilipi:
“Mlifanya vema, mliposhiriki nami katika dhiki yangu. Nanyi pia, ninyi wenyewe mnajua, enyi Wafilipi, ya kuwa katika mwanzo wa Injili, nilipotoka Makedonia, hakuna kanisa lingine lililoshirikiana nami katika habari hii ya kutoa na kupokea, ila ninyi peke yenu. Kwa kuwa hata huko Thesalonike mliniletea msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja. Si kwamba nakitamani kile kipawa, bali nayatamani mazao yanayozidi kuwa mengi, katika hesabu yenu. Lakini ninavyo vitu vyote na kuzidi, tena nimejaa tele; nimepokea kwa mkono wa Epafrodito vitu vile vilivyotoka kwenu, harufu ya manukato, sadaka yenye kibali, impendezayo Mungu.”—Flp. 4:14-18.
16 Kwa kuwa washiriki wa kundi la Kikristo wanatofautiana kwa kadiri wanavyofanya maendeleo ya kiroho na kwa kuwa kila mtu aweza kufanya uamuzi wake mwenyewe, hatuwezi kutazamia watu wote wawe na roho ya ukarimu kwa kadiri ile ile ya Wafilipi. Walakini, kwa kuwa wengi wanaitikia sana uongozi wa roho ya Mungu hiyo yahakikishia kabisa wanafunzi wa Yesu Kristo wenye kushikamana naye kwamba kuna njia yenye kutegemeka ya kupata msaada nyakati za majaribu na mikazo.
17. Roho ya Mungu inaweza kuongoza uwezo gani katika wasioamini, kuwafanya wachukue hatua kwa ajili ya Wakristo wa kweli?
17 Kwa kuwa roho ya Mungu inaweza kuongoza hata watu wasio waabudu wa Yehova wasaidie watumishi wake, hiyo inatia moyo sana. Hiyo yawezekanaje? Mwanadamu alifanywa kwa mfano wa Mungu. (Mwa. 1:28) Hii yamaanisha kwamba kwa ujumla wanadamu wana sifa fulani za kimungu—haki ya hukumu, hekima, upendo, na uwezo wa namna bora kuliko ule wa wanyama. Wanadamu wana uwezo wa dhamiri pia, maono ya ndani ya kuamua mambo yaliyo haki na makosa. (Rum. 2:14, 15) Kwa hiyo, roho takatifu inaweza kukumbusha watu wasio watumishi wa Yehova waliojitoa mambo yatakayochochea dhamiri zao zichukue hatua.
18, 19. Ni matukio gani siku za Mordekai na Esta yanayoonyesha kwamba Yehova anaweza kutumia wasioamini wafaidi watu wake?
18 Chukua mfano wa Mfalme Ahasuero (Xerxes wa Kwanza) katika wakati wa Mordekai na Esta. Alikuwa amempa Hamani mamlaka, mmoja wa wakuu wake wenye vyeo vya juu zaidi, atoe amri ya kuangamiza Wayahudi wote. Amri hiyo ilimtia ndani malkia wa mfalme, Esta, ingawa mfalme hakujua hivyo, naye Esta hakuwa amefunua wazi yeye ni mwanamke Myahudi, na amri hiyo ilitia ndani Mordekai pia, binamu ya Esta, ambaye Hamani hakumtaja alipokuwa akipendekeza Wayahudi waharibiwe. Usiku mmoja baadaye Ahasuero hakuweza kulala na kwa sababu fulani aliagiza asomewe maandishi rasmi. Yaliposomwa akafahamu kwamba wakati mmoja Mordekai alifichua mpango wa kutaka kuua mfalme. Alipogundua kwamba Mordekai hakupewa thawabu yo yote, Ahasuero alifadhaishwa na jambo hilo lisilo haki akaamua kumthawabisha Mordekai.—Esta 3:1-15; 6:1-3.
19 Kwa hiyo, wakati Hamani alipofika mapema asubuhi iliyofuata kuomba Mordekai atundikwe mtini, kilitokea kinyume chake. Badala ya kuweza kufanya ombi lake, Hamani alilazimishwa kumpa Mordekai heshima mbele ya watu wote. (Esta 6:4-11) Hiyo ndiyo iliyokuwa hatua ya kwanza ya mfululizo wa matukio yaliyofanya amri tofauti ikatolewa iliyowezesha Wayahudi watetee maisha zao. Kwa wazi, mkono wa Mungu ulikuwa katika jambo hilo. Katika wakati uliofaa roho yake ilichochea akili ya Ahasuero akataka asomewe maandishi rasmi na baada ya hapo akasahihisha jambo lililokuwa limesahauliwa.
20. Ilikuwaje kati ya Ezra na Mfalme Artashasta na maafisa wengine?
20 Wengine pia walishuhudia matokeo ya nguvu ya utendaji ya Mungu juu ya akili na mioyo ya watu wenye mamlaka. Ezra kuhani alitoa shukrani zinazofuata kuhusu msaada aliotoa Mfalme Mwajemi Artashasta (Longimano) kupamba hekalu Yerusalemu: “Na ahimidiwe [Yehova], Mungu wa baba zetu, aliyetia neno kama hilo katika moyo wa mfalme, kuipamba nyumba ya [Yehova] iliyoko Yerusalemu. Naye amenifikilizia rehema zake mbele ya mfalme, na washauri wake, na mbele ya wakuu wote wa mfalme wenye mamlaka.” (Ezra 7:27, 28) Angalia kwamba roho ya Mungu iliongoza washauri wa mfalme na wakuu wenye vyeo vya juu pia wawe na nia nzuri juu ya shughuli ya Ezra.
21. Matendo ya zamani ya kuokoa kwa Mungu yapaswa kutupa uhakikisho gani?
21 Lo! kumbukumbu la vile Yehova alivyosaidia watumishi wake waliojitoa zamani latia moyo namna gani! Linatusaidia tufahamu kwamba msaada unaohitajiwa huja kwa njia mbalimbali. Usipokuja kwa njia moja, bila shaka utakuja kwa njia nyingine. Mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alisema hivi: “[Yehova] hatawatupa watu wake.” (Zab. 94:14) Hivyo ndivyo Mordekai alivyoona wakati yeye na wananchi wenzake walipokabiliwa na amri ya kuangamizwa. Alipokuwa akimsihi binamu yake Esta atetee watu wake, alisema hivi: “Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine.”—Esta 4:14
22. Kwa sababu gani yatupasa tuwe na hakika Yehova ana uwezo wa kusaidia hata hali ionekanapo kuwa bila tumaini kwa maoni ya kibinadamu?
22 Kwa maoni ya kibinadamu, huenda hali ikaonekana bila tumaini. Huenda ikaonekana haiwezekani kuwe na faraja. Walakini, ikiwa jambo fulani ni mapenzi ya Mungu, hakuna linaloweza kuzuia yasitimizwe. Yehova Mungu alieleza jambo hilo wazi sana wakati Waisraeli walipopaza kilio cha kulalamika juu ya nyama. Jibu lake alilotoa kupitia kwa Musa lilikuwa hili: “[Yehova] atawapa nyama, nanyi mtakula. Hamtakula siku moja, wala siku mbili, wala siku tano, wala siku kumi, wala siku ishirini; lakini mtakula muda wa mwezi mzima.” Musa alisema hilo lisingewezekana: “Watu ambao mimi ni kati yao, ni watu sita mia elfu waendao kwa miguu; nawe umesema, Nitawapa nyama, ili wale muda wa mwezi mzima. Je! makundi ya kondoo na ng’ombe yatachinjwa kwa ajili yao, ili kuwatosha? au samaki wote wa baharini watakusanywa pamoja kwa ajili yao, ili kuwatosha?” Yehova alimjibu hivi: “Je! mkono wa [Yehova] umepungua urefu wake? Sasa utaona kwamba neno langu litatimizwa kwako, au sivyo.” Mkono wa Yehova haukuwa mfupi mno. Alifanya upepo ukapeleka kware tele ndani ya kambi ya Israeli.—Hes. 11:18-23, 31.
23. Je! tumtazamie Yehova atuokoe kwa mwujiza tusiuawe au tusiteswe vikali? Kwa sababu gani wajibu hivyo?
23 Ingawa ni wazi kabisa kwamba Yehova Mungu aweza kufanya miujiza kwa ajili ya watu wake, tusitazamie Mungu aahidi kabisa kwamba atatuokoa kwa mwujiza tusiuawe au tusiteswe vikali. Huenda kusudi la Yehova likatimizwa aruhusupo wengine wa watumishi wake wafe kwa uaminifu au wapatwe na mateso mabaya sana, kama Mwanawe mzaliwa wa kwanza, Yesu Kristo, Kwa kuvumilia kwa uaminifu, watumishi wa Mungu wana pendeleo la kuhakikisha kwamba hawaabudu wakifikiria faida zao tu. Kwa njia hii wanahakikisha shtaka la Shetani ni la uongo. lililofanywa kuhusu Ayubu. “Yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.”—Ayubu 2:4
24. Shadraki, Meshaki na Abednego walionyeshaje maoni yanayofaa juu ya uwezo wa Yehova kusaidia watumishi wake?
24 Wakati wa utawala wa Mfalme Nebukadreza, wahamishwa watatu Waebrania katika Babeli—Shadraki, Meshaki na Abednego—walieleza maoni yafaayo juu ya uwezo wa Mungu kusaidia watumishi wake. Walipoelekea kuhukumiwa kufa katika tanuru ya moto wakiendelea kukataa kuiinamia sanamu iliyofanywa na Nebukadreza, walisema kwa ushujaa hivi: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.”—Dan. 3:17, 18.
25. Ni jambo gani la maana zaidi kuliko kuokoa uhai wako kwa muda, na kwa sababu gani?
25 Jambo la maana si mtu yeyote aokoe uhai wake kwa muda mfupi katika taratibu hii. Jambo la maana zaidi ni kuendelea kuwa na uhusiano wenye kukubaliwa na Yehova Mungu na Yesu Kristo. Akikaza fikira kwenye hilo, Yesu alisema: “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.” (Yohana 12:25) Mtu anayeacha uhusiano wake mwema na Muumba na Mwanawe ili aepuke kufa mapema isivyo kawaida aweza kupoteza nafsi yake milele, yaani, haki aliyopewa na Mungu ya kuwa kiumbe hai. Kwa upande mwingine, mtu awezaye kufa akiwa mwanafunzi wa Yesu Kristo mwenye kushikamana naye ahakikishiwa kwamba atafufuliwa, akiwa na tumaini la kuishi milele.
26. Sikuzote twaweza kutazamia msaada wa kufanya nini kutoka kwa Yehova, na kwa sababu gani?
26 Ingawa huenda wengine wetu mmoja mmoja tukauawa na wanadamu ili kuhakikisha tumejipa kwa Yehova Mungu bila kutikisika, twaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatuacha. Atatusaidia tuendelee kuwa watumishi wake anaowakubali. Maadamu tunajitahidi kumtumikia, uhusiano wetu naye u salama. Mtume Paulo aliandika akasema, “Nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Rum. 8:38, 39) Kwa hiyo, hata tuwe tutapatwa na jambo gani wakati ujao, sikuzote na tutegemee uwezo wa Yehova wa kutusaidia tuendelee kuwa na uhusiano wenye kukubaliwa naye.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Macho ya mtumishi wa Elisha yalifunguliwa aone kwamba Yehova ni Msaidiaji asiye na kifani