Kuzitangaza Habari Njema Duniani Pote
SIKUZOTE Yehova Mungu amekuwa na mashahidi wa kuitangaza enzi kuu yake. Habili ndiye aliyekuwa shahidi wa kwanza. (Mt. 23:35; Ebr. 11:4; 12:1) Baadaye, wakati suala lilipotokea kati ya mataifa juu ya Uungu wake, Yehova aliliambia hivi taifa zima la Israeli: “Ninyi ni mashahidi wangu.” (Isa. 43:10-12; 44:8) Yesu Kristo ndiye Shahidi mkuu Zaidi wa Mungu. Alijiita “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.”—Ufu. 3:14.
Kwa hiyo, wafuasi wote wa kweli wa Yesu Kristo ni mashahidi wa jina la Yehova na makusudi yake yanayotimizwa kupitia kwa Kristo. Mungu ndiye aliyelianzisha kundi la Kikristo, kama vile mtume Petro alivyoonyesha alipokuwa akitoa ushuhuda mbele ya baraza yenye kuongoza Wakristo katika karne ya kwanza. (Matendo 15:7, 8, 14; 1 Pet. 2:9) Nyakati za hukumu zilipofika, jina la Mungu na makusudi yake yalitangazwa kote kote. Tunaweza kuonyesha mfano ulio wazi wa miaka 40 iliyotangulia kumalizika kwa taratibu ya mambo ya Kiyahudi mwaka 70 W.K., wakati Yerusalemu ulipoharibiwa. Yesu na wanafunzi wake ndio waliokuwa watangazaji wa makusudi ya Mungu juu ya taifa hilo, nao waliongezeka wakawa wengi sana machoni pa watu, hata machoni pa adui zao. (Matendo 17:6; 28:22) Vilevile, kabla ya gharika ya siku za Nuhu iliyotukia duniani pote, na kabla ya Yerusalemu kuharibiwa mara ya kwanza na Wababeli mwaka 607 K.W.K., onyo lilitolewa waziwazi sana, nalo halikupasa kupuzwa—2 Pet. 2:5; Yer. 25:8-12.
Kwa hiyo leo, katika mwisho wa taratibu hii ya mambo, lazima onyo litangazwe kufika mbali hata zaidi. Nalo linatangazwa sasa. Katika nchi 210, kutia na nchi ambako Mashahidi wa Yehova wanalazimika kufanya kazi kwa siri, watu zaidi ya milioni mbili wanazihubiri “habari njema” wakifundisha watu juu ya ufalme wa Mungu wenye haki na kutoa onyo juu ya kuharibiwa kwa uovu duniani.
MASHAHIDI WA YEHOVA NYAKATI ZA KISASA
Kazi ya kisasa ya Mashahidi Wakristo wa Yehova ilipata nguvu karibu na mwaka 1872 wakati wanaume wachache walipotaka sana kujua habari ambazo Biblia inasema juu ya kurudi kwa Kristo. Wanaume hao walikaza fikira nyingi pia juu ya fundisho la Biblia linalohusu dhabihu ya ukombozi iliyotolewa na Yesu Kristo. Hasa Charles Taze Russell alijitahidi sana kuanza madarasa ya kujifunza kati ya wenye kupendezwa. Wanafunzi hao waliona inafaa kujulisha watu wengine mambo waliyojifunza baada ya kuichunguza Biblia, basi wakaanza shirika la kisheria walitumie kueneza vitabu vya lugha mbalimbali vyenye kweli za Biblia. C. T. Russell alichaguliwa awe msimamizi (president) wa shirika ambalo sasa linajulikana kama Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Liliandikishwa kisheria mwaka 1884. Mashirika mengine yameanzwa pia katika nchi nyingi ili yashirikiane na Sosaiti iliyotangulia kutajwa.
Msimamizi wa pili wa Watch Tower Bible and Tract Society alikuwa Joseph F. Rutherford, aliyetumikia tangu kufa kwa Russell mwaka 1916 mpaka kufa kwake mwenyewe mwaka 1942. Kuanzia wakati huo Nathan H. Knorr alitumikia katika cheo hicho, mpaka alipokufa Juni 8, 1977, kisha Frederick W. Franz akachaguliwa awe msimamizi.
JINSI VITABU VYENYE HABARI ZA BIBLIA VINAVYOTAYARISHWA
Vitabu vinavyoeleza habari za Biblia vinatayarishwa kwa usimamizi wa baraza fulani yenye kuongoza inayokaa Brooklyn, New York. Gazeti Mnara wa Mlinzi ndicho chombo kikuu kinachotumiwa na Mashahidi wa Yehova kueneza kweli za Biblia. Gazeti hilo lilianza kuchapwa katika Kiingereza likiwa na nakala 6,000 Julai 1879, na kufika Agosti 1, 1977 lilikuwa likienezwa nakala 10,400,000 katika lugha 79. Gazeti linaloenezwa pamoja na hilo, yaani, Amkeni!, lilianza kuchapwa katika Kiingereza likiitwa Golden Age mwaka 1919 kisha likaitwa Consolation au Faraja (kuanzia 1937 mpaka 1946). Kufika Agosti 8, 1977, gazeti Amkeni! lilichapwa nakala 10,125,000 katika lugha 33.
New World Translation of the Holy Scriptures ni tafsiri ya Biblia nzima yenye usemi wa kisasa, nayo imetokana na maandishi ya kwanza ya Kiebrania na Kigiriki. Biblia hiyo ilitayarishwa na halmashauri ya Wakristo wenye kujitoa kabisa kwa moyo. Halmashauri iyo hiyo ndiyo iliyotayarisha The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures yenye maandishi ya Kigiriki ya Westcott na Hort, nayo inatafsiri maandishi ya Kigiriki neno kwa neno katika Kiingereza, kisha inaonyesha katika safu ya mkono wa kulia maneno yaliyomo katika New World Translation. Vitabu hivyo vimesaidia sana watu kujifunza Biblia. New World Translation of the Holy Scriptures imetafsiriwa kutoka Kiingereza ikaingizwa katika Kiholandi (Dutch), Kifaransa, Kijeremani, Kiitalia, Kireno na Kispania, nayo ile sehemu ya Maandiko ya Kigiriki imetafsiriwa katika Kidenmark, Kifinland, Kijapan na Kisweden.
Kati ya vitabu vingi vinavyochapwa na Mashahidi wa Yehova, kitabu kinachofuata Biblia kwa kuenezwa zaidi ni Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele. Hasa hicho ni kitabu cha mafundisho. Kufika Agosti 1, 1977, kitabu hicho chenye jalada ngumu na kurasa 192, kilichotolewa mwaka 1968 katika Kiingereza na 1969 katika Kiswahili, kilikuwa kimechapwa nakala 84,000,000 katika lugha 101. Mamia ya maelfu ya mafunzo ya nyumbani ya Biblia yanaendeshwa kwa watu wanaopendezwa kwa kutumia kitabu hicho na vinginevyo.
Waandikaji na watu wa nchi nyingi wanasaidia kutoa makala za kutumiwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kuna waandikaji fulani pia katika makao makuu ya Brooklyn, New York, wanaoandika habari fulani na kutayarisha makala zilizochangwa na watu ili zichapwe.
VIWANDA
Mashahidi wa Yehova wana kiwanda kikubwa cha uchapaji katika Brooklyn, New York, nacho kinasaidiwa na kiwanda kingine cha uchapaji kilicho karibu na Wallkill, New York. Viwanda vingine vya uchapaji vinaendeshwa Australia, Brazil, Canada, England, Finland, Ufaransa, Ujeremani, Ghana, Ugiriki, Italia, Japan, Nigeria, Jamhuri ya Philippine, Afrika. Kusini, Sweden na Switzerland. Kati ya matawi 97 yanayotumiwa kuongoza kazi katika nchi 210, 31 yanajichapia magazeti au vitabu vingine. Katika mwaka wa utumishi wa 1975 mpaka 1976 (Septemba mpaka Agosti) walichapa Biblia 2,484,919 na vitabu na vijitabu 102,638,842 vyenye kueleza habari za Biblia. Vilevile, magazeti 513,282,880 yalichapwa. Wafanya kazi wa viwanda hivyo hawalipwi mshahara, na wote ni Mashahidi wa Yehova. Wanatumikia katika viwanda hivyo na katika maafisi ya matawi, kisha wanapewa vyumba na chakula pamoja na msaada mdogo wa pesa. Wageni wanatembezwa bure katika maafisi hayo ya matawi, katika makao hayo na viwandani,
Vitabu vyenye habari za Biblia vimesaidia sana Mashahidi wa Yehova kuzitangaza “habari njema” kwa watu wengi sana katika wakati mfupi uliobaki kabla taratibu hii ya mambo haijaondolewa. Vitabu hivyo vinaachwa kwa watu wanaopendezwa kwa mchango mdogo. Watu wengi wasioweza kuchanga wanapewa pia vitabu vya bure. Mashahidi wa Yehova wanawarudia watu wanaopendezwa, tena wanawafundisha Biblia wale wanaotaka kujua habari zaidi juu ya Neno la Mungu na kusudi lake, katika nyumba za watu hao.
Mashahidi Wakristo wa Yehova wameeneza Biblia, vitabu na vijitabu zaidi ya bilioni moja na mabilioni ya magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Tena kuna mamilioni ya watu wanaoandikisha wawe wakiyapokea magazeti hayo.
MPANUKO KATIKA ULIMWENGU WOTE
Makumi ya miaka iliyopita, hasa tangu mwaka 1950, Mashahidi wa Yehova wamepanua ajabu kazi yao ya kuwapa watu ushuhuda. Katika makundi zaidi ya 40,000 ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni mbili wanazihubiri sana “habari njema.” Mamilioni ya watu wengine wanashirikiana nao katika mikutano yao ya makundi, nao wanajifunza makusudi ya Mungu na kuzoezwa kuifanya kazi iyo hiyo ya kuhubiri. Jumapili ya Aprili 3, 1977, katika mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo, yaani, “chakula cha Bwana cha jioni,” watu zaidi ya 5,089,000 walihudhuria.—1 Kor. 11:20; Mt. 26:20-30.
Wamisionari wameanzisha kazi katika nchi nyingi. Shule iitwayo Watchtower Bible School of Gilead ilifunguliwa mwaka 1943 ili kuzoeza wamisionari hao. Tangu wakati huo wanafunzi karibu 6,000 wamehitimu. Wengi wao wangali wakitumikia kama wafanya kazi wa wakati wote duniani pote. Mtu anahudhuria Shule hiyo kwa kupewa ukaribishaji wa pekee. Wanafunzi wanaochaguliwa ni Mashahidi wa Yehova wanaofanya kazi ya wakati wote ya kuwapa watu ushuhuda, ambao afya na hali zao zinawawezesha kustahili kutumikia katika nchi nyingine. Kitabu kikuu cha mafundisho kinachotumiwa katika Shule hiyo ni Biblia. Masomo makuu wanayopewa ni mafundisho yaliyomo katika Biblia, tena wanafundishwa jinsi makundi yanavyoendeshwa, jinsi ya kuwapa watu ushuhuda na kuwafundisha vizuri, na vilevile kujifunza lugha nyingine tofauti au ya kigeni. Sasa mtaala huo unachukua miezi mitano tu, lakini kunakuwa na mambo mengi sana ya kujifunza.
Baada ya kuhitimu wanafunzi wanapewa mgawo waende kwenye makao ya wamisionari au maafisi ya matawi yanayopewa riziki na kuendeshwa na Mashahidi wa Yehova. Hivyo hawana haja ya kuhangaikia mahitaji yao ya kila siku, na wanaweza kutumia wakati wote wakiwatangazia watu “habari njema” kwa kuwafikia nyumbani kwao. Wamisionari wa Mashahidi wa Yehova wanajifunza lugha ya nchi wanayokwenda kisha wanawaendea watu na kuwahubiri “habari njema” kwa bidii katika eneo walilogawiwa. Wanaanzisha makundi kisha wanashirikiana na watu waliomo, wakiwazoeza wenye kuzikubali “habari njema” waijue kazi ya kuwapa, watu ushuhuda na kuwafundisha, kazi ya kundi na ya kusimamia makusanyiko madogo na makubwa. Katika nchi nyingi ambazo kazi ilianzishwa na wamisionari hao, sasa wenyeji wa nchi hizo ndio wenye daraka la kuisimamia kazi. Wamisionari wanafurahi sana wanapotumikia pamoja na ndugu hao wenzao, walio Wakristo wema.
MAKUSANYIKO MAKUBWA
Kusanyiko lililo kubwa zaidi ambalo Mashahidi wa Yehova wamepata kuwa nalo ni lile lililofanywa Yankee Stadium na Polo Grounds mjini New York mwaka 1958, hata wanja hizo zikajaa pomoni zikiwa na watu 253,922. Kila mwaka kunakuwa na “makusanyiko ya mizunguko” yenye wahudhuriaji mamia au maelfu kadha, lakini pia kunakuwa na makusanyiko mengine makubwa zaidi “ya wilaya,” ya taifa zima au ya mataifa yote. Kwa kawaida makusanyiko kadha yanafanywa mahali panapofaa nchini, ili wengi iwezekanavyo waweze kuhudhuria. Habari zinazotolewa makusanyikoni zinalingana kila mahali ulimwenguni pote. Ripoti fulani ilionyesha kwamba watu zaidi ya 3,360,000 walihudhuria makusanyiko “Utumishi Mtakatifu” yaliyofanywa ulimwenguni pote mwaka 1976 katika nchi 96.
Katika kila kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, mipango inafanywa kuwe na ubatizo wa watu wote ambao wamekuwa wakifunzwa na Mashahidi wa Yehova, wanaotaka kufuata mfano wa Kristo kwa kuzamishwa majini. Kwa kufanya hivyo na kuiamini dhabihu ya Kristo ya upatanisho, wanaonyesha kwamba wamejiweka wakf kwa Mungu. (Mt. 3:15; 28:19, 20) Katika miaka mitatu ya 1974 mpaka 1976 jumla ya watu waliobatizwa na Mashahidi wa Yehova ilikuwa 789,601. Kila mwaka hesabu ya wenye kuzisikia “habari njema” na kujiunga na wenye kuzihubiri inaongezeka, tena watu wengi zaidi wanalisikia onyo linalosema kwamba taratibu hii ya mambo inakaribia sana kumalizwa, na kwamba utawala wa Kristo wenye haki wa miaka elfu umekaribia sana kwa kusudi la kuondoa dhambi, magonjwa na kifo duniani.—Ufu. 21:1-4.
Pictures katika ukurasa wa 18]
Charles T. Russell
Joseph F. Rutherford
Nathan H. Knorr
Frederick W. Franz
[Picha katika ukurasa wa 19]
Kila mwaka kiwanda hiki kinachapa mamilioni ya vitabu vyenye habari za Biblia katika Brooklyn, New York, na kusaidiwa na kiwanda kingine kilicho karibu na Wallkill, New York (kilichoonyeshwa chini). Viwanda hivi vinatimizia Mashahidi wa Yehova mahitaji yao ulimwenguni pote
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mashahidi wa Yehova wanatumia mashine zaidi ya 70 zinazochapa vitabu kwa mabamba ya mviringo; hii iko Japan