Wewe Unaweza Kuuingia Mlango Uliofunguka?
“Nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao Hapana awezaye kuufunga.”—Ufu. 3:8.
1. Kwa sababu gani nafasi kubwa za utumishi zingali zinapatikana katika kundi la Kikristo?
AMRI ambayo Yesu Kristo aliwapa wafuasi wake wahubiri na kufanya wanafunzi inapaswa kutimizwa upesi sana. Jambo hilo linaonekana wazi katika ahadi yake: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.” (Mt. 28:20) Kwa hiyo, bado kuna nafasi nyingi kubwa za utumishi wakati “habari njema ya ufalme” inapoendelea kuhubiriwa kwa bidii mlango kwa mlango. (Mt. 24:14) Vilevile, kwa sababu ya ukuzi wa kundi la mashahidi Wakristo wa Yehova ulimwenguni pote, wafanya kazi hodari na wenye nia wanahitajiwa sana ili kujenga waamini wenzao na kufanya utumishi mwingine wa maana sana wa kuendeleza faida za kiroho. Tena, watu kila mahali wanahitaji kuzisikia “habari njema” waweze kuziunga mkono au kuzipinga kabla Mungu hajafikiliza hukumu yenye haki juu ya ulimwengu huu usiomcha.
2. (a) Kwa sababu gani kundi la Kikristo linahitaji uongozi unaotoka mahali pakuu paliposawazika? (b) Kichwa cha kundi kilitumia nani karne ya kwanza W.K. kutoa uongozi huo?
2 Ili kutimiza mambo yote ya lazima kwa utaratibu mzuri, lazima uongozi utoke mahali fulani pakuu, paliposawazika. (1 Kor. 14:33) Katika karne ya kwanza W.K., Yesu Kristo, kichwa cha kundi, alitoa uongozi huo kupitia kwa mitume na wazee wengine wa kundi la Yerusalemu. Vilevile, Paulo, aliyekuwa amechaguliwa moja kwa moja na Bwana Yesu Kristo awe mtume kwa mataifa, alijenga sana makundi kiroho. Njia ambayo Paulo na wenzake walitumia kutimiza agizo la kuhubiri na kufanya wanafunzi walilopewa na Yesu ilikubaliwa kabisa na baraza ya wazee katika Yerusalemu.—Gal. 2:1-9.
3, 4. (a) Kwa sababu gani ni vizuri kwamba wanaume wanaoshirikiana na shirika la uchapaji la Mashahidi wa Yehova wanatolea waamini wenzao ulimwenguni pote msaada mkuu, uliosawazika? (b) Daraka kuu la wazee ni nini, nayo baraza inayoongoza katika Betheli ya Brooklyn imelitimizaje?
3 Namna gani leo? Mwanzoni sana katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova, washiriki wa kundi la zamani zaidi walikuja kushirikiana na shirika lao la uchapaji, Watch Tower Bible and Tract Society. Leo, kati ya wanaoishi “Betheli,” makao makuu ya kazi ya Watch Tower Society katika Brooklyn, New York, wako watu zaidi ya 250 ambao wameendeleza faida za kiroho kwa bidii nyingi zaidi ya miaka kumi. Wengi wamefanya hivyo muda mrefu zaidi. Wametumia maisha yao yote wakimtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu kama wanafunzi waliojitoa wa Mwanawe. Wakati huo wamepata ujuzi mwingi katika maisha ya Kikristo na katika kusaidia waamini wenzao na matatizo yao. Vilevile wameongeza ufahamu wao juu ya Neno la Mungu. Kati yao wako wale wanaume wenye kujitoa wanaofanyiza baraza inayoongoza kundi la Mashahidi wa Yehova lililo ulimwenguni pote. Ingawa kwingineko kuna ndugu wengi hodari na wenye ujuzi, hapana mahali pengine duniani ambapo wazee wengi hivyo wanapatikana wakiwa pamoja kuweza kuendewa upesi. Kwa hiyo, Betheli ya Brooklyn ni mfano bora sana wa maarifa na ujuzi wa Kikristo ambao umepatikana na kundi la watu wa Mungu lililo ulimwenguni pote. Ndivyo ilivyo juu ya jamaa ndogo za Betheli zinazoshirikiana na afisi za matawi ya Watch Tower Society katika sehemu nyingine za dunia.
4 Basi, wazee katika makundi mengine wanaposumbuliwa na matatizo fulani, wanaiandikia Sosaiti au matawi yake ili kupata usaidizi wa Maandiko. Nyakati nyingine majibu ya Biblia yanayohitajiwa yanakuwa yale ambayo yanaweza kufaidi makundi duniani pote. Inapokuwa hivyo, habari hizo zinaandikwa, kama ilivyokuwa karne ya kwanza W.K. Tena, kwa kuwa mojawapo madaraka makubwa ya wazee ni kufundisha, baraza kuu ya wazee inatumia halmashauri zake kusimamia utayarishaji na uchapaji wa habari za kuwapa watu maagizo ya kiroho ndani na nje ya kundi la Kikristo ulimwenguni pote.
5. Ni kazi gani ya maana sana inayofanywa Betheli, na kwa sababu gani kila mtu anayefanya kazi huko anahitajiwa?
5 Ni wazi kwamba wafanya kazi wengi sana wanahitajiwa Brooklyn kufanya kazi yote iliyo ya maana ya kutoa msaada na uongozi wa kuendeleza faida za kiroho duniani pote, pamoja na misaada ya kimwili inapokuwa lazima. Ingawa wengine wanahusika katika kutayarisha hasa habari za Biblia au kuagiza mambo yanayohitajiwa kufanywa kwa ajili ya ushirika wa ndugu, wengine wote wanafanya utumishi wa maana unaowezesha habari hizo kufikia miisho ya dunia. Kwa hiyo, wengi wa wale wanaotumikia Betheli wana cheo kama cha Timotheo, Marko na wengine waliotumikia wazee katika kundi la karne ya kwanza. Bila ya wao kuwapo, baraza inayoongoza ingeona ni vigumu sana kuangalia faida za kiroho za makundi ulimwenguni pote.
UTUMISHI WA BETHELI
6. (a) Kwa sababu gani vijana hasa ndio wanaohitajiwa Betheli? (b) Kama inavyoonekana katika habari ya Timotheo, mtu anayejitoa atumikie Betheli anatazamiwa awe namna gani?
6 Kwa kuwa kazi nyingi inayofanywa Bethelia inahitaji watu wenye nguvu, vijana hasa ndio wanaohitajiwa. Ikiwa wewe ni kijana, je! umepata kufikiria kujitoa ufanye kazi ngumu ya mikono kwa ajili ya ndugu zako wa kiroho, na vilevile kwa ajili ya watu ambao huenda siku moja wakawa ndugu zako? Bila shaka, hilo si shauri la kuwa na uwezo na nia ya kutumikia tu. Sifa za kiroho zinahitajiwa pia. Kwa mfano, tunasoma yafuatayo juu ya Timotheo: “Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio.” (Matendo 16:2) Naam, Timotheo alikuwa amejihakikisha kuwa kijana mwenye sifa nzuri katika kundi la kwao lililokuwa Listra, na katika kundi jirani lililokuwa Ikonio. Bila shaka aliheshimiwa na kutumainiwa na waamini wenzake kwa sababu ya maneno na matendo yake. Ingawa alikuwa kijana, alikuwa imara katika Maandiko, maana mama yake na nyanya yake walikuwa wamemfundisha Maandiko hayo tangu alipokuwa mtoto mchanga.—2 Tim. 3:14, 15.
7. (a) Wazee katika Listra, pamoja na Eunike, walikuwa na maoni gani mazuri juu ya kutumikia kwa Timotheo pamoja na Paulo? (b) Kwa habari ya utumishi wa Betheli, ni nani leo wanaoweza kufaidika kutokana na mfano wake, na kwa sababu gani?
7 Bila shaka vijana wenye sifa kama za Timotheo ni wenye faida nyingi kwa kundi lo lote. Bila shaka ndugu katika Listra walithamini sana mambo ambayo Timotheo aliweza kuwafanyia. Bila shaka alifurahisha sana moyo wa mama yake Eunike, hasa kwa sababu baba yake hakuwa mwamini. Lakini, wakati mtume Paulo aliposema alitaka kwenda na Timotheo katika safari zake, baraza ya wazee haikuwa na choyo ikijaribu kumzuia kijana huyo ili abaki katika kundi lao. Sivyo, wazee hao walijiunga na mtume kumwekelea Timotheo mikono afanye utumishi wa pekee. (Matendo 16:3; 1 Tim. 4:14; 2 Tim. 1:6) Kwa hiyo wakati vijana wanaostahili leo wanapotaka kujitoa watumikie Betheli, inafaa sana wazee na washiriki wa jamaa yenye kuamini wawatie moyo na kuwasaidia kwa moyo wote.
8. Kwa sababu gani utumishi wa pekee ambao Timotheo alifanya na mtume Paulo ulikuwa mgumu?
8 Ingawa utumishi katika Betheli unaleta thawabu nyingi za kiroho, si jambo jepesi. Wala mgawo wa Timotheo haukuwa mwepesi. Zaidi ya kuendeleza faida za kiroho akiwa chini ya uongozi wa mtume Paulo, Timotheo alifanya kazi kwa mikono yake ili kujipatia vitu alivyohitaji. (Linganisha 2 Wakorintho 12:14-18; 1 Wathesalonike 2:9; 2 Wathesalonike 3:7, 8.) Yeye pia alipatwa na hatari na matatizo ambayo mtume alieleza katika barua yake ya pili kwa Wakorintho: “Katika kusafiri mara nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang’anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi.”—2 Kor. 11:26, 27.
9. Ni jambo gani lililomwezesha Timotheo akae katika utumishi wake wa pekee badala ya kurudi nyumbani akafurahie maisha ya utulivu?
9 Ijapokuwa alipatwa na yote hayo, Timotheo aliendelea kufanya kazi pamoja na Paulo karibu miaka kumi na mitano, si muda mfupi tu, mpaka mtume alipouawa kwa sababu ya kushikamana na imani. Ni jambo gani lililomwezesha Timotheo ashikamane na kazi hiyo badala ya kurudia kundi la kwao akaishi maisha ya utulivu? Ni unyofu wake wa kutaka kutumikia wengine bila kujali hasara ambazo angejipatia kwa sababu ya kufanya hivyo. Mtume Paulo angeweza kusema hivi juu ya Timotheo: “Sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. Maana wote wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu. Ila mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili.” (Flp. 2:20-22) Tena, Timotheo alikuwa mnyenyekevu, akakubali kwamba alipungukiwa katika mambo fulani. Hakutumia ushirika wake na Paulo kama njia ya kujidaia mamlaka kwa kiburi. (Linganisha 1 Timotheo 4:1-14; 2 Timotheo 1:6, 7; 2:1.) Bila shaka, kwa kufanya kazi pamoja na mtume, Timotheo alijifunza mengi na mwishowe akastahili kuyachukua madaraka ya mzee katika kundi la Kikristo.
10. (a) Kama inavyoonekana katika mfano wa Timotheo, ni sifa gani zinazotakiwa sana ili mtu afurahie kutumikia wengine? (b) Ni mambo gani mabaya yanayotokana na kiburi, kutaka ukubwa na uchoyo, na inampasa mtu afanye nini anapoona waamini wenzake wakiwa na tabia hizo zisizopendeza?
10 Kama ilivyokuwa juu ya Timotheo, unyenyekevu, roho ya kujinyima na kupendezwa sana na watu ni mambo ya lazima ili kufurahia utumishi katika Betheli au mahali penginepo katika tengenezo la Yehova. Hata mtu akitumikia wapi, kiburi, tamaa ya kujitakia ukubwa na uchoyo ni mambo yatakayommalizia furaha na kufanya wengine wasifurahie maisha. Kwa sababu ya kutokamilika, ni lazima watumishi wa Mungu waendelee kushindana na tabia hizo zisizopendeza, wala haiwapasi kuudhika mno waonapo wengine wakionyesha sana tabia hizo. Nyakati zote inafaa kujitahidi kusitawisha roho inayofaa, maana thawabu haitatoka kwa wanadamu, bali kwa Yehova Mungu. Tena, mtu akiwekea wengine mfano mwema, anaweza kuwajenga.
KUTUMIKIA KAMA PAINIA AU KUSAIDIA MAHALI PENGINE
11. Ni nafasi gani zilizo wazi katika kuhubiri na kufanya wanafunzi, na inampasa mtu awe na kusudi gani anapozitumia? (Mt. 22:37-39)
11 Bila shaka, utumishi wa Betheli ni mlango usioweza kuingiwa na watu wote wanaoshirikiana na makundi ya watu wa Mungu ulimwenguni pote. Lakini ziko nafasi nyingine nzuri zilizo wazi kuhusiana na kazi ambayo lazima ifanywe. Kwa mfano, watumishi wa Mungu wana pendeleo la kutumia wakati wote wanaoweza kupata waifanye kazi ya maana ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Hakuna kikomo walichowekewa cha wakati wanaoweza kutumia katika utumishi huo. Hakika sote tunataka kutumikia kwa nafsi yote. Ili kufanya hivyo, huenda wengi wakapaswa kutumia karibu saa 60 kwa mwezi waifanye kazi hiyo wakiwa “mapainia wasaidizi” au karibu saa 90 au zaidi kwa mwezi wakiwa “mapainia wa kawaida.” Je! wewe umeuingia mlango ulio wazi wa upainia au unapanga kufanya hivyo? Unapopainia, nyakati zote kusudi lako liwe ni kumpenda Yehova Mungu na wanadamu wenzako.
12. Mfano wa mtume Paulo unaonyeshaje mambo yanayotakiwa kwa watu wanaotaka kufaulu wafanyapo utumishi mtakatifu mahali pengine?
12 Kama vile Paulo na Barnaba walivyoanza kutumikia pamoja na kundi la Antiokia kwa sababu kulikuwa na uhitaji mkubwa huko, ndivyo wewe pia unavyoweza kuhamia mahali pengine kuendeleza faida za kiroho. Tena, unyenyekevu, kujinyima na kutaka sana kuona watu wakiwa na hali njema ni mambo yanayoweza kukusaidia sana ufanye mabadiliko ya kuzoea mazingira mapya. Ndivyo mtume Paulo alivyofanya akasema hivi juu yake mwenyewe: “Ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. . . . Nimekuwa hali zote kwa watu wote.” (1 Kor. 9:19-22) “Nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo. Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa.” (Flp. 4:11, 12) Kwa kumtumainia Yehova kabisa Paulo aliweza kuvumilia hali zenye majaribu magumu sana.
13. Kwa sababu gani mtu anayefikiria utumishi wa mmisionari anapaswa kuhesabu gharama, na ni baadhi ya mambo gani anayoweza kufikiria kwa sala aone kama anaweza kushiriki katika utumishi huo?
13 Mtu anatakiwa ajinyime na kuwa na nia ya kutumikia wengine ili kwenda katika eneo jingine, au kuwa mmisionari katika sehemu nyingine ya ulimwengu. Mambo hayo yanapaswa yafikiriwe mapema kupitia kwa sala. (Linganisha Luka 14:28-32.) Kwa mfano, mtu ambaye amekuwa na motokaa ya kutumia sikuzote katika utumishi apaswa afikiri kama atakuwa na nia ya kutembea maili nyingi katika nchi yenye vibonde-vibonde na mawe-mawe huku jua kali likimwangukia, au kama atakuwa na nia ya kuvumilia kusafiri katika magari yaliyosongamana watu, yasiyoonekana kwa wingi. Ikiwa anasitasita kufanya mambo hayo sasa, huenda akatatizwa sana kuzoea mazingira mapya kabisa. Vivyo hivyo, inawapasa watu wanaotatizwa kuzoea hali tofauti, mazingira tofauti na watu tofauti wenye hali za maisha, desturi na tabia tofauti wajitahidi kuondoa tatizo lao ili kustahili kueneza Injili katika nchi ya kigeni.
NAFASI ZA KUWA WATUMISHI NA WAZEE
14. Wale wanaowekwa kuwa watumishi au wazee katika kundi wanatakiwa wawe namna gani?
14 Mlango mmoja ulio wazi kwa wanaume katika kundi la Kikristo ni kuhudumia waamini wenzao kwa kuwa watumishi au wazee. Sifa zilizoonyeshwa katika Maandiko zinaeleza wazi kwamba wale wanaotumikia hivyo lazima wawe watu wenye maoni ya kiroho, watu wenye kuwekea wengine mfano mwema katika maisha ya Kikristo, wanaume wenye kuheshimiwa na kutumainiwa na kundi kwa ujumla. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Kwa sababu wazee wana madaraka ya kufundisha, inawapasa pia wawe wanaume wanaojifunza Neno la Mungu kwa uangalifu. Ni vigumu sana mwanamume asiyesoma Biblia mara nyingi au ambaye labda hajamaliza kuisoma yote kabisa kufikiriwa kwamba anastahili kufundisha waamini wenzake kutokana nayo.—Linganisha 1 Timotheo 1:6, 7; Yakobo 3:1.
15. Kama inavyoonekana kutokana na maneno ya Yesu katika Mathayo 20:25-27. ni jambo gani hasa ambalo mwanamume anatakiwa kuwa nalo ili kustahili kuwa mtumishi au mzee katika kundi?
15 Kulingana na Maandiko, watumishi wa kundi na wazee si watu wakubwa bali ni watumwa wa ndugu zao. Yesu Kristo aliwaambia mitume wake hivi: “Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu.” (Mt. 20:25-27) Kwa hiyo, jambo moja kuu linalofanya mtu astahili kuwa mtumishi kundini au kuwa mzee ni kutaka kuwa mtumwa wa ndugu zake, kujinyima wakati na nguvu zake kwa ajili yao.
16. Ni jambo gani hasa linalofanya mwanamume awe mtumishi au mzee wa kweli?
16 Wale ambao ni watumishi na wazee wa kweli wanafikiriwa na ndugu zao kuwa watumwa wanyenyekevu walio na nia na shauku ya kujitoa kwa moyo wote wawasaidie. (Matendo 20:25-35; 1 Pet. 5:2, 3) Kundi linaheshimu sana watumishi na wazee hao, linawafurahia na kuwapenda kwa sababu wanatia bidii kuendeleza faida za kiroho. (1 The. 5:12, 13; Ebr. 13:17) Wao ni wanaume wanaotimiza kazi waliyopewa kwa kuwekwa. Ndivyo hasa wazee wenye kusafiri wanavyopaswa kuwa. Makundi yana haki ya kuwatazamia wawe wanaume wenye maoni ya kiroho, wenye unyenyekevu wa ajabu.—Linganisha Luka 12:48.
17. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba wanaume wenye kujitakia makuu na cheo hawajaanza kufikilia cheo cha mwangalizi?
17 Ni wazi kwamba wanaume wanaotaka ukubwa na cheo, badala ya kuitaka kazi ya mtumwa, hawastahili kuwa watumishi wala wazee. Hawajaanza ‘kufikilia cheo cha mwangalizi.’ Kwa sababu gani? Kwa sababu hawaitafuti “kazi nzuri” inayohusika.—1 Tim. 3:1, tafsiri ya Kiingereza ya New World.
18. (a) Nafasi zote zinazohusiana na utumishi mtakatifu zinahitaji nini, na kwa sababu gani? (b) Tunaweza kutazamia kupata nini tukijitoa tutumiwe kabisa kulingana na majaliwa tuliyopewa na Mungu?
18 Nafasi zilizo wazi kwa wanafunzi wa Yesu Kristo si vyeo vya fahari na heshima machoni pa wanadamu. Nafasi zote hizo zinahitaji mtu ajitahidi kwa moyo wote, bila kutaka kujifaidi mwenyewe, aifanye kazi hiyo ngumu. Inafaa atazamiwe kufanya hivyo, maana Yehova Mungu na Mwanawe wametuwekea mfano mkamilifu wa kufanya kazi, nasi tunatakiwa tuufuate. Yesu Kristo alisema: “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi.” (Yohana 5:17) Basi, sisi sote na tuwe hivyo pia, tujitoe tutumiwe kabisa kulingana na majaliwa tuliyopewa na Mungu. Tukifanya hivyo, maisha yetu yatajawa na furaha na uradhi huku tukitazamia baraka ya Yehova. Maneno ambayo mtume Paulo aliwaandikia Waebrania yanatutia sana moyo: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia. Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.”—Ebr. 6:10-12.
—Kutoka The Watchtower, June 1, 1977.
[Maelezo ya Chini]
a Hilo halihusu Betheli ya Brooklyn peke yake, hali pia matawi mengine makubwa ya Watch Tower Society, yanayochapa vitabu au magazeti.