Kuhukumu kwa Haki, Hekima na Rehema
Inapendekezwa msomaji asome makala hii kabla ya kujifunza makala mbili zinazofuata.
MARA nyingi sisi wanadamu hufanya makosa ya kuhukumu. Hasa ni kwa sababu ya kutokamilika. Umepata kumsikia mtu akisema unafanya mambo ukiwa na makusudi mabaya au akikulaumu kwa sababu ya kupashwa habari zisizo za kweli? Je! ilipokuwa hivyo uliona kwamba hukuonyeshwa rehema? Kwa upande mwingine, je! nyakati nyingine wewe mwenyewe hukuhukumu mtu isivyofaa, kwa sababu ya kukosa kuangalia mambo yote yanayohusika? Je! nawe pia hukukosa kuonyesha rehema? Tukiwa wenye nia ya kuona makosa yetu, tutakubali kwamba sote tunapungukiwa sana katika jambo hilo.
Ili kuhukumu kwa haki, hekima na rehema, lazima tufuate kanuni iliyo bora kuliko yo yote iliyowekwa na wanadamu. Kanuni hiyo imewekwa na Mungu. Licha ya kupendezwa na kanuni hiyo, yatupasa kuongozwa nayo. Kwa sababu gani? Kwa sababu Yehova Mungu, “mwamuzi wa watu wote,” ataitumia tutakapolazimika kusimama mbele za kiti chake cha hukumu. (Ebr. 12:23; Rum. 14:10) Kwa hiyo, je! haitupasi kuongozwa na mambo anayosema ni haki? Hilo ndilo jambo la upendo na hekima. Matendo au maamuzi yo yote tufanyayo yatakuwa na faida zenye kudumu tukiongozwa na maoni ya Mungu tu ya kuamua mambo.
Ni wapi leo tunapoweza kuona watu wakihukumiwa vizuri kulingana na kanuni za Mungu zenye haki? Inasemekana kwamba hata sasa kuna wakuu na watu wa kawaida wanaoweza kutoa hukumu bila kupendelea. Lakini, leo wale wanaolifahamu Neno la Mungu na mambo ya hakika wanasadiki kwamba, kwa ujumla ulimwengu huu hauongozwi na kanuni za haki. Umo katika mamlaka ya yule mwovu; naam, unadanganywa naye. (1 Yohana 5:19; Ufu. 12:9) Hiyo yatia ndani Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ambayo Biblia inaitaja kuwa kama mwanamke mchafu. (Ufu. 17:3-5; 18:2-4) Watu wa Mungu ambao wametoka kwake wanashukuru kwamba hawapatwi tena na madhara yanayotokana na uamuzi wake mpotovu juu ya mambo ya imani na adili. Wao wanautumaini mpango ambao Yehova amerudisha ndani ya kundi la kweli la Kikristo ambamo wazee waaminifu waliowekwa wanahukumu kama ilivyotabiriwa katika Isaya 1:26: “Nami nitarejeza upya waamuzi wako kama walivyokuwa hapo kwanza, na washauri wako kama hapo mwanzo; baada ya hayo utaitwa, Mji wa haki, mji mwaminifu.”
Katika historia ya watu wa kale wa Mungu, kwa mara ya kwanza waamuzi waliwekwa kwa wingi muda mfupi baada ya Israeli kuondoka Misri mwaka 1513 K.W.K. Musa alikaribia kujichosha sana kwa kujaribu kushughulika na mambo yote yaliyohitaji maamuzi ya Mungu wa kweli yafanywe kulingana na sheria zake. Baba-mkwewe, Yethro, alimshauri agawie wengine madaraka fulani ili umati wa watu uliokuwa ukiongozwa jangwani uangaliwe vizuri zaidi. Maelfu ya wanaume hodari walichaguliwa wamsaidie Musa. Kazi yao ilikuwa ya kushughulika na matatizo au maulizo ya kawaida yaliyotokea. Musa ndiye angeendelea kuchukua daraka kubwa la kufahamisha watu sheria na kanuni za Mungu, na kuwajulisha njia iliyowapasa kufuata na kazi waliyopaswa kufanya. Mpango wenye utaratibu mzuri sana ulipendekezwa: “Utajipatia katika watu hawa watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu; ukawaweke juu yao, wawe wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini, na wakuu wa kumi; nao wawaamue watu hawa sikuzote; kisha, kila neno lililo kubwa watakuletea wewe, lakini kila neno dogo watauchukua huo mzigo pamoja nawe. Kwamba utafanya jambo hili, na Mungu akikuagiza hivyo, basi utaweza kusimama wewe, na watu hawa wote nao watakwenda mahali pao kwa amani.”—Kut. 18:13-23.
Baadaye, walipokwisha kukaa muda wa kutosha katika nchi ya Kanaani, Yehova aliwainulia waamuzi, si kwa kusudi la kusikiliza kesi tu zilizohusu kuvunja sheria, bali pia kukomboa watu wake mikononi mwa waonezi. (Amu. 2:18) Waamuzi hao waliwekwa wawe viongozi na vilevile walisaidia watu waijue sheria ya Mungu na kuitumia. Walikuwa watu kama Gideoni, Baraka, Samsoni, Yeftha na Samweli, nao walitenda matendo hodari na vilevile “walitenda haki,” kulingana na yaliyoandikwa katika Waebrania 11:32, 33. Waamuzi wengine katika Israeli ya kale, waliotumikia kama wanaume wazee katika mtaa, walifanya kazi za usimamizi, licha ya kushughulika na kesi.—1 Nya. 26:29; 2 Nya. 19:4-7.
Hata wafalme wa Israeli walitakiwa kusoma kitabu cha torati, wajifunze kumwogopa Yehova na kushika neno lake. (Kum. 17:19, 20) Waliagizwa waamue mambo vizuri ikiwa walitazamia kufanikiwa na kupata upendeleo wa Mungu.—2 Nya. 1:9-12.
JINSI WAZEE WANAVYOKUWA WAAMUZI LEO
Leo ni mpango gani unaotumiwa kuamua mambo kati ya watu wa Mungu? Yehova ameinua wazee walio katika cheo cha kutumikia kama waamuzi na washauri. Lazima wanaume hao watimize matakwa yaliyowekwa katika 1 Timotheo 3:1-7 na Tito 1:5-9. Daraka lao halihusu kushughulika na kesi tu. Wao hufundisha pia na kueleza watu matakwa ya Mungu na kuwatia moyo wamtolee utumishi wa nafsi yote na kutii kanuni zake za haki kwa uaminifu.—Kol. 3:23; 1 The. 5:21; l Pet. 1:22.
Sisi twauonaje mpango huo unaopatikana katika kundi letu wenyewe? Haitupasi kuwa kama wengine waliokuwa katika kundi la Korintho karne ya kwanza wakashtakiana mbele ya wasioamini. Mtume Paulo aliwakaripia, akisema: “Nasema hayo nipate kuwatahayarisha. Je! ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake? Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao wasioamini.” (1 Kor. 6:5, 6) Kwa kuendea mahakma za kilimwengu wakaamue mambo ambayo yangaliweza kuamuliwa ndani ya kundi la Kikristo, walikuwa wakijitatiza au kujishinda kiroho. Hakuna ye yote kati yetu anayetaka kuaibika wala kujuta baadaye kwa sababu ya kushindwa kuwa na maoni yanayofaa juu ya mpango ulioko leo wa kuhukumu kupatana na Maandiko. Bali, yatupasa tuthamini kwa moyo mipango hiyo ya kitheokrasi. Kwa kutii mashauri na uamuzi mwema unaotokana na wale ‘wanaotuambia neno la Mungu,’ twaonyesha kwamba tunataka kushirikiana kufanya kazi na jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” na kumnyenyekea Kristo.—Ebr. 13:7, 17; Efe. 5:24; Mt. 24:45-47.
Wakati hukumu za Yehova zinapodhihirishwa sasa, tunajifunza kuthamini kanuni bora ambazo lazima tuishi kupatana nazo. Tunasaidiwa kuamua mambo ya kipekee na ya kundi pia, ingawa tungali hatujakamilika. Tunaletwa karibu na Yehova zaidi na kuonyeshwa mfano mdogo wa jinsi taratibu yake mpya yenye haki itakavyokuwa. Tunapoutazamia sana wakati huo mtukufu, twaweza kumwambia Yehova hivi tukiwa na tumaini hakika: “Hukumu zako zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki.”—Isa. 26:9.