Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Mtu akiisha kutia sahihi Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu, je! mpango huo unaweza kukomeshwa?
Ulizo hilo linahusiana na uandalizi ambao hautumiki katika nchi zilizo nyingi. Kwa hiyo acheni kwanza tuone huo mpango wa muda usiopaswa kuchezewa uko namna gani.
Mnara wa Mlinzi wa Agosti 15, 1977, ulizungumza tatizo moja lililo katika nchi fulani-fulani. Ingawa Mungu anaruhusu talaka juu ya sababu za Kimaandiko, serikali fulani-fulani hazina uandalizi wa talaka. (Mathayo 19:9) Au huenda sheria ikafanya iwe vigumu sana kupata talaka, labda jambo hilo litakwe kuchukua miaka mingi. Kwa sababu hiyo, toleo la gazeti hilo lilieleza kwamba Mashahidi wa Yehova wana mpango fulani wa kuiruhusu unaotumika tu katika nchi kama hizo; huo unahusu Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu. Fikiria mfano mmoja wa mpango huo:
Mwanamke anakuja kwenye maarifa ya ukweli wa Kikristo huku akiishi pamoja na (labda pia akiwa na watoto kutokana na) mwanamume ambaye tangu muda mrefu amekuwa katika hali ya kutengana na mke wake wa kisheria. Mwanamke huyu aliyeanza kupendezwa karibuni ni mwaminifu kwa mwanamume huyo na anataka aolewe naye, lakini jambo hilo haliwezekani kwa sababu sheria haimruhusu mwanamume ataliki mke wake wa kisheria. Kwa sababu hiyo, ikiwa wazee wa kundi wanasadiki kwamba uhusiano wa mwanamke huyo pamoja na mwanamume huyo ungekubaliwa na Mungu kwa njia fulani, wao watamruhusu mwanamke huyo atie sahihi katika Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu. Humo yeye anakuwa akisema kwamba amefanya yote ambayo anaweza ili kuandikisha kisheria uhusiano huo; kwamba yeye anakiri mbele za Mungu kuwa Tangazo Rasmi hilo ni lenye kifungo cha kudumu; na kwamba yeye anaahidi kuolewa kisheria mara tu jambo hilo likiwezekana, na hivyo akomeshe Tangazo Rasmi lililokuwa limemwezesha awe sehemu ya kundi la Kikristo.
Ijapokuwa hivyo, ulizo linatokea: Yeye (au mtu ye yote aliye katika hali hiyo) akiisha kuingia ndani ya kundi akiwa chini ya Tangazo Rasmi kama hilo, je! kuna njia nyingineyo yote ambayo linaweza kukoma au lingeweza kukomeshwa?
Tangazo Rasmi lenyewe linasema kwamba mwenye kulitia sahihi ‘anatambua uhusiano wake, awe ni mwanamume au mwanamke, kuwa ni kifungo chenye kudumu mbele za Yehova Mungu na mbele ya watu wote, kinachopasa kushikiliwa na kuheshimiwa kupatana kabisa na kanuni za Neno la Mungu.’ Hivyo, kutokana na maoni ya kundi, Tangazo Rasmi hilo ni kifungo chenye kudumu kiadili kama ndoa ya kisheria. Ijapokuwa hivyo, kifo cha mwenzi kinamaliza ama ndoa ama muungano ulio chini ya Tangazo Rasmi kama hilo. (Warumi 7:2) Biblia inasema kwamba ikiwa mwenzi wa ndoa wa mtu ana hatia ya por·neiʹa (ukosefu wa adili wa ngono nje ya muungano ule), mwenzi asiye na hatia anaweza kupata talaka. (Mathayo 5:32; 19:9) Kwa kutoa ulinganifu, chini ya Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu, ukosefu wa adili wenye kutendwa na mwenzi wa ndoa unaweza kuwa msingi wa kukomesha muungano ule, ikiwa yule asiye na hatia anachagua hivyo. Mkristo asiye na hatia angepaswa athibitishie wazee uhakikisho wa kwamba kitendo cha kutoaminika kilifanywa. Jambo hilo lingekomesha Tangazo Rasmi lile; baada ya hapo yule asiye na hatia angekuwa huru Kimaandiko.
Kutambua kwamba kundi linafikiria Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu kuwa ni kifungo cha kudumu kiadili kama ndoa ya kisheria kunatokeza suala linalohusiana na hilo. Jambo hilo linatokea wakati kinapoondolewa kizuizi kile kilichokuwa kikizuia ndoa. Kwa mfano, katika kisa kilichotangulia kutajwa, mke wa kisheria wa mwanamume huyo angeweza kufa au serikali ingeweza kuandikisha kisheria talaka yao, naye awe na nia ya kumwoa kisheria mwanamke yule Mkristo. Inapokuwa hivyo, dada yule hawezi kuendelea kuwa chini ya Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu, hata kwa sababu zinazofanana na jambo la kwamba inatia haya kufunga ndoa kisheria sasa au kwa sababu dada huyo angeweza kupoteza faida fulani za kimwili. Kupatana na Tangazo Rasmi lake, ni lazima yeye sasa achukue hatua za kuandikisha kisheria muungano wao. Au sivyo, kundi lingetangua Tangazo Rasmi lile, na dada huyo angelazimika kujitenga na mwanamume yule au sivyo atengwe na ushirika.
Ingawa hivyo, namna gani ikiwa yule asiyeamini anakataa kuoa kisheria dada yule? Wakati dada alipotia sahihi Tangazo Rasmi, kundi liliuona muungano huo kuwa kifungo cha kudumu na cha kiadili. Sasa muungano huo haugeuki kuwa usio wa adili ati kwa sababu tu dada ameshindwa kulazimisha mwenzi wake asiyeamini aandikishe muungano wao kisheria. Kwa hiyo angeweza kuendelea kuwa mwenzi mwaminifu, asihitaji kujitenga na mwanamume huyo, ingawa inampasa dada aendelee tu na jitihada zake kuelekea kufanya muungano ule uandikishwe kisheria. (Hiyo inarekebisha maelezo katika “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi wa Novemba 1, 1985.)—Linganisha Waamuzi 11:35; Luka 18:1-5.
Bila shaka, hali iko tofauti ikiwa wote wawili walitia sahihi Tangazo Rasmi na wakawa Wakristo waliobatizwa. Ikiwa hivyo, wote wawili walijikabidhi bila mchezo katika wajibu wa kuingia ndani ya ndoa ya kisheria kizuizi cha kiserikali kikiondolewa, kwa maana hapo ndipo Tangazo Rasmi lingekomeshwa. Wao wana wajibu wa kufanya hivyo katika muda fulani wa kiasi kinachofaa, au sivyo watengane ili kubaki katika kundi. (Linganisha “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi wa Februari 1, 1983.) Wakitengana, bado Tangazo Rasmi lile lililo kifungo cha kudumu kiadili linatumika kwao, kwa hiyo hakuna ye yote kati yao aliye na uhuru wa kuingia ndani ya muungano pamoja na mtu mwingineye yote.—Linganisha 1 Wakorintho 7:10,11.
Ingawa katika mahali pengi mpango wa Tangazo Rasmi la Kuahidi Uaminifu hautumiki, mazungumzo yaliyotangulia yanategemea kiwango cha Biblia kinachotumika kila mahali: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atahukumu waasherati na wazinzi.”—Waebrania 13:4, NW.