Kupata Kilicho Bora Kuliko Mali
Imesimuliwa na Shozo Mima
Katika mwaka wa 1946 nilirudi Kyoto, Japan, baada ya kutumia miaka minne katika Manchuria na China nikipigana katika Vita ya Pili ya Ulimwengu. Kwa kweli nilikuwa heri—mamilioni wengi hawakurudi.
Huko nyumbani, nchi yetu ilikuwa imeachwa ukiwa. Miji mizima ilikuwa imeangamizwa. Watu walikuwa wamevurugika na walikuwa wakitaabishwa na njaa. Akina mama walikuwa wakionekana wakitafuta-tafuta vipande vya vyakula kwa ajili ya watoto wao waliokuwa wakifa njaa. Hata hivyo, wakati ule ule, sikuzote matajiri waliweza kujinunulia walichohitaji katika “njia za magendo.” Nilikuwa nimekuwa maskini, na sikutaka hata kidogo kuwa maskini tena. Kwa hiyo, lengo langu kubwa maishani likawa kutafuta fedha.
Walakini, kama utakavyoona, nilipata kitu kilichokuwa bora kuliko utajiri wa mali za kimwili.
MAMA yangu alikufa nilipokuwa wa miaka mitatu, nikalewa na nyanya yangu. Tuliishi mashambani karibu na Kyoto mpaka nilipohitimu katika shule ya sekondari nikiwa na miaka 16. Sikupenda sana masomo ya shule, kwa hiyo nikaamua nisaidie baba katika biashara yake iliyokuwa ikiuza vitu vilivyotengenezwa kwa majani makavu, kama vile mifuko, kamba, mikeka, na vinginevyo. Niliendelea kukaa hapo mpaka Japan ilipoingia katika vita ya pili ya ulimwengu. Ndipo katika mwaka wa 1941, nilipokuwa na miaka 20, niliitwa niingie katika jeshi.
Katika siku hizo nilikuwa nikitaka sana kujua kinachompata mtu anapokufa. Wengi wetu sisi vijana tulikuwa tukiwaza sana juu ya mauti, kwa kuwa tulijua kwamba huenda vijana waliokwenda vitani wakauawa. Niliona kwamba ni jambo lisilofaa kabisa kwamba wazee wanajifurahisha maisha, nami nitalazimika kufa katika ujana wangu. Ijapokuwa dini ya Shinto ndiyo iliyoenea pote katika Japan wakati huo, haikuweza hata kidogo kunipa kitu kilichonisaidia kwa kiroho.
Baada ya kurudi kutoka vitani, nilimwoa mke mjane wa ndugu yangu aliyefia vitani kulingana na desturi ya Mashariki. Upesi baada ya hapo aliuawa na ugonjwa wa kifua kikuu. Kwa kufuata desturi nyingine ya Japan, baba yangu alifanya mpango kupitia kwa mpatanishi nioe mke wangu niliye naye sasa, Mitsue.
Nilikuwa na elimu kidogo sana. Nami nilishindwa kujua nifanye nini nijitafutie riziki. Kwa kuwa tulikuwa tumepoteza vitu vyote vya kimwili tulivyokuwa navyo wakati wa vita, jambo lililokuwa la maana sana kwangu lilikuwa kuwa na usalama unaoletwa na fedha. Ndiyo, nilitaka kuwa na fedha nyingi iwezekanavyo. Niliona kwamba kufanya kazi kwa bidii na kuwa na maarifa ndiyo njia ya kupata mafanikio, wala si kuwa na elimu bora. Baada ya muda fulani nilianza biashara mpya ya kusafirisha masanduku ya mboga na matunda kutoka sehemu za mashambani kupeleka sokoni.
Nilifanya kazi kwa nguvu sana mchana na usiku nikijaribu kusitawisha biashara hiyo. Nayo ilianza kufanikiwa, ingawaje sikuwa tajiri kama nilivyokuwa nikitumainia. Ndipo nilipoanza kupatwa na matokeo mabaya ya kazi ngumu niliyokuwa nikijilazimisha kufanya kupita kiasi. Nikawa mgonjwa sana, nikalazwa hospitalini.
Mke wangu alilazimika kunitunza kwa majuma mengi. Nilidhani kwamba ugonjwa wangu hauponyeki, kwamba huenda nikafa. Kwa hiyo nilianza tena kufikiri sana juu ya kifo, na jambo linalompata mtu anapokufa.
JE! DINI INA MAJIBU?
Niligeukia dini ili nipate jibu. Mapema maishani mwangu nilikuwa nikijifunza jambo fulani juu ya madhehebu ya dini ya Buddha ya Shinshu, kwa hiyo sasa nilianza kupendezwa nayo. Imani ya Buddha inafundisha kwamba kuna ulimwengu wa roho zisizoweza kufa, na kwamba kila mtu anayekufa anajiunga na ulimwengu huu wa roho. Inafundisha pia kwamba roho za watu fulani zitateswa katika “moto wa mateso.”
Niliamini hivyo, na kwa hiyo nilikuwa na hakika kwamba wanadamu wana sehemu ya mwili wao isiyoweza kufa ambayo wakati wa kufa inauacha mwili ikaishi katika ulimwengu huo wa roho. Nilitamani kuhakikishiwa kwamba uzima huu wangu wa ndani unaosemekana haungeenda mahali pa mateso, bali ungejifurahisha wakati ujao baada ya kufa. Walakini, mtu yule aliyekuwa akinifundisha juu ya dini ya madhehebu ya Buddha ya Shinshu alikufa, nikakata tamaa sana, kwa kuwa sikuweza kupata majibu niliyotaka.
Hata hivyo bado niliendelea kutafuta njia ya wokovu kwa kuhudhuria mikutano mingine ya dini ya Buddha. Hata nilienda katika makanisa fulani ya Waprotestanti na Wakatoliki. Jambo la kupendeza ni kwamba, niliona kwamba hawa walifundisha sawasawa na walivyofanya Wabuddha, yaani, kwamba mtu anaweza kutumia maisha yake ya wakati ujao ama katika mahali pa mateso ya moto au ajifurahishe wokovu mbinguni, ikitegemea namna ya maisha aliyoishi alipokuwa hapa duniani. Walakini, sikutosheka na majibu hayo. Vilevile, nilipata kuona choyo na pupa ya makanisa haya nikaacha kwenda humo.
Wakati nilipokuwa mgonjwa, Lois Dyer, Mwaustralia mmisionari wa Mashahidi wa Yehova, alinitembelea. Alijitolea ajifunze nasi Biblia kwetu nyumbani, nami nikakubali kwa furaha. Walakini, funzo lilipoendelea, furaha yangu iligeuka ikawa uchungu.
Sana sana hii ilikuwa kwa sababu Biblia ilifundisha kwamba nafsi ya kibinadamu inaweza kufa. Lois alinisomea maandiko kama Ezekieli 18:4, NW, linalosema: “Nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe ndiyo itakayokufa.” Nilikasirika sana niliposikia hivyo, kwa hiyo hata nilijaribu kuacha kujifunza. Vilevile, nyakati nyingine funzo lilionekana likiwa gumu, likinifanya nijiulize hivi: “Kwa sababu gani imempasa mtu ajifunze mambo magumu namna hiyo ili apate wokovu? Je! hakuna njia iliyo nyepesi zaidi?”
Lois alieleza kwamba, kwa sababu ya uongo ambao dini zimefundisha kwa muda wa mamia mengi ya miaka, mawazo mabaya yameimarika sana katika mioyo ya watu. Kwa hiyo, kujifunza kwa uangalifu kunahitajiwa ili mtu aweze kutofautisha kweli na uongo. Pia alisema kwamba kweli peke yake ndiyo itakayoongoza watu kwenye uzima wa milele.
Baada ya maelezo yake, nilianza kuona uhitaji ulioko wa kujifunza kwa uzito ili nijue kweli za Mungu. Andiko hili linalopatikana katika Biblia lilinivutia sana: “Ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha [Yehova], na kupata kumjua Mungu.” (Mit. 2:4, 5) Nikaanza sasa kuifurahia Biblia. Tulipoendelea kuchunguza mafundisho yake, yale tuliyokuwa tukijifunza yalianza kupatana na akili.
Niliweza kuona ni kweli kwamba, wanadamu ndio nafsi, na ya kwamba nafsi inakufa mtu anapokufa. Wafu hawana fahamu. (Mhu. 9:5, 10; Zab. 146:4) Walakini Mwenyezi Mungu ana uwezo wa kuwafufua watu waishi tena, nayo ahadi yake iliyo hakika ni kwamba atafanya hivyo. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Pia Biblia inafundisha waziwazi kwamba dunia hii tunayoishi ndani yake itageuzwa iwe makao mazuri ya kukaliwa na wanadamu wanaomtii Mungu. (Ufu. 21:3, 4) Mafundisho haya ya Biblia yalianza kunivutia sana na kugeuza maisha yangu.
Upesi nikapata nafuu nikaweza kufanya kazi tena nitegemeze biashara yangu iliyokuwa ikiharibika. Lakini maoni yangu juu ya kupata mali za kimwili, na juu ya imani za Kibuddha, yalikuwa yamegeuka. Nilianza kumhubiri kuhani wa Kibuddha mambo niliyokuwa nikijifunza kutoka kwa Biblia. Hiyo ilimkasirisha baba yangu sana akatufukuza tutoke nyumbani mwake. Kwa hiyo tulitengeneza upya mojawapo vyumba vya nyumba yangu ya biashara tukaenda kuishi humo.
KUFUATA LENGO TOFAUTI
Katika siku hizo mahali pa mkutano wa Mashahidi wa Yehova palikuwa umbali wa saa moja kwenda kwa bas. Palikuwa mahali pa watu wote, chumba kidogo cha kukodishwa kilichojengwa katika mtindo wa Kijapan, chenye ukubwa wa kama metres nne kwa saba (futi 13 kwa 23). Watu waliokuwa katika vyumba vile vingine walikuwa wakicheza mchezo wa sataranji wa Kijapan unaoitwa Go, au wakijifunza kutumia chombo kiitwacho abacus, nao walikuwa wakifanya kelele nyingi sana. Nilivutwa sana na unyofu na shauku ya wale waliohudhuria mikutano hiyo, kutia na vijana wengi, waliosikiliza kwa makini sana habari waliyokuwa wakijifunza ijapokuwa kulikuwa na mambo hayo mengi yaliyovuta fikira kwingine.
Sikuzote nitakumbuka Ukumbusho wa mauti ya Kristo niliohudhuria mara ya kwanza katika mwaka wa 1955. Kama ujuavyo, unaitwa “chakula cha Bwana cha jioni” au “Kijio cha Bwana.” (1 Kor. 11:20) Kwa kutokujua ni chakula cha namna gani kingetolewa, nilihudhuria nikiwa pamoja na mwanafunzi mwingine wa Biblia nikivalia suti yangu iliyo nzuri zaidi bila kula chakula cha jioni. Tulipokuwa tukirudi nyumbani sisi wawili, tulikuwa tukiona njaa sana!
Ndipo nilipoanza kuhudhuria makusanyiko ya mzunguko ya Mashahidi wa Yehova ya kila miezi sita iliyokuwa ikichukua muda wa siku mbili au tatu. Nilipokuwa mbali nikihudhuria, nilikuwa nikipatwa na wasiwasi sana juu ya biashara yangu. Walakini ushirika wa furaha pamoja na watu hawa wazuri ulikuwa umekuwa jambo la maana sana kwangu kuliko kutafuta fedha.
Lilionekana kuwa jambo la akili kwamba ikiwa Biblia ilikuwa ndiyo njia ya wokovu, jambo linalofaa peke yake ni kushiriki kweli zake na wengine. Baada ya muda fulani nilifanya maendeleo kiasi cha kusaidia wengine wajifunze Biblia nyumbani mwao. Funzo langu la kwanza nililofanya kwa ukawaida nilijifunza na fundi mpaka rangi. Usiku mmoja uliokuwa na theruji nyingi sana, nilipokuwa nikirudi nyumbani, maswali yalikuja fikirani mwangu: “Kwa sababu gani niwe nikifanya hivi usiku sana namna hii? Kwa sababu gani nisijifurahishe tu wokovu wangu? Najua maana ya kazi hii, lakini kwa sababu gani . . . ?”
Kwa hiyo, nilipokuwa nikijikokoteza juu ya theruji, nilimwomba Yehova juu ya jambo hilo. Ndipo nilipokumbuka yale aliyoniambia yule mmisionari nilipomwuliza juu ya njia nyepesi zaidi ya kupatia wokovu. Alisema: “Mungu ni upendo, nazo choyo na chuki zatoka kwa Ibilisi.” Ndiyo, watu wengi wanafuata njia ya kichoyo ya kutafuta mali za kimwili. Walakini niliweza kuona kwamba kazi hii ya kuhubiri ni jambo lisilokuwa la uchoyo hata kidogo; ni kazi ya Mungu. Kupitia kwayo Yehova anataka kukusanya watu wanaotaka kusikiliza, na kuwazoeza ili wapate wokovu.
Wakati huo nilifahamu zaidi juu ya upendo wa Mungu, na umuhimu wa kazi zetu za upendo. Kabla ya kulala usiku huo nilimshukuru Yehova kwa moyo wote kwa ajili ya ufahamu aliokuwa amenipatia. Jambo hilo nalikumbuka vizuri sana mpaka leo hii.
KUYASHINDA MAGUMU
Nilianza sasa kupingwa na jamaa na watu wa ukoo, pamoja na wale nilioshirikiana nao. Sababu moja kubwa ilikuwa kutoshiriki kwangu katika utendaji ambao mara nyingi unahusiana na mambo ya kidini, kama vile mazishi.
Mke wangu hakupendezwa na mabadiliko niliyofanya, kwa hiyo akaomba talaka, jambo ambalo lilinishtua sana. Walakini, niliweza kumpa sababu za kumwonyesha namna kitendo kama hicho kingekuwa cha upumbavu sana. Baadaye, yeye vilevile alianza kujifunza Biblia. Nilifurahi sana alipoweka maisha yake wakf kwa Yehova akabatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1957.
Sana sana lilikuwa jambo gumu sana kulea wasichana wetu wawili wachanga katika njia ya Ukristo wa kweli, kwa sababu watu wa mtaa wetu wana juhudi sana katika sikukuu za dini zisizo za Kikristo ambazo zinavutia watoto sana. Nilijaribu kufundisha binti zetu sababu gani sikukuu na mazoea fulani hayampendezi Mungu. Tulikuwa tukijikumbusha pamoja nao mambo tuliyokuwa tumejifunza mikutanoni yetu ya Kikristo tulipokuwa tukirudi nyumbani, na mara nyingi niliwapongeza ikiwa waliyakumbuka vizuri. Jambo hili liliwatia moyo wawe wakisikiliza. Vilevile, mimi na mke wangu tulijiangalia sana tuishi maisha yanayopatana na mafundisho yetu, na ‘kuwekea watoto mfano mwema sikuzote.
MAISHA BORA ZAIDI NA YENYE FURAHA
Katika mwaka wa 1957, katika kusanyiko lililokuwako Osaka, ilitangazwa kwamba wamisionari waliokuwa Kyoto wangeondoka kwenda katika migawo mingine. Wakati wa kusanyiko hilo kuhitajiwa kwa wahubiri “mapainia” wa wakati wote kulizungumzwa. Kwa hiyo nilianza kufikiria kama naweza kuwa painia kwa kupanga wakati wangu kwa hekima.
Tuliporudi nyumbani, nilijaribu kufanya upainia kwa muda, nikifanya kazi kwa muda tu katika biashara yangu. Kisha nikaajiri mtu wa kuangalia biashara yangu nilipokuwa nje katika kazi ya kuhubiri. Baada ya mwaka mzima biashara yangu ilikuwa ikiendelea vizuri. Hivyo, nikaanza upainia wa kawaida. Baadaye, katika mwaka wa 1964, niliamua kuuza biashara hiyo. Kwa kutumia fedha zilizotokana na kuuza biashara hiyo, na kwa kufanya kazi kwa muda tu katika kampuni ya kuzalisha na kufuga samaki, nimeweza kuruzuku jamaa yangu na kuendelea katika kazi ya upainia mpaka hivi leo.
Nimepata faida nyingi sana kwa kufuata shauri la Yesu la ‘kuacha kujiwekea hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali tujiwekee hazina mbinguni.’ (Mt. 6:19, 20) Mojawapo baraka hizo ni kujengwa kwa Jumba la Ufalme katika mwaka 1965 katika uwanja wangu.
Nilipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova walikuwako wahubiri wa Ufalme 10 katika Kyoto waliokuwa wakikutana katika chumba hicho kidogo walichokodisha. Lakini sasa kuna makundi tisa yanayositawi, yakiwa na zaidi ya wahubiri 700 na mapainia 96 katika Kyoto! Na kuna Majumba ya Ufalme 6 mazuri sana. Mimi mwenyewe nimeshuhudia na kushiriki katika ukuzi huu wote wa ibada ya Yehova katika muda wa miaka 23 iliyopita.
Jambo lenye kuthawabisha ambalo sitasahau hata kidogo lilikuwa kuhudhuria kusanyiko la mataifa yote la 1958 katika Yankee Stadium na Polo Grounds katika mji wa New York. Kwa kuwaona watu kama 180,000 waliohudhuria katika siku ya kwanza, nilipata kufahamu kwamba bila shaka Yehova Mungu anawakusanya watu wa lugha zote na wa mataifa yote wawe waabudu wake wa kweli.
Hasa nimefurahia sana kutazama ukuzi wa kiroho wa wale ambao nimejifunza nao Biblia. Wengine wao wanatumikia sasa kama mapainia, nao wanawasaidia wengine wajifunze njia ya wokovu. Mke wangu ameshirikiana nami kwa uaminifu miaka hii yote, nasi tunajifurahisha kazi ya kuhubiri kwa ukawaida tukiwa pamoja. Sasa binti zetu wawili wamekwisha olewa, nao wameshiriki kikamilifu katika utumishi wa upainia.
Ninapokumbuka wakati ambapo lengo langu kubwa maishani lilikuwa kupata utajiri wa mali ya kimwili, siwezi kulinganisha na furaha ambayo nimepata tangu nilipobadili lengo langu. Kwa kweli hakuna kitu kinachoweza kulinganishwa na uradhi na kutosheka kunakotokana na kutumia maisha ya mtu katika utumishi wa Muumba wetu Mkuu.
[Picha katika ukurasa wa 4]