Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 8/15 kur. 374-381
  • Kuendelea Kuheshimu Ndoa Mbele za Mungu na Wanadumu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuendelea Kuheshimu Ndoa Mbele za Mungu na Wanadumu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUAMUA UHALALI WA NDOA
  • MAMBO AMBAYO KAISARI ATAKA KUJUA KATIKA NDOA
  • MAHALI AMBAKO KAISARI HATAMBUI NDOA
  • KUWEKA WAZI KANUNI ZILIZO KUU
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kwa Nini Ndoa Inapaswa Kuonwa Kuwa Takatifu?
    Amkeni!—2004
  • Heshimu “Kile Ambacho Mungu Ameunganisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Ikiwa Ndoa Imo Katika Hatua ya Kuvunjika
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 8/15 kur. 374-381

Kuendelea Kuheshimu Ndoa Mbele za Mungu na Wanadumu

“Tukijipendekeza kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.”​—2 Kor. 4:2, NW.

1. (a) Yampasa Mkristo aangalie nini katika ndoa yake? (b) Ni maulizo gani yanayoweza kutokea juu ya sheria za wakuu wa serikali zinazohusu ndoa? (Marko 12:17)

ILI watu wa Mungu waendelee kuwa na upendeleo wake, ni lazima waendelee kuheshimu ndoa. (Ebr. 13:4) Kila Mkristo aliyeoa au kuolewa apaswa kuangalia sana ndoa yake iwe yenye kuheshimika machoni pa Mungu na wanadamu. Ulizo latokea kuhusu habari hiyo, Mamlaka za kibinadamu, kutia na serikali za kisiasa na wakuu wa miji, zinahusikaje katika ndoa? Je! uhalali wa ndoa unategemea kutambuliwa na wakuu wa mji tu, na je! wanapoihalalisha wao ndio wanaoamua jinsi Yehova Mungu, Mwanzishi wa ndoa, anavyoiona ndoa hiyo?

2. Ni masharti gani ya ndoa yasiyokuwa katika sheria ambayo Waisraeli walipewa na Mungu?

2 Katika makala iliyotangulia tumeona kwamba ndoa za Waebrania zilishughulikiwa na jamaa au kabila. Taifa la Israeli lilipoanzwa, Mungu aliwapa sheria yake, iliyokuwa na mipango mingi sana ya ndoa, kutia na makatazo ya kutofanya zinaa ya haramu, kanuni zenye kuonyesha wajibu ulio katika ndoa na mipango kama hiyo. (Mambo ya Walawi, sura 18 na 20) Lakini, watu hawakutakiwa wakachukue hati au leseni kwa makuhani ili kuoana, wala haikuwa lazima kuhani ahudhurie ndoa kuihalalisha. Wala haikuwa lazima wajumbe wa serikali ya Israeli wafanye hivyo. Bali, maadamu sheria ya Mungu ilifuatwa sana, ndoa ilikubaliwa kuwa halali na yenye kuheshimika katika mtaa ambao wenye kufanya arusi waliishi.

3. Je! njia ya kushughulika na ndoa na talaka ilibadilika Waisraeli walipotawalwa na mamlaka za kigeni?

3 Baadaye, taifa la Israeli lilitawalwa na mamlaka za kigeni, yaani, Babeli, Mwungano wa Wamedi na Waajemi, Ugiriki na Rumi. Jambo hilo lilibadilije mipango ya ndoa kati ya Waisraeli? Kulingana na historia, inaelekea kwamba waliruhusiwa na mataifa yenye kuwatawala waendelee na mambo yao kama kawaida. Ingawa walikuwa wametiishwa, inaonekana kwamba masuala au hata magomvi, kama yanayohusu talaka, yalishughulikiwa na wazee Wayahudi hasa, na mahakma zao. Lakini, ni wazi kwamba kama Mwisraeli alipeleka kesi ya ndoa kwenye mahakma za taifa lenye kuwatawala alipaswa kuwatazamia waamue kesi hiyo wakitegemea sheria zao wenyewe za ndoa.

4. Ndoa zilipoanza kuandikishwa, kusudi lilikuwa nini?

4 Inadhaniwa kwamba baadaye katika nyakati za Biblia ndoa zilianza kuandikishwa, ingawa hakuna uhakika. Kwa vyo vyote, inaonekana kwamba ndoa iliandikishwa baada ya kufanywa. Hivyo, badala ya kuamua usafi wa ndoa, serikali ya mji iliweka maandishi yenye kuhakikisha kwamba ndoa ilifanywa.

5. (a) Je! leseni za ndoa zilitolewa katika karne za kwanza za kundi la Kikristo? (b) Ni wakati gani wakuu wa serikali walipoanza kujishughulisha na ndoa?

5 Hali ilikuwaje katika karne za kwanza za kundi la Kikristo? Inaelekea kwamba ndoa iliendelea kushughulikiwa na jamaa kama katika Israeli. Tena, kama huko nyuma katika Edeni na kati ya Waisraeli (na hata kati ya watu wengi wa wakati huo), haikuwa lazima mkuu fulani wa dini au wa serikali atoe leseni ya ndoa au aje kuihalalisha na kuifanya yenye kuheshimika.a Inaonekana wakuu wa serikali hawakujishughulisha na ndoa mpaka mmoja wa waliooana, au wote wawili, walipowaendea wakawatatulie kisheria matatizo au magomvi. Wakati huo waliamua kama ndoa ilikuwa halali au haikuwa halali, kwa kutegemea jinsi ilivyopatana na sheria zao. (Kwa mfano, sheria ya Kirumi haikukubali ndugu aoe dada yake.)

6. (a) Ni jambo gani hasa lililoongoza uhusiano wa ndoa katika kundi la Kikristo? (b) Je! maoni ya watu katika mtaa ambamo Wakristo wanaishi yanapaswa kuwaongoza katika mambo wanayofanya kuhusu ndoa zao?

6 Hata hivyo, ilikuwa lazima kufuata sheria ya Mungu ili ndoa ionekane kuwa yenye kuheshimika ndani ya kundi la Kikristo. Hivyo, wakati mtume Paulo aliposikia kwamba katika kundi la Korintho ‘mtu ana mke wa babaye,’ pasipo kukawia alilaumu jambo hilo kuwa “zinaa.” Alionyesha pia kwamba kundi lilipaswa kufikiria kanuni za mtaa walimoishi, kwa maana “hata katika Mataifa” jambo kama hilo halikufanywa.​—1 Kor. 5:1, 2.

7, 8. (a) Kwa sababu gani kundi la Kikristo linafanya vizuri kujishughulisha na ndoa zinazofanya na washiriki wake? (b) Historia yaonyesha Wakristo wa kwanza walifanyaje kuhusu ndoa za washiriki wa kundi?

7 Kundi la Kikristo lilijichukua kama ‘ushirika wa ndugu’ wenye washiriki wa “nyumba ya Mungu,” hapo neno “nyumba” likiwa na maana ya jamaa, kama inavyoonekana kwa kulinganisha Maandiko kama Mathayo 10:12, 35, 36; Matendo 16:30-31; 1 Timotheo 3:4, 5; 5:4, 8. Kwa hiyo, kwa kuwa kundi ni kama jamaa, lilijishughulisha na mapatano ya ndoa ya washirika wake.

8 Kikieleza juu ya maoni ya Wakristo wa kwanza, Hasting’s Encyclopcedia of Religion and Ethics (Vol. VIII, ukurasa 435) chasema: “Kwanza, ndoa ni jambo la kijamaa. Katika kipindi cha mwanzoni kundi la Kikristo lilijichukua kama jamaa ya kiroho, na kila mshiriki alitaka kufaidi kundi zima maishani mwake. . . . Ushuhuda wa Mababa [wa kanisa], tangu katikati ya karne ya 3, waonyesha kwamba tunazoita ndoa za kiserikali sasa zilikuwa zinajulikana, labda zilifanyika kwa ukawaida, lakini zilikatazwa sana na Kanisa.”

9. (a) Kulingana na Maandiko na historia inayohusu kuhalalishwa kwa ndoa na serikali, twaweza kukata maneno tusemeje? (b) Kuheshimika kwa ndoa kulitegemea nini?

9 Hivyo, ushuhuda unaopatikana katika Maandiko na historia waonyesha kwamba haikuwa kawaida serikali kuhalalisha ndoa zamani zile. Inaonekana kwamba haikuwa lazima ndoa ihalalishwe ili iweze kuheshimiwa na Wakristo. Inaonekana kwamba ndoa iliheshimika kundi la Kikristo lilipokubali kwamba ilipatana na kanuni za kimungu, vilevile na maoni na kanuni za watu wa mtaa ambamo Wakristo waliishi. Kama mtume Paulo, Wakristo walipaswa wajitahidi ‘kujipendekeza kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu,’ na kujaribu ‘kutokosesha Wayahudi wala Wayunani wala kanisa la Mungu’ kwa ‘kufanya yote kwa utukufu wa Mungu.’​—2 Kor. 4:2; 1 Kor. 10:31, 32.

10, 11. (a) Wakuu wa serikali walipataje kujishughulisha na ndoa na kuihalalisha? (b) Ni maoni gani juu ya kuhalalisha ndoa yanayopatikana sana katika nchi zenye Waprotestanti wengi sana?

10 Lakini, ni jambo la hakika kwamba, majuzi katika sehemu nyingi za dunia, wakuu wa serikali wamezidi kushughulikia ndoa na kuzihalalisha. Basi, ni lazima Wakristo wakumbuke jambo hilo wanapojaribu kufanya ndoa zao ziwe ‘zenye kuheshimiwa na watu wote’ nyakati zote. (Ebr. 13:4) Tunapochunguza jambo hilo, inafaa tuangalie jinsi maoni hayo tofauti yametokea. Kitabu Encyclopoedia of Religion and Ethics chasema (ukurasa 437; sisi ndisi tumelaza maneno): “Katika serikali ndoa huchukuliwa kuwa mkataba wa kisheria ambao lazima uongozwe na Serikali kwa ajili ya makusudi yanayofaa. Kulingana na maoni ya Kikristo, ndoa ni hali takatifu ambayo Kanisa laweza kudai kuongoza kwa faida za dini na usafi. Ujuzi waonyesha kwamba nyakati zote mamlaka mbili hizo zitaelekea kupingana, na kwa hiyo, huenda magumu yakatokea mara nyingi. . . . Tangu wakati Matengenezo ya kanisa yalipofanywa [na Waprotestanti] siku hizi ndipo suala limetokea wazi juu ya mamlaka mbili hizo na jinsi zinavyohusiana hasa. . . . ”b

11 Kwa hiyo inaonekana kwamba wakuu wa serikali wanahalalisha ndoa zaidi nyakati za kisasa kuliko zamani zote zilizopita. Nchi zenye Waprotestanti wengi sana zimekuwa na maelekeo mengi zaidi ya kuona kwamba wakuu wa serikali hasa ndio wanaopaswa kuamua uhalali wa ndoa (na talaka). Kwa hiyo watu wengi wanaona kanisa halina daraka la kuamua uhalali wa ndoa (na talaka).

KUAMUA UHALALI WA NDOA

12. Kwa kuwa wakuu wa serikali wamekwisha anza kujishughulisha na ndoa na kuzihalalisha, mtumishi wa Mungu anapata maulizo gani?

12 Yampasa Mkristo afanye nini akiwa katika hali hizo? Bila shaka hawezi kupuza hali iliyopo ikiwa ataka ndoa yake iwe yenye kuheshimika ‘kati ya watu wote.’ Hawezi kusema kwamba zamani wakuu wa serikali hawakutegemewa kuhalalisha ndoa. Lakini, maulizo haya yatokea: Je! wakuu wa serikali ndio wanaopaswa kuonwa kama wenye mamlaka ya kuamua uhalali wa ndoa, inapoanzwa au labda inapomalizwa na talaka? Uamuzi wao unamhusuje Mungu?

13. Kwa sababu gani hatuwezi kuwachukua wakuu wa serikali kama wenye mamlaka ya kuamua kabisa mambo ya ndoa? (Matendo 5:29)

13 Je! kweli wakuu wa serikali ndio wanaopaswa kukata maneno juu ya kama ndoa (au talaka) ni halali au si halali machoni pa Mungu? Twaweza kuona kwamba kama ingalikuwa hivyo kungalikuwa na maoni yenye kupingana juu ya linalotakiwa ili kupata baraka ya Mungu katika ndoa. Kwa sababu gani? Kwa sababu maoni ya wakuu wa serikali yanatofautiana sana mahali mahali, na zaidi ya hilo, nyakati nyingine yanapingana na kanuni zilizomo katika Biblia.

14. Biblia inatoa maoni gani juu ya kuoa wake wengi hata sheria za nchi fulani zinaporuhusu kufanya hivyo?

14 Kwa mfano, katika nchi nyingine watu hukubaliwa kisheria waoe wake wengi, na kila mke huonekana kuwa halali sawa na wake wale wengine. Lakini, Kristo Yesu na mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu walionyesha kwamba Mungu amewekea mwanamume kanuni ya kuwa na mke mmoja tu.​—Mt. 19:4, 5; 1 Kor. 7:2; 1 Tim. 3:2.

15. Sheria za wanadamu zinazohusu talaka zatofautianaje na sheria ya Mungu katika nchi nyingi?

15 Vilevile, nchi nyingine huruhusu mtu ataliki mwenzi wake kwa sababu nyingi, nyakati nyingine kwa sababu ndogo sana. Lakini, nchi nyingine hazimpi mtu haki ya kutaliki mumewe au mkewe hata kwa sababu ya uasherati, na hivyo hazimpi uhuru wa kuoa au kuolewa tena. Kwa upande mwingine, Biblia yasema kuna sababu moja tu iliyo halali ya kutoa talaka, yaani, uasherati, nayo yaonyesha kwamba wale wanaotoa talaka kwa sababu hiyo wanakuwa huru kuoa au kuolewa tena. (Mt. 5:32; 19:3-9) Hivyo mambo mengine yanayokubaliwa na Serikali hukataliwa na Mungu, na mengine yanayokataliwa na Serikali huruhusiwa na Mungu.

16. Mamlaka ya Serikali katika kuamua uhalali wa ndoa yapaswa kuonwaje? (Rum. 13:1; 1 Pet. 2:13, 14)

16 Basi, ushuhuda waonyesha kwamba serikali ina haki ya kiasi tu ya kuamua uhalali wa ndoa (au talaka), lakini Mungu ana haki kamili ya kufanya hivyo. Ili kupata maoni yaliyosawazika juu ya mamlaka ya kiasi ambayo Serikali inayo (inayoitwa “Kaisari” katika Biblia), inafaa kuangalia mambo ambayo serikali hutaka kujua kuhusu ndoa, na jinsi Mkristo anavyopaswa kuitii.

MAMBO AMBAYO KAISARI ATAKA KUJUA KATIKA NDOA

17, 18. Ni jambo gani kuu ambalo wakuu wa serikali wamejishughulisha nalo katika ndoa, na kwa sababu gani?

17 Je! serikali hushughulika na masuala ya usafi na dini hasa yanayohusu ndoa, au hushughulika na jambo jingine? Tukumbuke kwamba encyclopedia iliyotajwa mapema ilisema kwamba, katika serikali, “ndoa huchukuliwa kuwa mkataba wa kisheria ambao lazima uongozwe na Serikali kwa ajili ya makusudi yanayofaa.” Hilo linaonyeshwa wazi na historia ya sheria za serikali zinazohusu ndoa na talaka. Historia hiyo yaonyesha kwamba serikali zimejishughulisha kwa sababu zinahusika katika mambo kama urithi na haki za kuwa na mali, hasa wakati kuvunjwa kwa “mkataba” wa ndoa (kwa njia ya talaka au kifo) kunapofanya haki hizo zitiliwe mashaka. Kinapohakikisha kwamba ndivyo ilivyo leo, Encyclopcedia Britannica (Macropaedia, 1976, Vol. 7, kurasa 166, 167) chasema:

“Sheria . . . inashughulika hasa na haki za mume na mke na mzazi na mtoto na wajibu wao, hasa katika masuala ya kutafuta riziki.” “Katika nchi nyingi leo . . . ndoa inahalalishwa kisheria kwa kuandikishwa hasa. Kwa hiyo, kulingana na sheria ndoa ni kuanzwa kwa haki au wajibu fulani kama kutafuta riziki, kulinda haki za ndoa na za urithi, na kulinda watoto wadogo wa halali.”

18 Kwa hiyo “Kaisari” (serikali za kisiasa) amejishughulisha na ndoa hasa kwa sababu amepelekewa masuala hayo ya kisheria katika mahakma zake ayaamue, si kwa sababu anajishughulisha na mambo ya kidini au ya usafi wa ndoa. Amejishughulisha pia kuzuia magonjwa yasienee, hasa kisonono na kaswende, na madhara yanayotokana na uzazi (kama kati ya watoto wanaozaliwa na watu wa jamaa moja), naye amefanya hayo kwa “makusudi yanayofaa.” Ndiyo sababu hata serikali zinazopinga dini na zisizoamini kuna Mungu zimeweka sheria za kuhalalisha ndoa.

19. Kwa sababu ya shauri la Yesu ‘kumlipa Kaisari yaliyo ya Kaisari, ni ulizo gani laweza kuulizwa juu ya ndoa na talaka?

19 Namna gani maagizo ya Yesu ‘kumlipa Kaisari yaliyo ya Kaisari’? Kundi la Kikristo linapojaribu kutii amri hiyo, je! linatakiwa kuona kwamba Kaisari ndiye anayepaswa kukata maneno juu ya uhalali na usafi wa ndoa au talaka?​—Mt. 22:21.

20. (a) Ni jambo gani lililomfanya Yesu anene habari za ‘kumlipa Kaisari yaliyo ya Kaisari’? (b) Ni kwa kadiri gani kanuni hiyo inahusika katika ndoa ya Mkristo?

20 Kwanza, yatupasa tujue kwamba suala lililomfanya Yesu anene aliyonena lilihusu kodi. Kaisari hutoa utumishi wa namna nyingi na astahili ‘kulipwa’ kwa ajili ya utumishi huo. (Mt. 22:17-21) Lakini, Kaisari siye aliye na mamlaka ya kuwapa watu haki ya kuoa au kuolewa. Haki hiyo hasa yatokana na Mungu, Mwanzishi wa ndoa. (Mwa. 1:27, 28; 2:18, 22-24; 9:1; linganisha 1 Timotheo 4:1-3.) Kwa hiyo, Kaisari siye mwenye mamlaka ya kukata maneno juu ya yaliyo haki na yasiyo haki katika ndoa (au talaka). Jambo ambalo Kaisari aweza kufanya ni kutambua kisheria na kulinda haki za ndoa katika mahakma zake. Mkristo anayetaka ndoa yake ‘iheshimiwe na watu wote’ ana haki ya kutumia mipango hiyo alinde haki na faida za jamaa yake. Ili kutambuliwa na kupata haki hizo yampasa ‘amlipe Kaisari’ kwa kufuata sheria ambazo Kaisari amewekea watu wanaotaka kupokea haki hizo. Huenda hiyo ikatia ndani mambo kama malipo ya leseni, kukubali kuchunguzwa afya, au mambo kama hayo.

21. Ndoa ya Mkristo yapaswa kuongozwaje na mamlaka ya Kaisari?

21 Lakini, Mkristo anapomlipa Kaisari kwa ajili ya faida anazopata kwa kutambuliwa naye kisheria hapaswi kusahau kwamba mamlaka ya Kaisari katika ndoa ni ya kiasi tu. Mungu hana lazima ya kufuata maamuzi ya Kaisari, tena aweza kukataa mambo yanayokubaliwa na Kaisari, au kukubali yanayokataliwa na Kaisari. Yampasa Mkristo afikirie sana mipango ya Kaisari ya ndoa na talaka, lakini sikuzote atafikiria zaidi Mamlaka Iliyo Kuu Zaidi, Yehova Mungu. (Matendo 4:19; Rum. 13:1, 5) Akifanya hivyo atapata kibali na baraka ya Mungu.

22, 23. Kwa sababu gani yampasa Mkristo ajaribu kufanya ndoa yake itambuliwe kisheria?

22 Hivyo Mkristo anafahamu kwamba, ingawa sheria za Kaisari sizo zinazokata maneno juu ya uhalali wa ndoa yake machoni pa Mungu, lazima atii agizo hili la Maandiko: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote.” (Ebr. 13:4) Lazima ajitahidi awezavyo ahakikishe kwamba ndoa yake inaheshimiwa na watu wote. Ni kweli kwamba katika nchi nyingine huenda watu wengi wasipendezwe na mtu aliyeoa au aliyeolewa na mwingine asiye wa kabila au dini iliyo kubwa zaidi. Hata hivyo, yampasa Mkristo atafute njia yo yote anayoweza kupata atambuliwe kisheria, asije akaachilia ndoa yake ilaumiwe vikali au ionekane na wengine kuwa isiyo na maana sana. (2 Kor. 6:3; 1 Pet. 2:12, 15, 16; 3:16) Ataka ndoa yake iletee Mwanzishi wa ndoa heshima.

23 Wale wanaotaka kuwa washiriki waliobatizwa wa kundi la Kikristo, ambao ndoa zao hazijatambuliwa kisheria, wanatazamiwa wajitahidi wawezavyo ndoa zao zitambuliwe na kuandikishwa. Kufanya hivyo kutasaidia kuondolea watu kwa ujumla mashaka yo yote juu ya kuheshimika kwa mwungano wao. Lakini je! nyakati zote inawezekana kufanya hivyo, na ikiwa haiwezekani, wanaweza kufanya nini?

MAHALI AMBAKO KAISARI HATAMBUI NDOA

24. Huenda mwanamume aliye katika nchi isiyoruhusu talaka akapatwa na tatizo gani?

24 Tutasaidika tukielewa mamlaka ya kiasi ambayo Kaisari anayo kuhusu ndoa. Kwa mfano, fikiria maeneo ambako kwa sababu ya ukubwa wa dini fulani au kwa sababu nyinginezo, sheria hairuhusu talaka yo yote hata kukiwako sababu za Maandiko za “uasherati” (por·neiʹa). Huenda mwanamume ambaye mkewe amefanya uasherati akawa alikwisha mwacha, na baada ya hapo akaoa mke mwingine, ambaye pengine amemzalia jamaa. Huenda sasa akajifunza kweli ya Neno la Mungu na kuitii kwa kutaka kubatizwa awe mwanafunzi wa Mwana wa Mungu. Kwa sababu sheria ya taifa haikubaliani na sheria ya Mungu kuhusu talaka na kuoa tena, hawezi kupata talaka na kuandikisha kisheria ndoa yake ya sasa. Aweza kufanya nini?

25. Mwanamume anayehesabiwa na Mungu kuwa ametoa talaka lakini nchi yake haiwezi kutambua talaka hiyo kisheria awezaje kuthibitisha kwamba haishi katika uzinzi?

25 Hali zake zikiruhusu, aweza kwenda nchi iliyo jirani inayotoa talaka kisha aoe tena akiwa chini ya sheria za nchi hiyo. Huenda kufanya hivyo kukaongezea ndoa yake heshima, ingawa arudiapo nchi ya kwao huenda ndoa yake isitambuliwe na “Kaisari” anayetawala huko. Ikiwa hawezi kupata talaka, yampasa atengane kisheria na mwenzi wake halali aliyemwacha, au afanye jambo jinginelo linaloruhusiwa na sheria ya nchi. Baada ya hapo yampasa aandikie kundi la kwao kuahidi atakuwa mwaminifu kwa mwenzi wake wa sasa na kutangaza amekubali kupata hati ya kisheria ya ndoa baadaye, mke halali aliyemwacha akifa au hali nyingine zikimwezesha kupata hati hiyo. Ikiwa mwenzi wake wa sasa ataka kubatizwa, yeye pia atapaswa kuandika taarifa hiyo na kuitia sahihi.

26. Mtu aweza kufanya nini ikiwa wakuu wa serikali hawataki kutambua ndoa yake kisheria?

26 Katika nchi moja ya Amerika ya Kusini, ingawa sheria inaruhusu kufuta ndoa mtu akiwa ana wenzi wawili, mara nyingi “Kaisari” hajishughulishi na maombi ya kuifuta. Basi, fikiria mwanamume ambaye ametengana na mkewe wa halali aliye hai, akaoa mwanamke mwingine na kupata hati ya kisheria kwa kusema uongo. Akiisha kujifunza kweli ya Biblia atake kubatizwa, huenda akaona anashindwa kuandikisha ndoa yake ya sasa kisheria kwa sababu wakuu wa serikali hawataki kushughulika na jambo hilo. Akishindwa kufanya ndoa yake ya sasa itambuliwe na mahakma au wakuu wa Kaisari, atafanyaje? Aweza kutia sahihi tangazo linalofanana na la Kaisari akiahidi kuwa mwaminifu na kupelekea kundi tangazo hilo liwekwe katika faili. Ndipo aweza kukubaliwa abatizwe, na mwenzi wake pia aweza kukubaliwa akifanya vivyo hivyo.

27. Je! ni lazima mtu aache kubatizwa ikiwa ndoa yake haiwezi kutambuliwa kisheria mpaka miaka kumi iishe? Kwa sababu gani?

27 Katika nchi fulani ya Afrika magharibi, huenda ikachukua hata miaka kumi kupata talaka. Je! mtu anayehitaji talaka ili kuhakikisha kisheria kwamba sasa ameoa au ameolewa atalazimika kuacha kubatizwa kwa kipindi cha miaka mingi? Kwa sababu Kaisari hataki kumtambua kisheria, haionekani inafaa azuiwe kuonyesha anaamini dhabihu ya Kristo yenye uwezo wa kulipia dhambi kwa kuchukua hatua bora ya ubatizo na kupata pendeleo la kuwa na uhusiano unaokubaliwa na Mungu. (Linganisha maneno ya mtume katika Matendo 11:17 yanayoonyesha wanadamu hawawezi “kumpinga” Mungu asikubali watu.) Mifano ya Biblia yaonyesha kwamba si vizuri kukawia kubatizwa bila sababu. (Matendo 2:37-41; 8:34-38; 16:30-34; 22:16) Akiisha kuanza kufuata mpango wa kisheria wa kutafuta talaka, mtu huyo sasa atalipa kundi taarifa yenye kuahidi kwamba atakuwa mwaminifu, hivyo ahakikishe kwamba amekaza nia kuendelea kuheshimisha ndoa yake ya sasa huku akijitahidi kuifanya itambuliwe kisheria na Kaisari.

28. Ikiwa ndoa yaweza kutambuliwa kisheria baada ya mtu kupata talaka, lakini talaka haiwezi kupatikana katika nchi yake, je! hiyo yamaanisha kwamba waliooana lazima watengane ikiwa wanataka kubatizwa?

28 Huenda watu wakahamia nchi nyingine, wakajifunza kweli wakiwa huko na kutaka kubatizwa. Ili ndoa yao ya sasa itambuliwe kisheria, huenda kwanza wakapaswa kupata talaka waachane na wenzi wao wa zamani. Pengine nchi ambayo wamehamia ina mipango ya talaka, lakini huenda wasiweze kufanyiwa mipango hiyo maana ni wageni. Kwa mfano, watu wengi kutoka nchi nyingine za Ulaya wamehamia Ujeremani wakitafuta kazi. Ingawa Ujeremani ina mipango ya talaka, watu wasio raia za nchi hiyo hawawezi kufanyiwa mipango hiyo. Katika visa vya namna hiyo, watu wanaotaka kubatizwa na kuhakikisha kwamba ndoa yao inaheshimika na ni ya kudumu watapaswa kutia sahihi tangazo la kuahidi kuwa waaminifu.

29. Mkristo awezaje kuhakikisha kwamba kulingana na Maandiko ana uhuru wa kuoa au kuolewa tena katika nchi ambazo haziruhusu kutoa talaka?

29 Kanuni izo hizo zitatumika kwa Mkristo aliyebatizwa asiyeweza kutambuliwa na sheria za “Kaisari” ili kutumia haki alizopewa na Mungu za kutoa talaka na kuoa au kuolewa tena. Kwa mfano, katika nchi zisizotambua haki iliyotolewa na Mungu ya kumpa talaka mwenzi mzinzi na kuoa au kuolewa tena, mtu ambaye mwenzi wake amekuwa asiyeaminika (na ambaye ameamua kuachana naye, asimsamehe) apaswa kuwapa wazee wa kundi ushuhuda ulio wazi juu ya kutoaminika kwa mwenzake. Halafu, wakati ujao yeye (au mwenzake) aweza kuoa au kuolewa na mtu mwingine kwa njia yenye kuheshimika akitaka, kisha wote wawili watie sahihi katika taarifa za kuahidi kuwa waaminifu na kukaza nia wajitahidi kutambuliwa kisheria wakati wo wote iwezekanapo.

30. Kundi lapaswa lioneje tangazo la watu la kuwa waaminifu katika nchi ambazo ndoa inayopatana na Maandiko haitatambuliwa kisheria katika hali fulani?

30 Kundi linaona kwamba mwenye kutia sahihi taarifa hiyo ya kuahidi kuwa mwaminifu anajiweka katika kumbukumbu mbele za Mungu na wanadamu kwamba atakuwa mwaminifu kwa ndoa yao ya sasa kama vile ambavyo angekuwa kama ndoa hiyo ingehalalishwa na wakuu wa serikali. Tangazo hilo linaonekana kuwa lenye kudumu kama lile linalofanywa mbele ya mkuu wa ndoa anayewakilisha serikali ya “Kaisari” ya ulimwengu. Kwa kweli, namna ya hati inayoandikwa siyo inayolifanya liwe jambo lisilo la mchezo, bali ni uhakika wa kwamba mtu huyo amefanya tangazo mbele za Mungu.

31, 32. Tangazo la kuwa na uaminifu laweza kutaja mambo gani makuu, na lapaswa lifanyiweje?

31 Tangazo hilo laweza kuandikwaje? Laweza kuwa na maneno kama yanayofuata:

“Mimi, . . . . . . . , natangaza hapa kwamba nimemkubali . . . . . . . . . .awe mwenzi wangu katika uhusiano wa ndoa; kwamba nimejitahidi niwezavyo kufanya uhusiano huu utambuliwe kisheria na wakuu wa serikali na kwamba, kwa sababu’ nimeshindwa kutambuliwa, nafanya tangazo hili niahidi kuwa mwaminifu katika uhusiano huu wa ndoa. Natambua kwamba uhusiano huu ni wenye kudumu mbele za Yehova Mungu na mbele ya watu wote, nami napaswa kushikamana nao na kuuheshimu kulingana na kanuni za Neno la Mungu. Nitaendelea kutafuta njia za kufanya uhusiano huu utambuliwe kisheria na wakuu wa serikali, tena naahidi kuandikisha mwungano huu kisheria hali zikibadilika ziniwezeshe kufanya hivyo.

“Limetiwa sahihi siku hii ya . . . . . . . . . . ya . . . . . . ...,  19. . . .. Mashahidi wa sahihi yangu: . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . ”

32 Kama ilivyoonyeshwa juu, tangazo hilo lapaswa kutiwa sahihi na mwenye kulifanya na washuhudiaji wengine wawili vilevile, na tarehe pia iandikwe. Inashauriwa kila mmoja wa watu wanaohusika aweke nakala ya taarifa ya kuahidi kuwa mwaminifu, hata kundi wanaloshirikiana nalo, na nakala moja ipelekwe kwenye afisi ya Tawi ya Watch Tower Society katika eneo hilo. Kwa habari ya Wakristo waliobatizwa ingefaa pia kundi litangaziwe kwamba tangazo hilo limefanywa ili wote wazijue hatua za uaminifu zinazochukuliwa kuhakikisha kwamba ndoa ni yenye kuheshimika.

33. Lazima mtu ajichukulie mwenyewe daraka gani linalohusiana na tangazo la uaminifu?

33 Ikiwa mtu ameshindwa kutambuliwa na “Kaisari” lakini akachukua hatua zinazofaa kuhakikishia kundi habari za ndoa yake, lazima ajue kwamba itakuwa juu yake kupambana na mambo yo yote yatakayompata huko nje ulimwenguni. Kwa mfano, suala fulani la kisheria linalohusu mali au haki za urithi likitokea kwa sababu ya ndoa yake ya zamani, hawezi kudai “Kaisari” amtetee mahakmani kuhusu ndoa yake mpya isiyotambuliwa.

KUWEKA WAZI KANUNI ZILIZO KUU

34. Kwa habari ya ndoa na talaka, ni maandishi gani yanayopaswa kukatia Mkristo maneno?

34 Katika nchi mbalimbali, sheria za ndoa na talaka zinatofautiana sana. Badala ya Mkristo au anayetaka kuwa mwanafunzi wa Mwana wa Mungu kuvurugwa akili kwa kujitia katika mambo magumu sana, aweza kuongozwa na kanuni kuu za Maandiko zinazotumika katika visa vyote.

35. Maandiko yanatoa maoni gani juu ya kuwa na mke wa kuwekwa tu na kufanya zinaa?

35 Maoni ya Mungu ndiyo yanayopaswa kufikiriwa kwanza. Kwa hiyo, kwanza lazima mtu afikirie kama uhusiano wake wa sasa, au uhusiano ambao anafikiria kuingia, unaweza kukubaliwa na Mungu au unavunja kanuni za Neno Lake. Kwa mfano, fikiria mwanamume anayeishi na mke lakini anatumia wakati fulani akiishi na mwanamke mwingine wa kuwekwa tu. Maadamu mwanamke huyo wa kuwekwa angalipo, uhusiano wake naye hauwezi kamwe kupatana na kanuni za Kikristo hata ye yote kati yao akifanya tangazo. Njia ya pekee inayofaa ni kukomesha uhusiano huo. Ndivyo ilivyo pia ikiwa mtu anaishi katika zinaa pamoja na mtu wa jamaa yao hasa, ikiwa ni hanithi (mume mwenye kuishi katika ndoa na mume mwenzake), au ikiwa ana hali nyingine kama hiyo inayokatazwa na Neno la Mungu. (Mt. 19:5, 6; 1 Tim. 3:2; 1 Kor. 5:1) Uhusiano wa namna hiyo haukataliwi kwa sababu ya kutohalalishwa kisheria; unakataliwa kwa sababu haupatani na Maandiko, na kwa hiyo ni ufisadi. Kwa hiyo, mtu aliye katika hali hiyo hawezi kufanya ‘tangazo la uaminifu’ la namna yo yote, maana haliwezi kuwa na ubora wo wote machoni pa Mungu.

36. Mtu ambaye hakuheshimu sana mpango wa ndoa kabla ya kujifunza kweli atakiwa afanye nini?

36 Ikiwa uhusiano unaweza kukubaliwa na Mungu, kanuni ya pili inayopaswa kufikiriwa ni ile inayosema kwamba yampasa mtu ajitahidi awezavyo ahakikishe kwamba ndoa yake inaheshimika machoni pa watu wote. (Ebr. 13:4) Huenda mtu anayetaka kubatizwa akawa alitengana zamani na mwenzi wake wa kisheria bila kupata talaka, kisha akaoa au akaolewa na mtu mwingine. Huenda wakati mwingi ukawa umepita, na amepata watoto. Kwa hiyo, baada ya mtu huyo kujifunza kweli, hawezi kutazamiwa arudie mwenzi wake wa kwanza ajaribu kupatanisha maisha yake na hali zake za zamani. Lakini sasa, kwa kuwa ‘ameachana na dhambi,’ lazima aamue kwamba tangu sasa ataishi kulingana na mapenzi ya Mungu.​—1 Pet. 4:1-3; linganisha 1 Wakorintho 7:17-24.

37. Huenda ikampasa mtu achukue hatua gani ili ndoa yake ya sasa itambuliwe kisheria?

37 Tusemeje basi? Ikiwa talaka inaweza kupatikana, hatua hiyo yapaswa kuchukuliwa sasa ili baada ya kupata talaka (kwa kutegemea sababu zo zote zinazoruhusiwa na sheria), ndoa ya sasa itambuliwe na serikali. Mambo hayo hayo yatahusu mtu ambaye, kabla ya kujifunza kweli, amekuwa na hatia ya kuwa na wenzi wawili wa ndoa. Yampasa achukue hatua zilizo za lazima kumaliza tatizo hilo kisheria (kwa kufuta ndoa na/au kutoa talaka) ili sasa aweze kutambuliwa kuwa mwenzi wa kisheria wa mtu mmoja tu.

38. Mtu aweza kuonyeshaje kwamba ataka ndoa yake inayokubaliwa na Mungu iwe yenye kuheshimika ingawa ameshindwa kuifanya itambuliwe kisheria?

38 Mwisho, ikiwa ndoa haipingani na kanuni za Neno la Mungu, na mtu amejitahidi awezavyo kuifanya itambuliwe na wakuu wa serikali lakini akakataliwa, aweza kutia sahihi tangazo la kuahidi kuwa mwaminifu. Kama tulivyoona, huenda ndoa isihalalishwe kisheria kwa muda wa miaka mingi kwa sababu wakuu wanakawia mno. Au labda gharama zinakuwa nyingi mno hata zinamfanya mtu huyo ahitaji miaka mingi kuweza kuzilipa. Inapokuwa hiyo tangazo la kuahidi kuwa mwaminifu litalipa kundi msingi wa kuona ndoa ya sasa kuwa yenye kuheshimika, huku mtu huyo akiendelea kwa uaminifu kujitahidi awezavyo aandikishe ndoa kisheria. Linalostahili kuangaliwa ni kwamba katika mitaa mingi, na hata katika nchi nzima, watu wenyewe hawaoni kuandikisha ndoa kuwa jambo la maana, nao wanaongozwa hasa na mambo wanayoona yanahakikisha ndoa zao ni zenye uaminifu. Hata ikiwa hivyo, yampasa Mkristo ajitahidi kuchukua hatua zo zote anazoweza, ahakikishe kabisa kwamba ndoa yake ni yenye kuheshimika.

39. Wakristo wanaweza kuwa na hakika gani wanapojaribu kuendeleza ndoa katika hali yenye kuheshimika?

39 Kwa kukumbuka kanuni kuu zilizotolewa, Mkristo ataweza kuwa na maoni yaliyosawazika, bila kudharau uhalali unaotolewa na serikali na bila kuuheshimu kupita kiasi. Yampasa sikuzote afikirie kwanza maoni ya Mungu juu ya ndoa yake. Tena, yampasa ajitahidi awezavyo aweke mfano mwema wa kuwa mwaminifu sana kwa mwenzi wake, hivyo aendelee kufanya ndoa yao ‘iheshimiwe na watu wote.’ Atabarikiwa na Mungu na kumletea Mwanzishi wa ndoa, Yehova Mungu, heshima na sifa.​—1 Kor. 10:31-33.

​—Kutoka The Watchtower, Mar. 15, 1977.

[Maelezo ya Chini]

a Katika sheria ya Kirumi, “sharti la pekee lililohusu ndoa” ni “kukubaliana kwa wenye kuoana,” nayo leseni haikutakiwa, wala sherehe wala uhakikisho. (The New Schaff-Herzog Religious Encyclopedia, Vol. VII, kur. 198, 199) Hivyo, ikiwa mwanamume alichumbia mwanamke akakubali kuolewa, hilo peke yake ndilo lililotakiwa na sheria ili ndoa iwe halali.

b Kama vitabu vinavyoonyesha, Kanisa Katoliki mwishowe lilijidai kuwa na haki ya pekee ya kuweka sheria zinazohusu ndoa, likatokeza sheria na vizuizi vyake lenyewe na kushikilia kwamba lazima wakuu wa serikali waongozwe na sheria hizo. Waprotestanti wenye kufanya Matengenezo ya kanisa walikuwa tofauti sana wakaachia wakuu wa serikali waamue karibu mambo yote yaliyohusu ndoa. Katika Uingereza, Scotland na Ireland sherehe ya kiserikali ilianzwa mwaka 1653 ili kukomboa Kanisa na mambo ya kilimwengu. Sheria ya Kifaransa ya 1792 ilifanya iwe lazima sherehe ya kiserikali ifuatwe na raia wote kwa kutegemea kanuni ya kwamba “raia ni mali ya Serikali, hata awe wa dini gani.” (The New Schaff-Herzog Religious Encyclopedia, Vol. VII, kur. 199, 200)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki