Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 6/1 kur. 246-253
  • Ukubwa wa Kikristo Hutokana na Kutumikia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukubwa wa Kikristo Hutokana na Kutumikia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTUMIKIA NA KUTUNZA WENGINE
  • KUTUMIKIA NDUGU WENYE SHIDA
  • UTUMISHI WA MAANA HATA ZAIDI
  • HAKUNA NAFASI YA NIA YA KUJIONA MKUBWA
  • Kutumikia kwa Umoja Kama Ushirika wa Ndugu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Kuona Ubora wa Hazina ya Utumishi Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Wewe Unaweza Kuuingia Mlango Uliofunguka?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 6/1 kur. 246-253

Ukubwa wa Kikristo Hutokana na Kutumikia

“Mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu.”​—⁠Mt. 20:26.

1. Ni kwa njia gani maisha ya Yesu yanatofautiana na ya watu wengi sana leo?

UKRISTO wa kweli unategemea kutumikia. Wakati Mwana wa Mungu alipokuwa duniani alisema kwamba, hakuja “kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28) Maisha yake yalikuwa tofauti sana na nia ya watu wengi sana leo wanaojitafutia faida zao wenyewe tu na kujitakia makuu bila kuona shida za wengine. Yesu aliwekea wafuasi wake wote wa kweli kielelezo bora cha kufuata kwa kuishi maisha ya kutumikia bila kufikiria faida zake mwenyewe tu. Maisha zao zimepaswa kutofautishwa na utumishi na roho ya kutoa, kama yake.

2, 3. (a) Pana tofauti gani juu ya neno la ‘kutumikia’ lililotumiwa katika Mathayo 20:28 na maneno mengine ya Kigiriki yanayohusu utumishi? (b) Sasa tunapendezwa na kujua nini?

2 Neno lililotafsiriwa ‘kutumikia’ ambalo mwandikaji wa Biblia Mathayo alitumia alipokuwa akitaja maneno ya Yesu linafaa tulifikirie. Katika Kigiriki cha asili ni kiarifa (au verb) di·a·ko·neʹo. Viko viarifa vingine vya Kigiriki vinavyomaanisha utumishi na kila kimoja kina namna yake chenyewe ya kutia mkazo juu ya sehemu fulani ya utumishi. Huenda kiarifa kimoja kikakazia unyenyekevu unaohusika katika kutumikia kama mtumwa (dou·leuʹo; Kol. 3:24), kingine kukazia utakatifu wa utumishi wa kidini (la·treuʹo; Mt. 4:10), na kingine kukazia utumishi unaotolewa hadharani ya watu (lei·tour·geʹo; Matendo 13:2, NW). Kwa upande mwingine, Di·a·ko·neʹo linakazia utumishi wa mtu bi nafsi kwa mtu mwingine. Kama vile ushuhuda mmoja usemavyo, kiarifa hicho ‘kinaelekea zaidi wazo la utumishi wa upendo.’​—⁠Theological Dictionary of the New Testament, Vol. 11, ukurasa 81.

3 Basi, ni mambo gani yanayotiwa ndani ya utumishi wa Kikristo? Je! yanayotiwa ndani ni kuhubiri Neno la Mungu, kufanya wanafunzi au kutumikia mahitaji ya kiroho ya waliomo kundini tu? Neno tunalolizungumza (di·a·ko·neʹo) laonyesha nini?

KUTUMIKIA NA KUTUNZA WENGINE

4. Kwa kufaa Biblia inaonyeshaje maana ya msingi ya neno la Kigiriki ‘kutumikia’ tunalozungumza?

4 Wakati Biblia inapolitumia neno inaonyesha kwa kufaa maana ya msingi ya utumishi wa mtu bi nafsi (unaotajwa si na kiarifa cha Kigiriki tu bali pia na majina yanayohusiana nacho di·aʹkonos [mtumishi, mhudumu] na di·a·ko·niʹa [utumishi, huduma]).a Matumizi mamoja ya mwanzoni mwanzoni ya neno hilo yanamaanisha ‘kutumikia mezani.’ Luka analitumia hivyo anapotaja maneno ya Yesu juu ya ‘kutayarisha kwa mtumwa chakula cha bwana wake cha jioni kisha kumtumikia [di·a·ko·neʹo] alapo chakula chake.’ (Luka 17:7-10, NE) Katika Luka 12:35-38 (NE) Yesu aliwapa wanafunzi wake mfano ambamo bwana, akifananisha Yesu mwenyewe, alibadilishana madaraka na watumwa wake waliokuwa wamengoja kwa uaminifu afike kutoka kwenye karamu yake ya arusi. Yesu alisema hivi juu ya bwana aliyemo katika mfano: “Atajifunga mshipi wake, awaketishe mezani, aje na kuwatumikia [di·a·ko·neʹo; kuwahudumia, New World Translation].”b

5, 6. (a) Ni Kwa njia gani wanawake fulani wa Kikristo walifanya utumishi wa namna hii? (b) Haya yote yanaonyesha nini juu ya yanayotiwa ndani katika neno la Biblia tunalolizungumza?

5 Walakini, si ‘kutumikia mezani’ tu kulikotiwa ndani ya neno hilo, bali utumishi wote wa mtu bi nafsi ulitiwa ndani. Biblia inaeleza habari za wanawake fulani wa Kikristo ‘waliotimiza,’ ‘waliotumikia’ au ‘waliohudmia’ mahitaji ya Yesu na mitume wake “kutokana na mali zao,” katika Galilaya na Yerusalemu pia. (Luka 8:1-3; Mt. 27:55; Marko 15:41; NE, NW) Pengine walikuwa wakienda madukani na kupika, kushona viraka na kufua nguo, au pengine walifanya kazi nyingine kama hizo, hata kutumia pesa na mali zao wenyewe ili kutoa vifaa vilivyohitajiwa.

6 Kwa hiyo, twaona kwamba neno hilo halihusu utendaji ‘wa kidini’ tu bali latia ndani utumishi wa namna nyingi.

KUTUMIKIA NDUGU WENYE SHIDA

7. Ni kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo wanauthamini sana utumishi wa namna hii, bila ya sisi kuudharau?

7 Hatupaswi kamwe kuwa na shaka kama Yehova Mungu na Mwanawe Yesu Kristo wanauthamini sana utumishi wa namna hii. Yesu mwenyewe alipatwa na shida za kibinadamu kama njaa na kiu. Bila shaka alifurahi sana wakati walipokuja “malaika wakamtumikia [di·a·ko·neʹo]” baada ya kufunga kula kwa siku 40. (Mt. 4:11) Katika mfano alioutoa karibu na mwisho wa utumishi wake wa kidunia, Yesu alisimulia hukumu yake juu ya jamii mbili za watu, jamii moja ikifananishwa na “kondoo,” na ile nyingine na “mbuzi.” “Kondoo,” ambao walikubaliwa na kubarikiwa, walikuja kusaidia ndugu za Kristo walipowaona wakiwa na shida. Lakini “mbuzi,” waliolaaniwa, waliwaona wakiwa na njaa na kiu, wakihitaji kukaribishwa na kupewa mahali pa kulala, wakiwa bila mavazi au wakiwa wagonjwa au wakiwa gerezani nao ‘hawakuja kuwasaidia [di·a·ko·neʹo; ‘hawakuwatumikia’ au ‘kuwahudumia,’ Int; NW] .’​—⁠Mt. 25:31-46, Jerusalem Bible.

8, 9. (a) Ni kwa njia gani Wakristo katika karne ya kwanza walionyesha kwamba walifahamu sana ubora wa kutumikia mahitaji ya kimwili ya ndugu zao? (b) Ni kwa njia gani mtume Paulo alionyesha alitaka sana “utumishi” huu ufanywe kwa njia inayofaa?

8 Wanafunzi wa kweli wa Yesu walijihakikisha kuwa ‘wenye mfano wa kondoo’ wakati wa karne ya kwanza kwa nia na matendo yao. Wakati Wakristo wa Makedonia na Akaya walipopata habari kwamba ndugu zao Uyahudi wana shida, walikusanya vitu vya kuwasaidia wakawapelekea, hivyo wakafanya “huduma ya kuondolea taabu [di·a·ko·niʹa].” (Matendo 11:29; 12:25, NW) Hiyo ni kwa sababu walijua kwamba ndugu wa Uyahudi walikuwa wamewafanyia utumishi bora sana wa kiroho na kwamba wao walikuwa na ‘deni’ ya kulingana na utumishi huo hata ikawafaa ‘wawafanyie utumishi wa vitu vya kimwili’ (An American Translation); ‘kuwahudumia hadharani kwa vitu vya mwili wa nyama’ (NW). (Rum. 15:25-27) Hilo lilikuwa jambo la kusifika sana kwa upande wa makundi ya Makedonia. Ingawa wao wenyewe walikuwa katika hali ya umaskini, walikuwa “wenye mikono iliyokunjuka.” Kama asemavyo Paulo: “Kama mimi niwezavyo kushuhudia, wao walitumia kiasi chote cha mali zao na hata zaidi ya kiasi hicho, wakatuomba-omba sana, kwa hiari yao wenyewe, waruhusiwe kushiriki katika utumishi [di·a·ko·niʹa; kuwahudumia, UV] huu wa ukarimu kwa Wakristo wenzao.” (2 Kor. 8:2-4, NE) Lo! huo ni mfano bora namna gani kwetu leo wa kutumikia bila kufikiria faida zetu wenyewe tu!

9 Mtume Paulo alitaka sana kuona msaada huo wa kuondolea shida ukigawanywa vizuri, ili kusiwe na “lawama juu ya kusimamia kwetu [di·a·ko·niʹa;] zawadi hii ya ukarimu” kutoka kwa wenye kuitoa au kutoka kwa wenye kuipokea. Kwa hiyo, wengine, “wajumbe wa makundi yetu,” ‘wakawekwa kwa kufaa wasafiri’ na Paulo na Tito (ambaye Paulo alimwita “mwenzi wangu na mshirika wangu”)​—2 Kor. 8:19-23, NE.

10. Ni matokeo gani mema yanayotokana na kutumikia hivyo bila choyo mahitaji ya wengine, kama inavyoonyeshwa na 2 Wakorintho 9:1, 11-14?

10 Baadaye Paulo mwenyewe aliburudika aliposaidiwa na wanaume kama Onesimo kwa ‘kumtumikia’ na kumtunza’ (di·a·ko·neʹo) nyakati za majaribu. (2 Tim. 1:16-18; Flm. 10-13, NE) Alipokuwa akiwaandikia Wakorintho, aliwaonyesha jinsi utumishi wa namna hiyo usio wa choyo unavyokuwa na matokeo mazuri na kumletea Mungu sifa na kuendeleza habari njema. Kwa habari ya “kuwahudumia” ndugu wa Uyahudi, alisema hivi: “Maana utumishi wa huduma hii hauwatimizii watakatifu riziki walizopungukiwa tu, bali huzidi sana kuwa na faida kwa shukrani nyingi apewazo Mungu; kwa kuwa mkijaribiwa kwa utumishi huo, wanamtukuza Mungu kwa ajili ya utii wenu katika kuikiri Injili ya Kristo, na kwa ajili ya ukarimu wenu mliowashirikisha wao na watu wote. Nao wenyewe, wakiomba dua kwa ajili yenu, wawaonea shauku kwa sababu ya neema ya Mungu iliyozidi sana ndani yenu.”​—2 Kor. 9:1, 11-14.

11. (a) Ni kwa njia zipi kufikiria kwetu mahitaji ya kimwili ya wengine kunasaidia kupanua ibada safi? (b) Ni nini mojawapo ya njia tunavyoweza kuonyesha ‘pendo kwa jina la Mungu,’ kulingana na Waebrania 6:10?

11 Naam, habari njema za ufalme wa Mungu huwa za maana kwa watu wakati waonapo matokeo yazo juu ya nyutu za wenye kuzitangaza, wakati waonapo zikiwafanya wenye kuzitangaza waonyeshe ukarimu na upendo kwa jirani zao. Utumishi huo wa kufikiria wengine na kuwapa vitu ‘humpa Mungu shukrani nyingi’ licha ya kufanya wapokeaji washukuru wapaji wa kibinadamu. Hupendekeza Ukristo wa kweli kama njia bora ya maisha, kama ibada ya kweli ya Mungu mfadhili na mwenye upendo. (Linganisha Yakobo 1:26, 27; 2:14-17; 1 Yohana 3:16-18) Ndiyo sababu Paulo angeweza kuandikia Wakristo Waebrania waliokuja kusaidia ndugu zao na kuwahakikishia kwamba “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia [di·a·ko·neʹo;] watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.”​—⁠Ebr. 6:10; linganisha 10:32-34; 1 Wakorintho 16:15, 16.

12, 13. (a) Ni kwa njia gani serikali za kilimwengu zinaweza kusimuliwa kuwa “watumishi” wa Mungu? (b) Pana tofauti gani kati ya utumishi wao na ule unaotolewa na wanafunzi wa Yesu?

12 Kwa sababu maneno hayo ya Kigiriki ya kutumikia yalipanuliwa yatie ndani aina zote za utumishi wa mtu bi nafsi, si ‘kutumikia mezani’ tu, yanaweza kutumiwa hata kwa serikali za kilimwengu. Kwa hiyo “mamlaka zilizo kuu” za taratibu iliyopo ya mambo zinaitwa “watumishi” wa Mungu kwa maana ya pekee. Katika Warumi 13:4 (An American Translation) mtume mwenye kuongozwa na Mungu asema hivi juu ya wakuu hao wa serikali: “Wao ni mawakili wa Mungu [di·aʹkonos ni mtumishi wa Mungu, UV] kukufaidi wewe. Lakini ukifanya mabaya waweza kuogopa, maana hawachukui panga bure. Wao ni watumishi [di·aʹkonos] wa Mungu, kufikiliza ghadhabu yake juu ya watenda mabaya.” Mungu huruhusu taratibu hizo za kisiasa ziendelee kuwako kwa muda na kutoa utumishi fulani wenye kufaidi watu wake duniani na wenye kusaidia kuendeleza utengemano na ulinzi juu ya kuasi sheria. Katika maana hiyo wao ni “watumishi” wake.

13 Lakini, serikali hizi za kilimwengu hazitumikii kwa sababu ya kupenda Mungu wala wanafunzi wa kweli wa Mwanawe. Bali, zinatoa utumishi huo kwa wote bila ubaguzi kwa faida ya raia zao wote. Kwa hiyo, utumishi wao hauwaletei thawabu wapatayo wale wanaomtumikia Yehova Mungu kwa sababu ya kumpenda yeye na jirani zao.

UTUMISHI WA MAANA HATA ZAIDI

14, 15. (a) Ingawa kuangalia mahitaji ya kimwili ya wengine ni upande wa maana sana wa Kikristo, ni upande upi mwingine ulio wa maana hata zaidi? (b) Masimulizi yaliyomo katika Matendo 6:1-4 yaonyeshaje hili?

14 Kutokana na yale ambayo tumeona ni wazi kwamba kuangalia mahitaji ya kimwili ya wengine, hasa ya ndugu zetu wa Kikristo, ni sehemu ya maana ya utumishi wa Kikristo. Ye yote kati yetu asijione kamwe kuwa mkubwa sana kutoweza kutumikia katika njia hizi, wala asiudharau ubora wa utumishi huo machoni pa Mungu. Hata hivyo, kuna upande wa maana hata zaidi wa utumishi ambao imewapasa Wakristo wa kweli wafikirie sana kuutoa. Upande upi huo? Ni kutumikia mahitaji ya kiroho hasa ya wengine.

15 Kutumikia mahitaji ya kimwili ya wengine kunaonyeshwa wazi kuwa na maana ndogo kunapolinganishwa na kutumikia mahitaji yao ya kiroho katika masimulizi yaliyomo katika Matendo 6:1-4 (NE). Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W. K. kulitokea tatizo kwa sababu upendeleo ulikuwa ukifanya wajane fulani “wasahauliwe katika ugawaji wa kila siku [di·a·ko·niʹa; upakuaji wa kila siku wa chakula, New American Standard Bible].” Mitume walipopashwa habari hizo ‘waliita jamii nzima ya wanafunzi waje pamoja wakasema, Lingekuwa kosa kubwa sana kwetu kuliacha neno la Mungu ili tutumikie mezani [di·a·ko·niʹo; kuweka hesabu, AT].’ Kwa hiyo wakawaagiza ndugu watafute wanaume saba “wenye sifa njema kati ya hesabu yenu,” ili mitume, kwa kutumia uwezo wa kuweka, waweze ‘kuwaweka washughulikie mambo haya, huku sisi tukijitoa kwa sala na kwa huduma [di·a·ko·niʹa; utumishi, Int; utoaji, AT] ya Neno.’

16. Je! mitume walikosa kupakua chakula wenyewe kwa sababu ugawaji wa chakula kwa wajane hao ulikuwa utendaji usiohusu kundi?

16 Bila shaka kugawia wanawake hao wenye kusahauliwa chakula kulikuwa sehemu ya lazima ya utumishi wa Kikristo. Kwa hiyo, haukuwa utendaji usiohusu kundi, bali lilikuwa jambo la kiroho lenye kulihusu. Maneno ya mwanafunzi Yakobo katika Yakobo 1:26, 27 yaonyesha kwamba hiyo ni sehemu ya wazi ya “dini” iliyo safi. Hata hivyo mitume walijua kwamba kama wangalitumia wakati wao kusimamia hasa ugawaji wa vitu hivyo vya kiwili badala ya kukaza fikira juu ya kusimamia mambo ya kiroho kabisa, hasa utoaji wa chakula cha kiroho na uongozi kwa akina ndugu kutoka katika Neno la Mungu, wangalikuwa wakionyesha hawana busara.

17. Makundi ya mahali penginepo yalifuataje uongozi wa kundi la Yerusalemu Katika mambo hayo?

17 Makundi yalipositawi nje ya Yerusalemu, kanuni hiyo ilifuatwa. Fikira zilikazwa kwanza juu ya kutumikia mahitaji ya kiroho hasa lakini bila kusahau au kukosa kuona ubora ustahilio mambo ya kimwili. Baraza za wazee ziliwekwa kutumikia kama wachungaji na waangalizi wa kiroho katika makundi. (Matendo 20:17, 28) Ili kuwawezesha wakaze fikira juu ya kujenga na kushauri akina ndugu, baraza za wasaidizi zilifanya kazi chini ya usimamizi wao kuangalia kazi zisizo za kiroho kabisa.​—⁠Flp. 1:1.

18. Je! mtu ye yote tu angeweza kutumikia kama mmoja wa watumishi wa huduma (di·aʹko·nos) katika kundi? Hiyo inaonyeshaje kwamba utumishi uliofanywa na hawa haukuwa wa kudharauliwa machoni pa Mungu?

18 Hivyo, baada ya kumpa Timotheo maagizo juu ya sifa za watakaowekwa kuwa wazee, mtume Paulo aendelea kusema hivi: “Wasaidizi [di·aʹko·nos; watumishi, Int; watumishi wa huduma, NW; mashemasi, UV] nao lazima wawe wenye kufikiria mambo mazito, wanaume wenye kusema mambo waziwazi, si wenye kuzoea divai wala faida ya udanganyifu, bali wenye kushikilia kweli ya kimungu ya imani wakiwa na dhamiri safi. Kwanza wajaribiwe, na baadaye, ikiwa hakuna kosa la kuonekana kwao, wanaweza kutumikia kama wasaidizi [di·a·ko·neʹo; kutumikia kama wahudumu, NW] . . . Wale wanaofanya utumishi mwema kama wasaidizi [wanaohudumu vizuri, NW] wanajipatia msimamo mwema na matumaini makuu katika kumwamini kwao Kristo Yesu.”-​—1 Tim. 3:8-13, AT.

19, 20. (a) Kwa hiyo, neno la Kigiriki di·aʹko·nos (mtumishi) lilitumiwaje kwa njia ya pekee katika kundi la kwanza? (b) Sasa kunatokea ulizo gani juu ya uhusiano kati ya “watumishi” hao wa kundi na wale waliowekwa kuwa wazee?

19 Kama vile neno la Kigiriki pre·sbyʹte·ros, linalomaanisha “mwanamume mzee,” lilivyopata kuwa cheo cha mwanamume mwenye mgawo wa kundi wa utumishi, yaani, ule wa kuwa “mzee,” ndivyo di·aʹko·nos, linalomaanisha “utumishi,” lilivyopata kuwa na maana ya cheo cha mwanamume mwenye mgawo mwingine wa kundi. Ikieleza matumizi mbalimbali ya neno la Kigiriki di·aʹko·nos, Theological Dictionary of the New Testament, Volume 11, ukurasa wa 89, unasema hivi chini ya kichwa “B. The Deacon as a Church Official”:

“1. Tofauti inaweza kufanywa kati ya matumizi haya yote ya jumla na kutumiwa kwa neno hilo kama ‘jina lisilobadilika la mwenye cheo fulani cha wazi’ kama diakonos katika umbo lenye kusitawi la Kanisa. Hii inaonekana katika mafungu ya maneno ambako [Latin] Vulgate ina neno la kuazima diaconus badala ya neno [la Kirumi] minister linalotumiwa kwingineko (linganisha Flp. 1:1; 1 Tim. 3:8, 12).

“Washiriki wa jamii ya watu [ya Kikristo] wanaoitwa mashemasi kwa wema wa utendaji wao wa kawaida wanaonekana kwanza katika Flp. 1:1, ambapo Paulo apeleka salamu kwa watakatifu wote katika Filipi syn episkoʹpois kai diakoʹnois [pamoja na waangalizi na watumishi, Int]. Tayari katika fungu hilo la maneno latokea wazo la kutufahamisha cheo chenyewe, yaani, kwamba mashemasi wanaunganishwa na maaskofu [waangalizi] na kutajwa baada yao. Kwa hiyo wakati wa kuandikwa kwa waraka huu viko vyeo viwili vinavyolingana.

“. . . hapa masimulizi yameonyesha cheo halisi.”

20 Kwa hiyo, ndugu hao waliitwa “watumishi” wa kundi, wenye kutumikia kwa unyenyekevu mahitaji ya ndugu zao katika kazi walizogawiwa. Je! hiyo iliwapa ndugu waliokuwa “wazee” haki ya kujiona wakubwa kuliko ndugu zao (wale ambao waliwekwa watumikie kama di·aʹko·nos) kana kwamba sasa wazee ndio “mabwana-wakubwa” wao?

HAKUNA NAFASI YA NIA YA KUJIONA MKUBWA

21. Kwa sababu gani hakuna sababu ya mzee kujiona kuwa “mkubwa” kuliko wale wanaotumikia kama “watumishi” wa kundi?

21 Sivyo, kwa maana hiyo isingepatana na shauri la Yesu na kanuni aliyofundisha mitume wake. Kwa kweli, wote waliotumikia kama “wazee” walikuwa watumishi pia wa ndugu zao, kutia na wale wanaoitwa “watumishi” wa kundi (“watumishi wa huduma,” NW). Yesu Kristo mwenyewe alikuwa amekuja, ‘si kutumikiwa, bali kutumika.’ Mtume Paulo mwenye kuongozwa na Mungu alisema kwamba Yesu “alipata kuwa mtumishi [di·aʹko·nos] wa Wayahudi ili kuendeleza kweli ya Mungu.” (Mt. 20:28; Rum. 15:8, NE) Paulo alijitaja mwenyewe (na vilevile wafanya kazi wenzake, Timotheo na wengine) kama “mtumishi” (di·aʹko·nos). (Efe. 3:7; Kol. 1:23, Int) Kwa kutaja hivyo hakumaanisha kwamba yeye alikuwa wa baraza ya watumishi wa kundi (“watumishi wa huduma” au “mashemasi”) katika kundi fulani, bali kwamba alikuwa amepewa mgawo atumikie kundi lote la Kikristo. Akisema juu ya kundi hilo, anena hivi: “Nikawa mtumishi wake [di·aʹko·nos; mhudumu, UV] kwa nguvu ya daraka nililogawiwa na Mungu kwa faida yenu: ili kuupeleka ujumbe wake wote.”​—⁠Kol. 1:24-26, NE.

22, 23. (a) Ni kwa njia gani mtu anavyoonyesha ni mtumishi wa kweli wa mwingine? (b) Mtume Paulo alionyesha ushuhuda wa namna gani kuhakikisha alikuwa mtumishi wa kweli wa Mungu na wa Kristo?

22 Ili kuwa “mtumishi” wa mwingine mtu angepaswa kuvumilia kwa unyenyekevu magumu, kuvumilia hali zisizopendeza. Kuwa au kutokuwa kwa mtu na nia ya kufanya hivyo kungeonyesha kama anatumikia yule mwingine kwa njia ya kweli au sivyo. Kwa sababu wengine walikuwa na maelekeo ya kumdharau Paulo kwa kumlinganisha na wengine, yeye alitoa uhakikisho kuonyesha alikuwa mtumishi wa kweli wa Kristo na Mungu. Aliandika hivi kwa Wakristo wa Korintho, ambako wengine wa wenye kumdharau walikuwa: “Kama watumishi [di·aʹko·nos; wahudumu, NW] , twajaribu kujipendekeza katika hali zote kwa uvumilivu wetu thabiti: katika dhiki, magumu, na shida kubwa sana; tunapopigwa viboko, kutiwa gerezani, kushambuliwa na makundi ya watu wenye ghasia; kufanyizwa kazi kupita kiasi, kukosa usingizi, kufa njaa.”​—2 Kor. 6:4, 5, NE.

23 Aliwauliza hivi wenye kumdharau, “Je! wao ni watumishi [wahudumu, NW] wa Kristo?” kisha akaendelea kusema, “Mimi naweza kuwapita. Nimefanyizwa kazi ya kupita kiasi kuliko wao, nimepigwa mijeledi mikali zaidi kuliko wao, nimetiwa gerezani mara nyingi zaidi kuliko wao, mara nyingi nimeelekeana na kifo uso kwa uso. Mara tano Wayahudi wamenichapa viboko thelathini na tisa; mara tatu nimepigwa kwa fito; mara moja nilipigwa mawe; mara tatu nimevunjikiwa na merikebu, na kwa saa ishirini na nne nilielea katika bahari pana. Sikuzote nimekuwa njiani; nimepatwa na hatari za mito, hatari za wanyang’anyi, hatari za wananchi wenzangu, hatari za wageni, hatari katika miji, hatari katika nchi, hatari katika bahari, hatari za marafiki wa uongo. Nimefanya kazi ya taabu na ya kulemea sana, mara nyingi nimekosa usingizi; nimekuwa mwenye njaa na kiu, mara nyingi nimefunga kula; nimepigwa na baridi na nimekuwa uchi.”​—2 Kor. 11:23-27, NE.

24. Hivyo mtume atusaidiaje tuendelee kuwa na maoni yanayofaa tunapokadiri ukweli wa utumishi wetu wenyewe?

24 Hapa kweli ulikuwapo ushuhuda wa kuwa mtumishi wa kweli! Hakuna kujisifia mambo ya kustaajabisha yaliyotimizwa, kama vile kujenga majumba yenye fahari; hakuna kutaja habari za kuvuta makundi makubwa ya watu waje kumsikia; hakuna kujitwalia sifa ya mpanuko mkubwa uliotokea katika uenezaji wa habari njema. Badala yake, ni kumbukumbu la utumishi wa unyenyekevu, kama mtumishi ambaye atoka nje hata usiku wa manane, akivumilia mvua nzito, masumbufu na hatari bila ya kujisifu, apeleke ujumbe fulani aliotumwa na bwana wake. Tunaweza kufikiria hilo tunapokadiri ukweli wa utumishi wetu wenyewe kwa Mungu. Walakini, tunaweza kujikumbusha pia kwamba Paulo alitaja barua zake za sifa, yaani, wanafunzi wa Kikristo aliokuwa amefanya kuhakikisha utumishi wake,​—⁠ 2 Kor. 3:1-3.

25. Paulo alionyeshaje unyenyekevu wake alipokuwa akiwaandikia waliokuwa Korintho, ambako alikuwa amefanya kazi ngumu kwa bidii sana?

25 Paulo hakuwa kamwe na hatia ya kujikuza wala ya kutaka wengine wamtegemee yeye kwa kumheshimu kama ‘mkuu’ zaidi kati yao. Yeye alisema hivi kwa Wakorintho hao aliokuwa ametaabikia mwaka mmoja na nusu, akiwaeleza habari zake mwenyewe kama mfanya kazi mwenzao: “Apolo ni nini? Au Paulo ni nini? Ni watumishi tu [di·aʹko·nos, wahudumu, UV] ambao kupitia kwao mlipata kuwa na imani, kama Bwana alivyompa kila mmoja wetu nafasi. Mimi nilipanda, Apolo alitia maji, lakini Mungu ndiye aliyeikuza mimea. Kwa hiyo wala mpanzi wala mtia maji si bora kwa lo lote, bali Mungu peke yake akuzaye mimea. . . . Sisi tu wenzi-wafanya-kazi wa Mungu, nanyi m shamba la Mungu, jengo la Mungu.”​—1 Kor. 3:5-9, AT.

26. Twawezaje kujaribu kuwa wakubwa na bado tusiwe wenye kujitakia makuu na wenye kiburi?

26 Bila shaka, kujaribu kuwa mkubwa kwa njia hii ya kujitoa kufanya utumishi wa unyenyekevu, si kwa kupata umashuhuri, heshima wala uwezo, ni mradi wa kutamanika. Huo ni ushuhuda wa kumpenda Mungu na jirani, si wa kujitakia makuu wala kiburi wala choyo. Sote leo na tutafute ukubwa huo, hivyo tumpe Yehova Mungu sifa, ambaye aliianzisha kanuni hii ya ukubwa, na kumheshimu Mwanawe kwa njia hiyo, ambaye aliweka mfano wa kufuata kanuni hiyo kama asivyopata kufanya mtu mwingine ye yote. Tukitafuta “ukubwa” wa Kikristo tutajipatia wenyewe faida kubwa pamoja na wengine. Hiyo itafanya roho takatifu ya Mungu imiminike kwa wingi, kisha kutakuwa na umoja wa ajabu na mapatano kati yetu, kama ielezavyo makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Kulingana na watungaji wa kamusi, neno di·aʹko·nos linatokana na neno la Kigiriki koʹnis, maana yake “mavumbi,” hivyo linaeleza mtumishi mwenye mavumbi kwa sababu ya kufanya kazi fulani au kupeleka ujumbe fulani wa bwana wake.

b Tunaona mifano mingine ya aina hii ya kutumikia (“ministering,” NW) katika masimulizi ya karamu ya arusi katika Kana (Yohana 2:1-9), katika utumishi uliofanywa na mamamkwe wa Petro (Mt. 8:14, 15), na ule uliofanywa na Martha.​—⁠Luka 10:40; Yohana 12:2; tazama Kingdom Interlinear Translation.

[Picha katika ukurasa wa 247]

Neno la Kigiriki di·a·ko·neʹo linakazia utumishi wa mtu bi nafsi kwa mtu mwingine

[Picha katika ukurasa wa 248]

Utumishi wa Kikristo unatia ndani kuangalia mahitaji ya kimwili ya Wakristo wenye upungufu; upaji wa namna hiyo huleta sifa kwa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 250]

Wakristo wa kwanza walitumikia mahitaji ya kiroho ya wengine kwanza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki