Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 10/1 kur. 447-455
  • Toka Chini ya Mti Huo “Mzuri”!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Toka Chini ya Mti Huo “Mzuri”!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • HAKIKA “MTI” HUO UTAANGUKA
  • KUOMBOLEZA ANGUKO LA “MTI”
  • “UZURl” WAKE UNAOONEKANA NA WANADAMU HAUTAUOKOA
  • HATUA INAYOFAA YAHITAJI KUCHUKULIWA HARAKA!
  • “Mti” Ambao Anguko Lake Lashtua Ulimwengu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Je, Wajua?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Tutakuwa Upande wa Nani Taabu ya Ulimwengu Ifikiapo Upeo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 10/1 kur. 447-455

Toka Chini ya Mti Huo “Mzuri”!

1. Ni kwa njia gani mataifa yaliyo kama mti yameuonea wivu “mwerezi katika Lebanoni”?

TARATIBU hii ya kisiasa iliyofanywa na wanadamu inaonekana kuwa nzuri kupita vitu vyote, kama “mwerezi katika Lebanoni” uliosimuliwa na Yehova katika unabii wa Ezekieli, sura ya 31. Kama vile Yehova alivyosema katika Ezekieli 31:8, 9, “bustanini mwa Mungu hamkuwa na mti wo wote uliofanana naye kwa uzuri. Nalimfanya kuwa mzuri [yaani mwerezi halisi unaotumiwa kama mfano] kwa wingi wa matawi yake; hata miti yote ya Adeni, iliyokuwa ndani ya bustani ya Mungu, ilimwonea wivu.” Taratibu hii ya kisiasa iliyopo ulimwenguni pote imezaa matanzu (matawi) mengi ili kuendelea kuwa na majani yenye uvuli, kulinda na kutimiza mahitaji ya mataifa ya ulimwengu. Kila taifa lililo mfano wa mti lingependa kuwa mamlaka ya ulimwengu, litawale mataifa mengine yote, na kuwa tengenezo lenye kuonewa wivu.

2. Ni kwa njia gani wanadamu wanaonyesha kwamba wanauona “mwerezi katika Lebanoni” kuwa mzuri kuliko vitu vyote?

2 Watu wote wanaoamini kwamba mwanadamu anaweza kujitawala bila kumtegemea Yehova Mungu wanapendezwa sana na ule ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ wakidhani kwamba hakuna mwingine wa kuupita. Ili mtu mwenye akili nzuri afahamu hivyo, inampasa aangalie bidii nyingi zinazofanywa ulimwenguni pote kutukuza mataifa au enzi zao. Inampasa pia aangalie jinsi mataifa makubwa yanavyong’ang’ania kutawala ulimwengu. Duniani pote Serikali inaabudiwa. Wakaaji wote wa dunia wanatakiwa waiabudu. Wivu huo unaoonyeshwa na mataifa wanapoustaajabia ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ unalingana na ibada iliyotabiriwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia, katika Ufunuo 13:3, 4, 15:

3. Ibada ya Serikali ilifananishwaje katika Ufunuo 13:3, 4, 15?

3 “Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule. Wakamsujudu yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye? Akapewa kutia pumzi katika ile sanamu ya mnyama, hata ile sanamu ya mnyama inene, na kuwafanya hao wote wasioisujudu sanamu ya mnyama wauawe.”

4. Kwa sababu gani waabudu wa Mungu mmoja aliye hai na wa kweli hawawezi kushiriki katika ibada hiyo?

4 Katika maelezo hayo ya unabii juu ya mambo yatakayokuja, tunaona kwamba watu wangelazimishwa kufanya ibada hiyo duniani pote, tena wasingemwabudu Mungu Yehova, bali kiumbe cha kibinadamu na “sanamu” yake. Ibada hiyo ikoje? Je! waabudu wa Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, yaani, Muumba atakaye kuabudiwa peke yake, wanaweza kushiriki kuabudu kiumbe hicho? Hapana! (Kut. 20:1-6) Muumba huyo anajisemea mwenyewe maneno yafuatayo, kulingana na Tafsiri ya American Standard ya Biblia: “Mimi ni Yehova, hilo ndilo jina langu; nao utukufu wangu sitampa mwingine, wala sifa yangu sitazipa sanamu za kuchongwa.”​—Isa. 42:8.

5. Kwa habari ya maneno hayo ya kimungu, ni mtu gani tunayeweza kufuata mfano wake leo na kuwa salama? Kwa sababu gani?

5 Katika ulimwengu huu wenye kutukuza mataifa, je! sisi mmoja mmoja tutaona ubora wa maneno hayo, ingawa yalisemwa zaidi ya miaka 2,700 iliyopita? Katika habari hiyo kuna mtu mmoja ambaye twaweza kufuata mfano wake na kuwa salama, na huyo ndiye Yesu Kristo. Wakati Shetani Ibilisi, yaani Joka wa mfano, aliposema angempa Yesu ulimwengu autawale akifanya tendo moja la kumwabudu, Yesu alijibu hivi: “Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.”​—Mt. 4:8-10.

6. Mungu anauonaje “mwerezi katika Lebanoni,” na kwa hiyo inatupasa tuchague kufuata kati ya miendo gani bila kukawia?

6 Yesu alipokataa toleo la Shetani alionyesha kwamba ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ haukuwa “mzuri” kwake. Wala wanafunzi wa kweli wa Kristo hawajapata kuiona taratibu hiyo ya kisiasa iliyofanywa na wanadamu kuwa ‘nzuri,’ wala hawajaiabudu. Ni kweli kwamba Yehova Mungu anausimulia “uzuri” wa ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ kulingana na maoni ya ulimwengu, lakini kwa maoni Yake kitu kinachofananishwa na huo “mwerezi katika Lebanoni” (Farao mfalme wa Misri na watu wake) si ‘kizuri.’ Ni kiovu; na ndiyo sababu anasema: “Nimemfukuza [au “nitamfukuza,” tafsiri ya New World, Kiingereza] kwa sababu ya uovu wake.” (Eze. 31:11) Je! leo sisi tuna maoni kama ya Yehova Mungu juu ya “mwerezi” wa mfano, na je! tunaamini kwamba maneno Yake yatakuwa na utimizo wa mwisho hivi karibuni? Hali yetu ya kusadiki jambo hilo au kutolisadiki ndiyo itakayotuamulia ulizo hili: Je! tutafuatana na mataifa na kukaa chini ya “mwerezi” wa mfano, au tutatoka chini yake bila kukawia?

HAKIKA “MTI” HUO UTAANGUKA

7, 8. Ni lazima tuchukue hatua ya haraka kwa sababu Yehova amekaza nia kufanya nini na “mwerezi katika Lebanoni”?

7 Inatupasa tufanye uamuzi wa haraka kuhusu jambo hilo. Hakika “mwerezi” wa mfano (yaani wale wanaofananishwa leo na Farao na watu wake) utaanguka vibaya sana. Mungu amekaza nia tukio hilo lenye maana ulimwenguni pote litukie. Baada ya kuueleza “uzuri” wenye kuonewa wivu wa ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ unabii uliotolewa kupitia kwa Ezekieli unaendelea kusema:

8 “Bwana [Yehova] asema hivi; Kwa kuwa umetukuzwa kimo chako, naye ameweka kilele chake kati ya mawingu, na moyo wake umeinuka kwa urefu wake; mimi nitamtia katika mikono yake aliye mkuu kati ya mataifa; naye atamtenda mambo; nimemfukuza kwa sababu ya uovu wake. Na wageni, watu wa mataifa watishao, wamemkatilia mbali na kumwacha; juu ya milima na katika mabonde yote matawi yake yameanguka, na vitanzu vyake vimevunjika karibu na mifereji yote ya nchi; na watu wote wa dunia wameshuka [mlimani], wakitoka katika uvuli wake na kumwacha. Juu ya magofu yake ndege wote wa angani watakaa, na wanyama wote wa jangwani watakuwa juu ya matawi yake; kusudi mti wo wote, ulio karibu na maji, usijitukuze kwa sababu ya kimo chake, wala usitie kilele chake kati ya mawingu, wala mashujaa wake wasisimame katika kimo chao kirefu, naam, wote wanywao maji; maana wote wametolewa wafe, waende pande za chini za nchi, kati ya wanadamu, pamoja nao washukao shimoni.”​—Eze. 31:10-14.

9. Yehova anawaitaje watu watakaoukata “mwerezi katika Lebanoni,” na je! walipotajwa mataifa yenye kukaa chini yake yalishtuka?

9 Huo “mwerezi katika Lebanoni” uliofika angani juu, kando ya mlima, ulipaswa kukatwa na wachanja kuni. Labda “mataifa makuu” yenye kukaa chini ya uvuli wake yangesema jambo hilo lisingewezekana, lakini Yehova Mungu angehakikisha kwamba maneno yake yametimizwa. Angeagiza “mti” huo wa mfano ushambuliwe na “aliye mkuu kati ya mataifa.” “Mkuu” huyo angekuwa wa mataifa mengi ya kigeni yasiyokaa chini ya “mwerezi” wa mfano, yaani, “wageni, watu wa mataifa watishao.” ‘Mataifa yote makuu’ yaliyokaa chini ya “mwerezi” huo yangeshindwa kuyazuia mataifa hayo mengine yenye kutisha yasiukate mti huo ulioyakinga. Kwa kuwa watu hao wenye kuuangusha mti wanasemekana kuwa “aliye mkuu kati ya mataifa,” “watu wa mataifa watishao,” bila shaka walipotajwa tu mioyo ya wenye kukaa chini ya. “mwerezi” huo mrefu, wenye matawi marefu, ilishtuka.

10. Ni nani “aliye mkuu kati ya mataifa” aliyetumiwa na Yehova kama shoka lake la kufishia, na mwishowe “mwerezi” uliacha kufanya nini?

10 Mungu Mwenye Nguvu Zote, asiyesema uongo, alitimiza unabii wake juu ya mwerezi huo wa kale. Alipeleka mamlaka ya ulimwengu iliyokuwa imetokea karibuni, yaani Milki ya Babeli, ikashambulie “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake.” Huyo “aliye mkuu kati ya mataifa” hakuwa rafiki ya Farao na watu wake, bali alikuwa na watu waliokuwa “wageni” kwao. Watu hao wakatili waliuchukulia hatua “mwerezi,” yaani Misri, wakiwa kama “mataifa watishao.” Walikuwa wamejitokea wakautawale ulimwengu kwa njia ya uonezi, naye Yehova aliwatumia kama shoka la kufishia. Wakati Farao mfalme wa Misri na wanajeshi wake walipokubali ombi la Mfalme Sedekia wakaja kuusaidia Yerusalemu uliozingirwa, walipigwa na Wababeli waonezi wakarudishwa walikotoka. Kwa hiyo, mwaka 607 K.W.K. Farao na majeshi yake waliona Yerusalemu ukiharibiwa pamoja na hekalu lake takatifu. Karibu miaka kumi na sita baadaye Yehova alimpa Mfalme Nebukadreza nchi ya Misri iwe malipo ya utumishi wa kufisha aliomfanyia. (Eze. 29:17-20) Ndipo kweli mikono hodari ya Farao ilipovunjwa isiweze kutengenezwa tena, wala hakuthubutu tena kutawala ulimwengu.​—Eze. 30:20-26.

11, 12. Ni jamii gani ya mataifa yenye kuogofya tunayokumbuka sasa, lakini kwa sababu gani siyo “aliye mkuu kati ya mataifa” anayetumiwa na Mungu?

11 Lakini, hayo ni mambo ya zamani yaliyotukia zaidi ya mileani mbili na nusu zilizopita. Tunalotaka kujua leo ni hili, ‘Aliye mkuu kati ya mataifa’ ni nani sasa, nao ‘wageni, watu wa mataifa watishao’ ni nani? Wao ni jamii ya mataifa yenye kuogofya ya Kikomunisti, au siyo?

12 Tunalijibu ulizo hilo moja kwa moja na kusema, Siyo! Hiyo ni kwa sababu mataifa ya Kikomunisti yanakaa chini ya matanzu yanayoenea ya ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ sawasawa na mataifa ya kidemokrasi. Wao ni sehemu ya ulimwengu huu, tena wanaendesha mambo yao kulingana na taratibu hii ya kisiasa iliyofanywa na wanadamu. Wao wanatukuza mataifa yao, wanaabudu Serikali na wana maelekeo ya kuitawala dunia yote kwa kutumia mawazo na njia zao za kisiasa. Kwa hiyo, hatuwezi kuwatazamia waukate ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ yaani kile kinachofananishwa leo na Farao wa kale wa Misri na watu wake. Wao hawataacha kuendesha mambo yao kwa kupenda kwao wenyewe! Danieli 11:40 mpaka 12:1 inaonyesha kwamba watanaswa pamoja na mataifa mengine yote katika ‘wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.’

13. Kwa sababu gani Yehova hatatumia mashahidi wake Wakristo kutimiza kazi kama ya “aliye mkuu,” au “watu wa mataifa watishao”?

13 Basi, Yehova atatumia nani kufanya kazi kama ile iliyofanywa na ‘aliye mkuu kati ya mataifa’ siku za nabii Ezekieli, aukate ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’? Hatawatumia mashahidi wake Wakristo, ambao leo ni karibu milioni mbili duniani pote, katika nchi 210. Wao si wadhalimu, waonezi, wala hawashtui mioyo ya watu, na ndiyo sababu wanateswa wazi-wazi kama wanadini wachache wasio na mtu wa kuwasaidia. Yehova atatumia chombo hodari cha kimbinguni, si kidude kidogo tu cha duniani.

14, 15. Basi, Yehova atatumia nani, kama inavyoonyeshwa na Yesu katika Mathayo 24:29-31?

14 Chombo cha Yehova ni Yesu Kristo aliyetukuzwa pamoja na majeshi yake ya malaika wa mbinguni. Wanasiasa wa leo wenye vichwa vigumu huenda wakacheka kusikia hivyo. Lakini hata Mfalme Senakeribu wa Ashuru ya kale angaliweza kucheka akisikia kwamba malaika wa Yehova angeua kabisa askari zake hoi 185,000, katika usiku mmoja. (2 Fal. 19:35, 36) Kwa hiyo, katika unabii wake juu ya mwisho wa taratibu ya mambo, Yesu Kristo alisema:

15 “Nguvu za mbinguni zitatikisika; ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi. Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda.”​—Mt. 24:29-31.

16. Mungu ameutia “mwerezi” mikononi mwa nani pamoja na wote wanaokaa chini yake, na lazima tufanye nini tusije tukapotelea mbali pamoja nao?

16 Yehova ameitia taratibu nzima ya mambo, pamoja na mataifa yote ya kilimwengu ambayo yamekimbilia chini yake, mikononi mwa Mwanawe Yesu Kristo, “Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme.” Yeye, pamoja na malaika zake wa mbinguni, ataukata na kuuangusha ‘mwerezi katika Lebanoni’ wenye sura nzuri. (Ufu. 11:15; 17:14; 19:11-16) Shina lililokatwa (linaloitwa ‘magofu’ na Union Version) la huo ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ yaani, “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake” wa kisasa, watalala nchini wawe ukumbusho wa ushindi wake katika Har–​Magedoni, katika ‘vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.’ (Ufu. 16:13-16) Watakuwa kama watu wafao na kuingia ‘pande za chini za nchi,’ naam, ‘katika shimo’ la maziko. (Eze. 31:14) Ulizo ni hili, Je! sisi tuishio katikati ya taratibu hii ya mambo tunataka tushuke pamoja nao? Ikiwa hatutaki, lazima tutoke mahali po pote pa ulinzi na kimbilio chini ya ‘mti’ huo uliohukumiwa maangamizi! Na tujiangalie tusiharibiwe pamoja nao uangukapo!

KUOMBOLEZA ANGUKO LA “MTI”

17, 18. Kulingana na Ezekieli 31:15-17, kwa sababu gani hivi karibuni ulimwengu wote utaomboleza?

17 Karibuni siku itafika wakati ulimwengu wote utakapoomboleza. Utaomboleza kuanguka kwa kitu cha maana kuliko ‘mwerezi mzuri katika Lebanoni,’ ambacho kimestaajabisha ulimwengu. Utaomboleza anguko la taratibu ya mambo iliyopo ulimwenguni pote pamoja na wenye kuiendesha, yaani, “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake” wa kisasa. Haitupasi kamwe kutia shaka, kwa maana unabii wa kimungu unaendelea kusema:

18 “Bwana [Yehova] asema hivi; Katika siku ile alipotelemka mpaka kuzimu naliamuru matanga, nalikifunika kilindi [shimo refu mno, LXX] kwa ajili yake, nikiizuia mito yake, nayo maji makuu yalizuiwa; naliamuru Lebanoni kumwombolezea, na miti yote ya kondeni ilizimia kwa ajili yake. Niliwatetemesha mataifa kwa mshindo wa kuanguka kwake, hapo nilipomtupa chini mpaka kuzimu, pamoja nao washukao shimoni; na miti yote ya Adeni, miti iliyo miteule na iliyo mizuri ya Lebanoni, yote inywayo maji, ilifarijika pande za chini za nchi. Hao nao walitelemka kuzimuni pamoja naye kwa watu waliouawa kwa upanga; naam, wale waliokuwa mkono wake, waliokaa chini ya uvuli wake kati ya mataifa.”​—Eze. 31:15-17.

19. Yesu alisema makabila yote ya dunia yangefanya nini yaionapo “ishara” ya kuja kwake, na ni jambo gani litakaloyashtua?

19 Kupatana na maneno hayo ya Yehova Mungu, Bwana Yesu Kristo alisema kweli aliponena kwamba makabila yote ya dunia yataomboleza yatakapoiona mbinguni “ishara” ya kuja kwake kufikiliza hukumu ya kimungu juu ya waovu, akiwa chombo cha Yehova. (Mt. 24:30) Makabila yote ya dunia yatafahamu kwamba taratibu hii imehukumiwa kuangamia mapema, watakapoona vionyesho vilivyo wazi kuliko kazi ya mashahidi Wakristo wa Yehova ya kuhubiri ulimwenguni pote. Ndipo mwishowe watakaposadiki kwamba hawawezi kuizuia taratibu isianguke, ijapokuwa wamejikaza sana kufanya hivyo. Watashtuka weee watakapojua kwamba uharibifu wake unaletwa na Muumba wa mbingu na dunia. Watahuzunika kuona kitu ambacho wamestaajabia sana ‘uzuri’ wake kikipatwa na uharibifu upesi. Hasara watakayopata itawaumiza weee.

20. Ni kwa njia gani “mwerezi” wa mfano umekuwa sana mnywa maji’?

20 Makabila, watu wa mataifa, wamekuwa kama maji ya kunywesha “mwerezi katika Lebanoni,” kama “kilindi” au shimo refu mno, ambalo maji yake yameiendea mizizi ya taratibu hii ya mambo iliyopo ulimwenguni pote. Mizizi ya taratibu hii ya mambo imemeza sana vitu ambavyo watu wameipa kuiendeleza. Kwa njia hiyo huo ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ umekuwa ‘mnywa maji.’ Unafanana na milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, Babeli Mkuu, inayosemekana kwamba ‘imeketi juu ya maji mengi.’ Si maji halisi, bali “yale maji uliyoyaona [mtume Mkristo Yohana], hapo aketipo yule kahaba, ni jamaa na makutano na mataifa na lugha.” (Ufu. 17:1, 15) Leo watu, yaani wakaaji wa ulimwengu, wameongezeka wakawa milioni elfu nne. Kwa hiyo ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ una “kilindi” kikubwa sana kinachoupa nguvu.

21. Yehova atavizuiaje vijito vya mfano pamoja na maji yale mengi yasiufikie “mwerezi” wa mfano?

21 Je! wakaaji wa dunia wataweza kuiendeleza taratibu ya mambo iliyo kama mwerezi, kwa sababu tu ya kuzidi kuwa wengi? Je! itaweza kuendelezwa na utawala wa watu wengi? Yehova, ambaye enzi yake iko juu ya mbingu zote na dunia, asema Hapana! Asema kwamba ‘ataizuia mito yake’ na kwamba yale “maji makuu” ‘yatazuiwa.’ (Eze. 31:15) Atafanyaje hivyo? Kwa kuagiza ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ ukatwe na kuangushwa, wajapopinga watu wote waupendao.

22. “Kilindi” kitakuwa na faida gani hapo chini ya shina la mti liiilokatwa?

22 Tena, wakati mti unapokatwa na kuangushwa, shina lake lililokatwa (linaloitwa “magofu” na Union Version) linapata faida gani hata chini yake pakiwa na “kilindi”? Vijito vya kilindi vinazuiwa visilifikie shina la mti lililokatwa na kutenganishwa na mizizi yake. Maji yale mengi yanazuiwa yasilifikie jiti hilo. Mapenzi ya Yehova ndiyo yanayoshinda, si ya watu. Usemi wa Kirumi unaosema, Vox populi, vox Dei (Sauti ya watu [ndiyo] sauti ya Mungu) si wa kweli.

23. Kwa sababu gani Yehova atakapokata “mwerezi” atashtua sana vijengo vyote vidogo vilivyojengwa katika taratibu ya mambo?

23 Wakati hii taratibu mbovu ya mambo itakapokatwa na chombo cha Yehova, anguko lake kubwa litaduwaza ulimwengu mzima, kwa sababu mataifa yote, watu, makabila na lugha zote zitahusika. Lazima zihusike. Wakati taratibu yote iangushwapo kwa kupigwa dharuba na Mungu, kijengo kidogo ambacho kimejengwa katika taratibu hiyo ya duniani pote chawezaje kubaki? (Gal. 1:4) Ikiwa mti ulio mkubwa na mzuri zaidi hautaruhusiwa kubaki umesimama na kuitawala dunia yote, miti ile mingine yote itawezaje kubaki imesimama, bila ya kulindwa na taratibu iliyo mfano wa mwerezi? ‘Itazimia,’ ipotewe na fahamu, mioyo yao iache kufanya kazi. Litakaloipata limeonyeshwa vizuri na maneno ya Yehova: “Miti yote ya kondeni ilizimia kwa ajili yake.”​—Eze. 31:15.

24. Kutetemeka kwa mataifa kwa sababu ya anguko la “mwerezi katika Lebanoni” kutamaanisha nini kuyahusu?

24 Tukikumbuka kwamba “mwerezi katika Lebanoni” unafananisha “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake,” na tuangalie vile Yehova anavyoendelea kusema: “Niliwatetemesha mataifa kwa mshindo wa kuanguka kwake, hapo nilipomtupa chini mpaka kuzimu, pamoja nao washukao shimoni.” (Eze. 31:16) Twaweza kusema kwamba, anguko la ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ litaleta mshindo mkubwa sana kiasi cha kuitetemesha dunia na kushtua mataifa yote. Wakati mataifa ambayo yameipendelea enzi ya taratibu hii mbovu ya mambo yatakapotetemeshwa, yataanguka yawe magofu na kuondolewa. Ndivyo mambo ya kudai mipaka yatakavyomalizwa kabisa. Enzi za mataifa zitapotelea mbali. (Ebr. 12:26, 27; Hag. 2:6, 7) Basi watu watalazimishwa kuuacha huo “mwerezi katika Lebanoni” wenye kujisingizia.​—Eze. 31:12.

25. Ni wakati gani mataifa yatakapouacha huo “mwerezi katika Lebanoni”?

25 Hilo litatukia lini? Si wakati wa vita ya tatu ya ulimwengu ya kutupiana makombora ya atomiki kati ya mataifa maadui, bali wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika uwanja wa Har–​Magedoni. Vita inafananishwa na “upanga.” ‘Mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ utalazwa pamoja na mataifa na mamlaka za ulimwengu ambazo zimekwisha malizwa kwa upanga. Tunaelezwa jambo hilo na usemi wa Yehova: “Na miti yote ya Adeni, miti iliyo miteule na iliyo mizuri ya Lebanoni, [miti] yote inywayo maji, ilifarijika pande za chini za nchi. Hao nao walitelemka kuzimuni pamoja naye [yaani pamoja na mwerezi wa mfano] kwa watu waliouawa kwa upanga; naam, wale waliokuwa mkono wake, waliokaa chini ya uvuli wake kati ya mataifa.”​—Eze. 31:16, 17; Septuagint ya Kigiriki (LXX);; Syriac Version; Rotherham.

26. Ni katika maana gani mataifa hayo ambayo yamekaa chini ya uvuli wa “mwerezi katika Lebanoni” yanaweza kutajwa kuwa “uzao” wake?

26 “Mkono wake” (au “uzao wake,” kulingana na tafsiri ya Kiingereza ya New World), uliokaa chini ya uvuli wa “mwerezi katika Lebanoni” kati ya mataifa, unafananisha matengenezo ya kisiasa, ya kijeshi na kitaifa yaliyotokana na taratibu hii mbovu ya mambo. Matengenezo hayo yamekua yakiitegemea taratibu ya mambo ya kilimwengu. Mengi ya matengenezo hayo ya kitaifa yamekwisha, yakafa na kushuka pande za chini za nchi, yaani kwenye makao ya wafu, yakapotelea mbali.

27. Matengenezo ya mataifa yaliyo chini ya “mwerezi katika Lebanoni” yatafarijiwaje na anguko lake?

27 Kwa hiyo yameacha kuwa miti ya mfano, ingawa taratibu nzima ya mambo inaendelea, na nyakati zote inazidi kukaribia uharibifu. Wakati hiyo yenyewe itakapokatwa ianguke milele, miti mingine yote ya mfano iliyo pande za chini za nchi, yaani katika ‘shimo’ la watu wote, Sheol au makao ya wafu, itafarijika sana. Tunajua kwamba hakuna mtu anayependa kufa peke yake, kwa hiyo “miti” hiyo ya mfano ambayo imekwisha angushwa na “upanga” wa jeuri itafurahi sana kufa pamoja na ule “mwerezi katika Lebanoni” wenye fahari. Itafarijika kuiona taratibu hii inayotawala ulimwengu ikidhoofika kama vile “miti” hiyo mingine ilivyodhoofika kabla ya kuuawa na “upanga” wa Yehova.​—Linganisha Isaya 14:12.

28. Hivyo, wakati ujao ni “bustani ya Mungu” ipi ambayo “mwerezi katika Lebanoni” hautaruhusiwa kufunika?

28 Kwa hiyo taratibu hii ya mambo itakuwa dhaifu sawasawa na wenye kuiunga mkono, wanaokimbilia chini ya uvuli wake wenye ulinzi. Yehova hataki huo ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ ufunike ‘bustani halisi ya Mungu’ itakayorudishwa duniani baada ya yeye kufanya vita katika Har–​Magedoni na kumfunga shimoni Shetani Ibilisi, “mungu wa taratibu hii ya mambo.”​—2 Kor. 4:4, tafsiri ya Kiingereza ya New World.

“UZURl” WAKE UNAOONEKANA NA WANADAMU HAUTAUOKOA

29, 30. Ni wapi ambapo Yehova anaeleza kwamba hii taratibu mbovu ya mambo itamalizwa mwishowe, ingawa inafanana na mwerezi ulio mzuri zaidi katika Lebanoni?

29 Wanadamu wana maelekeo ya kuabudu viumbe. Wamejiacha wauabudu “mti” huo mzuri wa mfano, yaani ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni.’ Taratibu hii ya kilimwengu inajiona kuwa nzuri na yenye kupendeza kuliko ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Masihi wake, Yesu Mwanawe. Naam, kulingana na maoni ya wanadamu, uzuri wa taratibu iliyopo unafanana na uzuri wa “mwerezi katika Lebanoni” uliofika angani. Lakini, uzuri huo unamfika wapi Mpanzi wa mierezi halisi ya Lebanoni? Yeye aiambia hivi taratibu hii iliyozunguka dunia nzima:

30 “Umefanana na nani, hivi katika utukufu na ukuu, kati ya miti ya Adeni? [Ujapokuwa umetukuka, utapatwa na jambo gani?] lakini utashushwa pamoja na miti ya Adeni, hata pande za chini za nchi; utalala kati ya hao wasiotahiriwa; pamoja na hao waliouawa kwa upanga. Huyu ndiye Farao, na jamii yote ya watu wake, asema Bwana [Yehova].”​—Eze. 31:18.

31. Je! kujitakia haki kwa “Farao na jamii yote ya watu wake” kungefanya Mungu awaachilie, kwa hiyo wote wangepatwa na msiba wa nani?

31 Hapo kale, labda “Farao, na jamii yote ya watu wake” walikuwa wakitahiriwa, kwa hiyo labda walijidhani kuwa watu safi na wenye haki, kama Waisraeli, wazao wa Ibrahimu Mwebrania. Labda “Farao, na jamii yote ya watu wake” walidhani wasingepatwa kamwe na msiba na kuzikwa pamoja na mataifa yasiyotahiriwa, na mamlaka za ulimwengu. Lakini kulingana na maoni ya Yehova Mungu, kujiona kwao kuwa wenye haki kulikuwa bure tu. Kwa hiyo, katika wakati wake, utawala wa ukoo wa Hamu katika nchi ya Mto Nailo, yaani Misri ya kale, ungekoma. Kwa njia hiyo “Farao, na jamii yote ya watu wake” wasingeepuka msiba ambao ungepata matengenezo mengine yote madogo, ati kwa sababu ya kutahiriwa na kuwa tengenezo lenye uzuri wa kilimwengu.

32. Taratibu hii ya mambo iliyo ‘nzuri’ itapatwaje na jambo kama lile lililopata “Farao na jamii yote ya watu wake,” na kwa sababu gani?

32 Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu aliamuru “Farao, na jamii yote ya watu wake” wauawe na chombo chake wakawe mahali pamoja na wafu wengine wote wachafu. Tengenezo lao la kisiasa lilikuwa baya, naye Yehova alisema ‘angelifukuza kwa sababu ya uovu wake.’ (Eze. 31:11) Ndivyo ilivyo kuhusu “Farao, na jamii yote ya watu wake” wa kisasa. Taratibu ya mambo iliyofananishwa na Farao na watu wake ilikataliwa na Yehova Mungu. Yeye anauona uovu uliomo ndani yake, hata ijapoonekana kuwa ‘nzuri’ sana na wanadamu wenye kuiabudu. Inastahili kutendwa kama “mwerezi katika Lebanoni” ulio mzuri ajabu, yaani, kuangushwa na “upanga” wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–​Magedoni. (Ufu. 16:13-16) Iangukapo mataifa yote ya dunia yatatetemeka kwa kujua kwamba yatapotelea mbali kama taratibu hiyo nzima ya ulimwengu. Itaangushwa kwa sababu imesimama kishupavu iupinge ufalme wa Mungu wa Kimasihi.

HATUA INAYOFAA YAHITAJI KUCHUKULIWA HARAKA!

33. Ni katika maana gani shoka sasa ‘limewekwa penye mashina’ ya “mwerezi katika Lebanoni” ulio mzuri?

33 ‘Mwerezi wa mfano katika Lebanoni’ umo katika hali ambayo Yohana Mbatizaji alitaja kuhusu taratibu ya mambo ya Kiyahudi ya siku zake, “Shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa.” (Mt. 3:10) Wakati unakaribia ambapo Yehova ataagiza “wageni, watu wa mataifa watishao,” walitumie shoka kuikata taratibu hii mbovu ya mambo. Anguko lake linazidi kukaribia. Ijapokuwa wanadamu wanaiona kuwa ‘nzuri’ sana, haikuanzwa na Yehova wala si sehemu ya tengenezo lake. Ni sehemu ionekanayo ya tengenezo la Shetani Ibilisi. “Kulingana na uovu wake nitaufukuzia nje,” asema Yehova.​—Eze. 31:11, 12, tafsiri ya Kiingereza ya New World.

34. Wenye kuendesha shughuli katika taratibu hii mbovu ya mambo ni “uzao” wa nani?

34 Katika taratibu hii mbovu ya mambo, watu wa kisasa wanaofananishwa na “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake” wamekuwa wakiendesha shughuli zao zaidi ya miaka elfu nne tangu Babeli ya kale ilipoanzwa, siku za Nimrodi. Viongozi hao wa kilimwengu hawakupewa cheo na Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova. Wao si “uzao” (au “mkono,” UV) wa Baba wa mbinguni; si “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu, ambao alitoa ahadi yenye tumaini kuuhusu, katika ‘bustani ya Edeni’ ya kwanza. Wao ni “uzao” wa Nyoka Mkubwa, yaani, Uzao wa Shetani Ibilisi. (Mwa. 3:15) Huenda huo ukawa ni usemi mkali, lakini unapatana kabisa na vile Yesu alivyowaambia wapinzani wa siku zake: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake.” (Yohana 8:44) “Uzao” huu wa kisasa wa Adui mkuu wa Mungu uko sawa na Farao wa kale na watu wake, maana haumtumikii Mungu. Huo ni “Misri” ya kiroho, tena unafanana na Farao na watu wake.​—Ufu. 11:8.

35. Kulingana na mambo yaliyotangulia kufunuliwa, inatupasa tufanye nini wakati huu wenye hatari, na twawezaje kufanya hivyo?

35 Kulingana na mambo hayo tuliyofunuliwa, na kwa sababu unabii wa Ezekieli juu ya “mwerezi katika Lebanoni” unakaribia kutimizwa, inatupasa tufanye nini? Itakuwa afadhali tufanye nini? Inatupasa tufanye jambo gani wakati huu wenye hatari? Jambo lenyewe ndilo hili: Kutoka chini ya “mti” huo wa mfano. Uangukapo kwa mshindo, hatutaki kupatwa na msiba wa milele. Kwa hiyo inatupasa tuiache taratibu hii mbovu ya mambo, iliyofananishwa “Farao mfalme wa Misri, na . . . watu wake.” Inatupasa tujipange upande wa tengenezo la Yehova. Tumekuwa hatuliungi mkono tengenezo hilo muda ambao tumekuwa sehemu ya ulimwengu huu wa watenda dhambi. Tumekuwa “wafu kwa sababu ya makosa na dhambi [zetu]; ambazo [tuliziendea] zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme [Shetani Ibilisi] wa uwezo wa anga.” (Efe. 2:1, 2) Inatupasa tuache kutembea “kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu.” Lazima tuache kukaa chini ya uvuli wenye ulinzi wa kilichofananishwa na “Farao, na jamii yote ya watu wake.”

36. Tukiisha toka chini ya tengenezo lionekanalo la Shetani, inatupasa tutiije shauri la Isaya 31:1?

36 Tukiisha toka chini ya tengenezo lionekanalo la Adui mkuu wa Mungu, haitupasi kulikimbilia tena likatusaidie na kutulinda. Tutakuwa na hekima ya kimungu tukiyatii maneno haya yaliyoongozwa na Mungu: “Ole wao watelemkao kwenda Misri wapate msaada, na kutegemea farasi; watumainio magari kwa kuwa ni mengi, na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli, wala hawamtafuti [Yehova].”​—⁠Isa. 31:1.

37, 38. Tunapata onyo gani katika mfano wa mabaki Wayahudi walioachwa nyuma baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu?

37 Tuna mfano wa kutuonya tusikimbilie Misri iliyohukumiwa maangamizi ikatusaidie. Unabii wa Ezekieli ulitolewa mwaka wake wa kumi na mmoja wa kuwa utumwani, mwezi wa tatu, siku ya kwanza. (Eze. 31:1) Siku ya tisa ya mwezi wa nne (Tamuzi 9, 607 K.W.K.) Babeli, “aliye mkuu kati ya mataifa,” iliuteka Yerusalemu. Mwezi uliofuata waliuharibu mji huo, wakahamisha waokokaji na kuwapeleka Babeli. Mwezi wa saba (Tishri, 607 K.W.K.) gavana wa walioachwa nyuma aliuawa.

38 Basi mabaki hayo ya Wayahudi waliamua kuiacha nchi ya Yuda na kukimbilia Misri wakawe chini ya ulinzi wa ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ kwa sababu ya kuogopa kuchukuliwa hatua na Wababeli. Nabii Yeremia aliwashauri wasifanye hivyo. Aliwaonya kwamba mfalme wa Babeli angeishinda Misri, waendelee kuwa chini ya mamlaka yake. Mabaki ya Wayahudi hawakutii onyo la Yeremia, bali walikimbilia Misri, wakampeleka nabii wa Yehova huko. Lakini Misri haikuwasaidia, kwa maana miaka kadha baadaye mfalme wa Babeli aliteka nchi ya Misri akaiongeza katika milki yake. Kama ilivyokuwa zamani, Misri ilishindwa kuwasaidia Wayahudi wasiokuwa na imani, lakini Neno la Mungu halikukosa kutimizwa.​—2 Fal. 25:1-26; Eze. 29:17-20; Yer. 40:7 mpaka 43:13.

39. Basi, tumaini la wanadamu ni nini, na kwa sababu gani?

39 Taratibu ya mambo ya kilimwengu sasa imo katika siku zake za mwisho. Kama vile Misri ya kale ilivyoshindwa kulinda waliokimbilia chini ya matawi marefu ya ‘mwerezi wa mfano katika Lebanoni,’ taratibu hii itashindwa kusaidia wale wanaoitumaini na kuiendea iwasaidie na nguvu zake za kijeshi na za kiuchumi. Utawala wake juu ya mambo ya dunia utamalizwa. Ufalme wa Yehova unaokuja ndio utakaoumaliza kwa kumtumia Mwanawe Yesu Kristo, aliye mfalme. Tumaini la wanadamu ni ufalme huo wa Mungu, kwa maana utaleta taratibu mpya ya mambo yenye haki, itakayokuwa ‘nzuri’ kikweli. Itarudisha duniani “bustani ya Mungu,” paradiso halisi iliyo mfano wa Edeni, na kuipamba dunia nzima kwa utukufu na uzuri wake.

40. Kwa sababu gani haitupasi kuwa wenzi wa ulimwengu huu, lakini tukiwa kama Yesu na mitume wake tutapata nini?

40 Wakati huu ambao hali ya mambo ya ulimwengu si nzuri sana, haitupasi kuwa wenzi wa ulimwengu huu wa watu wasiomcha Mungu uliohukumiwa maangamizi, pamoja na taratibu yake ya mambo. Ikiwa tunataka kuzipata baraka za milele ambazo Mfalme Yesu Kristo atawapa raia zake, lazima tuwe sawasawa na vile alivyosema yeye na mitume wake walikuwa: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14, 16) Tukijitenga hivyo na ulimwengu, hatutapatwa na uharibifu wa huu “ulimwengu wa wasiomcha Mungu.” (2 Pet. 2:5; 3:6) Tutaokolewa tufurahie kukaa milele chini ya taratibu mpya yenye haki, ambamo Yesu Kristo na wenzi wake waliotukuzwa, si Farao na watu wake, ndio watakaotumikia kama wafalme na makuhani wa Mungu ili kubariki wanadamu.​—Ufu. 20:4, 6.

​—Kutoka The Watchtower, May 15, 1977.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki