Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 1/15 kur. 9-14
  • “Mkakae kwa Amani Ninyi kwa Ninyi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mkakae kwa Amani Ninyi kwa Ninyi”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUPOKEA WENGINE KWA JINA LA KRISTO
  • Kutumikia kwa Umoja Kama Ushirika wa Ndugu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vile Unyenyekevu Unavyoweza Kukulinda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Somo Muhimu Kuhusu Unyenyekevu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Unaweza Kujifunza Nini Kutoka kwa Watoto?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 1/15 kur. 9-14

“Mkakae kwa Amani Ninyi kwa Ninyi”

“Mwe na chumvi ndani yenu, mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi.”​—⁠Marko 9:50.

1. Kwa sababu gani ni vizuri watu wanaofanya kazi pamoja waendelee kuwa na amani?

NYAKATI zote ni vizuri watu wanaofanya kazi pamoja wawe na amani wao kwa wao. Kazi wanayotaka kufanya inaweza kuharibika wakiwa na ugomvi, mashindano, au wakitengana. Wote wanaweza kuharibiana mambo kwa sababu ya kutupiana maneno ya ubishi. Wakiwa na amani, wote watafaulu, wataifurahia kazi kwa sababu ya kuifanya vizuri.

2. Ni mwalimu wa namna gani aliyesema maneno haya: “Mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi”?

2 Wachezaji wa kikoa kimoja, watu wa jamii moja, watu waliooana, na jamaa pia zitafaidika zikitii maneno haya: “Mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi.” Ni nani aliyesema maneno hayo? Ni mwalimu wa kale aliyeona mapema kwamba mwishowe kungekuwa na amani ulimwenguni pote. Mwalimu huyo hakufundisha katika darasa moja tu la chuo fulani. Yeye alikwenda katika hadhara ya watu, akachangamana nao, akawafundisha faraghani na katika makusanyiko yao ya hadharani. Kitabu alichotumia kufundisha watu ni mkusanyo wa Maandiko yaliyoongozwa na Mungu na kuandikwa kwa lugha yake ya kienyeji, yaani, Kiebrania. Mafundisho yake yamedumu zaidi ya karne kumi na tisa, nayo yametafsiriwa katika lugha zaidi ya elfu moja. Mwalimu huyo mashuhuri hakuwa Buddha wala Confucius, bali alikuwa Yesu Kristo, yule “mwana” wa Mfalme Daudi na wa Ibrahimu mzee wa ukoo.

3. Ni nani ambao Yesu aliambia waendelee kuwa na amani wao kwa wao, na kwa sababu gani tunashangazwa na jambo hilo?

3 Ni watu gani ambao Yesu Kristo aliambia wakae kwa amani wao kwa wao? Tunashangaa kujua kwamba ni wanaume wateule waliokuwa wamefuatana naye miaka miwili au zaidi katika kazi yake ya kusafiri-safiri akifundisha watu. Alikuwa amewaita wanaume hao kumi na wawili mitume. Jina hilo lilionyesha kusudi la kuwachagua, kwa maana neno “mitume” lina maana ya “waliotumwa.” Walipaswa kuwa waalimu kama yeye, naye alikusudia kuwatuma hata sehemu zilizo mbali na nchi ya kwao, wakafanye watu wa mataifa yote wawe wanafunzi wake. Alitaka kuanzisha kundi la wanafunzi wake ulimwenguni pote. Mitume wangekuwa kama mawe ya msingi ya kundi hilo.

4. Je! mitume hao hawakuwa wameyafahamu mafundisho ya Yesu juu ya amani, na kwa hiyo ni jambo gani lililomfanya awashauri juu ya amani?

4 Mitume walilifahamu sana fundisho la Yesu juu ya amani. Mwaka uliokuwa umetangulia waliyasikia Mahubiri yake mashuhuri juu ya Mlima, karibu na Bahari ya Galilaya, na humo alitaja heri fulani. Mojawapo heri hizo ni hii: “Heri wapatanishi [au “wenye kutaka amani,” NW] ; maana hao wataitwa wana wa Mungu.” (Mt. 5:9) Sasa, wakati Yesu alipokuwa katika mji wa Kapernaumu, uliokuwa kando ya bahari, ni jambo gani lililomlazimisha awaambie wanafunzi hao wateule hivi: “Mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi”? (Marko 9:50) Kwa sababu gani akawaambia rafiki zake wakubwa maneno hayo? Bila shaka kulikuwa na sababu ya kutoa shauri hilo. Bila shaka kuna jambo lililokuwa likiharibu uhusiano wao na kuwazuia kutimiza lengo lao kwa umoja. Ili kupata sababu iliyomfanya Yesu awaambie maneno hayo waziwazi, inatupasa tuangalie masimulizi yanayotangulia wakati huo, katika Injili ya Marko, sura ya tisa. Ndipo tutakapoweza kufahamu kwa nini shauri ambalo Yesu aliwapa mitume linatufaa sisi pia leo.

5. Ni jambo gani lililokuwa limetukia katika mlima mrefu karibu na Kaisaria Filipi, na baadaye ni kisa gani cha mtu aliyekuwa na shetani kilichoshughulikiwa?

5 Yesu alikuwa amekuwa pamoja na mitume wake upande wa kaskazini, karibu na Kaisaria Filipi, karibu na mahali ambako Mto Yordani unaanza kutiririka ukishuka kusini na kuiingia Bahari ya Galilaya. Yesu alipokuwa katika mlima mrefu, labda Mlima Hermoni ulio katika safu ya milima iliyo mashariki ya Mlima Lebanoni, aligeuka sura kwa mwujiza, huo ukawa mfano mdogo wa utukufu ambao angekuwa nao katika ufalme wa Mungu. Mitume Petro, Yakobo na Yohana ndio peke yao walioona Bwana wao akigeuka sura. Aliposhuka kutoka mlimani, Yesu alikutana na kivulana mwenye shetani, ambaye mitume wale wengine tisa walishindwa kuponya bila ya Yesu kuwa pamoja nao. Yesu alisihiwa na baba mwenye wasiwasi wa kivulana huyo, kisha akamfukuza shetani huyo aliyekuwa na kichwa kigumu sana. Hivyo ndivyo baba huyo alivyopata thawabu kubwa kwa sababu ya kumwamini Yesu, nayo imani yake ikatiwa nguvu.​—⁠Marko 9:14-29; 2 Pet. 1:16-18.

6. Baada ya kufika Kapernaumu, mitume walionaje Yesu alipowauliza ulizo?

6 Mji wa Kapernaumu ulikuwa karibu maili 25 (kilometres 40) kusini ya ujirani huo, kwa kupitia Galilaya. Yesu na mitume wake kumi na wawili walitembea kwa miguu wakiwa wamenyamaa, bila kusema na watu, wakaufikia mji huo uliokuwa umekuwa makao makuu ya Yesu, hata ukapata kuitwa “mjini kwao.” (Mt. 9:1) Juu ya yaliyotukia katika mwendo wao wa kuelekea kwenye mji huo uliokuwa kando ya bahari, tunasoma yafuatayo katika Injili ya Marko: “Wakafika Kapernaumu; hata alipokuwamo nyumbani, akawauliza, Mlishindania nini njiani? Wakanyamaza; kwa maana njiani walikuwa wakibishana wao kwa wao, ni nani aliye mkubwa.”​—⁠Marko 9:33, 34.

7. Kwa sababu gani si ajabu kwamba ubishi wao ulihusiana na Ufalme?

7 Ni wazi kwamba mitume walikuwa wamebaki nyuma ya Kiongozi wao, Yesu. Lakini, kwa njia fulani yeye akafahamu kwamba ubishi mkali ulitokea kati yao. Ilifaa amalize ubishi wo wote ukitokea kati ya wafuasi wake. Njia yake ya kuumaliza inaonyesha alijua jambo walilokuwa wakizungumza. Kulingana na maneno ambayo Yesu alikuwa ametangulia kuwaambia katika Marko 9:30-32, walijua kwamba Kiongozi wao alikuwa karibu kufa. Waliamini kwamba ndiye Masihi, aliyetazamiwa kuwa Mfalme wa Israeli. Walikuwa wamemsikia akitoa mifano mingi juu ya Ufalme; na muda mfupi tu kabla hajageuka sura katika mlima ule mrefu, walimsikia akiwaambia wote kumi na wawili hivi: “Amin, nawaambia, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapouona ufalme wa Mungu umekuja kwa nguvu.”-​—⁠Marko 9:1.

8. Basi, kwa sababu gani mitume walianza kujilinganisha wao kwa wao?

8 Ingawa walikuwa na matumaini kwamba ufalme wa Kimasihi ungeanzwa mapema, walikuwa na haki ya kufikiria vyeo mbalimbali ambavyo wangekuwa navyo pamoja na Kiongozi wao katika ufalme huo. Mambo yanapokuwa hivyo, maelekeo ya mwanasiasa huwa kujitukuza mwenyewe, badala ya kutukuza wapinzani wake wanaopigania uchaguzi. Hivyo ndivyo mitume walivyoanza kujilinganisha wao kwa wao. Mazungumzo yao hayakuwa ya kuona anayefaa kuwa katika cheo hiki au hiki, bali ya kuona anayestahili kupata cheo cha pili kwa Masihi mwenyewe.

9. Kwa Sababu gani hakuna mtume aliyejibu ulizo la Yesu?

9 Hawakuwa wakiongea habari za anayetaka kuwa karibu zaidi na Masihi katika Ufalme kwa sababu ya kumthamini zaidi. Wao walitaka kuwa na cheo cha pili kwake. Kati ya wanadamu wasiokamilika, choyo haiwezi kukosa katika mazungumzo kama hayo. Si ajabu kwamba mitume hao wenye kujitakia makuu ‘walinyamaza’ Yesu alipowauliza hivi: “Mlishindania nini njiani?” Waliona kwamba mambo waliyokuwa wamezungumza hayakuwa yenye kusifika. Walijua kwamba walionyesha choyo, kila mmoja akijitafutia mambo yake mwenyewe, akijitukuza katika jambo hilo. Basi hakuna aliyemjibu Yesu.

10. Yesu alionyesha nini kwa vile alivyoanza kulitatua tatizo lao, naye alitaja kanuni gani ya uongozi?

10 Lakini, haikuwa lazima Yesu amsikie ye yote kati yao akikubali kosa hilo. Unyamavu wao ulionyesha waliaibika. Lakini Yesu angeweza kwa kiasi fulani kujua mawazo ya watu, kwa hiyo alipata kufahamu jambo lililoleta mazungumzo yao. Alionyesha alilijua jambo hilo kwa vile alivyoanza kulitatua tatizo lao. “Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote.” (Marko 9:35) Kwa kusema hivyo Yesu alionyesha wazi kanuni iliyohusu vyeo katika ufalme wake.

11. Kwa hiyo, ni kwa njia gani wenye kushirikiana na Yesu katika ufalme wake walipaswa kutofautiana na wanasiasa walio katika falme za ulimwengu huu?

11 Ufalme wake ungekuwa tofauti na falme za ulimwengu huu, ambamo wanasiasa hutaka vyeo kwa sababu ya kujitakia makuu, na kutaka kutumikiwa na watu badala ya kuwatumikia. Hilo ni tendo la kujiona, ni ukosefu wa unyenyekevu. Yesu mwenyewe hakuonyesha nia ya namna hiyo. Iliwapasa wanafunzi ambao wangeshirikiana naye katika ufalme wake waonyeshe nia ile ile aliyokuwa nayo. Ndiyo sababu baadaye mtume Paulo aliandikia waliotazamiwa kuwa warithi wa ufalme wa mbinguni akawaambia hivi: “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.”​—⁠Flp. 2:5-8.

12. Yesu aliwekaje mfano wa kufuata kanuni ambayo yeye mwenyewe alikuwa ametajia mitume wake?

12 Je! Yesu hakujifanya “wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote”? Yeye ndiye kiumbe kilichoweka mfano mzuri zaidi wa unyenyekevu. Lakini alipewa cheo cha kwanza katika uumbaji wote kwa sababu ya kunyenyekea hivyo na kufanya huduma iliyomletea kifo hapa duniani. Mwana huyo wa Mungu alitukuzwa akawa ndiye wa pili kwa Muumba mwenyewe. Ni kwa sababu hakufikiria kujinyakulia mamlaka awe kama Baba yake wa mbinguni, Mungu Aliye Juu Zaidi. Kwanza, Yesu alikuwa na akili za kutosha kumwonyesha kwamba isingaliwezekana awe kama Mungu.​—⁠Zab. 148:13.

13. Kulingana na kanuni ya Yesu, ni nani anayekuwa mshiriki mwenye maana zaidi katika tengenezo lo lote, na kwa sababu gani?

13 Basi Yesu alionyesha kwamba kanuni aliyowaambia mitume wake ilimhusu yeye pia. Aliwekea mfano bora wote wale watakaojiunga naye katika ufalme wa mbinguni. Tena, itawapasa wote watakaokuwa duniani wakiwa raia za ufalme wake waige unyenyekevu wake na utumishi mzuri aliofanyia watu. Basi, ni nani mwenye maana zaidi katika tengenezo lo lote? Je! siye mtu aliye mnyenyekevu kiasi cha kukubali utumishi wa namna zote, na kutaka kutumikia watu wote? Mtu akitaka kuwa wa kwanza kwa sababu ya choyo, huyo hawezi kuinama afanyie watu wote walio katika tengenezo utumishi wa namna zote. Ingempasa ajione kuwa “wa mwisho kuliko wote” katika tengenezo ili kuwa na nia ya kufanyia mtu ye yote hata utumishi unaoonekana kuwa ovyo sana. Lakini kufanya hivyo hakupunguzi ubora wake wa ndani. Mtu wa namna hiyo anakuwa ndiye mwenye maana zaidi kwa sababu ya kutumikia watu wote bila kubagua.

14. Ni kwa njia gani mtu huyo mwenye kutumikia wengine vizuri anavyokuwa “wa kwanza” kuliko wote?

14 Kwa hiyo watu watasikitika mtu huyo mnyenyekevu na mwenye kuwatumikia vizuri asipokuwapo. Watajisikia wakiukosa utumishi wake. Ingawa huenda akawa siye wa kwanza katika cheo, yeye ndiye atakayekuwa “wa kwanza” kuliko wote kwa sababu ya utumishi mzuri anaofanyia watu. Jambo la maana ni kuwa hivyo machoni pa Mungu kuliko kuwa vingine machoni pa watu wenye vyeo vikubwa maishani.

KUPOKEA WENGINE KWA JINA LA KRISTO

15. Kwa kutumia mtoto mdogo kama mfano, Yesu alisema mwenye kupokea wengine angekuwa amefanya nini?

15 Kufikiria watu hata wakiwa na cheo kidogo sana kutatusaidia sana kuwa na mapatano. Yesu aliendelea kutoa mfano ili kukazia jambo hilo. Tunaelezwa habari hizo katika Marko 9:36, 37: “Akatwaa kitoto, akamweka katikati yao, akamkumbatia, akawaambia, Mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi; na mtu akinipokea mimi, humpokea, si mimi, bali yeye aliyenituma.”

16. Yesu alionyeshaje kwamba alipenda watoto hata nyumbani kwao Nazareti?

16 Kuna mifano iliyoandikwa kuonyesha kwamba Yesu alipenda watoto wadogo. Kwa kuwa ndiye aliyekuwa mwana mkubwa zaidi katika jamaa yao ya kidunia, bila shaka alipaswa kufanya kazi nyingi za kutunza wadogo wake wa mzazi mmoja naye (Yakobo, Yusufu, Simoni na Yuda) pamoja na dada zake wawili au zaidi, huko katika Nazareti, mji wa Galilaya. (Mt. 13:53-56) Hakuwadharau kwa sababu walikuwa wenye makosa. Hakuwawekea kikwazo kwa kushindwa kutafutia jamaa riziki, bali alitia bidii akiwa seremala stadi. (Marko 6:3) Alijifunza kuthamini sifa zilizoonyeshwa na watoto kwa moyo mweupe, na vilevile sifa za kitoto zilizo katika watu wazima. Alifanya vizuri akatumia watoto katika mifano yake.

17. Ni ulizo gani linalotokea juu ya kuweza kufikiwa na watu wenye sifa za kitoto?

17 Tunapokuwa na kazi nyingi sana, labda hatutaki kusumbuliwa na watoto. Huenda watu wanaojiona au kujisikia wakiwa na cheo chenye heshima nyingi wakafikiri watu wa hali yao hawapaswi kusikiliza watoto wenye akili ndogo au watu wazima wenye sifa za kitoto. Lakini namna gani ikiwa watu hao wenye sifa za kitoto ni Wakristo au ni wenye akili na wanataka kuwa Wakristo? Je! sisi ambao tumekwisha kuwa wanafunzi wa Kristo tutawafanya wajisikie wakitaka kutujia tusikilize mahitaji yao?

18. Kwa sababu gani mpokeaji wa namna hiyo angekuwa akimpokea Yesu pia?

18 Tukikataa kusaidia watu hao wenye sifa za kitoto, tutakosa pendeleo kubwa na baraka nyingi. Kama Wakristo waliokomaa kama mitume wa Yesu wangekataa kupokea Mkristo aliyebatizwa majuzi aliye mfano wa kitoto kidogo ambacho Yesu alikumbatia akakitumia kama mfano, wangekuwa wakikataa kumpokea Yesu mwenyewe. Kwa sababu gani? Kwa sababu Yesu alisema kwamba ye yote anayepokea “mtoto mmoja wa namna hii” anampokea yeye pia, kwa sababu anafanya hivyo “kwa jina” la Yesu. Maana yake ni kwamba, Yesu anaona yeye mwenyewe ndiye amepokewa kama Masihi au Kristo. Kwa upande mwingine, watu wenye sifa za kitoto wasipopokewa, anaona yeye mwenyewe ndiye hakupokewa!

19. Mtu anapopokea mwingine mwenye sifa za kitoto kwa njia hiyo, anakuwa na uhusiano mzuri na nani, na kwa sababu gani?

19 Tunapofanya kazi inayohitaji unyenyekevu “kwa jina” la Kristo au kwa sababu ya kuliheshimu jina lake, inakuwa vyepesi zaidi kuifanya kazi hiyo, nayo inatupendeza. Tunaifanya tukiwa na kusudi zuri sana. Tena, inatuletea uhusiano mzuri na Yesu Kristo, vilevile na Baba yake wa mbinguni. Jambo hilo linaonyeshwa na maneno ambayo Yesu aliongeza: “Na mtu akinipokea mimi [yaani, kwa kupokea “mtoto mmoja wa namna hii”], humpokea, si mimi, bali yeye aliyenituma.” (Marko 9:37) Yesu alitumwa duniani na Baba yake mwenyewe wa mbinguni, Yehova Mungu. Yesu Kristo hawezi kutenganishwa na Baba yake wa mbinguni. Kwa sababu wana umoja katika kusudi na utendaji wao, hawatenganiki. Kwa hiyo mtu akimfanyia Mwana jambo fulani, Yehova Mungu anakubali kwamba hata yeye amefanyiwa jambo hilo. Anaonyesha amekubali kufanyiwa hivyo kwa kumbariki mtu huyo aliyempokea vizuri.

20. Kanuni hiyo inahusikaje katika njia zetu za kushughulika na Wakristo wenzetu, na ni sifa gani ambayo lazima tuwe nayo ili kuwa na ushirika katika Ufalme huo?

20 Ni jambo la maana tukumbuke kanuni hiyo tunaposhughulika na Wakristo wenzetu, hasa wale walio ‘vitoto’ katika ufahamu wa Biblia au ushirika wa kundi la Kikristo. Mtume Petro alisema yafuatayo akiwaambia watu alioandikia barua yake ya kwanza kwa kuongozwa na Mungu: “Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili [au, “ya lile neno, NW] yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu; ikiwa mmeonja ya kwamba Bwana ni mwenye fadhili.” (1 Pet. 2:2, 3) Tunaweza kugawia walio kama “watoto wachanga” “lile neno,” ili wakue waufikie wokovu na kushikamana nao wakiwa Wakristo waliokomaa. Kwa hiyo wale wanaoonyesha nia ya kumpokea “mtoto mmoja wa namna hii kwa jina” la Kristo wanaonyesha kwamba wao wenyewe wana sifa za kitoto. Lazima wawe hivyo ili kuwa na ushirika katika Ufalme.​—⁠Mt. 18:2-4; Luka 18:16.

21. Kundi linafaidikaje kwa kuwa na unyenyekevu wa akili na wa nia, bila ya ugomvi na mashindano?

21 Kama vile inavyokuwa katika jamaa halisi ya kibinadamu, wakati washiriki wa kundi wanapokuwa wanyenyekevu kama watoto wadogo katika akili na nia, uhusiano wao unakuwa wenye amani. Wanajisikia wametulia na kustarehe vizuri akilini kwa sababu hawana mashindano ya kubomoana. Tukiwa na nia ya kufanya hata kazi zenye heshima ndogo sana, kwa kusudi la kutimizia watu mahitaji yao na kuwastarehesha, tunajenga kundi lote na kulitia nguvu na kuliongoza liwe na matendo mema.

22. Ni kitu gani tunachohitaji sana ili ‘kuendelea kukaa kwa amani sisi kwa sisi’?

22 Kwa njia hiyo hata mtu aliye mchanga zaidi, aliye nyuma zaidi katika ukweli wa Biblia na ujuzi wa Kikristo hasahauliwi. Kundi linafurahi kumkumbatia “kwa jina” la Kristo. Kundi likiwa na hali hiyo, roho ya Bwana Mungu Yehova inadumu. Nayo inahitajiwa sana ili kusaidia washiriki wa kundi ‘wakae kwa amani wao kwa wao.’ Ndivyo umoja unavyotokea kati ya ndugu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki