Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 2/15 kur. 8-13
  • Kushirikiana ili Kuleta Umoja Katika Jamaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kushirikiana ili Kuleta Umoja Katika Jamaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUFIKIRIA WATOTO INAVYOFAA
  • UHUSIANO WA MUME NA MKEWE
  • Faida Zenye Kudumu Kutokana na Kuifuata Biblia Kama Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kujenga Maisha ya Furaha ya Jamaa
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Kufanikisha Maisha ya Jamaa
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Je! Furaha Inaweza Kupatikana Katika Jamaa Zilizogawanyika?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 2/15 kur. 8-13

Kushirikiana ili Kuleta Umoja Katika Jamaa

1. (a) Inazipasa jamaa za Kikristo ziepuke maneno na hali gani? (b) Wakolosai 4:6 inatoa shauri gani jema?

“MIMI NILIKUAMBIA!” “Wewe hunisikilizi kamwe!” “Si nilikuambia?” Mara nyingi sana maneno hayo yanasemwa na wenzi wa ndoa na watoto wao. Yanasemwa kwa kuchukizwa ikiwa jambo fulani halikufanywa kama mwenzi alivyotaka. Lakini mwenye hekima aliandika hivi: “Ni afadhali kuishi peke yako katika jangwa kuliko kuishi pamoja na mke mwenye gubu na hasira.” (Mit. 21:19, New English Bible) Ayo hayo yanaweza kusemwa juu ya kuishi na mume mwenye gubu na hasira. Kamusi inatoa maelezo haya juu ya neno “gubu”: “Udhia (kusumbua), fujo, ghasia, hali ya kupenda kushikilia habari na kuinung’unikia.” Hakika fujo za namna hiyo hazipasi ziwe katika jamaa ya Kikristo. Lazima wenzi wote wawili wa ndoa wajiangalie wasiwe na hali hiyo. Sote tunapata shauri zuri katika maneno ambayo mtume aliandikia kundi la Kolosai: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” (Kol. 4:6) Mwenzi wa ndoa akimjibu mwenzake kwa njia hiyo, wote watakuwa na furaha.

2. Wasomaji wa gazeti hili walipashwaje habari kwa wakati wake juu ya fadhili?

2 Hivi majuzi, gazeti hili lilikuwa na makala iliyohusu fadhili. Kwa ufupi, lilisema hivi: “Yawapasa wanaodai kuwa Wakristo wajiangalie wasionyeshe fadhili chache kuliko . . . [zinazoonyeshwa] nyakati nyingine na watu wasio watumishi wa Mungu. . . . Tunaona na kusoma habari za fadhili za ajabu sana zilizoonyeshwa na wanadamu, ambazo zinakuwa nyingi sana zikilinganishwa na fadhili zinazoonyeshwa na wengine wanaodai kuwa watumishi wa Mungu walio wakf.” Looo! linaweza kuwa sikitisho kubwa namna gani tukikosa kuonyeshana fadhili katika jamaa yetu yenye waabudu walio wakf kwa Yehova.

3. Neno “kadhalika” linahusuje jinsi waume wanavyotendea wake wao?

3 Mtume Petro anawapa waume shauri jema lifuatalo akiwaeleza jinsi ya kufikiria wake wao inavyofaa: “Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” (1 Pet. 3:7) “Kadhalika” hiyo inayotajwa na Petro inahusu mashauri aliyotangulia kusema juu ya utii unaofaa na mambo kama hayo, kuanzia sura ya pili ya barua yake. Petro aliandika kwamba Bwana Yesu Kristo aliachia wafuasi wake kielelezo wakifuate. Alisema hivi juu yake: “Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.” (1 Pet. 2:23) Hizo zilikuwa fadhili kweli, tena ni mfano unaostahili kufuatwa na waume kadhalika.

4. Inawapasa wake “kadhalika” waonyesheje fadhili?

4 Bila shaka, Petro alitolea wake mashauri yenye hekima ili wao wayafuate “kadhalika.” Alisema wanawake wawe na “roho ya upole na utulivu, iliyo ya thamani kuu mbele za Mungu.” Hakika hivyo ndivyo inavyowapasa wake wanaojiita watumishi wa Yehova na wa Kristo Yesu waonyeshe fadhili.​—1 Pet. 3:1-4.

5. Onyesha jinsi shauri la Petro linahusu wote katika kuonyesha fadhili.

5 Lakini si hilo tu. Si wazazi peke yao wanaopaswa kuonyesha fadhili katika jamaa kwa kuepuka kunung’unika-nung’unika. Petro anaendelea kusema hivi: “Mwishowe, ninyi nyote mwe na nia iyo hiyo, mkifikiriana sana, mkioneana shauku ya kidugu, mkiwa na huruma nyingi sana, mkiwa wanyenyekevu katika akili.” Mistari michache tu baada ya hapo, Petro alionyesha thawabu nzuri inayotokana na kufuata shauri hilo, aliposema: “Kwa maana macho ya Yehova yako juu ya wenye haki, nayo masikio yake yanaielekea dua yao.” 1 Pet. 3:8, 12, NW.

KUFIKIRIA WATOTO INAVYOFAA

6. (a) Wanapofikiria watoto wao, lazima baba na mama watimizeje daraka lao? (b) Tunapewa shauri gani na Maandiko juu ya kuzoeza watoto?

6 Halafu tena, katika jamaa watoto wanapaswa kujengwa. Katika makala iliyotangulia tumesoma uzito wa daraka ambalo baba analo katika kulea watoto katika adabu na maonyo ya Yehova. (Efe. 6:4) Lakini ni wazi kabisa kwamba mama pia ana daraka kubwa la kutimiza jambo hilo la maana katika jamaa. (Mit. 6:20; Efe. 6:1, 2) Katika ulimwengu huu uliojawa na uasi, ambamo watoto na vijana wengi sana wanafanya uhalifu na jeuri, inaweza kuonekana vyepesi kwamba mazoezi ambayo wazazi Wakristo wanawapa watoto wao yanahusu uzima na mauti. Ikiwa wazazi wote wawili ni waamini, wanaweza kushirikiana watumie mafundisho yenye hekima ya Neno la Mungu yanayohusu kuzoeza watoto.​—Mit. 13:24; 22:6.

7. Inawapasa baba na mama wafanye nini ikiwa wanatofautiana maoni juu ya kutia mtoto adabu, na kwa sababu gani?

7 Wazazi wote wawili wakishirikiana kutia watoto wao adabu kwa upendo, wanaweza sana kuleta furaha katika jamaa. Ikiwa wazazi wanatofautiana katika maoni yao ya kutia watoto adabu, wanaweza kuelezana wakiwa peke yao, mahali wasipoweza kusikiwa na watoto, kisha wakifikia maamuzi mamoja, yanayofaa, watoto watafaidika. Kufanya hivyo kunaweza kutia watoto moyo wakue wakiheshimu mashauri na mafundisho ya adabu wanayopewa na wazazi wote wawili, wala hawatajaribu kugombanisha wazazi juu ya matatizo yanayotokea utotoni mwao.

8. (a) Lazima tukubali nini juu ya kulea watoto? (b) Basi, lazima wazazi wajitahidi kufanya nini?

8 Ni kweli kwamba watoto wengine hawaikubali kweli ya Neno la Mungu kwa moyo. Wanaikataa, kama vile Kaini, Esau na wengine. Hawaiachi iongoze maisha yao, ili kuleta mapatano katika jamaa. Hakika jambo hilo linaletea baba na mama waamini majonzi. ‘Kwani tumeshindwa kufanya nini?” huenda wakajiuliza. Ziko nyakati ambazo wazazi wamejitahidi iwezekanavyo kulea watoto wao katika njia za haki wakitumia mashauri na mafundisho ya Biblia, na bado watoto wao wakawa waasi na kukataa kuwa watoto watiifu wa Mungu. Hapo ndipo maneno ya Mithali 17:21 na 25 yanapotumika. Mwenye hekima aliandika humo hivi: “Baba wa mpumbavu hana furaha. Mwana mpumbavu ni huzuni kwa babaye, na uchungu kwa mamaye aliyemzaa.” Basi, ni jambo la maana sana wazazi wajitahidi wawezavyo kuwapa watoto wao mwanzo mzuri wanaostahili maishani! Wanaweza kufanya hivyo kwa kufuata mashauri ya Biblia juu ya kulea wazao wao. (Kum. 6:4-9) Jambo hilo linahitajiwa sana ili kushirikiana kuleta umoja katika jamaa.

9. (a) Ni jambo gani linalohitajiwa zaidi ya kujifunza Biblia na watoto? (b) Ni pande gani ambazo wazazi wanaweza kupendezwa na watoto wao?

9 Ni hekima kukumbuka kwamba kujifunza Biblia na watoto wetu hakutoshi ili kuwazoeza na kuwafundisha katika maonyo ya Yehova. Ni jambo la maana sana kutumia kanuni za Biblia katika maisha yetu wenyewe. Ikiwa wewe una watoto, utakuwa mzazi mwenye hekima ukiwawekea mfano kwa kuwa mwenye bidii. Je! ingekuwa hekima mama akiacha watoto wao wajitayarishie kiamsha-kinywa asubuhi, wajitayarishe kwenda shuleni na kujiendea zao, na huku mama huyo amelala? Inawapasa wazazi Wakristo wanaojaribu sana kuleta umoja katika jamaa wajitahidi kuamka pamoja na watoto wao asubuhi, kuwatayarisha kwenda shuleni, kuwapa kiamsha-kinywa na kuhakikisha kwamba wamejivika vizuri, isipokuwa kama ni wagonjwa au kuna sababu nyingine nzuri. Wanapaswa watake kujua jinsi watoto wao wanavyoendelea masomoni, na kuhakikisha kwamba sikuzote wanakuwa na mwenendo unaowapasa watumishi wa Yehova wenye mazoezi mazuri na adabu njema. Inawapasa wakaze kikiki ndani ya watoto hali ya kuheshimu watu wakubwa na mali za wengine. Mambo yote hayo, pamoja na mengine mengi, yanaweza kusaidia wazazi wawe na watoto ambao hawatawatia uchungu katika roho zao, bali watamsifu Muumba wao na kufurahisha mama na baba yao.

UHUSIANO WA MUME NA MKEWE

10, 11. Ni mwenendo wa namna gani unaoendelea kufuatwa na watu wengi siku zetu, na wengine wanatoa sababu gani?

10 Ndipo tunapofikia matatizo yanayotokea nyakati zote katika ngono za mwanamume na mkewe. Katika ulimwengu, habari nyingi sana zimeandikwa juu ya jambo hilo miaka michache iliyopita, na nyingi kati yazo hazipatani kabisa na mashauri mema ya Neno la Mungu. Leo watu wana kawaida ya kuishi pamoja bila kuoana kisheria. Bila shaka hilo si jambo jipya, lakini siku hizi watu wengi sana wanadhani wana maarifa kwa sababu ya kufanya hivyo bila kuficha watu, bila kujali maoni yao, wala mafundisho ya adili ya Neno la Mungu.

11 Hata katika nchi zinazodhaniwa kuwa za Kikristo, wanaoitwa watu “wa dini” wanaishi pamoja bila kuoana kisheria, huku wakisema kwamba viapo vinavyofanywa mbele ya watu au kipande cha karatasi kinachosema mtu ameoa au ameolewa hakina maana sana. Halafu wako watu wengi wanaoishi na wenzi wengi, wakiacha huyu na kuhama-hama ili kumwendea yule na yule. Bila shaka kufanya hivyo kumezidisha magonjwa ya kisonono na kaswende, kukawa na mitengano na watoto waasi. Lakini inaonekana watu wengi hawajali maadamu wanatosheleza tamaa zao za kichoyo.

12. Inawapasa mume na mke Wakristo wawe na maoni gani juu ya hali hizo za maisha?

12 Bila shaka, mume na mke Wakristo wanakatazwa na Mungu wasiwe na maisha ya namna hiyo, nao wana akili ya kujua kwamba kumpendeza Mungu na kufanya mapenzi yake ndilo jambo la maana zaidi katika maisha yao. Kunawaletea baraka yake. Hata hivyo, mume na mke Wakristo lazima wajiangalie ngono zao zisiharibiwe na mazoea yasiyo ya asili yaliyo kinyume cha kanuni zilizo katika Neno la Mungu. Wakati wanapotaka kulalana, inampasa kila mmoja afikirie vile mwenzake anavyojisikia.

13. Mume anawezaje kuonyesha kwamba anampenda mkewe?

13 Muumba wetu aliwaumba mwanamume na mwanamke wafurahie sana ngono. Ndiyo sababu mwanamke alifanywa awe “mkamilishaji” wa mwanamume, yaani, amfanye awe mtu kamili. Mwanamume na mwanamke wanapaswa kuwa “mwili mmoja.” (Mwa. 2:18, 21-24, NW) Ili wenzi wote wawili wafurahie ngono, kila mmoja atapaswa kufanya jambo fulani. Kwa mfano, mtume Paulo aliandika hivi: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.” (Efe. 5:28, 29) Ili mke awe mwenye furaha kikweli, anahitaji kujisikia kwamba anatakiwa, anapendwa. Inampasa mwanamume amwonyeshe mkewe upendo huo wanapofanya ngono, ili wote wawili waendeleze umoja na masikilizano katika jamaa.

14. Inawapasa waepuke uhusiano gani, na kwa sababu gani?

14 Inawapasa mwanamume na mkewe wategemee Neno la Mungu wanapopeana haki zao. (1 Kor. 7:3-5) Ingawa wanapaswa kufurahiana na kupendana sana katika ngono, inawapasa waepuke mazoea yasiyo ya asili, kama vile mume kuingiza mboo katika mdomo wa mkewe. Tunasema hayo ni mazoea “yasiyo ya asili” kwa sababu Muumba hakukusudia mwanamume na mwanamke wawe nayo, nalo Neno lake linakazia uhitaji wa kuepuka mazoea machafu yanayofanywa na ulimwengu.​—Law. 18:1-30; Rum. 1:24-27; 1 The. 4:3-8.

15. Lazima mtu aepuke nini ili kuuvaa utu mpya? (Linganisha Yuda 7.)

15 Katika taratibu hii potovu ambamo inawapasa Wakristo waishi na kuenenda kulingana na mafundisho ya Kikristo, lazima tuepuke kusitawisha mawazo na maoni ya watu wanaounga mkono mwenendo mbaya. Katika pande zote inaonekana kwamba ngono za kila namna zimekuwa kama kitu kinachoweza kununuliwa au kuuzwa na watu vyo vyote watakavyo. Watu wengi wanaoingia katika kweli wamekuwa na maisha hayo ya taratibu ya kale, na nyakati nyingine waliongozwa na mawazo yake. Sasa wamekwisha toka katika taratibu hiyo wakaingia katika tengenezo la Mungu. Wamebadili nia zao, wakauvaa utu mpya nao wanataka waishi kupatana na kanuni zenye haki za Neno la Mungu.​—Efe. 4:19-24.

16. (a) Lazima Mkristo ajiangalie asifanye nini anapofikiria mwenendo wake wa adili? (b) Mambo yaliyotukia siku za Nuhu na wakati wa Sodoma na Gomora yanahusikaje katika jambo hili? (c) Onyesha jinsi inavyofaa sana kutumia Warumi 2:12-16 katika habari hii.

16 Inafaa kabisa sisi sote ambao tumeitwa tutoke gizani na kuingia katika nuru ya ajabu ya ukweli wa Mungu tufikirie mawazo na matendo yetu bila mchezo. Haitupasi kuachilia mambo ambayo Mungu anakataza. Haitupasi kujaribu kukaribia kutenda makosa kama iwezekanavyo, tukijisikia kwamba tuna haki ya kujifanyia maamuzi fulani tukitaka. Wala haitupasi kujitafutia kisababu cha kufanya hivyo kwa kusema kwamba hakuna mahali ambapo Maandiko yanakataza waziwazi mwenendo fulani wenye kutiliwa mashaka. Hakuna lo lote linaloonyesha kwamba siku za Nuhu kulikuwa na sheria iliyoandikwa kukataza ngono ambazo malaika walifanya na binti za wanadamu. Hata hivyo, tendo lao lilikuwa ovu, la uasherati. Mungu aliona kwamba dunia ilikuwa imeharibiwa na kujazwa jeuri. Aliuharibu ulimwengu huo wenye maovu, akaokoa nafsi nane tu zenye haki. (Mwa. 6:11, 12; 1 Pet. 3:19, 20) Baadaye aliiharibu miji ya Sodoma na Gomora kwa sababu ya kuzoea ulawiti. Lakini katika Maandiko hakuna jambo linaloonyesha kwamba watu wa wakati huo walikuwa na sheria zo zote za Mungu zilizoandikwa waziwazi kuwakataza mazoea hayo. (Mwa. 13:13; 19:24, 25) Tangu mwanzo Mungu alikuwa ametia uwezo wa kutumia dhamiri katika mwanadamu. Mwanadamu anajua kwa asili yaliyo haki na yaliyo mabaya, anayajua mazoea maovu yanayokatazwa na Mungu. (Rum. 2:12-16) Anajua vile Mungu alivyokusudia alipotia nguvu za uzazi katika mwanamume na mwanamke na kuwawezesha wote wawili wazae watoto kwa kuungana katika ngono. Basi, kwa asili mwanadamu anajua kwamba ulawiti ni mbaya, kwamba ni vibaya mwanamume kuingiza mboo katika mdomo wa mkewe, kwamba ni vibaya kulala na mnyama, vilevile kufanya uzinzi, uasherati, kulalana na mwanamume au mwanamke mwenzake, na mazoea mengineyo. Ndiyo sababu lazima mume na mke watende mambo yanayopatana na mawazo ya kimungu, yanayopatana na kanuni za Neno la Mungu, ili waendeleze umoja wa jamaa. Ndipo wanapoweza kuleta furaha yenye kudumu katika jamaa.

17. Taja mtego mwingine unaopasa uepukwe katika ndoa.

17 Vilevile, haimpasi mtu kulazimisha mwenzi wake wafanye ngono ili ajifaidi mwenyewe tu. Mtume Paulo alishauri hivi: “Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Msinyimane isipokuwa mmepatana.” Inampasa kila mmoja afikirie mahitaji ya mwenzake katika ndoa, kama Paulo alivyoandika: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.”​—1 Kor. 7:3, 5; 10:24.

18. Tunapata wapi mashauri yanayofaa juu ya ndoa na juu ya kuiendeleza katika hali yenye kuheshimika?

18 Tengenezo la Yehova linaloonekana duniani limetoa habari nyingi zinazofaa kufikiriwa na waliooana, maana wanaweza kupata baraka. Mashauri hayo hayatoki kwa mwingine, ila kwa Yehova mwenyewe kupitia kwa Neno lake. Mtume Paulo aliandika waziwazi kabisa kwamba ndoa “iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi,” kwa hiyo wale wanaotaka kuwa na maisha yenye furaha katika ndoa wanaweza kuyapata kwa kushikamana sana na shauri hilo jema ambalo Paulo aliwapa Wakristo Waebrania.​—Ebr. 13:4.

19. Ni matatizo gani zaidi yatakayozungumzwa juu ya ndoa, umoja wa jamaa na amani kati ya watumishi wa Mungu?

19 Humu tumezungumza juu ya ndoa yenye furaha ya mume na mke ambao ni Wakristo waliojiweka wakf na kubatizwa wakiwa na miradi mimoja na mapendezi mamoja. Lakini, watumishi wengi wa Yehova wanakuwa wameoa au wameolewa na watu wasioamini, au wanakuwa wametengana na wenzi wao. Watu walio katika hali hiyo, walio na watoto wa kulea, wanawezaje kutatua matatizo yao mengi kwa sababu ya kutaka maisha yenye furaha? Neno la Mungu linawashaurije watumishi hao wa Yehova? Makala inayofuata itazungumza hayo.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wazazi wote wawili wanapaswa washirikiane kutia mtoto adabu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wewe unaamka mapema vya kutosha usaidie watoto wako wajitayarishe kwenda shuleni?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki