Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Je! ni vibaya kurekodi katika utepe sala zinazotolewa hadharani?
Wakristo fulani wanaona ni afadhali wasifanye hivyo. Lakini Biblia haikatazi watu kuweka kumbukumbu la maneno yaliyosemwa katika sala, kwa kuyaandika au kwa kutumia njia nyingineyo.—2 Nya. 33:18.
Huenda mtu akarekodi mkutano wa Kikristo katika tepu ili akajikumbushe baadaye au ukasikilizwe na wale ambao hawakuweza kuhudhuria. Wakati wa kurekodi mambo kama hayo, Wakristo wengine wanaanza kurekodi baada ya sala ya kufungua na kuacha kurekodi kabla ya sala ya kumalizia.
Huenda wakawa wanawaza kwamba sala si njia rasmi ya kufundisha watu. Bali, sala inafikiriwa kuwa maneno ambayo mtu mwenyewe anamwambia Mungu, ingawa huenda wengine waliopo wakasikiliza na kukubaliana naye kwa kusema “Amin.” Tena, mtu anayerekodi mkutano huo anajua kwamba baadaye hatasema “Amin” anaposikiliza sala aliyorekodi, kama kwamba sala hiyo inakwenda kwa Mungu kila mara anapoufungua utepe wake.
Hata hivyo, inafaa kuangalia kwamba sala nyingi zimeandikwa katika Biblia. (Mwa. 24:10-14; Mt. 26:36-39; Yohana 11:41, 42; 17:1-26; Matendo 4:23-30) Hatuzichukui sala hizo kama kwamba tunatakiwa tuseme “Amin” wakati tunapozisoma.—Rum. 8:26, 27.
Bila shaka, sala hizo ni sehemu ya Biblia; zimeandikwa humo kwa sababu Mungu alitaka ziandikwe. (2 Tim. 3:16) Tena huenda watu wengine wakaiona sala iliyorekodiwa katika utepe kwa njia iliyo tofauti na vile wanavyoiona sala iliyo katika Biblia. Kwa hiyo, ikiwa watu hawakuambiwa wasirekodi sala, Mkristo anaweza kujiamulia kama atazirekodi sala pia anaporekodi mkutano wa Kikristo katika utepe. Kulingana na Maandiko, hakuna ubaya wa kufanya hivyo.