Je! Inafaa Wafu Wo Wote Wawe Rafiki Zako?
WEKA kipande cha dhahabu pamoja na kingine cha fedha. Visonganishe pamoja kisha uviache vikae hivyo miezi kadha. Halafu vitenganishe. Utaona nini? Utaona sehemu fulani ya dhahabu katika fedha na sehemu fulani ya fedha katika dhahabu’ Imekuwaje?
Vimechanganyika kwa sababu ya kuwa karibu karibu.
Huo ni mfano mzuri wa kanuni moja ya Biblia. Wenzi wa mtu humbadili. Kama vile fedha ingeweza kuonekana katika kipande cha dhahabu na dhahabu katika kipande cha fedha baada ya kukaribiana kwa muda, ndivyo rafiki zako wanavyokupa tabia zao.
Mtume Mkristo Paulo alisema: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Kor. 15:33, NW) Paulo alikuwa akieleza habari za tumaini la ufufuo. Mtume alitaja ufufuo wa Yesu Kristo kuhakikisha kwa uthabiti mwingi sana kwamba Mungu aweza kufufua wafu. (1 Kor. 15:12-32) Lakini watu fulani walikuwa wakilikataa fundisho hilo. Kwa hiyo, mtume alieleza kwamba “mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri” kisha akahimiza hivi: “Tumieni akili kama ipasavyo, wala msitende dhambi; kwa maana wengine hawamjui Mungu. Ninanena hayo niwafedheheshe.” (1 Kor. 15:34) Wale walioandikiwa na Paulo barua iliyoongozwa na Mungu walipaswa kuamka katika usingizi wa fundisho baya, lililokuwa likipotoa wengine, kuwalaza na kuwaua kiroho. Kwa sababu gani ilikuwa hivyo? Kwa sababu walikuwa wakishirikiana na wenye kufundisha fundisho la uongo.
Ni wazi, basi, kwamba haifai watu wo wote wawe rafiki zako. Hali ya mtu ya kiroho inaweza kuharibiwa sana na watu anaochagua wawe rafiki zake. Lakini, yeye anaweza kuharibiwa katika mambo mengine pia.
Sulemani mwenye hekima alisema: “Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi; wala usiende na mtu wa ghadhabu nyingi.” Kwa sababu gani? “Usije ukajifunza njia zake; na kujipatia nafsi yako mtego.” (Mit. 22:24, 25) Mtu akishirikiana na mwingine mwenye hasira-hasira anaweza kuwa kama yeye kabisa. Huo unakuwa mtego, kwa maana anaingizwa katika mabishano, dhambi na mambo mbalimbali yasiyofaa.
Kwa hiyo, rafiki za mtu wanaweza kumbadili kwa njia nyingi. Si kwamba tu wanaweza kumharibia hali ya kiroho; wanaweza pia kumshawishi awe na tabia mbaya sana. Mambo yote hayo mawili yanaweza kumharibia Mkristo maisha yake.
Kwa upande mmoja, kushirikiana na wenye kufundisha fundisho la uongo na kukubali maoni yao kwaweza kufanya mtu apoteze uhusiano unaopendelewa na Mungu na kumfanya afukuzwe katika kundi la Kikristo kama mwasi imani. Kwa upande mwingine, mtu anayefuata maongozi mabaya na kuiga mwingine mwenye kukasirika-kasirika atajiletea ole. Huenda akaharibu uhusiano wake na Yehova Mungu na kundi la Kikristo. Hata iweje, watu wataacha kumheshimu, kwa maana Andiko latuambia: “Mwenye rehema huitendea mema nafsi yake; aliye mkali hujisumbua mwili wake.”—Mit. 11:17.
Tena, huenda mtu akaingizwa katika mwendo wa upumbavu au msiba kwa sababu anashirikiana na wapumbavu. Sulemani alisema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia”—Mit. 13:20.
Hapa neno la Kiebrania linalosema ‘mpumbavu’ halina maana ya mtu asiye na maarifa. Bali, linamaanisha kwamba “wapumbavu” hao hawataki kufuata adili zinazofaa. Wao ni watu wasiomcha Mungu. Kwa hiyo, yasemwa hivi katika Mithali 13:19: “Kujitenga na maovu ni chukizo kwa wapumbavu.” Ni wazi kwamba mtu mwenye kumcha Mungu asingetaka “wapumbavu” hao wasiomcha Mungu wampake njia zao.
Mkristo anakuwa mwenye hekima anapotii shauri lililomo katika maneno yanayosema kwamba, “enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima” (Mit. 13:20) “Wenye hekima” hao hawatambulishwi waziwazi hapa. Lakini, mahali penginepo twaambiwa hivi: “Kumcha [Yehova] ndio mwanzo wa hekima.” (Zab. 111:10) Kwa hiyo, waabudu wa Mungu wa kweli, wale ‘wanaomcha Yehova’ inavyofaa, ndio wenye hekima hasa ambao mtu apaswa kushirikiana nao.
Pana tofauti kubwa sana kati ya kushirikiana na wasiomcha Mungu na kushirikiana na wale wanaofuata ibada ya kweli! Ijapokuwa mwalimu wa fundisho la uongo aweza kuingiza mtu katika uangamivu wa kiroho, kushirikiana na wenye kumcha Mungu kwa kujifunza Biblia kunatutia nguvu za kiroho:. Mit. 11:9.
Tena: ijapokuwa kushirikiana na mtu “mwenye hasira nyingi” kunaweza kukuharibu, kufanya urafiki na watu wanaomcha Yehova kutakufaidi. Kwa njia gani? Utachochewa usitawishe matunda ya roho ya Mungu, zile sifa halisi za Kikristo, upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza.—Gal. 5:22, 23, NW.
Kama vile rafiki na wenzi wa mtu wanavyombadili sana, ndivyo kuhusiana sana na Yehova Mungu tukiwa watumishi Wake walio wakf kunavyotubadili sana, na sikuzote kunatuletea mema. Tena, tutapata furaha sikuzote kwa ‘kwenda na Mungu’ kwa unyenyekevu. (Mik. 6:8) Mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alisema: “Heri kila mtu amchaye [Yehova], aendaye katika njia yake.”—Zab. 128:1.
Bila shaka hakuna hatari ya kuwa na tabia mbaya tunapotembea na Mungu, kwa maana “[Yehova] ndiye mwenye haki, apenda matendo ya haki.” (Zab. 11:7) Mungu hutumia Neno Lake na roho yake takatifu kuwapa hekima wale wanaoitaka, nao wanakuwa wenye hekima kikweli. Tena, matokeo yanakuwa yenye kupendeza sana. Asema mwenye hekima, “Kwa sababu [Yehova] Mungu humpa yeye aliyemridhia hekima na maarifa na furaha.”—Mhu. 2:26.
Naam, haifai watu wo wote wawe rafiki zako. Wanakubadili kama dhahabu na fedha zinavyobadiliana zikiwa karibu karibu. Basi, ni hekima sana kuepuka washiriki wabaya na kujaribu kushirikiana na watu wanaomcha Mungu! Jambo linalofaa hasa ni kuhusiana sana kwa njia ya urafiki pamoja na Yehova, ‘atoaye hekima na maarifa na furaha.’