Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 12/15 kur. 17-20
  • Kutoka Babeli wa Kale Mpaka Karne ya 20 Katika Unabii wa Biblia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoka Babeli wa Kale Mpaka Karne ya 20 Katika Unabii wa Biblia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTOKA BABELI MPAKA UTAWALA WA “MWANADAMU”
  • NDOTO YA SANAMU YA NEBUKADREZA
  • “ISHARA” YA KUWAPO KWA KRISTO
  • Serikali za Wanadamu Zapondwa na Ufalme wa Mungu.
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Uwe na Imani Katika Ule Ufalme!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Kuinuka na Kuanguka Kwa Sanamu Kubwa Sana
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 12/15 kur. 17-20

Kutoka Babeli wa Kale Mpaka Karne ya 20 Katika Unabii wa Biblia

UNABII wa Biblia umekuwa na utimizo wa ajabu katika nyakati za kale. Je! wewe ulijua kwamba Maandiko yalitabiri pia mambo yanayohusu karne ya 20?

Kitabu cha Danieli kina njozi za unabii zinazopasa muda wote wa kupanda na kuanguka kwa mamlaka kuu za ulimwengu kuanzia na Babeli wa kale mpaka kizazi hiki chetu. Kwa mfano, katika karne ya sita K.W.K., Danieli aliota ndoto ya wanyama wanne wa mfano. Kulingana na maelezo ya Danieli ya wanyama hawa wa mfano, walikuwa:

(1) simba, kwanza akiwa na mabawa kama ya tai, kisha akayapoteza akawa na sifa za kibinadamu; (2) dubu aliyekuwa akila nyama nyingi sana; (3) chui akiwa na mabawa manne (yakiongeza mwendo wa kasi (mwepesi) sana) na vichwa vinne; na (4) mnyama asiyefanana na mnyama ye yote halisi, “mwenye kutisha, mwenye nguvu, mwenye uwezo mwingi.” Mnyama huyu wa nne alikuwa na meno makubwa ya chuma, pembe kumi, na pembe nyingine “ndogo” iliyozuka (iliyotoka) ikiwa na, macho na “kinywa kilichokuwa kikinena maneno makuu.”​—Dan. 7:3-8.

KUTOKA BABELI MPAKA UTAWALA WA “MWANADAMU”

Wanyama hawa wanne wanafananisha nini? Habari ya Maandiko inasema kwamba wanafananisha “wafalme,” au falme. (Dan. 7:17) Simba anafananisha Babeli, ambayo ndiyo iliyokuwa mamlaka iliyokuwa ikitawala katika Mashariki ya Kati wakati njozi hiyo ilipopokewa. (Yer. 4:5-7) Dubu anafananisha ufalme uliofuata Babeli kama mamlaka ya ulimwengu, ambayo ikawa mwungano wa Wamedi wa Waajemi. Chui aliyekuwa na vichwa vinne pamoja na mabawa anafananisha Milki ya Ugiriki. Na kwa habari ya vichwa vinne vya huyo chui, majemadari wake walishindania utawala wa milki hiyo baada ya kifo cha Aleksanda Mkuu, na mwishowe wanne wao wakapata utawala katika sehemu mbalimbali. Mnyama wa nne wa mfano katika njozi hii anafananisha mamlaka ya ulimwengu iliyoimaliza Milki ya Ugiriki, yaani, Rumi.

Namna gani juu ya zile pembe kumi za mnyama huyu wa nne pamoja na ile pembe nyingine iliyokuwa na macho na “kinywa kilichokuwa kikinena maneno makuu”? (Dan. 7:8) Nyakati nyingine Maandiko yanatumia pembe kufananisha watawala na nasaba za watawala. (Dan. 8:2-10, 20-22; Zek. 1:18-21; Luka 1:69-71) Kumi inaonyesha utimilifu, yote, hesabu kamili ya kitu kilichoko. (Mt. 25:1; Luka 15:8; 19:13, 16, 17) Historia inaonyesha kwamba Milki ya Kirumi mwishowe iligawanyika ikawa mataifa mbalimbali. Zile pembe kumi za mnyama huyu wa nne kwa wazi zinafananisha falme zote zilizotokana na kuvunjika kwa Rumi.

Kwa habari ya ile pembe “ndogo” iliyozuka kati ya zile kumi, katika karne ya 18 W.K., Uingereza, iliyokuwa sehemu ndogo tu iliyotawaliwa na Rumi wakati mmoja, ilijitokeza ikawa ndiyo mamlaka ya ulimwengu iliyo kuu katika mambo ya kibiashara na kisiasa. Kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na kuungana katika kufanya mambo pamoja, Uingereza na United States, mara nyingi hujulikana kama Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Uingereza na Amerika. Mamlaka hii inalingana vizuri sana na maelezo ya Biblia ya ile pembe “ndogo.”

Kwa kuwa Mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika bado ipo, njozi ya Danieli ya wale wanyama wanne inatabiri mfululizo wa matukio ya historia ya mwanadamu tangu wakati wa Babeli wa kale mpaka siku zetu hizi. Walakini ni jambo gani linalofuata wakati mfululizo huu wa falme za kisiasa za wanadamu unapofikia mwisho wake? Danieli anaongeza hivi:

“Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja na mawingu ya mbinguni akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.”​—Dan. 7:13, 14.

Ni jambo la kufurahisha kama nini kufikiri kwamba “mwanadamu,” Yesu Kristo, anachukua utawala juu ya “watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote,” na kwamba anafanya hivyo katika siku hizi zetu! Watu wanaoishi katika kipindi hiki cha wakati wana baraka za ajabu wanazoweza kutazamia.

NDOTO YA SANAMU YA NEBUKADREZA

Ndoto ya kinabii aliyoiota Nebukadreza ilikuwa na maana iyo hiyo. Mfalme huyu wa Babeli aliona katika njozi yake sanamu kubwa sana ya madini mbalimbali iliyokuwa na umbo la mwanadamu. Danieli anaeleza kwamba sanamu hii, “kichwa chake kilikuwa ni cha dhahabu safi; kifua chake na mikono yake ni fedha; tumbo lake na viuno vyake ni vya shaba; miguu yake ni ya chuma; na nyayo za miguu yake nusu ya chuma na nusu ya udongo.”​—Dan. 4:31-33.

Danieli alieleza kwamba kichwa hicho cha dhahabu kilifananisha Nebukadreza, au, kwa kuongeza, nasaba ya watawala wa Kibabeli iliyoanza na Nebukadreza. (Dan. 2:37, 38) Kifua na mikono ya fedha ilifananisha mamlaka ya ulimwengu iliyofuata ya mwungano wa Wamedi na Waajemi. Tumbo na miguu ya chuma ilifananisha “ufalme mwingine, wa tatu [tunapohesabu kuanzia na Babeli].” (Dan. 2:39) Hii ndiyo iliyokuwa Mamlaka ya Ulimwengu ya Ugiriki. Sehemu nyingine ya sanamu hiyo, miguu ya chuma, hapo mwanzoni ilifananisha Rumi. Hata hivyo, Rumi haiwezi kutimiza matakwa yote ya sehemu ya chuma ya sanamu hiyo. Kwa sababu gani?

Kwa sababu chuma kilifika hata kwenye nyayo za miguu ya sanamu hiyo, zikiwa nusu chuma na nusu udongo. Na kwa habari ya nyayo za sanamu hiyo, Biblia inaendelea kusema hivi: “Jiwe likachongwa bila kazi ya mikono, nalo jiwe hilo likaipiga sanamu miguu yake, iliyokuwa ya chuma na udongo, likaivunja vipande vipande. Ndipo kile chuma, na ule udongo, na ile shaba, na ile fedha, na ile dhahabu, vilivunjwa vipande vipande pamoja.”​—Dan. 2:34, 35.

Sehemu hii ya ndoto ya Nebukadreza ilikuwa na maana gani? Danieli anaeleza hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote [zinazofananishwa na sanamu hiyo yote] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”​—Dan. 2:44.

Kuvunjwa vipande vipande na kuangamizwa huku kwa falme zote za kidunia na mahali pake kuchukuliwa na utawala wa kimungu hakukutukia katika siku za Milki ya Kirumi. Kwa hiyo, sehemu ya chuma ya sanamu hii inafika hata kwenye mamlaka ya ulimwengu iliyofuata Rumi, mwungano wa Uingereza na Amerika. Kwa hiyo, njozi hii inalingana na ile ya wanyama wanne katika kutabiri mfuatano wa matukio makubwa ya historia ya mwanadamu kuanzia na Babeli wa kale mpaka kuchukuliwa kwa utawala wa kidunia na ufalme wa Mungu mikononi mwa “mwanadamu,” Yesu Kristo.

Je! tunaweza kutazamia jambo hilo litukie hivi karibuni?

“ISHARA” YA KUWAPO KWA KRISTO

Upesi kabla Yesu hajauawa, wanafunzi wake walimwomba “ishara ya kuwapo [kwake] na ya mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 24:3, NW) Kwa “kuwapo” walimaanisha kutawala kwake katika mamlaka ya Ufalme. Yesu alijibuje ulizo lao? Utafaidika ukisoma jibu kamili kama lilivyoandikwa katika Mathayo 24, 25, pamoja na habari zinazolingana katika Marko 13 na Luka 21. Hapa tunatoa tu mambo machache makuu.

Kulingana na habari katika Injili ya Luka, alitia ndani mambo haya kama sehemu ya ishara ya kuwapo kwake: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi; na njaa na tauni mahali mahali.” (Luka 21:10, 11) Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha ushuhuda uo huo wa kuwapo kwa Yesu akiwa mfalme, lakini katika lugha ya mfano. Katika maelezo ya yale yanayotokea duniani baada ya Yesu Kristo, akiwa ndiye mpandaji wa “farasi mweupe” wa mfano, apokeaye “taji” ya ufalme wenye kutenda juu ya ulimwengu wa wanadamu, tunasoma hivi:

“Akatoka farasi mwingine [na aliyempanda], mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa. [Linganisha na Luka 21:10 kuhusu ‘taifa kupigana na taifa.’] . . .

“Nikaona, na tazama, farasi mweusi, na yeye aliyempanda ana mizani mkononi mwake. Nikasikia sauti katikati ya hao wenye uhai wanne, ikasema, Kibaba cha ngano kwa nusu rupia [mshahara wa siku nzima katika wakati huo], na vibaba vitatu kwa nusu rupia, wala usiyadhuru mafuta wala divai. [Linganisha na Luka 21:11 kuhusu njaa.]. . .

“Nikaona, na tazama, farasi wa rangi ya kijivujivu, na yeye aliyempanda jina lake ni Mauti, na [kaburi la kawaida la wanadamu] akafuatana naye. Nao wakapewa mamlaka juu ya robo ya nchi, waue kwa upanga na kwa njaa na kwa tauni na kwa hayawani wa nchi. [Angalia kwamba Luka 21:11 inatia ndani tauni.]”​—Ufu. 6:1-8.

Je! wewe mwenyewe hujapatwa na mambo hayo? Je! kizazi cha watu kinachoishi leo hakikupatwa na taabu ya vita visivyo na mfano, upungufu wa chakula na magonjwa ya kipuku, kuanzia na Vita ya Kwanza ya Ulimwengu katika mwaka 1914 W.K.? Wala si mambo hayo tu yanayotiwa ndani ya ishara ya kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme.

Yesu aliongeza sehemu nyingine ya ishara hiyo: “Na kwa sababu ya kuongezeka kwa maasi, upendo wa wengi utapoa.” (Mt. 24:12) Je! wewe hukubali kwamba kuongezeka sana kwa maasi katika sehemu nyingi za dunia katika kizazi hiki kumefanya upendo wa watu wengi kwa Mungu na kwa wanadamu wenzao upoe?​—Linganisha 2 Timotheo 3:1-5.

Hali hizi za ulimwengu hata ziwe mbaya namna gani, zinatoa sababu yenye nguvu ya kuwafanya wale wanaoiamini Biblia wafurahi, kwa kuwa Yesu aliongeza hivi: “Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo, yote yatakapotimia.” Hiyo inamaanisha kwamba watu waliouona mwanzo wa nyakati hizi zenye taabu bado watakuwa hai wakati ufalme wa Mungu wa kimbinguni unapouleta mwisho wa taratibu iliyopo ya mambo.​—Mt. 24:8, 34.

Ni nini itakayochukua mahali pake? Ni taratibu mpya ya mambo chini ya utawala wa kimungu. Kikieleza namna hali zitakavyokuwa duniani wakati huo, kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinasema hivi: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”​—Ufu. 21:3, 4.

Je! wewe ungefurahia kuishi katika taratibu hiyo mpya ya mambo? Ikiwa ndivyo, kutimizwa kwa “ishara” aliyoitoa Yesu kunaweza kuwa na maana ya pekee kwako. Yesu alitaja hili, akisema: “Basi mambo haya yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.”​—Luka 21:28.

Lo! tumaini la ajabu namna gani! Hata hivyo, Mungu anaweka matakwa, ambayo si vigumu kuyatimiza, kwa wale wote watakaookoka na kuingia katika taratibu hiyo mpya ya mambo. (1 Yohana 5:3, 4) Je! wewe wataka kujifunza Biblia ili ujue matakwa hayo ya Mungu? Inakupasa kupata furaha kweli kweli katika kufanya hivyo. Mashahidi wa Yehova watafurahia kuongoza funzo la Biblia la nyumbani bila malipo. Vilevile, mikutano katika Majumba yao ya Ufalme ni ya bure na watu wote wanakaribishwa. Onana na Mashahidi wa Yehova upesi, upate ufahamu zaidi juu ya kutimizwa kwa unabii wa Biblia katika karne hii ya 20.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki