Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 6/1 kur. 253-259
  • Kutumikia kwa Umoja Kama Ushirika wa Ndugu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutumikia kwa Umoja Kama Ushirika wa Ndugu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUWA KAMA WATOTO WADOGO
  • HAKUNA KUIGA NJIA ZA ULIMWENGU
  • HAKUNA MTENGANO KUPITIA KWA VYEO VYA UKUU
  • “ZAWADI KATIKA WANAUME”
  • KUWA KAMA “ALIYE MCHANGA ZAIDI”
  • Vile Unyenyekevu Unavyoweza Kukulinda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Ukubwa wa Kikristo Hutokana na Kutumikia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Mkakae kwa Amani Ninyi kwa Ninyi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 6/1 kur. 253-259

Kutumikia kwa Umoja Kama Ushirika wa Ndugu

“Nyote m ndugu . . . msiitwe viongozi; maana Mmoja ndiye Kiongozi wenu, yaani, Kristo.”​—⁠Mt. 23:8-11, New American Standard Bible.

1, 2. (a) Ni nini kinachoonyesha watu wengi zaidi huona ni vigumu kuishi maisha ya utumishi wa unyenyekevu kama yale ya Mwana wa Mungu? (b) Je! mitume wa Yesu walifanya badiliko hilo bila ugumu?

WAZO la maisha ya utumishi wa unyenyekevu si jepesi kukubaliwa na kutumiwa na wanadamu wengi wasiokamilika. Angalia yaliyotukia katika Jumuiya ya Wakristo ambamo wanaume wenye kujidai kuwa wajumbe wa Kristo Yesu na watumishi walioamriwa (au “wahudumu”) wa Mungu wamejitofautisha na washiriki ‘wa kawaida’ wa kundi. Viongozi hao wa dini wanajiona kuwa wakubwa zaidi kuliko wale wengine waliomo kundini nao wanakubali vyeo vinavyoonyesha ukuu. Lakini hiyo siyo njia ya kuleta umoja wa kweli.

2 Hata kati ya wanafunzi wa kweli wa Yesu katika karne ya kwanza, haikuwa vyepesi kubadili nia ndiyo walikubali fundisho hilo la Mwana wa Mungu. Mara nyingi Yesu alilazimika kusahihisha wanafunzi wake kwa sababu walitaka sana vyeo vya ukuu.

3, 4. Wanafunzi wa Yesu walikuwa na mabishano gani walipokuwa wakielekea Kapernaumu, na kwa sababu gani jambo hili si la kushangaza?

3 Karibu na mwisho wa mwaka wa tatu wa utumishi wa hadhara wa Yesu, wanafunzi wake walianza kubishana walipokuwa wakitembea kurudi Kapernaumu. Walibishania nini? Masimulizi ya Marko yasema: “Wakati yeye [Yesu] alipokuwa ndani ya nyumba, akawauliza, ‘Mlikuwa mkibishania nini njiani?’ Wakanyamaza, kwa sababu njiani walikuwa wamekuwa wakizungumza habari za ni nani aliye mkubwa zaidi. Akaketi, akawaita wale Thenashara, akawaambia, ‘Ikiwa mtu ye yote ataka kuwa wa kwanza, lazima awe wa mwisho kati ya wote na awe mtumishi wa wote.”​—⁠Marko 9:33-35, New English Bible.

4 Je! inashangaza kwamba walifanya hivyo baada ya karibu miaka mitatu ya kufundisha kwa Yesu? Haishangazi tunapokumbuka kutokamilika kwao kwa kibinadamu na hali zao. Kutaka kwao kuwa wakubwa hakukuonyesha maelekeo ya mwili usiokamilika tu, bali pia kulionyesha hali ya maisha ilivyokuwa nyakati zao. Kitabu kimoja cha kihistoria kinachohusu desturi na nia zilizokuwa kati ya wafuasi wa karne ya kwanza wa dini ya Kiyahudi kinasema hivi: “Katika mambo yote, katika ibada, katika usimamizi wa hukumu, vyakulani, katika shughuli zote, sikuzote kulitokea ulizo juu ya aliye mkubwa zaidi, na sikuzote lilikuwa jambo la lazima na la maana sana kufikiria heshima aliyostahili kila mtu.”​—⁠Theological Dictionary of the New Testament, Vol. IV, ukurasa wa 532; linganisha Mathayo 23:6, 7.

KUWA KAMA WATOTO WADOGO

5. Yesu aliwapa shauri gani kusahihisha nia yao mbaya?

5 Masimulizi ya Mathayo juu ya kisa icho hicho yaonyesha kwamba Yesu aliita mtoto akamweka mbele ya wanafunzi akasema: “Nawaambieni hivi: msipogeuka na kuwa kama watoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa Mbinguni. Acheni mtu ajinyenyekeze hata awe kama mtoto huyu, naye atakuwa ndiye mkubwa zaidi katika ufalme wa Mbinguni. Ye yote apokeaye mtoto mmoja kama huyu kwa jina langu anipokea mimi. Lakini ikiwa mtu ni kikwazo kwa mmoja wa hawa wadogo walio na imani katika mimi, ingekuwa afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni pake na kuzamishwa katika vilindi vya bahari.”​—⁠Mt. 18:1-6, New English Bible.

6. (a) Pengine wengine wa wanafunzi wake walikuwa na maoni gani ya ukuu? (b) ‘Kugeuka na kuwa kama watoto’ kungekuwa na maana gani kwao?

6 Naam, Yesu aliwaonyesha kwamba kuwaza kwao kulikuwa kukiwaelekeza katika njia mbaya. Pengine Petro alidhani alikuwa na ukuu fulani juu ya wanafunzi wengine kwa sababu Yesu alimwahidi kumpa “funguo” fulani za kuelekeza kwenye ufalme. Au pengine Yakobo na Yohana walikuwa na mawazo kama hayo kwa sababu walikuwa kati ya wale watatu ambao Yesu alichagua wawe pamoja naye wakati wa kugeuka sura mlimani. (Mt. 16:19; 17:1-9) Vyo vyote iwavyo, Yesu aliwaambia, wote ‘wageuke na kuwa kama watoto,’ yaani, wawe wanyenyekevu, bila kujifanya wala kujitakia makuu kama vile watoto wasivyojitakia makuu kwa asili. Hawakupaswa kujifanya tu kuwa watoto kwa kuonyesha sifa hizo nje-nje, bali walipaswa kuzivaa sifa hizo, ili wawe hasa na roho ile ile inayoonyesha watoto ni wanyenyekevu. Watoto wadogo hawabaguani juu ya aliye mkubwa bali huonana kuwa sawa. Kwa hiyo, kwa kadiri ambavyo wanafunzi wa Yesu wangevaa unyenyekevu wa moyo, kwa kadiri ambavyo wangejiona kuwa wadogo mbele za Mungu na ndugu zao, kwa kadiri hiyo wangekuwa wakubwa katika ufalme wake.

7. Njia yao ya ‘kupokea wadogo’ ingeonyeshaje kadiri ya unyenyekevu wao, na ni nini kilichofanya jambo hilo liwe zito sana?

7 Wangeonyesha kadiri ya unyenyekevu wao kwa njia ambayo wangetendea wale waliokuwa kama ‘watoto wachanga’ kiroho katika kweli (kwa sababu ya kuwa wanafunzi karibuni), au wale waliokuwa kama watoto wadogo kwa kutokuwa na ukubwa au cheo cha madaraka kati yao. Kama mtu fulani, hasa mzee wa Kikristo, angejionyesha kuwa mashuhuri (wa maana) au kupigia wengine ubwana, angeweza kuwa kikwazo kwa wanyenyekevu hao. Hiyo ingeweza kuwa na matokeo mabaya sana kwa mwenye kukwaza, kama yaonyeshavyo maneno ya Yesu. Yeye angekuwa akitazama yenye kutendeka; na malaika wa Mungu pia wangekuwa wakitazama.​—⁠Mt 18:6, 10; Ufu. 2:23.

8. Ni kwa njia gani ilivyo kweli kwamba “yeye ajiongozaye kama mdogo zaidi” ndiye mkubwa kati ya Wakristo?

8 “Yeye ajiongozaye kama mdogo zaidi [mdogo zaidi kuliko wote, NE; aliye chini zaidi kuliko wote, New American Bible, maelezo ya pembeni] kati yenu nyote ndiye mkubwa.” (Luka 9:48, NW) Ingawa hilo lilikuwa tofauti sana na mawazo ya ulimwengu, je! hatulioni kuwa jambo la kweli katika uhusiano wetu na wengine? Ni nani aliye bora zaidi kwetu, ambaye tungehuzunikia zaidi akituacha au kufa​—⁠ mwenye kujionyesha kuwa mashuhuri na kutaka wengine wamheshimu, au mwenye kuhurumia wengine sana, mwenye kuwasaidia na mwenye fadhili? Kwa wazi ni huyu wa pili.

9. (a) Ni kwa njia zipi mtume Paulo aliweka mfano wa kanuni hii ya Kikristo? (b) Akina ndugu walionyeshaje wazi kwamba Paulo alikuwa mpendwa sana kwao, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na hili?

9 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, mtume Paulo aliiga mfano wa Yesu mwenyewe wa utumishi wa unyenyekevu. (1 Kor. 11:1) Akisema na wazee wa mji wa Efeso, Paulo angeweza kuwaambia hivi kwa ukweli: “Ninyi mwajua jinsi, tangu siku nilipokanyaga kwanza jimbo la Asia, kwa wakati wote nilipokuwa pamoja nanyi, nilimtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote kati ya huzuni nyingi na majaribu yaliyonijia . . . Kumbukeni jinsi kwa miaka mitatu, usiku na mchana, nisivyoacha kamwe kushauri kila mmoja wenu, na jinsi nilivyowalilia. . . . nyote mwajua kwamba mikono hii yangu ilichuma vya kutosha mahitaji yangu mwenyewe na wenzi wangu. Niliwaonyesha kwamba ni wajibu wetu kuwasaidia wanyonge kwa njia hii, kwa kazi ngumu, na kwamba imetupasa kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, ambaye mwenyewe alisema, ‘Furaha inategemea zaidi kutoa kuliko kupokea.” Si ajabu kwamba walipojua huenda wasimwone Paulo tena, “kukawa na vilio vikubwa vya huzuni kutoka kwa wote” na pia walimkumbatia wakambusu. Yeye alikuwa mpendwa sana kwao, si kwa sababu ya kuwa kwake mtume tu, bali kwa sababu ya aina ya utu aliokuwa nao. Alikuwa mfano kwa wazee wote wa Kikristo.​—⁠ Matendo 20:18, 19, 31-37, NE; linganisha 1 Wakorintho 2:1-5; 1 Wathesalonike 2:5-9.

HAKUNA KUIGA NJIA ZA ULIMWENGU

10. Ni wakati gani wa pili uliofanya Yesu awape tena wanafunzi wake shauri la kuwa na unyenyekevu?

10 Miezi michache baada ya kubishana kwa wanafunzi juu ya ukubwa, Yesu aliona tena ni lazima kuwashauri. Wanafunzi wake walidhani ufalme wake ulikuwa utawala wa kidunia. (Matendo 1:6) Walijua kwamba chini ya utawala mkuu wa Kiisraeli, wafalme walikalia viti vya enzi nao walikuwa na watumishi wenye vyeo mbalimbali barazani kwao. Siku zao waliona huku na huko watawala wa kilimwengu na wanaume wengine wenye kutumia mamlaka juu ya watu. Kwa hiyo, wawili wa mitume wa Yesu, Yakobo na Yohana (wakiwa pamoja na mama yao na wakiongozwa naye), walimwomba Yesu awape vyeo ‘vya juu-juu’ katika ufalme wake.​—⁠Mt. 20:20-23; Marko 10:35-40.

11. Je! mitume wale wengine walikuwa bila lawama katika jambo hili, naye Yesu aliwapa shauri gani?

11 Wanafunzi wenzao ‘waliudhika.’ Lakini mabishano yao ya hapo kwanza juu ya ukubwa yalionyesha kwamba wao wenyewe pia walikuwa wakijitakia makuu. Kwa hiyo Yesu akawaita wote akawaambia: “Mwajua kwamba katika ulimwengu, watawala hupiga ubwana juu ya raia zao, na wakuu wao huwalemeza ndiyo waone uzito wa mamlaka [hufanya ubora wao uonwe, New American Bible]; lakini sivyo itakavyokuwa kwenu. Kati yenu, ye yote atakaye kuwa mkubwa lazima awe mtumishi wenu na ye yote atakaye kuwa wa kwanza lazima awe mtumwa mwenye nia wa wote​—⁠kama Mwana wa Adamu; yeye hakuja kutumikiwa, bali kutumikia, na kuacha uhai wake kama ukombozi kwa wengi.”​—⁠Mt. 20:24-28, NE.

12, 13. (a) Kwa sababu gani haitupasi kuingiza katika kundi la Kikristo njia za kilimwengu za kusimamia mambo zinazoelekea kuwa na mafanikio? (b) Shauri la mtume katika Warumi 12:2, 3, 10, 16 linapatanaje na shauri la Yesu?

12 Naam, huenda likaonekana kuwa jambo la kawaida kuiga njia za watawala wa kilimwengu, wenye amri na wasimamizi. Lakini Yesu alisema: “Sivyo itakavyokuwa kwenu.” Hata wenye nguvu na matajiri wa ulimwengu pamoja na taratibu zao za kisiasa na za kibiashara waelekee kufanikiwa namna gani, sio waliopaswa kuwa mfano wa kuongoza kundi la Kikristo.

13 Shauri la baadaye la mtume Paulo linapatana na habari hiyo: “Msijifuatishe mwenendo wa ulimwengu unaowazunguka, lakini acheni mwenendo wenu ubadilike, ufanyizwe na akili yenu mpya.” Kwa wazi Paulo alikuwa akifikiria ugumu ule ule ambao Yesu alitolea shauri, maana aliendelea kusema hivi: “Nataka kusihi kila mmoja kati yenu asipige chuku juu ya ubora wake halisi. Lazima kila mmoja wenu aamue mwenyewe alivyo kwa utimamu kulingana na kanuni ya imani ambayo Mungu amempa. Pendaneni kwa kadiri iwapasavyo ndugu, na kuheshimiana sana. Tendeeni kila mtu kwa fadhili zinazolingana; msiwe kamwe mkionyesha wengine unyenyekevu wa uongo [enendeni na watu wanyenyekevu, NE; shirikianeni na wenye hali ya chini, New American Standard Bible; ambatanishweni na vitu vya chini chini, NW] . Msijiache mjikinai [msiendelee kuwaza jinsi mlivyo wenye hekima, NE].”​—⁠Rum. 12:2, 3, 10, 16, Jerusalem Bible.

14. (a) Ni mambo gani yaliyofanya iwapase sana mitume wa Yesu kujifunza sana somo alilokuwa akiwafundisha? (b) Takwa la ‘kutoshikilia kauli ya mtu tu’ linasaidiaje kuleta umoja kati ya wazee?

14 Kwa kuwa mitume wa Yesu, wakiwa baraza, ndio wangekuwa msingi wa kundi la Kikristo likianzishwa, lilikuwa jambo la maana zaidi kwao kujifunza sana somo alilowafundisha. (Efe. 2:19, 20) Ni kwa kufutilia mbali tu mawazo ya ukuu wa cheo kati yao wenyewe wangeweza kutenda kama baraza yenye umoja, bila ugomvi wala ushindani. (Linganisha Warumi 12:4-8, 10; 1 Wakorintho 12:4-7, 12-25, 31; 13:1-3.) Hiyo ndiyo sababu pia mojawapo ya sifa za wenye kutumikia katika baraza za wazee za makundi ni kwamba wasiwe ‘wenye kushikilia kauli yao tu.’ (Tito 1:7, NW) Neno la Kigiriki hapa lamaanisha kwa halisi, “mwenye kujipendeza mwenyewe” (“mwenye kujitanguliza,” Moffatt; “mwenye kiburi,” Revised Standard Version; AT; JB; “mgumu,” NE; “mwenye kutaka ugomvi,” Phillips; “mwenye kujidaia haki,” The Expositor’s Greek Testament). Kwa hiyo, sifa inayotajwa na mtume inahitaji mzee asiwe ‘mwenye kinaya’ wala “mwenye kujitegemea” kwa sababu ya kujifikiria sana kuwa mwenye uwezo mwingi na akili ya kuamua mambo. Mtu mwenye kushikilia kauli yake tu angeona ni vigumu kufanya kazi na wengine kama baraza kwa mapatano na unyenyekevu. Naye angekuwa mwenye kutatiza wenzake katika baraza hiyo.

15. Maneno yaliyoongozwa na Mungu yaliyomo katika Yakobo 3:13 yatasaidiaje wazee waache kujiona wakubwa na kujitegemea?

15 Mzee wa Kikristo akianza kujiona mkubwa kuliko wazee wenzake kwa sababu ya hekima, ingefaa atafakari juu ya aliyoandika mwanafunzi Yakobo katika Yakobo 3:13: “N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole [adabu, NE; unyenyekevu, AT] wa hekima.” Naam, mtu mwenye hekima ya kweli ni yule ajuaye mambo ya kutosha kuweza kujua kwamba​—⁠hata awe na ujuzi na maarifa kadiri gani​—⁠bado hajui mengi na kwamba ana mengi sana ya kujifunza. Yeye ajua pia kwamba​—⁠hata awe anajua mengi namna gani​—⁠hakuna mtu asiyeweza kumfunza jambo, hata mtu huyo awe nani au awe mwenye cheo cha chini namna gani. Yeye awatendea wote hao kwa heshima istahiliyo.

HAKUNA MTENGANO KUPITIA KWA VYEO VYA UKUU

16. Cheo “Rabi” kina maana gani, na kwa sababu gani hakikupaswa kutumiwa kwa ye yote wa wanafunzi wa Yesu?

16 Siku tatu tu kabla ya kufa kwake, Yesu alionya wanafunzi wake wasiwaige waandishi na Mafarisayo katika kupenda umashuhuri. Wanaume hao mara nyingi waliitwa “Rabi” na wengine, neno linalomaanisha kwa halisi, “aliye mkuu.” Lilikuwa “neno la mtu mwenye cheo cha juu na chenye kuheshimiwa. . . . Mwenye kuitwa Rabi anatambuliwa kwa sababu hiyo kuwa mwenye cheo cha juu zaidi kuliko mwenye kumwita hivyo.” (Theological Dictionary of the New Testament, Vol. VI, ukurasa wa 961) Walakini, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Msiitwe Rabi; kwa maana Mmoja ndiye Mwalimu wenu, na ninyi nyote m ndugu. . . . Wala msiitwe viongozi; maana Mmoja ndiye Kiongozi wenu, yaani, Kristo. Lakini aliye mkubwa zaidi kati yenu atakuwa mtumishi wenu.” (Mt. 23:6-12, New American Standard Bible) Kwa kufaa, Yesu aliacha aitwe “Rabi.”​—⁠Yohana 1:38, 49; 20:16; Mt. 26:49; Marko 9:5.

17. Majina ya Maandiko kwa wale waliogawiwa madaraka ndani ya kundi yanatia mkazo juu ya nini? (b) Ni kwa njia gani ndivyo ilivyo kwa jina “mtume,” na sababu gani wenye kuitwa hivyo hawakuwa sababu ya kujiona kuwa wakubwa kuliko ndugu zao?

17 Inastahili kuangaliwa kwamba, katika majina yote ya migawo ndani ya kundi la Kikristo baada ya kuanzishwa kwake katika Pentekoste​—⁠majina kama “mchungaji,” “mwalimu,” “mweneza injili,” na “nabii” (kwa halisi, mwenye kunena [Matendo 15:32])​—⁠mkazo zaidi u juu ya kusudi hasa la Kristo la kutoa hizi ‘zawadi katika wanaume,’ yaani, kujengwa na kuunganishwa kwa kundi, kuliko ulivyo juu ya cheo rasmi cha “zawadi” hizo za kibinadamu. (Efe. 4:12-16) Hata neno “mtume” lamaanisha “mwenye kutumwa,” yaani, mtu aliyetumwa kama mjumbe juu ya agizo la utumishi. Ingawa neno hilo lilitumiwa kwa njia ya pekee kwa mitume kumi na wawili waliowekwa moja kwa moja na Mwana wa Mungu, lilitumiwa kwa wanaume wengine pia waliotumwa wakatimize maagizo fulani ya utumishi, nyakati nyingine wakiwa wametumwa na makundi. (Linganisha Matendo 13:1-4; 14:14; 2 Wakorintho 8:23.) Kwa hiyo, jina “mtume” lilikazia mgawo wao wa utumishi badala ya kukazia cheo au daraja. Ni kweli kwamba lilimaanisha walikuwa watu wa kutumainiwa. Lakini halikuwakuza ‘wenye kutumwa’ wakawa wakubwa kuliko wale ambao wangetumikia, kama vile mtumishi asivyokuwa mkubwa zaidi kuliko mwenye kupokea ujumbe alio nao kutoka kwa bwana wake. Walakini, mpokeaji angekuwa mwenye wajibu kwa mwenye kumpelekea ujumbe. Pia, wenye kutumwa walikuwa na wajibu kwa wenye kuwatuma, wawe ni baraza ya wazee Yerusalemu au baraza ya kundi jingine lo lote. Walitoa ripoti ya walivyofanya. (Linganisha Yohana 13:16; Waefeso 6:21, 22; Wakolosai 1:7; 4:7-9.) ‘Wenye kutumwa’ kwa muda bila shaka hawakuendelea kuwa “mitume” maisha yao yote kama wale mitume kumi na wawili wa Kristo pamoja na Paulo.​—⁠Ufu. 21:14; Efe. 2:20, 21.

“ZAWADI KATIKA WANAUME”

18. Ni zawadi gani ambazo Kristo Yesu aliyetukuzwa alilipa kundi la Kikristo, na kwa kusudi gani?

18 Hata wawe walifanya utumishi gani, wanaume hao wote walipewa kwa kundi la Kikristo na Kristo Yesu kama ‘zawadi katika wanaume’ baada ya kupaa kwake akaonekane mbele za Baba yake mbinguni. (Efe. 4:8) Waefeso 4:11-13 (NE) yaonyesha kusudi la hilo, ikisema: “Na hizi ndizo zilizokuwa zawadi zake: wengine wawe mitume, wengine manabii, wengine waeneza injili, wengine mapasta [wachungaji] na waalimu, kutayarisha watu wa Mungu kwa kazi katika utumishi wake [ili watakatifu wote pamoja wawe umoja katika kazi ya utumishi, Jerusalem Bible], wakaujenge mwili wa Kristo. Ili mwishowe sote tuufikie umoja ambao asili yake ni imani yetu na kumjua kwetu Mwana wa Mungu​—⁠hata tufikie utu uliokomaa, usiopimwa na cho chote kinachopungua kimo kamili cha Kristo.”

19, 20. (a) Wanaume ‘waliopewa’ kwa njia hiyo wamepaswa wajaribuje kutimiza mradi wao? (b) Mtume Paulo anaonyeshaje wazi nia inayofaa kuendelezwa na hao?

19 Mradi wa wote hao walio “zawadi katika wanaume” ulipaswa kuwa utumishi wenye umoja kwa Mungu na Mwanawe. Wangefikia mradi huu, si kwa ‘kufanya ubora wao uonwe,’ kwa kutumia nguvu, bali kwa kuweka mfano wa utumishi wa unyenyekevu, wakijitoa kwa faida ya wote. Kwa hiyo, badala ya waliomo kundini kusema, “‘Mimi ni mtu wa Paulo’, au ‘Mimi ni wa Apolo’; ‘Mimi namfuata Kefa’, au ‘Mimi ni wa Kristo,”’ kama wengine Korintho walivyokuwa wakisema, nia iliyofaa kuwa nayo ilikaziwa na mtume Paulo alipowaambia ndugu wa huko hivi: “Kila kitu ni mali yenu ninyi​—⁠Paulo, Apolo, na Kefa, ulimwengu, uzima, na kifo, wakati wa sasa na wakati ujao, vyote hivyo ni mali yenu ninyi​—⁠lakini ninyi ni mali ya Kristo, na Kristo ni mali ya Mungu.”​—1 Kor. 1:12; 3:21-23, NE.

20 Naam, ijapokuwa Paulo alifanya utumishi wa ajabu, alikumbuka kwamba yeye pia alikuwa mojawapo ya “zawadi katika wanaume,” na kwamba yeye alikuwa kwa sababu hiyo “mali” ya kundi wala si kundi lililokuwa mali yake. (Linganisha 2 Wakorintho 1:24.) Kwa hakika mtumishi ye yote wa Mungu akijichukua kwa njia hiyo hawezi kutenda kama “bwana-mkubwa” juu ya ndugu zake, hata awe anafanya utumishi wa namna gani.

KUWA KAMA “ALIYE MCHANGA ZAIDI”

21. (a) Ni wakati gani na kwa sababu gani Yesu aliona ni lazima awashauri tena wanafunzi wake juu ya uhitaji wa kuwa na unyenyekevu? (b) Wakati huu alisema mambo gani zaidi?

21 Inaweza kuonekana kadiri tamaa ya ukuu ilivyotia mizizi katika wanadamu kutokana na uhakika wa kwamba, usiku wa mwisho wa maisha ya kidunia ya Yesu, yeye aliona ni lazima kurudia kutaja kanuni hizi kwa mitume wake. Usiku uo huo wanaume hao walianza mabishano makali juu ya ‘anayepaswa kuwa na daraja la juu zaidi’ kati yao. Akirudia na kuongezea aliyokuwa amewaambia hapo kwanza, Yesu alisema hivi: “Katika ulimwengu, wafalme hupiga ubwana juu ya raia zao; na wale walio na mamlaka huitwa ‘Wafadhili’ wa nchi yao. Sivyo itakavyokuwa kwenu: bali, aliye juu zaidi ya wote kati yenu lazima ajichukue kama aliye mchanga zaidi [mdogo, New American Bible] mkuu wenu kama mtumishi. Kwa maana ni nani mkubwa zaidi​—⁠yeye aketiye mezani au mtumishi mwenye kumtumikia? Kwa hakika ni yeye aketiye mezani. Lakini mimi hapa kati yenu nikiwa kama mtumishi.”​—⁠Luka 22:24-27, NE; linganisha 2 Petro 1:12-15.

22. Maana yake nini kujiongoza kama “aliye mchanga zaidi,” na hii inaonyeshwaje katika masimulizi ya Maandiko?

22 Maana yake nini kujichukua kama “aliye mchanga zaidi” au “mdogo”? Mara nyingi wanaume vijana waligawiwa kazi zisizo za ukubwa sana, ingawa zilikuwa za lazima. Kwa mfano, wakati Anania na mkewe walipouawa na Mungu, “vijana” ndio waliowachukua wakawazika. (Matendo 5:5, 6, 10) Baada ya kusihi wazee wenzake watumikie kama mifano ya unyenyekevu kwa kundi, mtume Petro alisema hivi: “Vivyo hivyo, enyi wanaume vijana, jitiisheni kwa wanaume wazee.” (1 Pet. 5:1-5, NW) Timotheo, aliyekuwa kijana sana akilinganishwa na mtume Paulo, anatajwa kuwa kati ya wale wenye kumtumikia Paulo kama “wasaidizi” wake au wenye ‘kumtumikia.’ (Matendo 19:22, NE; AT; JB; NW) Onesimo, yule mtumwa mtoro, ambaye Paulo mzee alimwita “mtoto wangu,” alikuwa ‘amemtunza au kumtumikia Paulo,’ ‘akimhudumia’ kama vile mwana afanyiavyo baba, wakati Paulo alipokuwa gerezani. (Flm. 9, 10, 13, NE; AT; NW; linganisha 2 Timotheo 1:16-18.) Kwa kufanya kazi kwa unyenyekevu pamoja na watumishi hawa wa Mungu wazee na wenye ujuzi, wanaume vijana walipata faida nyingi na mazoezi mengi.

23. Je! vijana ndio wanaopaswa kuonyesha unyenyekevu wa akili peke yao?

23 Ia akingawa huenda ikawa kazi zao zilionekana kuwa zisizo za heshima na fahari sana, mwendo wao unaonyesha nia inayofaa wote wawe nayo, hata wawe na umri gani. Kwa hiyo mtume Petro aendelea kusema hivi, baada ya kuwashauri wanaume vijana wanyenyekee wazee wao: “Lakini ninyi nyote jifungeni unyenyekevu wa akili kuelekeana, kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi [wenye kuonekana kuwa wakuu, Int], lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahilika.”​—1 Pet. 5:5, NW.

24. Ni faida gani kuu zinazotokana na mwendo huu, na hii inasaidiaje sana kuleta umoja wa Kikristo?

24 Inapendeza namna gani kutumikia pamoja wakati mnamokuwa na roho ya unyenyekevu kundini! Jinsi roho ya udugu inavyosaidia wakati wazee wa Kikristo wanapofanya kazi pamoja kama baraza kwa njia inayofaa, wakiondoa maelekeo ya mateto au ubishi mkali wenye kupoteza wakati! (1 Tim. 2:8) Kwa hakika hapa sote tuna mengi ya kutafakari. Je! tunatafuta ukubwa wa kweli unaotokana na utumishi huo wa unyenyekevu wenye kuongozwa na upendo wa kidugu? Acheni kila mmoja wetu aonyeshe hivyo kwa kusaidia, kuhurumia na kupendezwa na wote, kutia na walio na hali ya chini, tukiwapa wote heshima na ustahili wa kipekee. (Rum. 12:10, 15, 16) Kwa njia hiyo tutajihakikisha kuwa wanafunzi wa kweli wa Yeye apitaye wote katika utumishi, Mwana wa Mungu, Kristo Yesu.​—⁠Kutoka The Watchtower, Dec. 1, 1975.

[Picha katika ukurasa wa 254]

Ili kufundisha wanafunzi wake wawe na unyenyekevu, Yesu aliwaambia wawe kama watoto

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki