“Mti” Ambao Anguko Lake Lashtua Ulimwengu
“Niliwatetemesha mataifa kwa mshindo wa kuanguka kwake, hapo nilipomtupa chini mpaka kuzimu, pamoja nao washukao shimoni; na miti yote ya Adeni, miti iliyo miteule na iliyo mizuri ya Lebanoni, yote inywayo maji, ilifarijika pande za chini za nchi.”—Eze. 31:16.
1. Kwa sababu gani kuangusha mti kunaweza kuhuzunisha watu?
SISI wanadamu twaweza kupenda mti. Kwa sababu ya kupenda sana mti, mtunga mashairi alimteta mtu mwenye shoka akamwambia (kwa Kiingereza): “Ee Mchanja kuni, mti uache! Hata tanzu moja usiliguse! Mti ulinikinga ujanani, sasa mti nitaulinda nami.” Mti uliokwisha kua kabisa unaweza kupendeza sana watazamaji wengi unapokuwa wenye fahari. Uzuri wa miti ulimfurahisha sana mtunga mashairi huyo hata akasema (kwa Kiingereza): “Nadhani mimi sitaona kamwe shairi lapendeza kama mti. . . . Wapumbavu mashairi ni yetu. Mungu peke yake afanya mti.” Kuangusha mti kunaweza kuhuzunisha watu wanaothamini sana ufundi huo wa Mungu.
2. Kwa habari ya ibada ya miti, ni vizuri tujiulize maulizo gani?
2 Duniani pote watu wanaabudu miti. Linaloonyesha kwamba miti inaabudiwa ni vile wanadini wanaoadhimisha Desemba 25 kila mwaka wanavyosisitiza kwamba kipindi hicho kiwe na mti uliopambwa mno, mti usiokauka wenye taa zenye kung’aa. Kwa maelfu ya miaka kuna “mti” mmoja ambao umependeza sana wanadamu wote. Maoni yao na matendo yao juu ya mti huo yanahakikisha kwamba wanauabudu “mti” huo mashuhuri ulimwenguni pote. Kwa sababu ya kutoamini hivyo, na kwa sababu ya kutaka kujua habari hizo, huenda tukauliza, Huo ni “mti” gani? Je! mimi nauabudu?
3. Kwa sababu gani wanadamu wanadhani “mti” huo hautaanguka kamwe?
3 Ni “mti” wa zamani, na sasa una miaka zaidi ya 4,200. Kwa hiyo habari zake zilielezwa na kuzungumzwa zaidi ya mileani mbili na nusu zilizopita. Twaweza kupata maelezo mazuri kwa kusoma maandishi ya zamani juu ya mti huo ambao umesimama muda mrefu sana ukatia mizizi imara katika dunia yetu, hata wanadamu wakadhani kwamba hauwezi kuanguka hata iweje. Haya ndiyo maelezo yake:
4, 5. Kulingana na Ezekieli 31:3-9, ni nini kinachoongeza uzuri usio na kifani wa “mti” huo?
4 “Mwerezi katika Lebanoni, wenye matawi mazuri, na kifuniko chenye uvuli, na kimo kirefu; na kilele chake kilikuwa kati ya matawi mapana. Maji yalimlisha, vilindi vilimsitawisha; mito [ya vilindi] ilipita pande zote za miche yake; [navyo vilindi vilipeleka] mifereji yake kwa miti yote ya kondeni. Basi kimo chake kilitukuzwa kuliko miti yote ya kondeni.
5 “Na vitanzu vyake viliongezeka; matawi yake yakawa marefu, kwa sababu ya maji mengi, alipoyachipuza. Ndege wote wa angani walifanya vioto vyao katika vitanzu vyake, na chini ya matawi yake wanyama wote wa kondeni walizaa watoto wao, na chini ya uvuli wake mataifa makuu yote walikaa. Basi hivyo alikuwa mzuri katika ukuu wake, katika urefu wa matawi yake; maana mizizi yake ilikuwa karibu na maji mengi. Mierezi ya bustani ya Mungu haikuweza kumficha; misunobari haikuwa kama vitanzu vyake, na miamori haikuwa kama matawi yake, wala bustanini mwa Mungu hamkuwa na mti wo wote uliofanana naye kwa uzuri. Nalimfanya kuwa mzuri kwa wingi wa matawi yake; hata miti yote ya Adeni, iliyokuwa ndani ya bustani ya Mungu, ilimwonea wivu.”—Eze. 31:3-9.
6. Kwa sababu gani mwanadamu hawezi kujipatia sifa ya kupanda mierezi ya Lebanoni?
6 Jamhuri ya Lebanoni imekuwa ikitajwa sana katika matangazo ya ulimwengu miaka ya majuzi, lakini sifa ya mierezi ya milima ya Lebanoni imevuma mileani nyingi. (Angalia Waamuzi 9:15.) Hakuna mwanadamu aliyeipanda mierezi hiyo inayoenea sana. Mierezi ilikuwako kabla lugha ya wanadamu haijavurugwa katika Mnara wa Babeli na kutawanya wajenzi pande zote kutoka Babeli ya kale iliyo katika Mto Frati, katika karne ya pili iliyofuata gharika ya dunia nzima. Muumba wa mbingu na dunia ndiye anayepata sifa ya kupanda mierezi hiyo. Kwa hiyo Zaburi 80:10 inaitaja kuwa “mierezi ya Mungu,” nayo Zaburi 104:16 inaiita “mierezi ya Lebanoni aliyoipanda [Yehova].”
7. Mungu alisema mwerezi ulikuwa wapi, na je! hiyo inamaanisha kwamba Paradiso ilirudishwa duniani?
7 Uhakika wa kwamba mierezi hiyo, pamoja na misunobari na miamori, inatajwa kwamba ilikuwa Edeni na katika “bustani ya Mungu” haumaanishi kwamba bustani ya Edeni ilirudishwa baada ya gharika ya siku za Nuhu, mwaka 2370 K.W.K. Bali, maana ni kwamba mahali ulipokuwa mwerezi huo palikuwa pazuri sana, uzuri wake ukiwa mfano wa Edeni, makao ya kwanza ya mwanadamu. Neno la Kiebrania la kusema “bustani” (gan) lamaanisha hasa “mahali palipozungukwa na ua”; nasi twakumbuka kwamba “bustani ya Edeni” ya kwanza ilikuwa na njia “upande wa mashariki” ambapo Adamu na Hawa waasi walipitia walipofukuzwa, kisha Mungu akapaweka makerubi “kuilinda njia ya mti wa uzima.”—Mwa. 3:24.
8. Ezekieli 28:11-14 ilisema kwamba mfalme wa Tiro, bandari ya Lebanoni, alikuwa wapi, na kwa sababu gani?
8 Siku za unabii wa Ezekieli, nchi ya Lebanoni yenye kuvuma sifa ya mierezi ilikuwa nzuri sana hata Mungu akamwongoza Ezekieli kumwambia hivi mfalme wa Tiro (ambayo ni bandari ya Lebanoni): “Ulikuwa ndani ya Adeni, bustani ya Mungu . . . Wewe ulikuwa kerubi mwenye kutiwa mafuta afunikaye; nami nalikuweka hata ukawa juu ya mlima mtakatifu wa Mungu.” (Eze. 28:11-14) Basi, ilifaa sana katika karne ya saba K.W.K. mwerezi huo “mzuri” sana wa Lebanoni ukatajwa kama kwamba ulikuwa katika Edeni, katika “bustani ya Mungu.” Basi ulikuwa katika cheo kikubwa chenye upendeleo, ulikuwa na matumaini mazuri.
MAANA YAKE MWAKA 1977 W.K.
9. Mwerezi huo “mzuri” wa Lebanoni unafananisha kitu gani, kulingana na vitu vinavyosemekana kwamba vinakaa chini ya uvuli wake?
9 Sisi tunaoishi nyakati za kisasa hatupendezwi sana na mambo ya miaka zaidi ya 2,500 iliyopita, bali twapendezwa hasa na mambo ya siku zetu, yanayotuhusu na kutupata. Kwa hiyo, je! mti huo “mzuri,” huo “mwerezi katika Lebanoni,” unafananisha kitu cho chote cha kisasa? Tutajuaje bila kukosea? Kwanza, zaidi ya unabii kusema kwamba ndege walikaa katika matawi yake mapana sana, na wanyama-mwitu wakazaa chini yake, unasema pia kwamba “chini ya uvuli wake mataifa makuu yote walikaa.” Vilevile: “[Mimi Yehova] niliwatetemesha mataifa kwa mshindo wa kuanguka kwake.” (Eze. 31:6, 16) Maneno hayo yana maana ya kisiasa. Yanaonyesha kwamba huo “mwerezi katika Lebanoni” uliosimama wima unafananisha kitu cha kisiasa. Hivyo ndivyo ilivyo!
10. Kupatana na maana yake ya kisiasa, unabii juu ya “mwerezi katika Lebanoni” unapewa kwa nani?
10 Hata matumizi ya kale ya unabii wa Ezekieli yahakikisha kwamba “mwerezi katika Lebanoni” ulifananisha kitu cha kisiasa. Huko nyuma, unabii huo ulitolewa kumhusu nani? Ezekieli anatueleza, akisema: “Ikawa katika mwaka wa kumi na mmoja [607 K.W.K.], mwezi wa tatu [mwezi wa masika wa Sivani], siku ya kwanza ya mwezi [siku tano kabla ya sikukuu ya Pentekoste], neno la [Yehova] likanijia, kusema, Mwanadamu, mwambie Farao mfalme wa Misri, na jamii ya watu wake, Je! umefanana na nani katika ukuu wako? Tazama, Mwashuru alikuwa mwerezi katika Lebanoni, wenye matawi mazuri, na kifuniko chenye uvuli, na kimo kirefu; na kilele chake kilikuwa kati ya [mawingu, tafsiri ya New World, Kiingereza].”—Eze. 31:1-3.
11. Ni jambo gani inaonyeshwa kwa kulinganisha Farao na watu wake na “Mwashuru”?
11 Kumbe! Sasa tumejua! “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake” ndio waliofananishwa na mwerezi mrefu ajabu, wenye matanzu marefu, ulio katika mlima mmoja wa Lebanoni. Wanasemekana kwamba wanafanana na “Mwashuru” pia, lakini hasa unabii wenyewe umetolewa kuhusu “mwerezi katika Lebanoni” na kuhusu jambo litakaloupata mwerezi huo, si “Mwashuru.” Kwa kuwa wanalinganishwa na “Mwashuru,” hiyo yaonyesha kwamba walikuwa na nguvu nyingi za kijeshi na kisiasa. Kufika miaka 25 iliyotangulia unabii wa Ezekieli, Milki ya Ashuru ilikuwa imekuwa ndiyo mamlaka ya ulimwengu siku hizo, ikaishinda nguvu Milki ya Misri iliyokuwa mamlaka ya ulimwengu ya unabii wa Biblia. Hata ilikuwa imechukua sehemu fulani katika eneo la Misri. Lakini sasa, katika siku za nabii Ezekieli, Misri ndiyo iliyokuwa mshindani mkuu wa Milki mpya ya Babeli, Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu. Kwa hiyo Farao na watu wake wanapolinganishwa na “Mwashuru,” hiyo inaonyesha kwamba hata wakati huo Babeli ilipaswa kujihadhari na Misri.
12. Hata siku za Ezekieli, Misri ilikuwaje kama ule “mwerezi katika Lebanoni,” wenye kufunika miti mingine yote kwa urefu wake?
12 Hata wakati wa Ezekieli serikali ya Kiyahudi ya Yerusalemu ilikuwa imeomba Misri iwasaidie kupigana na milki ya Babeli yenye kupanuka. (Eze. 17:7-17) Bila shaka Misri bado ilikuwa ikitegemewa na mataifa mengine. (Yer. 37:5-7) Basi Farao mfalme wa Misri na watu wake walikuwa bado na nguvu nyingi za kisiasa na kijeshi, nyingi kuliko urefu wa mierezi ya Lebanoni inayoweza kuwa ya futi 100 (mita 30) au zaidi. Kama vile mwerezi wa Lebanoni unavyotandaza matawi yake ya chini mbali sana na kufanya mwerezi mrefu zaidi uonekane kama kidude kidogo tu, ndivyo Misri ya wakati huo ilivyopinga Babeli na kujitolea kuyapa uvuli mataifa yaliyotaka kufanya mapatano na jeshi lake lililokuwa mfano wa matawi yaliyotandaa kufika mbali. Mataifa yenye shida yaliona kwamba Misri ilikuwa ingali na “matawi mazuri,” nayo yalipendelea kufanya mapatano na Misri badala ya kuyafanya na Babeli, mamlaka iliyotumiwa na Yehova Mungu wakati huo kufikiliza ghadhabu Yake.
13, 14. Je! leo “mwerezi katika Lebanoni” unafananisha Misri ya siku zetu, na kuna uhakika gani wa Maandiko wa kusema hivyo?
13 Mambo hayo yalipendeza sana mileani mbili na nusu zilizopita, lakini namna gani leo? Bila shaka unabii wa “mwerezi katika Lebanoni” hauwezi kuihusu Jamhuri ya Waarabu ya Misri ya kisasa, inayosimamiwa na Waislamu. Twakubali kwamba unabii huo hauwezi kutumiwa hivyo leo. Hasa kwa sababu Biblia iliyoongozwa na Mungu haiutumii hivyo. Basi, mwerezi huo “mzuri” wa Lebanoni ni nini leo? Sasa Farao mfalme wa Misri na watu wake wanafananisha nini au nani, katika karne yetu ya 20? Leo ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ ni nini, ambao anguko lake litashtua ulimwengu hivi karibuni?
14 “Mti” utakaoangamia unafananisha kitu kisichotambuliwa na watu wengi leo. Kitu gani? Misri ya kiroho! Katika kitabu cha mwisho cha Biblia Takatifu, Ufunuo 11:8, mtume Yohana aliongozwa na Mungu kuandika hivi: “Na mizoga yao itakuwa katika njia ya mji ule mkuu, uitwao kwa jinsi ya roho Sodoma, na Misri, tena ni hapo Bwana wao aliposulibiwa.” Anayeitwa “Bwana wao” ni Bwana Yesu Kristo, na wale ambao mizoga yao ilikaa peupe katika njia kuu ya mji ni wafuasi au wanafunzi waaminifu wa Kristo. Katika Ufunuo 11:3, wanafunzi hao wa Bwana Yesu Kristo wanaitwa “mashahidi wangu wawili,” nao wanauawa kwa sababu ya kuhubiri ujumbe wenye kuhuzunisha, usiopendwa na mataifa mengi.
15. Ni jambo gani linalozuia neno “Misri” lililo katika Ufunuo 11:8 lisitumiwe kuhusu nchi halisi ya Misri?
15 Ni ‘mji mkuu’ upi ambamo “mashahidi” hao wa kisasa waliuawa, kisha mizoga yao ikaachwa peupe ili kuaibishwa hadharani? Si katika mji mkuu wa Misri ya kisasa. Bila shaka Yesu Kristo, “Bwana” wa mashahidi hao, hakutundikwa katika Misri ya karne ya kwanza, kwa maana Ufunuo 11:8 wasema kwamba “mashahidi” wa Bwana waliuawa na kuachwa peupe, mahali pale pale alipotundikwa mwaka 33 wa Wakati wetu wa Kawaida. Tunapata ufahamu tunapochunguza na kuona kwamba “mji ule mkuu” ni wa mfano, “uitwao kwa jinsi ya roho Sodoma, na Misri.” Kwa hiyo mji huo si Sodoma halisi, ambao wakati huo haukuwako, wala si Misri halisi, ambayo wakati huo ilikuwa chini ya Milki ya Rumi. Basi, katika maana ya kiroho, ni wapi ambapo Bwana Yesu Kristo alitundikwa, kisha wanafunzi wake wa kweli wakauawa na kuachwa peupe?
16, 17. Kwa hiyo, Bwana Yesu Kristo alitundikwa katika mji mkuu’ upi wa mfano?
16 “Mji” ni tengenezo la kisiasa, kwa hiyo “mji ule mkuu” ni tengenezo kubwa la kisiasa, taratibu kubwa ya serikali. Wakati fulani Sodoma ya kale ilikuwa tengenezo la kisiasa, nayo Misri ya kale ilikuwa nchi yenye taratibu hodari ya kisiasa iliyoiwezesha kuwa Mamlaka ya Kwanza ya Ulimwengu ya unabii wa Biblia, muda wa karne nyingi. Kwa hiyo, inayoitwa Misri “kwa jinsi ya roho” ni taratibu ya ulimwenguni pote ya utawala wa kisiasa, tengenezo la kisiasa la utawala wa serikali za kibinadamu. Bwana Yesu Kristo ‘alisulibiwa’ (‘alitundikwa,’ tafsiri ya New World) katikati ya ‘mji huo mkuu’ mwaka 33 W.K., nje ya mji wa Yerusalemu. Ulimwengu wa wanadamu umo ndani kabisa ya taratibu hii. Kwa hiyo Yesu Kristo alitundikwa kati ya wanadamu wanaoiunga mkono taratibu hii. Ndiyo sababu aliwaambia wanafunzi wake hivi:
17 “Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu.” (Yohana 9:5) “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.”—Yohana 15:18, 19.
18. Kuuawa kwa Yesu kama mwana-kondoo wa dhabihu Siku fulani kulipatanaje na wazo la kutundikwa kwake katika Misri ya kiroho?
18 Yesu Kristo alitolewa dhabihu kama “Mwanakondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu” katika iitwayo Misri halisi ambamo alitolewa wakati mmoja alipokuwa mtoto. (Mt. 2:13-21; Yohana 1:29, 36) Bwana Yesu Kristo hakutolewa dhabihu kama Mwana-Kondoo wa Mungu Siku ya Kupitwa ya mwaka 33 W.K., bila ya kutazamiwa kwamba angetolewa. Kwa sababu gani? Kwa sababu alikuwa amefananishwa mapema na mwanakondoo aliyetolewa kama dhabihu na Waisraeli Siku ya kwanza ya Kupitwa ya mwaka 1513 K.W.K., katika Misri ya kale. Wamisri wasiotoa mwana-kondoo wa Kupitwa kama dhabihu na kupaka damu yake katika vizingiti vya milango yao walifiwa na wazaliwa wao wa kwanza, wa wanadamu na wanyama. Jambo hilo lilimfanya Farao awaondoe Waisraeli utumwani, waende zao wakiwa mahuru.
19. Kwa hiyo wanafunzi wa Kristo wanakombolewa wapi kulingana na ukombozi wa Israeli katika Misri ya kale?
19 Nchi ya Misri ilifananisha nini katika ukombozi huo wa kale wa wateule wa Yehova? Tena, Farao na watu wake walifananisha nani? Nchi ya Misri iliyopata mapigo ilifananisha taratibu hii ya kilimwengu, naye Farao na watu wake walifananisha watawala wa taratibu hii. Katika ‘Misri hii ya kiroho’ ndimo “Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basi [wanafunzi wa Kristo] na tuifanye karamu.” (1 Kor. 5:7, 8) Kulingana kabisa na jambo hilo, Misri ambamo wanafunzi waaminifu wa Mwana-Kondoo Yesu Kristo wanakombolewa ni taratibu hii ya kilimwengu. Ndiyo sababu wanafunzi wa Kristo wanaambiwa maneno yafuatayo, katika Wagalatia 1:3, 4: “Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba, na kwa Bwana wetu Yesu Kristo; ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili ya dhambi zetu, ili atuokoe na dunia hii mbovu iliyopo sasa.”
20. Basi, “mwerezi katika Lebanoni” unafananisha nini siku zetu, nayo ilianza lini?
20 Basi, tunakataje maneno? Kwamba “mwerezi katika Lebanoni,” ambao siku za nabii Ezekieli ulifananisha “Farao mfalme wa Misri na . . . watu wake,” unafananisha kitu kikubwa zaidi leo. Unafananisha taratibu ya ulimwengu ambamo watawala wa kisiasa wanayaongoza mataifa yote ya dunia. Ingawa taratibu hii inafananishwa na mwerezi ulioonewa wivu na miti mingine yote katika Lebanoni ya mfano yenye uzuri kama wa Edeni, haikuanzwa na Yehova Mungu, aliyeipanda miti hiyo isiyokauka katika nchi halisi ya Lebanoni, ambayo wakati huo ilikuwa kama “bustani ya Mungu.” Kama maandishi ya Mpanzi, Biblia Takatifu, yanavyoonyesha, mwerezi wa mfano na wa kisiasa uliokuwa katika Lebanoni ulianzia duniani siku za mwindaji hodari, Nimrodi, mwanzishi wa milki ya kwanza ya Babeli, katika karne ya pili baada ya gharika ya siku za Nuhu. Kama vile Nimrodi, kitukuu cha Nuhu, kilivyoiasi enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mungu wa Nuhu, Yehova, ndivyo mwerezi wa mfano “katika Lebanoni” unavyoikaidi enzi kuu ya Mungu Aliye Juu Zaidi.—Mwa. 10:8-12; 1 Nya. 1:8-10.
21. Mataifa yote ya ulimwengu yamefuata mwendo gani kuhusu huo “mwerezi katika Lebanoni”?
21 Umetumia nguvu za kibinadamu ulizo nazo kama kilindi cha maji, ukajaribu kujitukuza juu ya Yehova Mungu, kama kwamba umefika mawinguni. Umezidisha matanzu yake na kutandaza matawi yake ili kutawala ‘mahali pa Mungu pa kuweka miguu,’ yaani, dunia. (Isa. 66:1; Mt. 5:35) Serikali zote za kibinadamu, hata “mataifa makuu yote,” zimekwenda kukaa chini ya mti huo imara, hata leo hii. (Eze. 31:4-6) Baadaye, hata taifa la Israeli ambalo Yehova Mungu aliweka katika Nchi ya Ahadi ya Palestina, lilishawishwa kufuata mwendo wa mataifa hayo ya kilimwengu, likapatwa na madhara makubwa. Lakini kuna tengenezo fulani ambalo halikufanya hivyo. Jipi? Je! tunataka kuwa katika tengenezo hilo tupate faida za milele, au tunataka kuiga mwendo wa “mataifa makuu yote”? Tunahitaji msaada sasa ili kufanya uchaguzi unaofaa!
[Picha katika ukurasa wa 442]
UTAWALA WA KISIASA ULIMWENGUNI POTE