Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Ubora wa rafiki
Mtu “mpweke” anayefanya kazi kwa bidii katika kulundika utajiri kwa hakika ana maisha yasiyo na maana. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Kuna mtu aliye peke yake, wala hana wa pili wake [yaani, mtu mpweke asiye na rafiki au mwenzi]; naam, hana mwana wala ndugu; hata hivyo [kazi yake ya bidii] haina mwisho, wala macho yake hayashibi utajiri. Basi asema, Ni kwa ajili ya nani nafanya kazi, na kujinyima nafsi yangu mema? Hayo nayo ni ubatili, naam, ni taabu kubwa.” (Mhu. 4:8) Namna yasivyo na maana maisha ya mpenda fedha asiye na rafiki, mwana au ndugu naye hata havuni faida kutokana na kazi yake ya bidii! Yeye anaendelea tu kulundika utajiri, asitake kutumia fedha zo zote kununua vitu ambavyo vyaweza kufanya maisha yake kuwa yenye raha na furaha zaidi. Hata hivyo, wakati wa kufa, analazimika kuacha kila kitu. Ubatili kama nini!
Ni afadhali sana mtu anayefanya kazi na rafiki mzuri. Mwenye hekima anaendelea hivi: “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja; maana wapata [zawadi] njema kwa kazi yao.” (Mhu. 4:9) Kufanya kazi kwao pamoja kunaleta faida, ‘zawadi njema,’ kwa namna ya usaidizi, faraja na ulinzi. Mfalme Sulemani anasema hivi: “Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake. [Hiyo ni kwa sababu haielekei kwamba wote wawili wataanguka wakati ule ule.] Lakini ole wake aliye peke yake aangukapo, wala hana mwingine wa kumwinua! Tena, wawili wakilala pamoja [kama vile inapokuwa lazima kukaa pamoja kwenye baridi wakati wa safari], hapo watapata moto; lakini mmoja aliye peke yake tu awezaje kuona moto? Hata ikiwa mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake [mtu ambaye aweza kuwa akisafiri katika barabara yenye hatari], wawili watampinga; wala kamba ya nyuzi tatu [ambayo ni yenye nguvu zaidi kuliko ile yenye uzi mmoja au nyuzi mbili] haikatiki upesi.”—Mhu. 4:10-12.
Je! wewe unaishi kulingana na maana ya maneno hayo? Kwa hakika kuna ubora mwingi wa kuwa na rafiki wenye kutegemeka.
Hata Cheo cha Juu Zaidi Ni Ubatili
Kati ya wanadamu kupendwa na wengi ni jambo la muda mfupi tu. Mtu mwenye kujulikana sana anasahauliwa upesi wakati mtu mwingine anapovutia zaidi mioyo ya watu. Hata wale wanaopata vyeo vya juu zaidi wanahusika.
Mfalme Sulemani mwenye hekima alisimulia kwa kweli jambo linaloweza kuwapata watawala. Twasoma hivi: “Heri kijana maskini mwenye hekima kuliko mfalme mzee mpumbavu, ambaye hajui tena kupokea maonyo. Kwa maana kutoka gerezani [kijana huyo] alikuja kumiliki; naam, hata katika ufalme wake alizaliwa hali ya umaskini.”—Mhu. 4:13, 14.
Mtu aweza kuona moyoni kwamba kuwa kwake na cheo cha juu zaidi, ufalme, pamoja na umri na ujuzi wake, kwapaswa kumstahilisha heshima na kuungwa mkono na watu wote. Walakini, kijapokuwa cheo na umri wake, mfalme hatapewa heshima ya kutoka moyoni iwapo anatenda kipumbavu, akikataa kusikiliza mashauri mazuri ya wengine. Cheo na umri, vyenyewe, havitoi uhakika wa kupata heshima. Hiyo ndiyo sababu kijana maskini lakini mwenye hekima ni afadhali sana kuliko mfalme ambaye wakati mmoja alitawala kwa hekima walakini katika umri wake wa uzeeni anashikilia njia zake naye hasikilizi mashauri mema. Kwa kutoyaongoza mambo vizuri mfalme huyo mzee aweza kuuingiza ufalme wote katika deni kubwa sana, akose kupatana na raia zake na hata aweza kupinduliwa na kufa katika aibu. Kwa upande mwingine, kijana anayeendelea kutenda kwa hekima, anaweza kupata heshima ile ile asiyopewa mfalme mzee lakini mpumbavu.
Kama vile Sulemani alivyoandika, kijana huyo mwenye hekima aweza kukwezwa kutoka gerezani mpaka kuwa na ufalme. Ndivyo ilivyokuwa kwa Yusufu. Farao wa Misri alivutiwa sana hata akamwambia hivi: “Hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe.” (Mwa. 41:39, 40) Hivyo Yusufu alikwezwa kuwa mtawala mwenye cheo cha pili katika Misri.
Kisha, akikaza fikira juu ya hali ya watu ya kuwa na kigeugeu kwa kubadilishwa kwa watawala, Sulemani anaandika hivi: “Nikawaona wote walio hai waendao chini ya jua, ya kwamba walishikamana na huyo kijana, huyo wa pili aliyesimama badala ya yule. Hawakuwa na kikomo hao watu wote, hao wote ambao alikuwa juu yao; lakini hata hivyo wale wafuatao baada yake hawatamfurahia. Hakika hayo pia ni ubatili, na kujilisha upepo.”—Mhu. 4:15, 16.
Sulemani alimaanisha nini kwa usemi “kijana, huyo wa pili”? Kwa wazi alikuwa akimtaja mrithi wa mfalme huyo. “Wote walio hai” wana shauku ya kuwa na mtawala mpya. ‘Hakuna kikomo kwa watu wote’ ambao anasimama mbele yao kama mfalme. Hiyo maana yake ni kwamba wote wanamwunga mkono, wakitegemeza utawala wake. Walakini kupendwa kwake na watu wengi hakuendelei milele. Wakati unafika upesi ambao katika huo yule ambaye watu walimsifu sana hafai tena kwao. Sasa wakiwa wamemkinai, wanaacha kumfurahia.
Vivyo hivyo, katika nyakati za kisasa, kikundi kimoja cha wanasiasa kinachukua mahali pa kingine. Kwaweza kuwa shauku ya kwanza kwa gavana, waziri mkuu au rais fulani. Walakini haiwachukui watu muda mrefu kabla ya kuacha kupendezwa na mtu huyo na maongozi yake. Upesi wanaanza kumtafuta mtu mwingine achukue uongozi wa serikali.
Basi, kwa hakika, hata cheo cha juu zaidi huwa bure, “ubatili.” Jambo hilo linakazia kwa nguvu kama nini kwamba katika ulimwengu huu mali yenye kuridhisha zaidi, si cheo, bali uhusiano mzuri pamoja na Baba wa milele, Yehova!