Kilichonifurahisha
Imesimuliwa na Maria Alves de Azevedo
NILIZALIWA Lamelas, kijiji kidogo katika wilaya ya Oporto ya Ureno, inayojulikana sana kwa sababu ya divai tamu zinazopatikana humo. Tuliishi katika nyumba kubwa ya mawe, yenye vyumba vya kulala orofani na vifaa vya mashambani. Huko chini tulikuwa na jiko kubwa ambalo pia lilitumiwa kama chumba cha kulia chakula. Humo tulikuwa na joko (oven) lenye kuwekewa kuni, tena ndimo tulimookea mkate wetu mtamu wa mahindi.
Tulipata maji ya kunywa katika chemchemi iliyokuwa nyuma ya nyumba yetu. Yalikuwa safi sana, na kando-kando yalikuwako matunda mazuri sana. Tena kijito safi kama kioo kilitiririka karibu na nyumba yetu.
Bado nakumbuka baadhi ya mambo hayo, tena nafurahia kutazama maji safi yenye kutiririka. Tangu utoto wangu nimefurahi sana kusoma katika Biblia habari za “mto wa maji ya uzima.” (Ufu. 22:1, 2) Nilifurahi sana pia nilipojua kwamba siku moja wanadamu wote wataishi kwa amani wakiwa chini ya mizabibu na mitini yao wenyewe.—Angalia Mika 4:3, 4.
Baba aliondoka kwenda Brazil akatafute pesa zaidi nilipokuwa na miezi mitatu tu. Mama nami tulimfuata miaka minne baadaye, mwaka 1917.
MAONGOZI YA DINI
Baba alikuwa amekuwa akitumikia katika, altare (madhabahu) alipokuwa kijana, katika kanisa Katoliki la huko Lamelas. Naye mama alikwenda nami kanisani sikuzote. Baadaye, shangazi Mpresbiteri alimwomba baba asome Biblia, na baada ya muda mfupi wazazi wangu wakawa Wapresbiteri.
Wakati huo nilikuwa na karibu miaka tisa, nami nilifurahia kusoma hadithi za Biblia juu ya Yusufu mwenye rehema na Ayubu mwenye subira. Ukamilifu wao ulikuwa ukinitoa machozi. Nilitaka niwe kama wao.
Baadaye tulihamia Olaria, kaskazini ya Rio de Janeiro. Huko, badala ya kuwa na kijito safi, kulikuwa na shimo kubwa katikati ya barabara lenye majani na magugu mengi. Shimo hilo liligeuzwa likawa mahali pa kupitishia takataka za watu, nalo lilitoa harufu mbaya weee. Namna gani mbu waliokuwamo? Acheni tuwasahau.
Ilikuwa lazima tufanye kazi nyingi tufikie mradi wetu wa kupata ufanisi wa kimwili. Kwanza, nilisaidia mama na kazi za nyumbani halafu wote wawili tukawa tukisaidia baba katika biashara yake ya kutengeneza viatu. Mama alifuga kuku pia, nami nilimsaidia kuuza mayai. Siku moja niliuzia watu dazan mbili za mayai (24) kwa bei ya juu zaidi. Nilitaka kununua tikiti ya bahati nasibu nikitumainia kushinda zawadi ya kitu cha kuchezea. Adhabu kali niliyopewa ilinionyesha sana ubora wa kuwa mwaminifu.
Nilipokuwa na miaka tisa nilibatizwa nikawa Mpresbiteri, halafu mwaka 1927 nilipokuwa na miaka kumi na minne nikapata kipaimara. Siku moja ya mwaka huo nilikutana na baharia aitwaye Raimundo F. Cabral, akasema ni “Mwanafunzi wa Biblia.” Alikuwa amechumbia msichana niliyekuwa nikijaribu kumwongoa aache mambo ya uchawi ajiunge na Kanisa la Kipresbiteri. Nilikuwa nikifundisha katika ibada ya watoto nikitaka kusaidia watu wajifunze habari za Mungu.
Lakini, baharia huyo alinionyesha katika Biblia kwamba si uchawi peke yake ulio mbaya, bali pia kwamba nafsi inaweza kufa na kwamba hell ndilo kaburi la wanadamu wote. Tulizungumza habari nyingine pia, nikajifunza mambo mengi ambayo sikujua. Hata hivyo, alioana na msichana huyo rafiki yangu wakaenda zao. Kwa muda wa miaka kumi na miwili sikuonana tena na Wanafunzi wa Biblia.
Wakati huo mambo mengi yalitukia. Mimi pia niliolewa, lakini ndoa yangu haikufurahisha sana. Mabaya yalikuwa mengi, mazuri yakawa machache. Nilitumainia sana kupata mtoto wangu wa kwanza. Je! baada ya kumzaa uhusiano wangu wa ndoa ungekuwa bora? Looo, nilimzaa akiwa amekufa. Mume wangu alikuwa amekwisha anza kuwa mtu wa kutanga-tanga tu. Huzuni haikwisha hata nilipozaa watoto watatu zaidi.
Sikuzote nilijaribu kuwaficha watu matatizo yangu, hasa wazazi wangu, kwa hiyo sikuwa na mtu wa kunifariji wala kunitia moyo. Dini yangu haikunipa tumaini. Hata nilidhani nilikuwa mmoja wa watu wenye kusoma Biblia bila kustahili kuifahamu. Kwa upande mwingine, niliamini lazima kuwe na watu “waongozao wengi kutenda haki.” (Dan. 12:3) Nilishindwa kujua hao ni watu gani. Nilitaka sana kuijua kweli inayoweka watu huru!—Yohana 8:32.
NILICHOKUWA NIKITAFUTA
Halafu, Januari mwaka 1939, Mwanafunzi wa Biblia yule yule alinitembelea tena, lakini wakati huu akajiita mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Niliandikisha Mnara wa Mlinzi wa Kireno kwa furaha, halafu nikapewa zawadi ya kitabu Riches (Mali) na vijitabu vitatu. Nilishangazwa na mjumbe wa maana sana uliokuwamo, nikawaonyesha jirani zangu bila kukawia. Nilipomaliza kusoma kitabu Riches nikaweza kusema kikweli kwamba: “Nimewapata watu wa Mungu!”
Aprili 4, 1939, nilihudhuria mkutano wangu wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova; ulikuwa ukumbusho wa kifo cha Kristo. Nilidhani watu wote wangezikubali kweli nzuri sana za Biblia zilizokuwa zikinifurahisha sana. Lakini nilipoanza kuzungumza makusudi mazuri ya Mungu pamoja na wazazi wangu, jirani zangu, watu wa ukoo na rafiki, wengine walisema nimekuwa mwenda-wazimu. Mume wangu alinikataza nisimtajie habari za Biblia. Mama yangu akaanza kuvaa mavazi meusi kama ishara ya kuomboleza, kama kwamba nilikuwa nimekwisha kufa!
Mambo hayo yote yalinijaribu sana. Hata hivyo niliweka maisha yangu wakf kwa Yehova, na Aprili 11, 1941 nikabatizwa majini, kuonyesha wakf wangu. Nilikata maneno nifanye vile Zaburi 26:1, ZSB inavyosema: “Nimetumainia [Yehova] pasipo kutetemeka” katika ukamilifu wangu.
Nilipokuwa nikipingwa, sikukosa mtu wa kunihurumia. Dada yangu mpenzi Ruth alizikubali kweli za Biblia nilizomweleza. Tulijifunza pamoja huku nikimfundisha kushona, ili tusijulikane tulikuwa tukifanya nini. Nikawa mshona nguo na mwalimu wa kufundisha ushonaji na kutia nakshi, ili niweze kutoka nyumbani nikahubiri watu. Hivyo siku haikupita bila kueleza watu mambo mema yaliyomo katika Neno la Mungu, na hilo ndilo limenifurahisha.
Baadaye wazazi wangu wakanionyesha urafiki tena. Kwa hiyo mwaka 1944 niliwakaribisha wahudhurie kusanyiko “Watangazaji Wenye Umoja” katika Sao Paulo. Nilifurahi walipokubali. Safari ya garimoshi kutoka Rio de Janeiro ilichukua zaidi ya saa kumi na mbili, lakini tulisahau uchovu wa kukalia viti vya mbao tulipoona furaha ya Mashahidi. Tuligawana chakula tukaimba nyimbo za Ufalme mpaka tukawa hoi.
Wazazi wangu walifurahishwa sana na upendo na umoja wa Kikristo uliokuwako, na vilevile programu ya kusanyiko, halafu tuliporudi Rio de Janeiro wakasema wanataka kufunzwa Biblia. Baada ya muda mfupi funzo hilo liliwezesha nyumba yao itumiwe kama mahali pa kukutania wakati wa kuhubiri. Baadaye, kuta fulani za ndani zilibomolewa ili kuwe na Jumba la Ufalme la kundi jipya la Olaria, lililokuwa la pili kuanzwa Rio de Janeiro. Leo nyumba hiyo bado inatumiwa kama Jumba la Ufalme, nalo kundi linafanya maendeleo ya ajabu. Lakini sasa Rio de Janeiro ina jumla ya makundi 95!
KUFUNDISHA WATOTO WANGU
Kweli za Biblia zilinionyesha madaraka mawili ya mke Mkristo, yaani, kumpenda mume wangu na kumheshimu, na kufundisha watoto wangu kanuni za kimungu. Kabla ya kulala nikawa nikiketi na watoto kitandani mwangu na kuwaeleza hadithi za Biblia. Kwa kawaida Noemi alilaza kichwa chake kidogo pajani mwangu. Paulo aliruka-ruka hadithi zilipomfurahisha sana, kama wakati nilipojifanya kuwa Daudi nikinyosha kombeo nimpige Goliathi, au Samsoni nikiangusha nguzo za hekalu la Dagoni. Wakati wote nilijaribu kukazia jinsi watumishi hao waaminifu wa Mungu, pamoja na wengine, walivyokuwa wakamilifu.
Haikuwa vyepesi kuzoeza watoto wangu katika kazi ya kueleza watu habari njema. Hata hivyo Paulo alionekana alikubali sana mazoezi ya Kikristo, akabatizwa akiwa na umri wa miaka kumi na minne. Lakini, alipofika miaka kumi na saba, michezo ilimvuta sana. Alikuwa mcheza mpira hodari katika kikoa cha shule yao, akataka sana awe mchezaji maisha yake yote. Huo ulikuwa wakati wa kufanya uamuzi wa maana, naye aliufanya asubuhi moja ya Jumapili alipokataa kwenda kutoa ushuhuda. Alisema: “Mama, mimi siitaki dini hiyo tena. Hata sijui kama ndiyo kweli.”
Nilipomaliza kushtuka, nilizungumza naye nikamsaidia kunyosha mawazo yake. Leo, anashukuru sana kwamba nilimsaidia, akasema kwamba huo ulikuwa wakati wa maana wa maisha yake. Tangu wakati huo hakurudi nyuma tena. Alisikiliza sana yaliyosemwa mikutanoni, akazipenda kweli za Biblia kwa moyo.
Septemba 1948, watoto wangu walinisaidia nikawa painia, nikahubiri saa zisizopungua 120 kwa mwezi. Binti zangu Elza na Noemi walibadilishana zamu za kupika chakula, naye Paulo akasaidia kazi zote, hata jikoni.
KUPATWA NA MSIBA
Asubuhi moja Noemi nami tulizungumza habari za ufufuo. Watu watafufuliwaje? Nilimweleza kwamba labda wataonekana kama walivyokuwa kabla hawajafa. Sikujua kwamba karibuni imani yangu mwenyewe juu ya ufufuo ingejaribiwa.
Oktoba 5, 1951, karibu na adhuhuri, nilikwenda kufanya ziara nyingine ya kurudia kwa mtu aliyependezwa na Biblia, nikamwambia Noemi arudi nyumbani na rafiki yake Nely. Nilipokwisha rudi nyumbani, Nely alikuja dirishani akipiga mbio akapaza sauti, “Ni Noemi! Amegongwa na gari!”
Nilifanya haraka kwenda hospitalini. Huko njiani nilipita mahali alipogongewa nikaona damu. Noemi alikuwa amegonganishwa na ukuta. Hospitalini, Ndugu Augusto Machado alinifariji sana. Akasema, “Noemi hataabiki tena, amekwisha lala.”
Hotuba ya maziko ilitolewa nyumbani kwetu. Kipaza-sauti kiliwekwa hata mamia ya watu wakaweza kuisikia. Huo ulikuwa ushuhuda mzuri sana juu ya uwezo wa Yehova kufufua watu katika wakati wake mwenyewe. Tena, ilisaidia sana kulainisha moyo wa mume wangu. Ndugu zangu Wakristo walinitia sana moyo kwa kunionyesha upendo na fadhili.
KUENDELEA KUMTUMAINI MUNGU
Miaka mingi mume wangu alinipinga utendaji wangu wa Kikristo. Alinifungia nisiingie nyumbani mwangu mwenyewe, akanitisha kwamba tungetengana kisheria, hata akaniogopesha na bunduki! Ndugu na dada zangu Wakristo, pamoja na watu wa ukoo wangu, walinifariji sana. Lakini zaidi ya yote, nilipata kujua kwamba nguvu zetu za kiroho zatoka kwa Yehova Mungu mwenyewe, ambaye tunapaswa ‘kumtumaini pasipo kutetemeka.’—Zab. 26:1, ZSB.
Baadaye, Paulo aliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko, kama vile wahudumu wenye kusafiri wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Kwanza hakutaka kuniacha peke yangu pamoja na baba yake mwenye kunipinga. Lakini nikamwambia: “Mwanangu, ukimtumaini Yehova, wewe wala mimi hatutakosa cho chote. Yehova atanipa nguvu za kuvumilia.” Leo Paulo bado anatumikia kama mwangalizi wa mzunguko pamoja na mkewe mchangamfu, Tereza. Nasikitika sana kwamba hayupo nami, lakini najua anamtumikia Yehova, kama nilivyotaka afanye sikuzote.
Wakati wenye majaribu magumu zaidi maishani mwangu ulifika mume wangu nami tulipoanza duka la kuoka mikate. Nikawa nikifanya kazi karibu siku nzima ili kulipia unga wa siku inayofuata. Kwa hiyo, nikakosa kuhudhuria mikutano mingi na kupunguza sana kazi yangu ya kutolea watu ushuhuda. Ndugu wengine hata walidhani nimeanza kupenda mali. Mwishowe, tuliweza kuliuza duka hilo la mikate. Lakini, mume wangu alianza kuonekana na dalili za ugonjwa ambao ulimwua baadaye, Novemba 1969. Nikawa peke yangu. Ningefanya nini?
Machi 1, 1970, nilipokuwa na umri wa miaka 57, nilianza jambo jipya maishani. Nikawa painia wa pekee, nikaanza kuzitangaza habari njema saa zisizopungua 150 kila mwezi.
Mgawo wangu wa kwanza pamoja na mwenzangu Felicia Migual ulikuwa Volta Redonda, nasi tuliona kundi jingine likianzwa huko. Halafu tulipewa mgawo twende Para de Minas, mji wenye Ukatoliki mwingi ambako tulitendwa mabaya mengi sana. Wakati mmoja nilishambuliwa upande wa nyuma, nikapigwa ngumi na kuangushwa. Hata hivyo kisa hicho kilinitia nguvu niendelee kusimama imara na kutafuta “kondoo” za Mungu.
Niliwapata katika mji huo. Mmoja wao alikuwa Jose Antonio, kijana aliyekuwa na kiu nyingi ya kweli ya Mungu hata akawa tayari kubatizwa baada ya miezi sita tu ya kujifunza Biblia. Sasa yeye ni mmoja wa wazee katika Kundi la Para de Minas. Mgawo wangu sasa ni Pitangui, mji mdogo ulio karibu na Para de Minas.
Ninapotazama nyuma na kuona miaka ambayo nimetumikia Kikristo, nakumbuka watu wasiopungua 70 ambao nimefurahia kusaidia wakawa Mashahidi Wakristo wa Yehova. Lakini mwisho bado! Naomba Yehova aniwezeshe kwa nguvu zake nyingi niendelee kumtumikia, halafu mwishowe nikafurahie kuuona uso wake mpaka umilele wote.—Ufu. 22:4, 5.
[Picha of Maria Alves de Azevedo on page 428]
[Picha on page 430]
Nimependelewa kupelekea watu wengi ujumbe wa Ufalme