Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 2/15 kur. 20-23
  • Je! “Agano la Kale” Ni la Maana kwa Wakristo Leo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! “Agano la Kale” Ni la Maana kwa Wakristo Leo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “IMEANDIKWA”
  • “KAMA MNGALIJUA MAANA YAKE”
  • “ILI LITIMIE”
  • ‘UKOMBOZI MKUU ZAIDI’
  • “Yaliandikwa Ili Kutufundisha Sisi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Funzo Namba 10—Biblia Asilia na Kweli
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Ukristo—Je! Yesu Alikuwa Ndiye Njia ya Kuongoza kwa Mungu
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 2/15 kur. 20-23

Je! “Agano la Kale” Ni la Maana kwa Wakristo Leo?

BIBLIA takatifu ndicho kitabu kinachouzwa zaidi ya kitabu kingine cho chote ulimwenguni pote. Kimepenya katika kila nchi ya dunia na kinasomwa na watu wa mataifa yote. Biblia yote au sehemu yake inapatikana leo katika lugha zaidi ya 1,575.

Kulingana na mgawanyo ulio wa kawaida sana wa vile vitabu 66 vya Biblia, zaidi ya nusu yavyo vinafanyiza liitwalo “agano la Kale.” Mkusanyo huu wa Maandiko, ulioandikwa katika Kiebrania na Kiaramu, ulimalizwa kuandikwa yapata miaka 443 kabla ya Wakati wa Kawaida. Je! Wakristo wanahitaji kujifunza Maandiko ya Kiebrania leo?

Ikiwa wewe unafurahia kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo kwa kawaida huitwa “Agano Jipya,” inaelekea umeona namna waandikaji wa Biblia Wakristo walivyotaja au kuelekeza kwenye Maandiko ya Kiebrania. Waliyaona maandishi hayo kuwa yenye maana kubwa sana kwa Wakristo. Kwa habari ya maandishi ya kihistoria juu ya namna Mungu alivyowatendea Waisraeli wa kale, mtume Paulo aliandika hivi: “Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi.”​—1 Kor. 10:11.

Licha ya historia yenye maana, ndani ya Maandiko ya Kiebrania mna mamia ya unabii wa matukio ya wakati ujao. Je! haya yaliandikiwa Wayahudi tu walioishi karne nyingi kabla ya Wakati wa Kawaida? Hata kidogo. Mtume Petro anasema hivi juu ya manabii Waebrania:

“Wakatafuta ni wakati upi, na wakati wa namna gani ulioonywa na Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao, ambaye alitangulia kuyashuhudia mateso yatakayompata Kristo, na utukufu utakaokuwako baada ya hayo. Wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni.”​—1 Pet. 1:11, 12.

Kati ya vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kijulikanacho sana kwa sababu ya kutaja mara nyingi sana “Agano la Kale” ni kitabu cha Waebrania. Juu ya hili, mwanachuo wa Biblia B.F. Westcott anasema hivi:

“Mawazo kadha yanajitokeza mara moja kwa mwanafunzi anayeifikiria mitajo hii kwa ujumla. (1) Inadhaniwa kwamba shauri fulani la Kimungu lilitenda kazi katika muda wa maisha ya Israeli. Katika ‘watu wa Mungu’ tunaonyeshwa ishara za kusudi la Mungu kwa wanadamu. Historia yote ni ya kiunabii. Haitoshi kufahamu kwamba [Agano la Kale] lina unabii mwingi: [Agano la Kale] ni unabii mmoja mkubwa sana.”

Tukikumbuka hili tutajifunza mengi tukiona namna Yesu na waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walivyoyataja na kutumia maandishi hayo ya Biblia yaliyoongozwa na Mungu yaliyotangulia Ukristo.

“IMEANDIKWA”

Bila shaka unafahamiana sana na masimulizi ya Injili ya namna Yesu ‘alivyojaribiwa na Ibilisi.’ (Mt. 4:1-11; Luka 4:1-13) Yesu alijibuje katika hali hii yenye kujaribu? Angalia majibu yake kwa yale majaribu matatu:

“Naye akajibu akasema, Imeandikwa, Mfu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha [Yehova]. [Kum. 8:3]. . . Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu [Yehova] Mungu wako. [Kum. 6:16]. . . Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie [Yehova] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. [Kum. 6:13].”​—Mt. 4:4, 7, 10.

Msingi wa matendo ya Yesu ulikuwa Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na Mungu, kwa kuwa alijua kwamba yalikuwa na maoni ya Mungu juu ya mambo. Jambo jingine linalopendeza, vilevile, ni namna Yesu alivyotoa sababu wakati Mafarisayo fulani ”‏[walipofanya] shauri, jinsi ya kumtega kwa maneno yake”:

“Na Mafarisayo walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mwaonaje katika habari za Kristo? Ni mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi katika Roho kumwita Bwana, akisema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwawekapo adui zako kuwa chini ya miguu yako? [Zab. 109:1, Septuagint (110:1, Kiebrania)] Basi, Daudi akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala hakuthubutu mtu ye yote tangu siku ile kumwuliza neno tena.”​—Mt. 22:15, 41-46.

Yesu na wanafunzi wake walikuwa wamefahamiana sana na “Agano la Kale,”‏ hivi kwamba nyakati nyingine waliweza kuthibitisha jambo fulani juu ya fundisho fulani la Kikristo ama kwa kutaja moja kwa moja kutoka kumbukumbu lao ama kwa kueleza kwa kutumia maneno machache kutoka kwa Maandiko mengi. Kwa mfano, tunasoma hivi katika Warumi 3:9-18:

“Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na na [Wagiriki] ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; hakuna mtenda mema, la! hata mmoja. [Zab. 13:1-3, Septuagint (14:1-3, Kiebrania)] Koo lao ni kaburi wazi, kwa ndimi zao wametumia hila. [Zab, 5:9] Sumu ya fira i chini ya midomo yao. [Zab. 139:3, Septuagint (140:3, Kiebrania)] Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu. [Zab. 9:27, Septuagint (10:7, Kiebrania)] Miguu yao ina mbio kumwaga damu. Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. Wala njia ya amani hawakuijua. [Isa. 59:7, 8] Kumcha Mungu hakupo machoni pao. [Zab. 35:1, Septuagint (36:1, Kiebrania)].”​—Mitajo yote ya Septuagint inatoka Chapa ya Bagster.

Matumizi haya ya Maandiko ni mfano bora kwa kila mtu anayetamani kumpendeza Mungu. Mtume Petro aliandika kwamba Wakristo wapaswa wawe ‘tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yao.’ (1 Pet. 3:15) Namna gani juu ya ufahamu wako wa Neno la Mungu lililoandikwa? Ikiwa mtu angeuliza juu ya imani yako ya kidini, je! ungetoa “sababu” za Maandiko?

“KAMA MNGALIJUA MAANA YAKE”

Ijapokuwa vitabu vitano vya kwanza vya Biblia vina torati ya Musa pamoja na mamia ya amri zake, Maandiko ya Kiebrania ni zaidi ya amri tu. Kujifunza kwa uangalifu Maandiko haya yaliyotangulia Ukristo kunaweza kuwasaidia watu wageuze njia zao za kufikiri zipatane na njia ya Muumba. Ebu lifikirie jambo hili lililompata Yesu:

“Wakati ule Yesu alipita katika mashamba siku ya sabato; wanafunzi wake wakaona njaa, wakaanza kuvunja masuke, wakala. Na Mafarisayo walipoona, walimwambia, Tazama! wanafunzi wako wanafanya neno ambalo si halali kulifanya siku ya sabato. Akawaambia, Hamkusoma alivyotenda Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wenziwe? Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaila mikate ile ya wonyesho, ambayo si halali kwake kuila wala kwa wenziwe, ila kwa makuhani peke yao? [1 Sam. 21:​1-6] Wala hamkusoma katika torati, kwamba siku ya sabato makuhani hekaluni huinajisi sabato wasipate hatia? [Hes. 28:8-10].”​—Mt. 12:1-5.

Hapa Yesu alitumia vizuri ufahamu wake wa Maandiko kwamba hayakumlaumu Daudi kwa kuula mkate jambo ambao katika hali za kawaida lingekuwa halali kwa makuhani peke yao. Wanafunzi wa Yesu walikuwa na lawama iliyo ndogo hata zaidi, kwa kuwa matendo yao hayakuvunja Maandiko, bali yalivunja sheria za kidini tu za marabi.a

Akielekeza kwenye namna moja yenye maana sana ya kuwaza kwa Mungu, Yesu alimalizia sababu zake kwa kutaja maneno mengine ya maana sana katika Maandiko ya Kiebrania: “Kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia. [Hos. 6:6]”​—Mt. 12:7.

“ILI LITIMIE”

Ingawa unabii wa Maandiko ya Kiebrania uliandikwa karne nyingi kabla Yesu hajaja duniani, u hai ukiwa na maana kwa Wakristo, Mara nyingi waandikaji wa Biblia Wakristo huanza mitajo ya Maandiko kwa misemo kama, “ili litimie neno lililonenwa na nabii.” (Mt. 13:35) Nyakati nyingine msemo kama huo unaonyesha utimizo wa moja kwa moja wa lililotabiriwa. (Mt. 2:5, 6; 11:10-15) Walakini mara nyingine, maneno hayo huwa yakionyesha vingine. Namna gani hivyo?

Kwa habari ya namna angesalitiwa baadaye na Yudasi Iskariote, Yesu alisema: “[Ili] andiko lipate kutimizwa, Aliyekula chakula changu ameniinulia kisigino chake.” ([Zab. 41:9] Yohana 13:18) Wakati huo Yesu alitaja aliyokuwa ameandika Daudi juu ya rafiki yake mkubwa (labda Ahithofeli mshauri wa Daudi aliyeheshimiwa), ambaye alikuwa amemgeuka, Mungu alijua kwamba Yesu angesalitiwa namna ile ile na rafiki mkubwa. Kwa hiyo Mungu alihakikisha kwamba yaliyompata Daudi yaliandikwa chini ya uongozi wa roho yake kama mfano wa unabii wa jambo hili.

Unaolingana na huo ni mtajo alioutumia Mathayo baada ya kueleza mfuatano wa mifano iliyotolewa na Yesu: “Haya yote Yesu aliwaambia makutano kwa mifano; wala pasipo mfano hakuwaambia neno; ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Nitafumbua kinywa changu kwa mifano, Nitayatamka yaliyositirika tangu awali.” ([Zab. 78:2] Mt. 13:34, 35) Asafu, mwandikaji wa Zaburi 78, kwa njia ya mfano aliyasimulia tena matendo ya Mungu kwa taifa la Israeli. Vivyo hivyo, Yesu alitumia maneno yenye mifano mingi iliyohusu “Israeli wa Mungu” wa kiroho.​—Gal. 6:16; Mt. 13:1-33; 36-50.

‘UKOMBOZI MKUU ZAIDI’

Mara nyingi Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanakuwa na habari za utimizo katika karne ya kwanza W.K. wa unabii ambao ulitumika kwanza juu ya kurudishwa kwa taifa la Israeli kutoka utumwa wa Babeli katika mwaka 537 K.W.K. Hivyo basi, utendaji wa Yohana Mbatizaji unasemekana ulitimiza unabii wa Isaya 40:3 juu ya “sauti ya mtu aliaye nyikani.”‏ (Mt. 3:3; Marko 1:3; Luka 3:4; Yohana 1:23) Naye mtume Paulo, alipokuwa akishauri Wakristo katika Korintho wajiepushe na mazoea ya kipagani, aliandika kama ifuatavyo akitumia Isaya 52:11: “Kwa hiyo tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], msiguse kitu kilicho kichafu.” (2 Kor. 6:17) Kwa habari ya matumizi ya unabii huo, mfafanuzi wa Biblia Albert Barnes anaeleza hivi:

“Sura za mwisho za Isaya, kuanzia ya [40], zinatabiri kurudi kwa Wayahudi kutoka Babeli; na kila hali iliyotajwa ilitukia waliporudi. Walakini lugha [iliyotumiwa] imepanuliwa na ni ya fahari zaidi ya ilivyotakiwa kuonyesha kurudi kwao. Vilevile itaonyesha kwa kufaa ukombozi wa maana zaidi na wa ajabu sana​—wa waliokombolewa chini ya Masihi, na kurudishwa kwa watu wa Mungu kwake, na kuenezwa kwa injili ulimwenguni pote; na kwa hiyo inaweza kusemwa unatimizwa katika kuja kwa Yesu, na kuenezwa kwa injili.”

Maandiko ya Kikristo hayatumii unabii huo kuhusu karne ya kwanza W.K. tu, bali yanapanua matumizi yake kufikia wakati ujao uliokuwa mbali sana wakati huo. Kwa mfano, kulingana na Isaya 65:17, Mungu alitabiri hivi: ‘‘Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” Andiko hili lilipata utimizo wake wa kwanza wakati Wayahudi waliporudi kutoka utumwani Babeli katika mwaka 537 K.W.K. Chini ya utawala wa gavana (liwali) Zerubabeli, akisaidiwa na Kuhani Mkuu Yoshua, wakiwa “mbingu mpya” za mfano, Waisraeli waliorudishwa walikuwa ‘‘dunia mpya,” au jamii mpya ikiitii serikali hiyo mpya yenye haki.​—Hag. 1:1, 14.

Lakini ebu angalia namna waandikaji Wakristo wa Biblia wanavyotumia unabii huu: “Tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.” (2 Pet. 3:13) “Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita.” (Ufu. 21:1) Vilevile, kwa kuwa Wakristo wa kweli wameletwa katika paradiso tukufu yenye nuru ya kiroho, Maandiko yanatoa ruhusa ya kutumia juu ya huu “wakati wa mwisho” wa taratibu hii iliyopo ya mambo masimulizi ya ajabu ya baraka za kidunia zinazopatikana katika unabii ambao hapo kwanza, ulitabiri kurudi kwa Wayahudi kutoka katika utumwa wa Babeli.​—Dan. 12:4.

“Agano la Kale” ni la maana kwa Wakristo kweli kweli. Ghala yake kubwa sana yenye kanuni, unabii, na historia ya kiunabii ni ya lazima kwa ibada ya kweli leo kama yalivyokuwa wakati ule yalipoandikwa kwa mara ya kwanza. Kwa kweli “Kila andiko [ni] lenye pumzi ya Mungu, [na] lafaa kwa mafundisho.”​—2 Tim. 3:16.

[Maelezo ya Chini]

a Kitabu cha mkusanyo wa mapokeo ya Kiyahudi kiitwacho Mishinah kinataja wazi namna 39 za kazi kubwa zilizokatazwa katika siku ya sabato, pamoja na kazi nyingine ndogo-ndogo. Kati ya kazi zilizokatazwa ni kupepeta, kupura, kusaga na kupembua. (Kijitabu Shabbath 7:2) Kitabu kiitwacho Palestinian Talmud kinatoa maoni ya marabi juu ya kazi kama hizo zilizokatazwa: ‘Ikiwa mwanamke anajongeza ngano ili ayatoe makumvi, hii inaonwa kuwa ni kupepeta; akisugua masuke ya ngano, inaonwa kuwa ni kupura; akitoa yanayokwama kando-kando, ni kupepeta matunda; akikwarusa masuke, ni kusaga; akiyatupa juu mikononi mwake, ni kupembua.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki