“Habari Njema”—Kwa Siku Zetu Pia!
“MKE wangu alikufa, mimi nikafutwa kazi, television na radio yangu ikaharibika. Nikapatwa na mkasa mbaya nikaumia, nami sasa naumwa sana. Sina tumaini maishani. Nitajiua tu ili nisiwe na shida tena.” Ndivyo mwanamume mmoja alivyomwambia mtu fulani asiyemjua hata kidogo katika Ohio. Ni wazi kwamba mwanamume huyo alihitaji sana “habari njema.” Lakini je! leo kuna “habari njema” zo zote zinazoweza kufariji mtu wa namna hiyo pamoja na mamilioni ya wanadamu wengine wenye taabu?
Kitabu kimoja ambacho kimekuwako muda wa karne nyingi ndicho chenye habari zilizo bora kupita zote. Mamilioni ya watu, pamoja na mwanamume yule aliyekuwa na wasiwasi katika Ohio, wametiwa moyo na kuchangamshwa na ujumbe wake. Kimewapa watu wengi tumaini walipokuwa wamekata tamaa, kisha kikawapa kusudi la uishi. Kitabu hicho kinapendeza watu ulimwenguni pote. “Habari njema” zilizomo zimeandikwa kwa ajili ya “kila taifa na kabila na lugha na jamaa.” (Ufu. 14:6) Basi imefaa kitabu hicho, yaani, Biblia, kikatafsiriwa chote au sehemu yake katika lugha na vilugha zaidi ya 1,575.
SABABU YA KUWAKO “HABARI NJEMA”
Ili kufahamu “habari njema” zilizomo katika Biblia ni nini hasa, tunahitaji kujua sababu inayotufanya tuishi katika ulimwengu wenye magonjwa mengi sana, maumivu, uvunjaji sheria, jeuri na kifo. Hapo tena, Biblia ndiyo inayotueleza sababu. Inatuambia nini?
Mungu hajapata kamwe kukusudia watu wataabike. Muumba, Yehova Mungu, aliwekea wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, taraja la kuishi milele duniani katika paradiso yenye kupendeza. (Mwa. 2:8, 9, 15) Lakini, Mfanyi mwanadamu alipanga uzima wa wanadamu utegemee kufuata sheria. Kwa mfano, lazima mwanadamu apumue, ale na kunywa ili aendelee kuishi. Vivyo hivyo, mwanadamu anahitajiwa atii sheria za Mungu ili aendelee kuishi. Basi, wakati Adamu alipokosa kutii sheria ya Mungu, alipoteza ukamilifu akaweza kuzaa watoto wasiokamilika kwa maana alikuwa mwenye dhambi baada ya hapo. Biblia inasema, “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu Wote wamefanya dhambi.”—Rum. 5:12.
Linalofurahisha ni kwamba, Yehova Mungu alikusudia kukomboa wanadamu katika dhambi na mauti wakati wake mwenyewe. Kabla ya kufanya hivyo, aliruhusu wanadamu wafuate tamaa zao wenyewe wala hakuwazuia wasipate faida zinazotokana na kawaida za maumbile alizoanzisha vizazi vingi vilivyopita, isipokuwa watu wachache tu. Ndiyo sababu mtume Mkristo Paulo aliwaambia yafuatayo Walistra waabudu sanamu. “Zamani zilizopita [Mungu] aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe. Lakini hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.”—Mdo 14:16, 17.
Bila shaka, wafu wakiamua kuipuza dhamiri yao au kupuza kawaida za maumbile kwa upumbavu, watajiletea shida wao wenyewe pamoja na watu wengine. Yehova Mungu haingilii mambo ili kuzuia sheria hii isiyobadilika isitimie: “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Kwa hiyo Aliye Juu Zaidi ameruhusu wanadamu wapatwe na mema na mabaya pia, huku akiwatayarishia mambo anayokusudia kuwapa.
KUKOMBOA WANADAMU
Maandiko yanaonyesha kwamba Yehova Mungu amekwisha weka msingi wa kukomboa wanadamu katika dhambi na mauti. Aliuweka kwa kutoa bei ya kuwakomboa. Alifanya hivyo kwa njia gani na kwa sababu gani?
Wakati Adamu alipoivunja sheria ya Mungu, alijipotezea mwenyewe na watoto wake wasiozaliwa uzima mkamilifu wa kibinadamu. Kwa njia hiyo wanadamu wakaingia katika utumwa wa dhambi na mauti, Bei ya ukombozi ilihitajiwa ili kuikomboa jamaa ya kibinadamu katika utumwa huo. Bei hiyo ilipasa ilingane kabisa na kitu ambacho Adamu alipoteza kwa kutotii, yaani, uzima mkamilifu wa kibinadamu.
Hakuna mwanadamu angeweza kuitoa bei kubwa hiyo, hata kwa kujitahidi sana. Mtunga zaburi anaonyesha kwamba ingalikuwa kazi bure kujitahidi kufanya hivyo, anaposema: “Hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake, (maana fidia ya nafsi zao ina gharama, wala hana budi kuiacha hata milele;) ili aishi sikuzote asilione kaburi.” —-Zab. 49:7-9.
Lakini, Yehova Mungu alifanya mwujiza akakitoa kilichohitajiwa. Alitumia roho takatifu yake, akahamisha uhai wa Mwanawe mzaliwa pekee kutoka mbinguni na kuuingiza katika tumbo la uzazi la Mariamu bikira Myahudi. Kwa njia hiyo huyo aliyepata kuitwa Yesu Kristo angeweza kuzaliwa akiwa ‘mtakatifu,’ bila dhambi. Malaika Gabrieli alionyesha jambo hilo wazi alipokuwa akimwambia Mariamu hivi: “[Roho takatifu itakujilia] juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu iyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.”—Luka 1:35.
Kwa kuwa Yesu alikuwa mkamilifu kama Adamu alivyokuwa alipoumbwa, angeweza kutoa uhai wake uwe dhabihu, na kwa njia hiyo aitoe bei ya ukombozi iliyohitajiwa. Kwa kufanya hivyo alikuwa akijitokeza awatetee wanadamu, ajitwalie mwenyewe adhabu ambayo wanadamu wenye dhambi walistahili kupata, yaani, kifo. Akieleza jambo hilo, mtume Petro aliandika hivi: “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.” (1 Pet. 2:24) Tangu wakati huo wanadamu wamepewa nafasi ya kuzikubali faida za mpango huo wa ukombozi, huku wakiyafuata masharti yaliyowekwa na Mungu.
UTAWALA WENYE HAKI UTAIBADILI DUNIA
Huko nyuma katika karne ya kwanza W.K., walioukubali mpango wa Mungu wa wakovu walipata nafasi ya kuweza kushirikiana na Yesu Kristo wakiwa makuhani-wafalme baada ya kumaliza maisha yao duniani kwa uaminifu, na kufufuliwa wapewe uzima wa mbinguni hata wasiweze kufa kamwe. Biblia inasema yafuatayo juu ya wale wanaochaguliwa wakawe warithi wenzi wa Kristo: “Heri, na mtakatifu, ni yeye aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hao mauti ya pili haina nguvu; bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu.”—Ufu. 20:6.
Basi, muda wa karne nyingi Mungu amekuwa akichagua watu watakaofanya kazi kama wafalme na makuhani pamoja na Mwanawe. Wale, wanaochaguliwa lazima watimize mambo yafuatayo, kulingana na uwezo wao wa kibinadamu: “Katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa.” (Ufu. 14:5) Watumishi waaminifu wa Mungu, waliojaribiwa, ndio wangeweza kuruhusiwa peke yao washiriki daraka zito la kurudishia wanadamu ukamilifu. Watashiriki kutumia faida za dhabihu ya Yesu walipie dhambi za wanadamu duniani, kama vile makuhani wa Israeli ya kale walivyotoa dhabihu za wanyama ili kulipia dhambi za watu.
Kwa hiyo Yehova Mungu atamtumia Yesu Kristo na makuhani-wafalme wenzake aitimize ahadi hii iliyo nzuri sana: “Naye atafuta kila chozi katika macho yao, Wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufu. 21:4.
Hizo ni “habari njema” weee! Utawala wa Yesu Kristo na wenzake utakomboa wanadamu kabisa katika mambo yote ambayo yamefanya maisha duniani yasipendeze. Kuondolewa kwa maumivu yote yasiyofaa kutamaanisha kwamba hata uhalifu, umaskini, jeuri, udhalimu, uonezi na njaa zitaondolewa. Magonjwa na uzee wenye kudhoofisha watu yataondolewa pia. Wanadamu wote watafurahia nguvu za ujana. Watu hawataona uchungu mwingi tena wakitiririsha machozi kwa sababu ya taabu wala kifo. Kwa sababu ya mambo yatakayotimizwa, tunaweza kufahamu sababu inayofanya Biblia izitaje ‘habari njema za ufalme.’—Mt. 24:14, NW.
Hata hivyo, jambo lenye kushangaza ni kwamba hizo ni “habari njema” kwa wakaaji wote wa dunia. Maandiko Matakatifu yanaonyesha kwamba ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Kristo ungekuwa na adui wengi na kwamba mataifa yangependelea kujitawala yenyewe. Lakini, watakuwa wamefanya kazi bure kujipanga waupinge ufalme wa Mungu. Unabii wa Danieli unatuambia hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Dan. 2:44) Naam, watawala wa kibinadamu pamoja na watu wote wanaowaunga sana mkono watashindwa kabisa na “MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA,” Yesu Kristo,—Ufu. 19:11-16.
Uharibifu wao utakuwa mkubwa sana hata ulingane na maelezo ya Biblia yanayosema kwamba kutakuwako “wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.” (Dan. 12:1) Ijapokuwa hiyo ‘dhiki kubwa’ itaogopesha sana watu itawafariji sana watu wote wanaotaka kikweli kuwa raia za ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Kristo. (Ufu. 7:14) Maandiko yanatuhakikishia hivi: ‘Yehova anajua jinsi ya kukomboa watu wa utawa katika jaribu, lakini kuhifadhi watu wasio haki kwa ajili ya siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.” (2 Pet. 2:9, NW) Katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo tunafahamu kwamba waokokaji Mtakuwa wengi. Wanasimuliwa kuwa “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.”—Ufu. 7:9.
Ndipo waokokaji hao, kutia na watoto wengi, watakapotawalwa moja kwa moja na Yesu Kristo. Atawahangaikia na kuwahurumia kama vile unabii unavyosema juu yake: “Atamwokoa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.” (Zab. 72:12-14) Vilevile watakuwa na pendeleo la kusaidiwa naye waondoe udhaifu wao mbalimbali na makosa yao ya kutokamilika, kisha mwishowe wasimame mbele za Aliye Juu Zaidi wakiwa wanadamu wasio na dhambi. Ufunuo 7:17 unaonyesha jambo hilo unaposema kwamba Mwana-Kondoo, Kristo Yesu, “atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai.”
Namna gani wale wanaokufa kabla ya hiyo ‘dhiki kubwa’ kuharibu adui wote wa ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Kristo? Watapewa nafasi ya kupata faida za dhabihu ya Kristo kwa kufufuliwa kwa wafu. Ebu waza jinsi waokokaji wa dhiki hiyo watakavyoshangilia wawakaribishapo watu hao kutoka kwa wafu—wanaume, wanawake na watoto—kwa utimizo wa maneno haya ya Yesu: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.
HAYO YATATOKEA LINI?
Habari zenye kutusisimua siku zetu ni kwamba ufalme wa Mungu unakaribia sana kuanza kusimamia mambo ya dunia. Kwa mfano, angalia vile Biblia inavyosema juu ya hali ambazo zingeonyesha kwamba “siku za mwisho” wa taratibu ya mambo isiyomcha Mungu zimefika: “Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake.”—2 Tim. 3:1-5.
Vivyo hivyo, Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake kwamba wangekombolewa wakati ambao kungekuwa na hofu nyingi na wasiwasi kati ya mataifa. Baada ya kusema kwamba dunia ingekuwa na “dhiki ya mataifa wakishangaa,” Yesu aliongeza maneno haya yenye kututia moyo: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” Ndipo alipoeleza maana ya maneno yake kwa kutoa mfano huu: “Utazameni mtini na miti mingine yote. Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu. Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie.”—Luka 21:25-32.
Je! si tumekwisha ona mambo hayo yaliyotabiriwa katika Biblia? Basi, je! hatuna sababu nzuri ya kutazamia ukombozi karibuni? Naam, maana yake ni kwamba wako watu walio hai leo ambao huenda wakauona mwisho wa taratibu hii isiyomcha Mungu, pamoja na udhalimu na uonezi uliomo ndani yake. Wale ambao huenda wakafa kabla ya wakati huo hawatazikosa baraka zinazoweza kuletwa na ufalme wa Mungu peke yake unaosimamiwa na Kristo, yaani, kukombolewa kabisa katika magonjwa, maumivu na kifo. Madhara yo yote waliyopata katika taratibu hii yataondolewa wafufuliwapo wawe na taraja la kuishi milele.
Hakika Biblia ina “habari njema” kwa siku zetu. Tunatiwa moyo namna gani kujua kwamba karibuni dunia hii itakuwa na amani, iwe paradiso ipendezayo, isiyo na magonjwa, maumivu wala kifo!