Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 1/1 kur. 8-10
  • Mzee Aliyepata Thawabu kwa Sababu ya Imani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mzee Aliyepata Thawabu kwa Sababu ya Imani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Alitimiza Tamaa ya Moyo Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Mtoto Aliyeahidiwa
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Mtoto wa Ahadi
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Mtoto wa Ahadi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 1/1 kur. 8-10

Mzee Aliyepata Thawabu kwa Sababu ya Imani

WATU walikuwa wakitazamia sana jambo fulani. Tukio lililokubwa zaidi katika historia ya kibinadamu lilikuwa likikaribia. Lilikuwa limetabiriwa kame nyingi mapema. Tukio gani hilo? Ni kutokea kwa Masihi, au Kristo.

Unabii wa Danieli ulionyesha kwamba Masihi angefika juma 69 za miaka baada ya kutolewa amri ya kujenga upya kuta za mji wa Yerusalemu. (Dan. 9:25) Wakati huo ungefika katika mwaka ambao sasa unajulikana kama 29 W.K., tukihesabu tangu wakati Nehemia alipozijenga upya kuta hizo.

Basi karibu na mwisho wa karne ya kwanza K.W.K. Wayahudi wazee hawakuwa na tumaini kubwa la kuishi muda wa kutosha waweze kuona utimizo wa tukio walilotazamia sana kuhusu Masihi. Lakini wako wanaume na wanawake fulani wazee waliotazamia tukio hilo kwa imani na shauku nyingi. Mmoja wao alikuwa Simeoni. Biblia inamtaja kuwa “mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli.” (Luka 2:25) Ingawa ni hakika kwamba Simeoni alikufa kabla Yesu hajatiwa mafuta na roho ya Mungu na kuwa Masihi au Kristo aliyeahidiwa, alipata thawabu kwa sababu ya kuwa na imani isiyotikisika kwamba Masihi angekuja. Kwa njia gani?

Yehova Mungu aliiona imani nyingi sana ya Simeoni akampa ufunuo wa pekee. Aliye Juu Zaidi alitumia roho yake kumjulisha kwamba asingekufa kabla ya kumwona Kristo. (Luka 2:26) Lilikuwa taraja zuri namna gani!

Siku moja, roho ya Mungu ilimwezesha Simeoni kuja katika eneo la hekalu. Papo hapo wakatokea pia mume na mke maskini wakiwa na kitoto kichanga. Wakitazamwa kwa nje, mwanamume huyo, mkewe na kivulana chao walionekana kuwa watu wasio wa maana sana. Hali yao ilionekana kuwa ya kawaida tu, kwa sababu mama ye yote Myahudi alitakiwa na sheria atoe dhabihu mwishoni mwa siku 40 za kipindi cha utakaso baada ya mtoto mwanamume kuzaliwa.​—Luka 2:27.

Lakini, jambo la maana sana lilitukia wakati huo, jambo ambalo Simeoni aliliona kama thawabu ya imani yake. Alijulishwa maana kamili ya jambo hilo kupitia kwa roho takatifu. Kitoto hicho kichanga ndicho kilichokusudiwa kuwa Masihi, yule Kristo. Simeoni alifurahi akakishika kitoto hicho mikononi mwake, kisha akaongozwa na roho ya Mungu kusema hivi: “Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, kwa amani, kama ulivyosema; kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, uliouweka tayari machoni pa watu wote; nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.”​—Luka 2:29-32.

Simeoni alijisikia akiwa na amani kwa sababu ya pendeleo alilopewa. Alijua kwa uhakika kwamba sasa Mungu alikuwa ameleta mpango wake mzuri sana wa wokovu. Alikiona kitoto hicho kichanga kwa macho yake mwenyewe, akakishika kwa mikono yake mwenyewe. Unabii ambao Simeoni alitoa kwa kusema kwamba hata mataifa yaliyokuwa katika giza la kutomjua Mungu na kutenda dhambi yangepata nuru ulipatana kabisa na Maandiko ya Kiebrania. Kwa mfano, kwa habari ya “mtumishi” aliye Masihi, Isaya 42:6 inasema hivi: “Mimi, [Yehova], nimekuita katika haki, nami nitakushika mkono, na kukulinda, na kukutoa uwe agano la watu, na nuru ya mataifa.”

Baada ya hapo, Simeoni aliwabariki Yusufu na Mariamu, akawatakia baraka ya Mungu wanapotimiza wajibu wao wa kukitunza kitoto hicho. Akisema habari ya Mariamu hasa, Simeoni aliendelea kusema hivi: “Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.” (Luka 2:34, 35) Naam, kutokea kwa Masihi kungebadili watu wake mwenyewe kwa njia mbalimbali.

Kama ilivyokuwa imeonyeshwa mapema katika unabii, watu wengi wangejikwaa juu yake, waendelee kukaa katika hali ya kutotubu na kutoamini. Nabii Isaya aliandika maneno haya: “Naye atakuwa . . . jiwe la kujikwaza na mwamba wa kujikwaa kwa nyumba za Israeli zote mbili, na mtego na tanzi kwa wenyeji wa Yerusalemu. Na wengi watajikwaa juu yake, na kuanguka na kuvunjika, na kunaswa na kukamatwa.” (Isa. 8:14, 15) Kwa watu wasioamini, Yesu angekuwa kama “ishara” au kitu cha dharau, mtu wa kutukanwa na kulaumiwa. Lakini, watu wengine ‘wangeinuliwa’ watoke katika hali ya kuwa wafu katika makosa na dhambi kwa sababu ya kumwamini, kisha wafurahie msimamo wenye haki pamoja na Mungu.

Matendo ambayo watu wangefanyia Masihi yangefunua kabisa mambo yaliyokuwa mioyoni mwao. Ni kama vile Simeoni alivyosema: “Ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.”​—Luka 2:35.

Mariamu angehuzunika sana kwa sababu Yesu angekataliwa na watu wengi. Simeoni alitaja jambo hilo, akasema: “Upanga utaingia moyoni mwako.” (Luka 2:35) Looo! jinsi Mariamu alivyoumia moyoni kumwona Yesu amegongomewa misumari mtini kama mhalifu mbaya sana! Alikuwa kama kwamba amechomwa kwa upanga.

Hakika Simeoni alipendelewa kwa kuweza kukiona kitoto kichanga Yesu, na kuongozwa na Mungu atoe unabii ambao ungemtia Mariamu nguvu aonapo mwanawe mzaliwa wa kwanza akitendwa udhalimu huo.

Inatupasa sisi leo tutiwe imani nguvu kwa kuangalia jinsi Mungu alivyoshughulika na Simeoni. Huenda mtu akakosa kuona utimizo aliotazamia sana wa ahadi za Yehova muda wa maisha yake. Hata hivyo, anaweza kuwa na hakika kwamba Aliye Juu Zaidi hatasahau jinsi amejitahidi kumtumikia kwa uaminifu. Baraka zo zote na uongozi atakaopokea muda wa maisha yake zitakuwa za kutosha kumhakikishia kwamba atafufuliwa kwa wafu, awe na tumaini la kuishi milele.

Mungu asiye na kigeu-geu anaangalia sana watumishi wake waaminifu leo kama alivyomwangalia Simeoni. Hivyo, Biblia inatuhimiza kwa kutuambia: “Huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.” (1 Pet. 5:7) Tunaweza kutazamia kupata thawabu kubwa kama Simeoni kwa sababu ya imani yetu. Jambo hilo linatutia sana moyo tuendelee kuishi kupatana na tumaini tulilopewa na Mungu, tuwe ‘wenye haki na wacha Mungu’ kama Simeoni.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki