Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Mathayo 10:9, 10, inaweza kupatanishwaje na Marko 6:8, 9?
Mistari hiyo inataja kidogo maagizo ambayo Yesu aliwapa mitume kumi na wawili alipokuwa akiwatuma wakahubiri. Mathayo 10:9, 10 inasema: “Msichukue . . . mkoba wa safari, wala kanzu mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake.” Nayo Marko 6:8,9 inasema: “Akawakataza wasichukue kitu cha njiani isipokuwa fimbo tu; wala mkate, wala mkoba, wala pesa za bindoni; lakini wajifungie viatu; akasema, Msivae kanzu mbili.”—Linganisha Luka 9:3.
Ni wazi kwamba Yesu hakuwatazamia mitume wafunge safari wakiwa na njaa, wakiwa uchi au bila viatu. Lakini haikuwa lazima wafanye matayarisho ya pekee, kama kununua au kuvaa “kanzu mbili.” Mavazi na viatu (ndara) ambavyo walikuwa wamevaa vilitosha. Vivyo hivyo, ikiwa walikuwa wamekwisha kuwa na fimbo, wangeweza kuichukua, lakini wasinunue wala wasitafute nyingine ya kutumia safarini.
Hasa, Yesu alikuwa akiwashauri hivi: ‘Nendeni kama mlivyo, mkiwa na mavazi, viatu na fimbo mlizo nazo. Msijifanyie mipango yenu wenyewe; wale watakaousikia ujumbe wenu na kuukubali watawakaribisha na kuwasaidia, kwa maana mfanya kazi anastahili chakula chake.’ Hayo yalipatana na mashauri ya Yesu katika Mahubiri juu ya Mlima. (Mt. 6:25-34) Badala ya kujitwika mzigo wa vitu vingi mno vya kimwili, mitume wangeweza kukaza fikira juu ya mgawo wao wakiamini uhakikisho waliopewa na Yesu kwamba wangetunzwa.