Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Je! Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu katika uhusiano wa ndoa unaoendelea lina udumifu ule ule kama ndoa iliyoandikishwa kisheria?
Jambo hilo linahusu ule mpango wa pekee unaokubaliwa utumike katika nchi zile tu ambako hairuhusiwi chini ya sheria kumpa talaka aliyekuwa mwenzi wa ndoa. Kwa kufaa Wakristo wanataka kujua jambo hilo, kwa maana Neno la Mungu linaonyesha jinsi yeye anavyouona kwa uzito mpango wa ndoa. Kwa kweli, mtume Paulo aliandika hivi: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Waebrania 13:4) Kwa hiyo, acheni tuangalie namna ya hali inayotokeza ulizo hilo:
Tuseme mwanamume na mwanamke wanafikiwa na ukweli wakiwa katika uhusiano wa ndoa ambao hauwezi kuandikishwa kisheria, na hali mmoja wao au wote wawili wanatamani kupata ubatizo wa Kikristo. Lile tangazo linakuwa la kuahidi uaminifu kwa uhusiano huo wa ndoa mpaka wakati ambao itawezekana kuandikisha kisheria muungano huo kulingana na sheria ya nchi. Mnara wa Mlinzi wa Agosti 15, 1977, ukurasa 380, ulipendekeza jinsi maneno ya tangazo hilo yanavyoweza kupangwa nao ukasema: “Tangazo hilo linaonekana kuwa lenye kudumu kama lile linalofanywa mbele ya mkuu wa ndoa anayewakilisha serikali ya “Kaisari” ya ulimwengu.”—Ona maneno ya Yesu kwenye Mathayo 22:21.
Lakini, hali inakuwaje ikiwa “Kaisari” anabadili sheria ya talaka, kama ilivyotukia majuzi katika Italia? Kwa kuwa sasa inawezekana kumpa talaka aliyekuwa mwenzi wa ndoa, Mkristo aliyebatizwa anayeishi katika uhusiano wa ndoa unaotegemezwa na Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu ni lazima achukue hatua bila kukawia, kulingana na lilivyosema tangazo lile, “kufanya uhusiano huu utambuliwe kisheria.” Hatua ya kwanza ingekuwa kumpa talaka aliyekuwa mwenzi wa ndoa hapo awali. Hatua inayofuata ingekuwa kuiandikisha ndoa kisheria pamoja na mwenzi wa sasa. Hata kama mwenzi wa sasa ni asiyeamini, huyo angehitajiwa aukubali uandikishaji huu wa kisheria wa ndoa. Mtu huyo asiyeamini akikataa kufanya hivyo, mwenzi Mkristo angelazimika kujitenga naye ili adumishe msimamo unaokubaliwa katika kundi. Sababu ya jambo hilo ni kwamba lile Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu haliwezi tena kutambuliwa na kundi kuwa halali, kwa sababu sasa njia imekwisha kufunguka ya kuwa na ndoa ya kisheria.
Lakini, njia hiyo inapofunguka na kwa kweli wale wawili wanaoana, ndoa hiyo ya kisheria inawafunga daima, tofauti na lile Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu, ambalo lilikuwa ni mpango wa muda fulani tu usiopasa kuchezewa.