Saidieni Vijana ‘Wawe Vielelezo kwa Waaminifu’
“Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”—1 Tim. 4:12.
1-3. (a) Kwa sababu gani wazazi wengi wanajisikia vizuri juu ya vijana wao? (b) Toa mifano, kutia na ya kwenu, kuonyesha jinsi vijana wameshikamana na kanuni za Kikristo. (c) Maandiko yanahakikishwaje kuwa kweli katika mifano hiyo?
MACHO ya ulimwengu sasa yanatazama vijana zaidi sana. Wanatazamwa sana. Wazazi wengi wanaheshimu sana watoto wao. Kwa ujumla, Mashahidi wa Yehova hasa wanajisikia vizuri sana kwa sababu ya vijana wao, na wana sababu nzuri. Kwa ujumla watoto wao wamejihakikisha kuwa mifano bora ya kufanya mema, wakati ambao watu hawafuati sana adili.
2 Kwa mfano, yuko Richard, Shahidi kijana, aliyesema: “Mwalimu wangu wa kiume alitaka niunge mkono fundisho la mageuzi katika darasa. Nikamwambia mimi ni Mkristo na dhamiri yangu yanikataza kufanya hivyo.” Aliangushwa katika mtihani kwa sababu ya imani yake imara juu ya uumbaji. Lakini, kijana huyo alijisikia amepewa thawabu moyoni kwa kubaki akiwa imara juu ya mambo aliyoamini ni ya kweli. Shahidi mwingine aitwaye Randy alikataa kudanganya wakati wa mtihani wa Kifaransa, katika mwaka wake wa masomo ya juu. Alisema, “Mimi peke yangu katika darasa sikupita mtihani.” Mwalimu alipouliza, “Kwa sababu gani hukuangalia ndani ya kitabu?” ambacho kiliwekwa karibu, yeye alisema: “Sikutaka kudanganya.” Ingawa mwalimu na watoto wale wengine walidharau uaminifu huo, Randy alijisikia amefanya haki. Kushikamana na kanuni kulikuwa kwa maana zaidi kwake kuliko kupita mtihani. Halafu kulikuwa na Shahidi mwingine kijana aitwaye Debora, aliyekuwa akifanya kazi katika chumba cha kuuzia ice-cream. Msimamizi wake alidai awe akivaa marinda mafupi zaidi anapofanya kazi au sivyo aondolewe kazini. Debora alimwendea msimamizi-mkuu akamweleza yeye ni shahidi wa Kikristo wa Yehova na kwamba desturi yake ni kuvalia kwa adabu. Hakuondolewa kazini, kwa sababu alikuwa mfanya kazi mwema. Hata hivyo, Debora alishinda kwa kufuata adili. Aliendelea kuwa mwaminifu kwa kanuni alizopewa na Mungu.
3 Zidisha mifano hiyo ya imani, ya uaminifu, ya usafi wa adili na ya kushikamana na kanuni na dhamiri mara elfu nawe utaweza kuona sababu gani wazazi kati ya Mashahidi wa Yehova wanajivunia vijana wao. Juu ya wazazi wenye watoto wa namna hiyo mithali inasema: “Baba yako na mama yako watafurahi, naye [mama] aliyekuzaa atakuwa na shangwe.”—Mit. 23:25, NW; 1 Pet. 2:12.
MFANO WA WAZAZI
4. (a) Ni mambo gani yanayohusika katika kufanya watoto wazidi kufuata adili kwa ukamilifu? (b) Watoto wanafaidikaje wazazi wanapoishi maisha mema?
4 Lakini, watoto hawajikuti tu wamekuwa wema katika ulimwengu wenye uchafu wa tabia—maana ‘watu hawachumi zabibu katika miiba, wala tini katika mibaruti.’ (Mt. 7:16-18) Ikiwa wazazi wanataka watoto wao ‘wawe vielelezo kwa waaminifu, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi,’ wao wenyewe lazima wawekee watoto wao kielelezo cha kufuata. (1 Tim. 4:12) Haitoshi kutaka tu watoto wafuate adili. Jitihada inatakiwa. Watoto hawazaliwi wakifuata adili kwa ukamilifu. Wanajua adili kwa kufundishwa na kutazama mambo yanavyofanywa. Baba anayeishi kulingana na sheria za adili za Biblia, na mke anayeweka mfano wa kufuata adili kwa ukamilifu, anafundisha kwa maneno na mfano. (Kum. 6:4-9) Njia hii ya kufundisha inatokana na mamlaka iliyo juu zaidi, kwa maana Yehova Mungu mwenyewe anatumia njia hiyo. Yesu alinena juu ya Baba yake wa kimbinguni hivi: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile. Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe.” (Yohana 5:19, 20) Kwa hiyo wazazi wenye shauku wanaweza kuonyesha watoto wao jinsi wanavyotaka waishi, kuwawekea mifano kwa maisha zao wenyewe “katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”
5, 6. (a) Inaweza kuwaje wazazi wasipofanya mambo wanayofundisha? Toa mfano. (b) Kwa sababu gani matumizi yanayofaa ya mamlaka ni ya maana?
5 Hivi karibuni, Lisa mwenye miaka kumi alimwambia mama yake na mkuu wa shule uongo kwa kusema alirudisha kitabu maktabani. Mama yake alishangaa akajiuliza: “Kwa sababu gani Lisa amesema uongo?” Na, jambo ambalo pengine ni la maana zaidi: “Amejifunzaje kusema uongo kwa urefu hivyo na kwa moyo mgumu?” Mama huyo alimshika msichana wake. Akamwambia, “Lisa, hujui hupaswi hata kidogo kusema uongo?” Lisa aliona ametatizwa naye akarudisha hivi: “Wewe na Baba husema uongo, Mnasema uongo mara nyingi sana. Sababu gani mimi nisiseme?” Mama ya Lisa angaliweza kusema upesi hivi: “Unadhani unasema na nani kwa njia hiyo? Mimi ni mama yako!” Pengine Lisa angalinyamaza, lakini tatizo lingalikwisha? Lisa hakutaka kuonyesha dharau kwa maneno yake. Mama ya Lisa alizungumza na msichana wake kwa utulivu, akakubali makosa aliyoonyeshwa na Lisa, akayaondoa, hivyo akatumainiwa na msichana wake.
6 Mara nyingi mabishano ya watoto na wazazi yanaonyesha wazazi wanatumiaje mamlaka. Ni kweli kwamba wazazi wamepewa haki na Mungu ya kutumia mamlaka, lakini mtume Paulo anawaonya wasiitumie vibaya, akisema: “Na ninyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova.” (Efe. 6:4, NW) Mamlaka inaweza kuogofya na hata kuadhibu wale wanaovunja sheria, lakini mamlaka peke yake haifundishi wa la haiwezi kufundisha vijana jinsi ya kutaka wawe wema.
7. Wazazi wanawezaje kuelekeza watoto kwenye haki na mema’
7 Wazazi wanatakiwa pia wafikie mioyo ya watoto wao na kuwasaidia wabadili nia zao, si tabia yao tu. (Rum. 12:1, 2) Nia ya kufanya mema lazima itoke ndani ya mtoto, ndipo aweze kubadilika vya kutosha awe mwema. Lazima watoto wajisikie ndani yao wenyewe wakiwa na uhitaji mwingi zaidi wa kuwa waadilifu. Wanaweza kufanya hivyo kwa kuiga wazazi wanaomtegemea Yehova Mungu kama Mfano wao wa wema. (1 Pet. 1:15, 16) Kwa njia hii watoto pia wanakuza tamaa ya kumpendeza Yehova. Wanapoona wazazi wao wakifuata adili, watoto wanaanza kuamini Mungu anaona mambo wanayofanya na kwamba anajali. (1 Pet. 3:12; 5:7) Kwa kuimarishwa na mafundisho ya Biblia na mifano myema ya watu wazima, akili na mioyo ya vijana inaelekezwa kwenye “haki na hukumu, na adili, na kila njia njema.”—Mit. 2:9.
KUSHINDANA NA TAMAA YA VITU VYA KIMWILI
8. Kwa sababu gani tamaa ya vitu vya kimwili ni jaribu kwa vijana, nayo Maandiko yanaonyaje juu ya tamaa hiyo?
8 Vijana wanaokua wakiwa katika nyumba za Kikristo wamepaswa kujua kwamba hatari mojawapo kwa hali yao ya kiroho ni kutaka sana vitu vya kimwili. Kwa sababu gani? Kwa sababu mtu akiwa na vitu vingi vizuri, kama nyumba nyingi, magari, mashua, televisheni, na vitu kama hivyo, anaonekana na wengine kuwa amefaulu sana, na vijana wanataka sana kufaulu. Ingawa hakuna ubaya wa kuwa na mali, Biblia inaonya juu ya “kupenda fedha” na ‘kutaka sana kuwa na mali.’ (1 Tim. 6:9, 10, 17; Luka 12:15-21) Inaonyesha utajiri unadanganya, kwa sababu hauwezi kuokoa mtu asife wala hauwezi kumpa afya wala uzima. Mali zinaweza kuondoa mtu katika imani, hata kumfanya asahau Yehova. (Kum. 8:10-14; Mit. 11:4) Kwa hiyo, Biblia inashauri kwa hekima hivi: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye [Mungu] mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Ebr. 13:5; 1 Tim. 6:8) Lazima vijana wathamini na kutumaini ahadi hiyo ya Mungu; kwamba hatawaacha. Ndipo watakapojua kwamba ‘baraka ya Yehova ndiyo hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.’—Mit. 10:22.
9. (a) Wazazi wanawezaje kusaidia vijana wajilinde na tamaa ya vitu vya kimwili? (b) Maandiko yanatoa mifano gani myema na onyo la upole juu ya habari hii?
9 Vijana Wakristo wanawezaje kulindwa na mitego isiyoonekana wazi ya kutamani sana vitu vya kimwili? Kwanza, wazazi wanaweza kusaidia sana kwa kuhakikisha katika maisha zao wenyewe ‘hawapendi fedha.’ kwamba wanaonyesha wanatosheka na vitu walivyo navyo, na kwamba wanaweka nyumbani hali ya kiroho yenye nguvu. Wazazi wanaweza pia kuelekeza fikira kwenye mifano ya Maandiko ya Yesu na mitume wake. Yesu alisema: “Mwana wa Adamu hana pa kulaza kichwa chake.” (Mt. 8:20; Flp. 2:7, 8) Petro alisema hivi: “Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata.” (Mt. 19:27) Paulo aliandika hivi: “Nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo.” (Flp. 3:8) Hiyo si kusema kwamba vijana Wakristo wanalazimishwa kufuata maisha yasiyo na mambo ya kujifurahisha hata kidogo. Sivyo! Yesu aliwaahidi kwamba wakitanguliza utumishi wa Mungu maishani, Mungu naye atawaongezea vitu vya kimwili wanavyohitaji. Lakini lazima wajinyime anasa wasizohitaji ndipo washinde tamaa ya vitu vya kimwili. (Mt. 16:24) Lazima mkazo uwe juu ya mambo ya kiroho,. (Mt. 5:3; Gal. 5:16) Mtume Paulo alishauri hivi: “Ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole. Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele.” (1 Tim. 6:11, 12) Ndipo hatutakuwa na tatizo la kutamani sana vitu vya kimwili.
KUFANYA KAZI HUONDOA UCHOVU
10. Ni jambo gani linaloweza kuleta uchovu, lakini uchovu unaweza kumalizwaje?
10 Nyakati nyingine vijana wanalalamika juu ya kuchoshwa na maisha. Kwa kawaida uchovu huja wakati akili na mikono imekuwa mivivu isifanye mambo yanayofaa. Zamani, kila mtu aliyeishi mashambani alitakiwa afanye kazi. Hata watoto wadogo walitumiwa kulisha kuku, kukama ng’ombe na kuvuna mazao. Watoto walihitajiwa, nao walijua walihitajiwa. Vijana bado wanataka kujisikia wanahitajiwa, kujisikia wana faida. Moyoni, kwa kawaida wao hutaka kuwa wafanya kazi na wapaji, si watazamaji na wapokeaji tu. Tamaa hiyo ni njema, kwa sababu Yesu alisema: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Paulo aliandika hivi: “Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.” (2 Kor. 9:7) Vijana wa leo wanaochoshwa na mambo wamepaswa wao wenyewe watumikie mara nyingi zaidi. Lakini kwa njia gani? Katika kundi, vijana Wakristo wanaweza kwenda dukani kununua vitu ambavyo waliozeeka wanahitaji, wanaweza kutembelea wagonjwa au kusaidia wenye udhaifu wa mwili na kazi za nyumbani. Na lo! laweza kuwa jambo la furaha namna gani kusomea wale wanaoishiwa nguvu za macho!
11. Watoto na wazazi wanaweza kumalizaje uchovu?
11 Nyakati nyingine kuzoeza mwili kutasaidia kuondolea akili uchovu. Wasichana wadogo huenda wakajaribu ufundi kwa kutengeneza nguo ya kike, kupika au kuoka. Wavulana wadogo wanaweza kujifunza kutengeneza vitu vilivyoharibika nyumbani, kujifunza umekanika mdogo mdogo au useremala. Kujifunza lugha mpya, hata usemi wa kutumia ishara, kunasaidia kuondoa uchovu. Wazazi wanaweza kusaidia watoto wao kwa kuwafundisha jinsi ya kuwa watunza nyumba halisi—jinsi ya kutandika sawasawa vitanda vyao, kukunja kimalidadi mavazi yao, kufagia na kung’arisha nyumba, na hata kushonelea vifungo mara kwa mara katika shati za baba yao. Vijana wanaokuwa wapaji na wafanya kazi wachangamfu wanajiona wana mambo mengi sana ya kufanya hata hawawezi kuchoshwa na maisha. Tena, wao wanakuwa mfano mwema sana kwa waaminifu wengine.—1 Kor. 15:58; 13:5; Mhu. 5:18-20.
MATEMBEZI YA WAVULANA NA WASICHANA YAWEZA KUHARIBU
12. (a) Ni nini linaloonyesha kwamba maoni ya kilimwengu juu ya matembezi ya wavulana na wasichana ni mabaya? (b) Ni hatari gani zinazoweza kuingia katika uhusiano wa kipumbavu wa wavulana na wasichana?
12 Mahali ambako kuna watoto wanaokua katika jamaa, baadaye litatokea tatizo la matembezi ya wavulana na wasichana. Wazazi wanaweza kusaidiaje? Wale wasioongozwa na kanuni za Biblia wanaweza kutoa kwa vyepesi mashauri mapotovu. Msichana aitwaye Kathy, anayetaja wazazi wake kuwa ‘Waprotestanti thabiti,’ asema hivi: “Nilianza kutembea na wavulana nilipokuwa darasa la tisa, nilipokuwa wa miaka kumi na minne.” Anakubali kwamba baba yake hakupendezwa na jambo hilo, lakini karibuni mama yake alimaliza mabishano kwa kuhakikishia baba kwamba Kathy alikuwa na umri wa kutosha. Umri wa kutosha kufanya nini? Kathy mwenyewe alikubali hakuwa tayari kuolewa hata alipokuwa wa miaka kumi na saba, achia mbali miaka kumi na minne. Na wasichana wengi wa umri wake hawawi tayari mwilini, moyoni wala akilini kutatua matatizo wala kuchukua madaraka ya ndoa. Basi kwa sababu gani wawe na matembezi na wavulana? Wasichana kama Kathy wanaona kutembea na wavulana ni jambo la kufurahisha au tafrija. Wanasema, ‘Kupapasana na kukumbatiana ni sawa maadamu hamruki mipaka.’ Lakini Kathy akubali kwamba wasichana wengi wa umri wake waliingia matatani, wakaruka mipaka, wakachukua mimba na kuzitoa au wakapata watoto. Badala yake, wazazi Wakristo wamepaswa kufundisha na kusadikisha watoto wao kwamba, kulingana na kanuni za Biblia, maoni kama ya Kathy ni mabaya, na kwamba Mungu anakataza mwenendo mpotovu. Mkristo kijana anayekuwa na mwenendo mchafu aweza kutengwa na ushirika wa kundi.—Gal. 5:19, 21, 1 Pet. 4:3
13. (a) Yehova ataka vijana waishije na kuenendaje? (b) Kwa sababu gani matembezi ya wavulana na wasichana si jambo la mchezo tu?
13 Yehova ni Mungu mwenye furaha,. na ataka vijana wafurahie maisha pia—si maisha mapotovu, bali maisha yenye heshima. (1 Tim. 1:11) Kwa hiyo, asema: “Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, . . . ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako; lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni. Kwa hiyo ondoa [udhia] moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako.” (Mhu. 11:9, 10) Mungu ataka vijana wawe na furaha wakiwa na wajibu kwake. Watamjibu Yeye kwa matendo yao. Ndiyo sababu matembezi ya wavulana na wasichana si jambo la mchezo tu. Matembezi ya wavulana na wasichana yaweza kusaidia kukutanisha watu wawili, si kwa kusudi la kupapasana wala kukumbatiana wala Kufanya mahaba, bali kufahamiana kirafiki kabla hawajaoana. Nje ya ndoa, nyege zaweza kuudhi, kusumbua moyo na hata kuleta mabaya kama kuondoa mimba na kujiua. Hata watu waliopanga kuoana hawana haki ya kuchezea ngono. Watu wasiooa wala kuolewa wanaofanya ngono, ambayo ni haki ya watu waliooana peke yao, watapoteza upendeleo wa Mungu na bila shaka hawataepuka adhabu.—1 Kor. 6:9, 10.
14. (a) Wazazi wanawezaje kukuza nia inayofaa juu ya matembezi ya wavulana na wasichana na ndoa katika watoto wao? (b) Watoto wanaweza kufanya nini watumie miaka ya ukuzi wao kwa faida?
14 Wazazi wanaweza kusaidia watoto wathamini sheria za Mungu kwa kuwaeleza mambo waziwazi na kuzungumza nao habari ya matembezi ya wavulana na wasichana na ndoa. Kwa njia hiyo watoto wanaweza kupata maarifa safi na kuona kwamba Mungu na wazazi wao wanawafikiria na kuwapenda. (Mit. 15:3; 1 Pet. 3:12) Watoto wanaweza kukumbushwa kwamba miaka yao ya ujana ina nafasi nyingi za kuwakuza wawe wanaume na wanawake halisi, halafu ikiwa baadaye watataka madaraka ya ndoa, watakuwa tayari kuyatimiza. Wanaweza pia kukua wakomae kiroho kwa ‘kuwa vielelezo’ wanapojitia katika utendaji wa kundi la Kikristo.
KUPATA RAFIKI WAAMINIFU
15. Urafiki unahitaji nini, nasi twawezaje kupata rafiki za kweli?
15 Kuwa na rafiki waaminifu katika ujana kunaweza kusaidia kushinda vipingamizi vingi. Lakini si vyepesi kupata rafiki za kweli. Urafiki unahusu watu wawili, na kila mtu apaswa kuwa mwenye urafiki—kukaribiana. Urafiki unataka ushikamanifu, kufikiriana na kupendezwa na hali njema ya mtu na mwenzake. Urafiki unategemea kupenda, si kupendwa. Mtu mwenye hekima aliandika hivi zamani, “Rafiki hupenda sikuzote.” (Mit. 17:17) Ikiwa tunataka rafiki za kweli lazima tuache wengine wajue tunayofikiria. Lazima tuache watujue tulivyo hasa, tuzungumze nao waziwazi mambo ambayo tumejifunza.—Yohana 15:15.
16. Kwa sababu gani ni hekima kuwa wateuzi tunapochagua rafiki?
16 Lakini, tunapotafuta rafiKi ni hekima kuwa wateuzi. Kwa sababu gani? Kwa sababu, tunaposhirikiana na wengine wakati mwingi kutosha tunaelekea kuwa kama wao. Tusipojiangalia, tunaweza kukuta tabia zetu zenye mafaa zimeharibika. (1 Kor. 15:33) Ni jambo la faida sana kuchagua rafiki wenye sifa njema za Kikristo. (Gal. 5:22, 23) Vijana wamepaswa kuchagua rafiki wanaofaa katika mambo yote.
SABABU GANI UENDE SHULENI?
17. (a) Wazazi wanawezaje kusaidia watoto wanaohuzunishwa na tabia za shule? (b) Watoto wanawezaje kujilinda na watu wasio na adabu?
17 Vijana wengi Wakristo wanahuzunishwa na tabia mbaya shuleni. Wazazi wanaweza kufanya nini kuwalinda na maongozi hayo mabaya? Wanaweza kukazia akili za vijana pendeleo walilo nalo kama mashahidi wa Yehova, la kutetea kweli na haki na kuzifuata katika maisha zao. Watoto, sawa na watu wazima, wanaweza kufaidika na sala ambayo Yesu alimtolea Mungu kwa ajili yao ili ‘awalinde.’ (Yohana 17:15) Ingawa kuonana na watu wasiofaa hakuwezi kuepukwa kabisa, vijana wanaweza kuonana nao mara chache zaidi, nyakati zinazohusu kazi za shule tu. Na wakikaza fikira juu ya masomo yao, na kujitahidi wafanikiwe katika masomo, wanaweza kwa vyepesi kupunguza ushirika wao na watu wasio na adabu. Ni vema pia kwa vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova kuacha wengine wajue upesi iwezekanavyo kwamba wao ni Wakristo wa kweli na kwamba wanakusudia kufanya mambo kwa bidii wanapokuwa shuleni. Itaonekana wazi kwamba wameweka mfano mwema “katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”
18. (a) Elimu ni nini, na kwa sababu gani ni ya lazima kwa maisha? (b) Watoto walio shuleni sasa wanapewa shauri gani?
18 Ijapokuwa shule ina matatizo mengi, ni ya maana kwa maisha. Kazi yake kuu ni kuzoeza akili za vijana zifikiri, ziwe zenye kufikiria kuvumbua na kuchunguza mambo bila ya kuambiwa saa zote. Elimu imeelezwa kuwa: “Mpango unaokuza watu na kuwawezesha waishi maisha ya maana.” Inaweza kuzoeza akili kukuza sasa utu, na kutoa matayarisho yafaayo ya maisha. Shule yapaswa kutayarisha vijana wachukue madaraka ya watu wazima. Kwa hiyo unayofanya shuleni yanaweza kuamua sana wewe utakuwa mtu mzima wa namna gani. Kwa hiyo, jibidiishe. (Gal. 6:7) Wakati wa miaka yako ya kwenda shule unaweza kujifunza uwezo na ufundi mbalimbali ambao karibuni utakufaa katika maisha yako ya mtu mzima, na vilevile baadaye katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu. (Isa. 65:22) Jifunze kusoma na kuandika vema. Ni jambo lenye faida kufikiria kuendeleza maneno ifaavyo, kujua kanuni za sarufi, na kupendezwa na matukio ya kihistoria na tarehe. Jifunze kutumia akili yako, kwa maana kadiri uitumiavyo zaidi ndivyo itakavyokufaa sasa na milele.—Mit. 2:10-13; 3:21-23.
19. (a) Wazazi wanawezaje kuangalia watoto wao kwa upendo? (b) Kwa sababu gani watoto wenye adabu na ukamilifu ni sifa kwa wazazi wao?
19 Watoto wenye kufuata adili kwa ukamilifu ni thawabu kweli kweli kwa wazazi waliowalea. Wao ni mifano myema pia kwa waaminifu wengine. Onyesheni mnawapenda kwa kutumia wakati mkiwa nao kila siku mkichunguza mambo na kujifunza, kuamsha mawazo mapya, kutazama picha au kuzungumza tu juu ya Biblia au mambo mengine yenye kujenga. Wazazi wanapopendezwa wazi hivyo na watoto, wanaweza kuongoza vizuri sana maisha zao. Maneno yenu ya upendo na shukrani yanaweza kuwafaidi zaidi kuliko sifa ya mtu mwingine ye yote. Watawaletea sifa. Nao watafuata sana upendo wenu, imani yenu, mwenendo wenu na usafi wenu wa adili kwa ‘kuwa vielelezo kwa waaminifu.’—1 Pet. 1:22.
[Picha katika ukurasa wa 33]
Utendaji mwingi mwema unaohitajiwa uko wazi kwa vijana Wakristo, kama vile kazi za nyumbani, kwenda dukani kununua vitu ambavyo waliozeeka kundini wanahitaji, kusomea wanaoishiwa nguvu za macho.—1 Kor. 13:4, 5.
[Picha katika ukurasa wa 34]
Kwa kujitia sana katika utendaji wa kundi na kueleza wengine habari njema—si kufanya utumishi mdogo tu—vijana ‘wanakuwa vielelezo kwa waaminifu’