Milki ya Wamedi na Waajemi Katika Unabii
MATUKIO yaliyotukia katika historia kuhusu mamlaka kuu zilizotawala sehemu kubwa za dunia hayakutukia vivi hivi tu bila mpango. Kuna Mtu fulani ambaye mara nyingine amejiingiza katika mambo ya kibinadamu, kisha kukawa na mabadiliko makubwa sana katika hali ya ulimwengu. Mtu huyo, yaani, Yehova Mungu, aliwatumia manabii wake kutabiri mapema sana juu ya kutokea na kuanguka kwa milki fulani.
Kutimizwa kabisa kwa unabii mbalimbali wa Biblia zamani zilizopita kunatupa msingi imara leo wa kuliamini neno hilo la unabii kuhusu matukio ya wakati ujao. Jambo la maana zaidi ni kwamba, linaweza kututia sana moyo tuishi kupatana na kusudi la Mungu, tukiwa na hakika kwamba ‘atalithibitisha neno la watumishi wake.’—Isa. 44:26.
Kitabu cha Danieli kinajulikana sana kwa sababu kina unabii mwingi. Yosefo, yule mwanahistoria Myahudi wa kale wa karne ya kwanza W.K., alivutwa hata akaandika hivi: “Mambo hayo yote ambayo Mungu alimfunulia aliyaacha katika maandishi yake, ili wale wanaoyasoma na kuona jinsi yalivyotimia ashangae juu ya vile Mungu alivyompa Danieli pendeleo kubwa.”
Mmoja wa unabii mwingi wa ajabu ulioandikwa na Danieli unahusu Milki ya Wamedi na Waajemi. Katika sura ya nane ya kitabu chake, Danieli anasimulia njozi fulani ambamo Milki ya Wamedi na Waajemi inafananishwa na kondoo wa kiume. (Dan. 8:20) Tunasoma hivi: “Tazama, mbele ya mto alisimama kondoo mume, mwenye pembe mbili; na pembe zile mbili zilikuwa ndefu; lakini moja ilikuwa ndefu kuliko ya pili, na ile iliyokuwa ndefu zaidi ilizuka mwisho.”—Dan. 8:3.
Hiyo maana yake nini? Kama inavyoonekana wazi kutokana na Danieli 8:21, 22, pembe zinafananisha wafalme au falme. Andiko hilo linasema: “Yule beberu, mwenye manyoya mengi, ni mfalme wa Uyunani [Ugiriki]; na ile pembe kubwa iliyo kati ya macho yake ni mfalme wa kwanza. Tena katika habari ya pembe ile iliyovunjika, ambayo badala yake zilisimama pembe nne, falme nne zitasimama kutoka katika taifa lile, lakini si kwa nguvu kama zake.”
Kwa hiyo, kwa kuwa pembe ya pili ya yule kondoo wa kiume ilitokea baadaye ikawa ndefu kuliko ile nyingine, huo ulikuwa utabiri wenye kuonyesha kwamba katika Milki ya mwungano wa Wamedi na Waajemi utawala wa Waajemi ndio ungepanda uupite ule mwingine wa Wamedi. Je! jambo hilo lilitukia?
Naam, lilitukia kama historia inavyohakikisha. Hapo kwanza Wamedi ndio waliokuwa na cheo cha kutawala. Lakini, Koreshi (wa Pili) alipokikalia kiti cha Anshan, aliunganisha majeshi ya Waajemi akajaribu kuwaondoa katika utawala wa Wamedi. Katika mwaka 550 K.W.K. Wamedi walisimamiwa na Astyagesi (Ishtumegu) nao Waajemi wakasimamiwa na Koreshi ili wapigane. Jeshi la Astyagesi lilimwasi likamtia pingu na kumpeleka kwa Koreshi. Baada ya hapo Koreshi aliukamata mji mkuu wa Umedi, yaani, Ekbatana. Tangu wakati huo Umedi ukawa katika cheo cha pili katika Milki ya mwungano wa Wamedi na Waajemi.
Ingawa sasa Wamedi walikuwa wametiishwa sana, Umedi na Uajemi uliungana ukawa mamlaka ya ulimwengu, kwa hiyo mamlaka hiyo ingeweza kufananishwa na kondoo wa kiume. Ni kama vile Danieli 8:20 inavyoeleza: “Yule kondoo mume uliyemwona, mwenye pembe mbili, hizo ndizo wafalme wa Umedi na Uajemi.” Kikieleza juu ya mwungano wa milki hiyo, kitabu History of the Persian Empire (Historia ya Milki ya Uajemi) cha Mtaalamu Olmstead kinasema hivi (ukurasa wa 37): “Uhusiano mwingi sana kati ya Waajemi na Wamedi haukusahauliwa kamwe. Mji Ekbatana uliotekwa nyara uliendelea kupendelewa uwe makao ya kifalme. Wamedi na Waajemi waliheshimiwa sawasawa; waliandikwa katika vyeo vikubwa tena walichaguliwa waongoze majeshi ya Kiajemi. Kwa kawaida watu wa mataifa mengine waliwataja Wamedi na Waajemi pamoja [kama vile Biblia inavyowataja pamoja kwa kawaida].”
Akiendelea na masimulizi yake juu ya yule kondoo wa kiume, Danieli anasema hivi: “Nikamwona huyo kondoo mume akisukuma upande wa magharibi, na upande wa kaskazini, na upande wa kusini; wala hakuna mnyama ye yote awezaye kusimama mbele yake, wala hakuna mnyama ye yote awezaye kupokonya mkononi mwake; lakini alitenda kama alivyopenda mwenyewe, akajitukuza nafsi yake.” —Dan. 8:4.
Hakuna mamlaka iliyoweza kusimama mbele ya Milki ya Wamedi na Waajemi wakati ilipokuwa imesitawi sana. Mfalme Koreshi alisonga upande wa kaskazini akauteka Babeli mwaka 539 K.W.K. Kambise mwanawe alielekea kusini akaishinda Misri. Dario wa Kwanza alishinda maeneo mengi na kuelekea magharibi, akaishinda Thrake na Makedonia.
Lakini, baadaye Milki ya Wamedi na Waajemi iliangushwa na mamlaka ya ulimwengu ya Ugiriki. Jambo hilo lilikuwa limekwisha tabiriwa katika unabii wa Danieli unaosema hivi: “Nami nilipokuwa nikifikiri, tazama, beberu akatoka upande wa magharibi, juu ya uso wa dunia nzima, bila kuigusa nchi; na beberu yule alikuwa na pembe mashuhuri kati ya macho yake. Naye akamwendea huyo kondoo mume mwenye pembe mbili, niliyemwona akisimama karibu na mto, akamshambulia kwa ghadhabu za nguvu zake. Nikamwona akimkaribia kondoo mume, akamwonea hasira kali, akampiga kondoo mume, akazivunja pembe zake mbili; na huyo kondoo mume alikuwa hana nguvu kusimama mbele yake; bali akamwangusha chini, akamkanyaga-kanyaga; wala hapakuwapo awezaye kumwokoa kondoo mume katika mkono wake.”—Dan. 8:5-7.
Kwa utimizo wa maneno hayo, mamlaka ya ulimwengu iliyofananishwa na yule kondoo wa kiume iliangushwa na Aleksanda Mkuu, aliyefananishwa na ile “pembe mashuhuri.” Inafaa kujua kwamba mbuzi alikuwa akitumiwa kama ishara ya kuifananisha Mamlaka ya Ulimwengu ya Ugiriki na Makedonia. Kamusi ya Biblia The Imperial Bible-Dictionary (Vol. 1, uku. 664) inatuambia hivi: “Kungali kuna mijengo ya ukumbusho yenye ishara hiyo, kwa mfano nguzo moja ya Persepolisi, yenye sanamu ya mbuzi mwenye pembe kubwa sana katika kipaji cha uso, pembe hiyo ikiwa imeshikwa na Mwajemi mmoja, kuonyesha vile Uajemi ulivyoitiisha Makedoni.” Lakini, kama Danieli alivyotabiri, utawala ambao Uajemi ulikuwa nao juu ya Makedonia ungekwisha. Kwa utimizo wa unabii huo, yule “kondoo mume,” yaani, Milki ya Wamedi na Waajemi, aliangushwa na “beberu” (mbuzi wa kiume), yaani, Milki ya Ugiriki.
Kwa kuwa unabii ulitimizwa mara hiyo, ni hekima tuchunguze yanayosemwa na Biblia juu ya matukio ya wakati ujao. Hapo tu ndipo tutakapoweza kuhakikisha kwamba maisha yetu yanapatana na lile neno la unabii. Tunahitajiwa sana tufanye hivyo ndipo tuweze kupata kibali na baraka za Mungu.—2 Pet. 1:19-21.