Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 11/15 kur. 515-520
  • ‘Kuendelea Kulishika Sana Neno la Uzima’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kuendelea Kulishika Sana Neno la Uzima’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUVUMILIA UGONJWA
  • KUVUMILIA MIKAZO
  • FARAJA KWA WALIOSHUKA MOYO
  • KUVUMILIA HUZUNI
  • KUMALIZA HAYA NA WOGA
  • KUEPUKA UFISADI
  • ‘KUNG’AA KAMA WAMULIKAJI’
  • Lifanye Funzo Lako la Kibinafsi Liwe Lenye Kuthawabisha
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
  • Ifanye Mikono Ya Milele ya Yehova Iwe Utegemezo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Unaweza Kuacha Kushuka Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Wewe Unajua Kuvumilia Huzuni Nyingi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 11/15 kur. 515-520

‘Kuendelea Kulishika Sana Neno la Uzima’

“Endeleeni kufanya mambo yote bila manung’uniko wala mabishano, ili mpate kuwa bila lawama na bila hatia, watoto wa Mungu wasio na waa kati ya kizazi kilichopotoka na kupindika, ambacho kati yacho ninyi mnang’aa kama wamulikaji katika ulimwengu, huku mkiendelea kulishika sana neno la uzima.”​—Flp. 2:14-16, tafsiri ya Kiingereza ya New World.

1-3. (a) Ungeonaje ukipokea barua ya baba yako mpendwa? (b) Ni “barua” gani ambazo zimepokewa kutoka kwa Yehova Mungu, nayo matokeo ya kutumia mashauri yaliyomo ni nini?

KAMA baba yako angekuwa akiishi nchi ya mbali, ungefanyaje ukipokea barua yake? Ungekawia kuifungua? Au, ungesoma sentensi moja, mbili, kisha uiweke pamoja na barua zile nyingine?

2 Ikiwa unampenda sana baba yako, ungeshukuru sana kupokea barua yake. Ungeifungua kwa hamu nyingi. Ungependezwa sana kusoma kila neno. Bila shaka ungethamini na kutumia mashauri yo yote mazuri ambayo yangekuwa baruani. Labda hata ungeisoma-soma mara nyingi kwa sababu ya furaha au kwa kusudi la kuhakikisha umeyaelewa yaliyomo. Sivyo?

3 Basi, ikiwa umeweka maisha yako wakf kwa Yehova Mungu, una kitu bora kuliko barua yo yote iwezayo kuandikwa na mzazi wa kibinadamu. Umepokea kutoka kwa Baba yako wa mbinguni kitabu kikubwa chenye “barua” 66, yaani, Neno takatifu la Mungu mwenyewe, Biblia. Kwa kutumia mashauri ya Neno hilo, wafuasi wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta wameendelea kuwa bila hatia “kati ya kizazi kilichopotoka na kupindika,” wakawa wamulikaji wa kiroho katika ulimwengu. Kama wewe ni mmoja wao au unatumainia kupata uzima wa milele duniani katika taratibu mpya ya Mungu iliyoahidiwa, inakupasa ‘ulishike sana neno la uzima.’​—Flp. 2:14-16.

4. “Neno la uzima” ni nini?

4 Hilo “neno la uzima” ni nini? Ni ujumbe wa Mungu unaohusu tumaini la kupata uzima, lililoanza alipotoa ahadi ya kutokeza Uzao. (Mwa. 3:15) Ahadi hiyo ilihakikisha kwamba haki ndiyo ingeshinda mwishowe. Muda wa karibu miaka elfu nne, Yehova aliliongeza “neno” hilo, mpaka Biblia ilipokamilika karibu na mwaka 98 W.K. Tangu wakati huo “neno la uzima” limekuwa na Maandiko Matakatifu yote. Maandiko hayo yanaonyesha kwamba Mungu amefanya watu waweze kupata uzima wa milele kupitia kwa Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Watu wanaotaka kibali ya Mungu na uzima wa milele lazima wafahamu Neno Lake, waeleze watu wengine habari za Neno hilo, Biblia, na kuishi kupatana na vile inavyosema, halafu kwa njia hiyo ‘watalishika sana neno la uzima.’

5. Kwa sababu gani kuna ubora mwingi wa ‘kulishika sana neno la uzima’?

5 Kuna ubora mwingi wa ‘kulishika sana neno la uzima.’ Mtu ye yote aliyelishika sana anaweza kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu. Vilevile, mtu huyo anakuwa katika hali bora ya kuweza kutatua matatizo ya maisha. Zaidi ya hilo, Mkristo anapata uwezo wa kuvumilia hali mbaya kwa sababu ya ‘kulishika sana neno la uzima.’ Tafadhali sasa angalia ukweli wa mambo hayo.

KUVUMILIA UGONJWA

6, 7. Watumishi wa Yehova wanaweza kupata faraja na nguvu wakijua nini juu ya ugonjwa?

6 Ugonjwa unapata maskini kwa matajiri. (Mhu. 5:16, 17; 6:1, 2) Yesu Kristo alisema ndugu zake wa kiroho wangekuwa wagonjwa sana nyakati nyingine. (Mt. 25:39, 40) Tena Wakristo wa kwanza kama Epafrodito, Timotheo na Trofimo walipatwa na ugonjwa. (Flp. 2:25-30; 1 Tim. 5:23; 2 Tim. 4:20) Kwa hiyo, watumishi wa kisasa wa Yehova wanaweza kufarijika kwa kujua kwamba ugonjwa si jambo geni kati ya watu wa Mungu leo.

7 Lakini, tunapata nguvu kwa kujua kwamba Yehova Mungu anaweza kuondoa ugonjwa. (Kum. 7:15) Mfano mmoja ni wa Mfalme Hezekia aliyepona uele wake. Mungu alimponya, akajibu sala ya Hezekia. (2 Fal. 20:1-11) Wakati Yesu Kristo alipokuwa duniani aliponya watu kimwili na kiroho pia. (Mt. 8:14-17; Isa. 53:4) Aliwaponya kwa kutegemea dhabihu ya ukombozi ambayo Mungu alitoa kupitia kwake, iliyokuwa upeo wa mwendo ambao alifuata baada ya roho ya Mungu kuja juu yake katika Mto Yordani mwaka 29 W.K. Basi, Wakristo wanaweza kuwa na hakika kwamba wanadamu watii watakombolewa kabisa na dhambi, magonjwa na kifo, kupitia kwa Yesu Kristo aliyefufuliwa na vilevile chini ya ufalme wa Mungu. Basi, ilifaa sana Daudi akamhimidi Yehova kwa kusema Yeye ndiye ‘anayetuponya magonjwa yetu yote.’​—Zab, 103:1-3.

8. Mkristo mwenye kuugua anaweza kufanya nini sasa?

8 Kwa sasa, Mkristo mwenye kuugua anaweza kufanya nini? Anapoendelea kupata dawa, anaweza kusali Yehova amwimarishe avumilie ugonjwa wake, na kumpa nguvu za kiroho aendelee kuwa mkamilifu kwa Mungu katika hali hizo zenye magumu. Mtu huyo anaweza kuwa na hakika kwamba ‘Yehova atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani.’​—Zab. 41:1-3.

KUVUMILIA MIKAZO

9, 10. (a) Ni jambo gani litakalosaidia mtu aendelee kuwa na kiasi anapokuwa na mikazo? (b) Masumbufu ya moyoni ya Mfalme Sauli yalitulizwaje?

9 Watu wengi, hata Wakristo wengine, wanatatizwa sana na mikazo leo. Hali zenye kutatiza sana na kusumbua sana akili ya mtu zinaweza kutokea maishani. Nyakati nyingine mikazo ya namna hiyo inazidi sana hata mtu anajisikia akiumwa sana akilini. Hata hivyo, ‘akilishika sana neno la uzima’ atasaidika aendelee kuwa na kiasi.

10 Ni jambo gani linaloweza kusaidia mtu mwenye mikazo mingi moyoni? Biblia inatufahamisha. Wakati Mfalme Sauli wa Israeli alipopatwa na roho mbaya ikamsumbua sana, Daudi alimpigia kinubi. Halafu ikawaje? Masimulizi ya Biblia yanasema: “Naye Sauli akaburudishwa, na ile roho mbaya ikamwacha.” (1 Sam. 16:14-23) Naam, muziki mtamu unaokwenda taratibu unaweza kuburudisha mtu na kumpa amani.

11. Msaada ulio mkubwa zaidi unaweza kupatikana wapi nyakati za mikazo?

11 Daudi mwenyewe alijua jinsi mtu anavyojisikia anapopatwa na mkazo. Mfalme Sauli mwenye kumwonea mashaka alijaribu zaidi ya mara moja kumfuma ukutani kwa mkuki. (1 Sam. 18:6-11; 19:9, 10) Sauli alimfanya Daudi awe haramia katika utawala wake, akamlazimisha kuishi kama mtoro mwenye kuwindwa. Bila shaka, wakati huo na nyakati zilizofuata Daudi alipatwa na mikazo. Alisali Yehova Mungu amsaidie. Daudi alimwomba Yehova akamwambia, “Uniangalie na kunifadhili, maana mimi ni mkiwa na mteswa. Katika shida za moyo wangu unifanyie nafasi, na kunitoa katika dhiki zangu.” (Zab. 25:16, 17) Basi, Yehova anaweza kutegemewa asaidie watumishi wake nyakati za mikazo? Hakika! Daudi aliweza kusema hivi: “[Yehova] atakuwa ngome kwake aliyeonewa, naam, ngome kwa nyakati za shida. Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe, maana Wewe, [Yehova], hukuwaacha wakutafutao.”​—Zab. 9:9, 10.

FARAJA KWA WALIOSHUKA MOYO

12, 13. (a) Je! ni kweli kwamba watumishi wa Yehova hawawezi kamwe kujisikia vibaya akilini? (b) Paulo aliwezaje kuvumilia magumu ambayo yangaliweza kumshusha moyo? (2 Kor. 12:7-10)

12 Watu ‘wanaolishika sana neno la uzima’ wanaweza pia kupata faraja katika Maandiko ikiwa hawajisikii vizuri akilini. Wataona kwamba watu wengine waliomtumikia Yehova zamani walishuka moyo nyakati nyingine. Bila shaka Isaka na Rebeka walishushwa moyo na wale wake wawili Wahiti walioolewa na mwana wao Esau, maana tunaambiwa hivi: “Roho zao Isaka na Rebeka zikajaa uchungu kwa ajili yao.”​—Mwa. 26:34, 35.

13 Ni wazi kwamba Wakristo wengine wa kwanza walishuka moyo, kwa sababu mtume Paulo alishauri waamini wenzake katika Thesalonike ‘wawatie moyo walio dhaifu.’ (1 The. 5:14) Paulo mwenyewe alipatwa na magumu yakamshusha moyo, lakini alivumilia hali hizo kwa kutegemea nguvu za Mungu. Mtume huyo aliandika hivi: “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi.” (2 Kor. 4:8, 9) Naam, mfano wa Paulo unatia Wakristo wote moyo.

14. Tukishushwa moyo na matatizo yetu binafsi, kwa sababu gani inatupasa tumkumbuke Nehemia?

14 Pengine wewe umeshuka moyo kwa sababu ya matatizo yako binafsi au kwa sababu ya mambo mengine yanayokusumbua sana. Ikiwa ndivyo, mkumbuke Nehemia. Alikuwa na majonzi alipokuwa mbele ya Mfalme Artashashta kwa sababu Yerusalemu na kuta zake zilikuwa katika hali ya uharibifu. Alipohojiwa na mtawala huyo Mwajemi, Nehemia ‘alimwomba Mungu wa mbinguni.’ Halafu akaomba ruhusa aende Yerusalemu akaujenge upya mji huo. Mfalme alikubali. Kweli “mkono mwema wa Mungu” ulikuwa juu ya Nehemia. (Neh. 2:1-8) Hata leo, inawapasa watu wa Yehova wamwombe msaada na uongozi kuhusu matatizo au mambo mengine yenye kuwasumbua. Ndipo wanapoweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakuwa pamoja nao, wakifuata uongozi wake.

15. Petro alionyesha inatupasa tufanye nini nyakati tunaposhuka moyo?

15 Nyakati tusipojisikia vizuri akilini, ni jambo la maana sana kumtegemea Yehova Mungu. Ni kama vile mtume Petro alivyosema: “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”​—1 Pet. 5:6, 7.

KUVUMILIA HUZUNI

16, 17. Kifo cha mpendwa kinaweza kuleta nini, kama Maandiko yanavyoonyesha?

16 Mara kwa mara wanadamu wanakuwa na huzuni. Inaletwa na mambo mengi. Mtunga zaburi alisema: “Naliona taabu na huzuni.” (Zab. 116:3) Jambo moja kubwa linaloleta huzuni nyingi ni kifo cha mpendwa.

17 Ibrahimu mzee wa ukoo alilia alipofiwa na Sara mke wake mpendwa. (Mwa, 23:2) Daudi alipatwa na kihoro alipofiwa na Absalomu, akalia akipaza sauti na kusema: “Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! mwanangu Absalomu! laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu!” (2 Sam. 18:33) Hata Yesu Kristo aliyekuwa mkamilifu ‘alilia machozi,’ akiwa amehuzunishwa sana na kifo cha Lazaro rafiki yake.​—Yohana 11:35.

18, 19. (a) Mtu aliyefiwa anaweza kusaidikaje avumilie huzuni? (b) Tunawezaje kupata faraja katika masimulizi ya Biblia?

18 Kulishika sana neno la uzima’ kunamsaidia aliyefiwa avumilie huzuni. Kwa kawaida, mtu akiyatamani mambo ya kufurahisha aliyofanya pamoja na aliyekufa, huenda akahuzunika zaidi. Kwa hiyo, ni afadhali kuufikiria wakati ujao! Biblia inaonyesha kwamba mabilioni ya wafu watafufuliwa. Paulo alikuwa na tumaini la kwamba kutakuwa na “ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Bila shaka, Mungu ndiye atakayeamua ni watu gani watakaofufuliwa Lakini, Mkristo mwaminifu atakayepata uzima duniani katika paradiso ya wakati ujao anaweza kuwa na tumaini la kumwona tena mtumishi mwingine aliyeshikamana na Yehova, akafa akiwa na tumaini ilo hilo.​—Yohana 5:28, 29.

19 Mtu aliyefiwa, ‘anayelishika sana neno la uzima,’ anaweza kufarijiwa na masimulizi ya Biblia. Kwa mfano, ebu waza jinsi Maria na Martha walivyofurahi wakati Lazaro ndugu yao wa kimwili alipofufuliwa na Yesu. (Yohana 11:38-44) Na je! unakumbuka ilivyokuwa wakati Yesu Kristo alipomfufua binti mdogo wa Yairo? Masimulizi yanasema, “Wazazi wake wakastaajabu sana,” wakiwa na furaha kweli kweli. (Luka 8:40-42, 49-56) Ebu fikiria jinsi wakaaji wa taratibu mpya iliyoahidiwa na Mungu watakavyofurahi watakapokuwa wakikaribisha wafufuliwa! Mtu anayehuzunikia kifo cha mpendwa anaweza kusaidiwa na mawazo hayo. Juu ya yote, Wakristo wanapofiwa wanapaswa kumkaribia Yehova katika sala, kwa maana yeye ndiye “Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote.”​—2 Kor. 1:3

KUMALIZA HAYA NA WOGA

20, 21. (a) Wenye haya wanaweza kujifunza nini kutokana na habari za Musa? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na habari za Yeremia? (Yer. 1:5-8)

20 Watu fulani ambao wameweka maisha yao wakf kwa Yehova Mungu wametatizwa sana na mawazo ya moyoni, kama haya na woga. Watu fulani wameona ni vigumu kueleza mambo wanayoamini moyoni kwa sababu ni wenye haya nyingi sana. Lakini wale ambao ‘wamelishika sana neno la uzima’ wanajua kwamba watumishi wengine wa Mungu wametatua matatizo kama hayo.

21 Kwa mfano, nabii Musa alikuwa na tatizo la kueleza maoni yake. Wakati Mungu alipomwambia Musa kwamba angemrudisha Misri akawaondoe Waisraeli utumwani, Musa alionyesha ubaridi mwingi na kusema: “Ee Bwana, mimi si msemaji, tokea zamani, wala tokea hapo uliposema na mtumishi wako; maana mimi si mwepesi wa kusema, na ulimi wangu ni mzito.” Hata hivyo Yehova alimtuma Musa Misri, akampa Haruni awe mnenaji wake. Lakini Musa hakukata tamaa, kwa kuacha anenewe nyakati zote na watu wengine. Baadaye, yeye mwenyewe alinena na Waisraeli bila wasiwasi.​—Kut. 4:10-17; Kum. 1:1-5.

22. Paulo alimpa Timotheo shauri gani juu ya woga?

22 Fikiria pia shauri ambalo mtume Paulo alimpa Timotheo. Hatuna hakika kama Timotheo alikuwa ameanza kuogopa kidogo. Lakini, Paulo alimwambia hivi: “Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”​—2 Tim. 1:7, 8.

23. Mtu anawezaje kuondoa haya na woga?

23 Mkristo anaweza kutatua matatizo kama lile ambalo Musa alikuwa nalo. Vilevile, inawezekana kuondoa haya na woga kwa kumwomba Yehova Mungu kwa bidii atupe nguvu. (Flp. 4:6, 7, 13) Wampendao Yehova wanaweza kutafuta kibali yake nyakati zote kwa kusali bila woga au hofu, tena wanaweza kueleza watu kweli za Mungu kwa ushujaa. Mtume Yohana aliandika akasema, “Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu. Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu.”​—1 Yohana 4:17, 18.

KUEPUKA UFISADI

24. (a) ‘Kicho cha Yehova’ kinawezaje kulinda mtu? (b) Uasherati unaweza kuleta nini?

24 Kwa upande mwingine, kuna woga unaofaa, na ndiyo sababu Biblia inasema kwamba “kicho cha [Yehova] ni kitakatifu,” nacho “ni kuchukia uovu.” (Zab. 19:9; Mit. 8:13) Kicho hicho si kuogopa kupita kiasi, bali kinahusu heshima na woga mzuri wa kujizuia tusimchukize Yehova. Woga huo unatulinda tusifuate mwendo mbaya. Kwa kawaida, mtu ‘anayelishika sana neno la uzima’ anajua kwamba Maandiko yanakataza mambo kama uasherati. (Kum. 5:18; 1 Kor. 6:9, 10) Biblia inaonyesha kwamba uasherati unaweza kuleta huzuni pia. Baada ya Amnoni mwana wa Mfalme Daudi kumnajisi Tamari, dada mzazi mmoja naye, alianza ‘kumchukia machukio makuu sana.’ Amnoni aliagiza Tamari aondolewe nyumbani mwake, maana kuwa humo kulimfanya Amnoni ajisikie yu mchafu.​—2 Sam. 13:1-19.

25. Kwa sababu gani mtu anaposhawishwa anaweza kufaidika kwa kuukumbuka mwenendo wa Yusufu?

25 Lakini, Yusufu mwana wa Yakobo ni mfano mwema sana kwetu! Aliposhawishwa-shawishwa na mke wa Potifa bwana wake, alikataa kabisa kulala naye. Ingawa Yusufu alishtakiwa uongo na kutiwa gerezani kwa sababu ya kukataa kufanya hivyo, hakumtenda Mungu dhambi. (Mwa. 39:7-23) Mtu mwenye ‘kulishika sana neno la uzima’ anaweza kufaidika akiukumbuka mwenendo wa Yusufu wakati ashawishwapo afanye uasherati.

‘KUNG’AA KAMA WAMULIKAJI’

26-28. (a) Mwisho, tunaweza kusaidikaje kwa ‘kulishika sana neno la uzima’? (b) Tunawezaje kuendelea ‘kung’aa kama wamulikaji’?

26 Basi, wale ambao ‘wamelishika sana neno la uzima’ wanapaswa sana kuvithamini vile vitabu 66 vya Biblia Takatifu vilivyoandikwa kwa uongozi wa Mungu. Jambo moja linalowezesha Wakristo kuvumilia ugonjwa na mikazo ni kutumia mashauri ya Maandiko. Wanapokuwa wameshuka moyo wanapata faraja katika Neno la Mungu. Biblia inawasaidia kuvumilia huzuni pia, kuondoa haya na woga, na kuepuka ufisadi.

27 Zaidi ya hilo, wale ‘wanaolishika sana neno la uzima’ wanakuwa na uwezo wa kubaki “bila lawama na bila hatia” ya matendo mabaya ya hiki “kizazi kilichopotoka na kupindika,” yaani, wanadamu waliotenganishwa na Mungu. Wakristo wanaendelea ‘kung’aa kama wamulikaji’ kati yao. (Flp. 2:14-16) “Mkutano mkubwa” walio na matumaini ya kuishi milele katika dunia itakayokuwa paradiso wanashirikiana na wafuasi wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta, ambao ndio wenye wajibu wa kwanza wa kuwa “wamulikaji” wa kiroho.​—Ufu. 7:4-9.

28 Wakristo wote waaminifu wakimtegemea Yehova Mungu, wataendelea kuangaza nuru ya kiroho. Kwa kusaidiwa naye wataendelea kuonyesha roho inayofaa, inayowapasa watu wanaomwabudu Yehova Mungu. Watajaribu kusitawisha na kuonyesha matunda ya roho ya Mungu, kisha wataonyesha hekima kwa kuzikumbuka sifa zile njema za Wakristo wa kwanza na watu wengine ambao wamemtumikia Yehova karne nyingi hata sasa. Halafu Bwana ataendelea kuwa pamoja na roho inayoonyeshwa na watu wote wanaomcha Mungu leo na ‘kulishika neno la uzima’ kweli kweli. Je! wewe ni mmoja wa wale wanaoonyesha roho inayofaa ya Kikristo, na je! umelishika “neno la uzima” barabara?

​—Kutoka The Watchtower, June 15, 1977.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki