Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 1/15 kur. 3-5
  • Sababu “Kupenda Fedha” Kunaangamiza Watu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sababu “Kupenda Fedha” Kunaangamiza Watu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Pesa
    Amkeni!—2015
  • Je, Pesa Ndio Chanzo cha Uovu Wote?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Pesa
    Amkeni!—2014
  • Mwenye Hekima Alikuwa na Maana gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 1/15 kur. 3-5

Sababu “Kupenda Fedha” Kunaangamiza Watu

KWA sababu gani kupenda pesa kunaangamiza sana watu? Kwanza, kunaweza kuzuia mtu asiwe na shauku ya kupenda watu wa jamaa yake. Kunaweza kummalizia furaha, kumfanya asitake kutumia pesa zake hata kidogo maishani, au kumwongoza atende wanadamu wenzake ukatili.

Mfano wa mabaya ya kupenda pesa ni Henrietta Howland Green wa United States. Mwanamke huyo alikufa akaacha shamba la karibu dola 95,000,000 (shilingi 760,000,000 au Zaire 82,608,700). Katika banki moja tu, alikuwa ameweka zaidi ya dola 31,400,000 (shilingi 251,200,000 au Zaire 27,304,348). Lakini mwanamke huyo tajiri alikataa kutafutia mwanawe uganga wa haraka huku akijaribu kutafuta kihospitali kisicho cha kulipa pesa. Kwa sababu ya kukawia sana, ikawa lazima mwanawe akatwe mguu. Mwanamke huyo aliishi kwa kunywa uji uliopoa, kwa maana aliona ataharibu pesa akiupasha moto. Mwishowe, ubongo wake ulikufa ganzi kisha yeye mwenyewe akafa kwa sababu ya kubishana akisema maziwa yasiyo na mafuta yana faida. Kweli pesa zilimwangamiza mwanamke huyo.

Kama Henrietta Green angaliyajua na kuyafuata mashauri mazuri ya Biblia yanayohusu pesa, angalifaidi watu badala ya kujiletea huzuni nyingi pamoja na mwanawe. Mashauri ya Biblia yanaweza kusaidia watu wengine wengi sasa hivi, wasije wakaumia kwa sababu ya kupenda pesa.

Mtume Paulo alionyesha maangamizi yanayotokana na kupenda pesa, akaandika hivi: “Shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani [wamejichoma] kwa maumivu mengi.”​—⁠1 Tim. 5:10.

Mtu anapositawisha upendo wa pesa, zinakuwa mungu wake. Anatumia akili na nguvu zake zote akifikiria kupata pesa zaidi. Hatosheki hata kidogo. Biblia inasema, “Apendaye fedha hatashiba fedha, wala apendaye wingi hatashiba maongeo [au, “mapato,” NW].” (Mhu. 5:10) Kwa kuwa ndivyo ilivyo, huenda mtu huyo akawa na nia ya kufanya jambo lo lote awezalo ili kuwa na pesa nyingi zaidi. Halafu anakuwa na kawaida ya kusahau kabisa kumtumikia Mungu na kutendea watu mambo mema.

Kwa mfano, kupenda pesa kunaweza kufanya mtu awe na mazoea mengi ya udanganyifu, pamoja na kutumia vifaa ovyo vya ujenzi, kuchanganya vyakula au vinywaji na vitu visivyofaa ili kuvifanya viwe vingi, kupimia watu vitu kwa udanganyifu, na mambo kama hayo. Mtu wa namna hiyo hafikirii jinsi vifaa ovyo vya ujenzi vinavyoweza kuweka nyumba katika hatari ya kuanguka na kuumiza watu vibaya au kuwaua, jinsi vyakula na vinywaji vinaweza kuharibu afya ya watu kwa sababu ya kuongezwa vitu vingine, na jinsi kudanganya watu kunavyoweza kuwataabisha sana, hasa wale wasio na pesa nyingi.

Watu wengine wanajaribu kutajirika upesi kwa kucheza kamari. Jinsi wanavyoendelea kuicheza, ndivyo wanavyoendelea kumaliziwa pesa. Lakini wao wanaendelea kuamini watashinda, warudishe pesa walizopoteza na kutajirika kiajabu. Kwa njia hiyo, pesa ambazo zingaliweza kutumiwa kuhusu mambo ya lazima zinapotea bure, halafu watoto wanaumia kwa sababu pesa hazitoshi kuwanunulia chakula wala mavazi wanayohitaji.

Mtu anawezaje kuepuka mtego kwa sababu ya kupenda pesa, asije akajiumiza mwenyewe pamoja na watu wengine? Jibu ni kuwa na kiasi katika mambo ya mali. Neno la Mungu, Biblia, linatusaidia sana katika habari hii.

Ingawa Maandiko yanatutia moyo tuwe wenye bidii, yanatushauri tusijaribu kujikusanyia utajiri mwingi sana. Yanatuonyesha kwamba haitupasi kufanya kazi ili kujifaidi wenyewe tu. Mtume Paulo alihimiza mtu ye yote aliyekuwa mwibaji “afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.” (Efe. 4:28) Kufikiria sana wenye shida kwa njia hiyo kunalinda mtu asiwe mpenda pesa mwenye kufikiria mambo yake tu.

Maandiko yanasaidia mtu awe na maoni mazuri pia juu ya mali, akijua kwamba mali hazikai muda mrefu. Mali zinaweza kupotea, kuibwa au kuharibiwa. Ingawa watu wanajua hivyo, mara nyingi wanaendelea kutumia pesa zao kama kwamba hawajui wanaweza kupatwa na mashaka maishani.

Wafikirie wale wanaopita kiasi kwa kujinyima vitu vinavyoweza kuwastarehesha zaidi maishani. Huenda wakafanya hivyo wakidhani kwamba wanaweka akiba ya watoto wao, wajukuu wao na vitukuu vyao. Bila shaka, si vibaya kutaka kuachia watoto urithi. Lakini lazima wazazi wajiangalie wasifikie hatua ya kuogopa kutumia pesa zo zote kwa matumizi yao wenyewe. Labda inafaa wajiulize kama wanaficha upendo wao mwingi wa mali kwa kusingizia kwamba wanataka kuachia watoto urithi.

Ni vizuri kukumbuka maneno aliyoandika Mfalme Sulemani juu ya vile watu wanavyoweza kukata tamaa na kuvurugika akili wanapojitahidi kukusanya mali nyingi. Wanaweza kupoteza zote upesi katika wakati wenye shida nyingi zaidi. Tunasoma hivi: “Kuna balaa mbaya sana niliyoiona chini ya jua, nayo ni hii, mali alizoziweka mwenyewe kwa kujinyima; na mali hizo zimepotea kwa bahati mbaya; naye akiwa amezaa mwana, hamna kitu mkononi mwake.”​—⁠Mhu. 5:13, 14.

Naam, linakuwa sikitiko wakati mali zote za mtu zinapopotea kwa sababu ya msiba fulani, vita, ukosefu mwingi wa mvua, moto, tetemeko la ardhi au dhoruba, baada ya yeye kutia bidii nyingi. Ikiwa mtu huyo alikataa kufurahia matunda ya kazi yake ngumu, maisha yake yamekuwa bila kitu. Msiba wake unaongezeka ikiwa aliendelea kukusanya mali nyingi halafu akawa baba watoto baada ya kuzipoteza.

Hata urithi usipoharibiwa na msiba fulani, hiyo haionyeshi inafaa kuishi maisha ya utafutaji wa mali tu. Mali zote zilizo ulimwenguni hazimfaidi mtu anapokufa. Biblia inasema waziwazi: “Alivyotoka tumboni mwa mamaye, atakwenda tena tupu-tupu kama alivyokuja; asichume kitu cho chote kwa ajili ya kazi yake, hata akichukue mkononi mwake.” (Mhu. 5:15) Basi, maisha ambayo yametumiwa kutafuta mali tu ni ya bure kama nini!

Tena, mtu hana njia ya kujua jinsi urithi alioacha utakavyokuwa baada ya kufa. Huenda warithi wake wakakosa kuuthamini na kuuponda upesi kwa sababu waliupokea bila kuufanyia kazi. Hata wakiutumia vizuri, hakuna uhakika wa kwamba msiba hautaumaliza. Ikiwa hivyo, kutakuwa na faida gani ikiwa hakuna mtu aliyefurahia matunda ya kazi nyingi iliyofanywa wakati wa kuutafuta?

Kujua kwamba maisha yamejawa na mashaka mengi kunaweza kusaidia mtu afahamu kwamba hawezi kupata furaha ya kutosha kwa kutafuta mali tu. Kujua hivyo kutamsaidia aone kama anataka pesa kwa njia isiyofaa. Vilevile ataepuka kufanya maisha yawe magumu kwa sababu ya kutotaka kutumia pesa zo zote. Anaweza kufurahia matunda ya kazi yake kwa njia inayofaa, na kujifaidi mwenyewe pamoja na watu wengine. Kwa njia hiyo ataepuka madhara yanayoweza kuja kwa sababu ya kupenda pesa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki