Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Yesu alikuwa na maana gani aliposema kwamba mtu hakati kiraka cha vazi jipya na kukitia katika vazi kuukuu au kuweka divai mpya katika viriba (chupa za ngozi) vikuukuu (vya zamani)?
Kwa msingi, yeye alikuwa akimaanisha kwamba Ukristo haungepatana, na kwa kweli haukuweza kupatanishwa na dini ya Kiyahudi ya wakati wake pamoja na mapokeo yake ya wanadamu yaliyokuwa yamesitawishwa.
Kulingana na habari ya Marko Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu ashonaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; ikiwa ashona, kile kipya kilichotiwa huliharibu lile vazi kuukuu, na pale palipotatuka huzidi. Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; ikiwa atia, ile divai mpya itavipasua viriba vile, divai ikamwagika, vile viriba vikaharibika. Bali hutia divai mpya katika viriba vipya.”—Marko 2:21, 22; Mt. 9:16, 17; Luka 5:36-39.
Yesu alikuwa ndipo anaulizwa sababu gani wanafunzi wake hawafungi kama walivyokuwa wakifanya viongozi wa dini, Mafarisayo. Kristo alijibu kwamba, alipokuwa na wafuasi wake, kufunga kama ishara ya kuomboleza hakungefaa. Ndipo aliposema hayo yaliyoandikwa hapo juu.
Mifano yake ilifaa sana. Ukishona kiraka kipya katika nguo kuukuu, hicho kiraka kipya kitapunguka na kupasuka wakati wa kusafisha vazi hilo. Au, ukiweka divai mpya katika viriba vikuukuu ambavyo vimepoteza hali yavyo ya kunyumbuka, viriba hivyo vitapasuka wakati hiyo divai mpya inapochachuka na kutokeza hewa ya carbon dioxide.
Kwa njia hiyo Yesu aliwasaidia wasikilizaji wake wajue kwamba hakuna anayepaswa kutazamia kwamba wafuasi wake wangefuata mazoea ya zamani ya dini ya Kiyahudi, kama vile desturi ya kufunga. Vilevile, mafundisho yake mapya yenye nguvu hayangepatana kwa kufaa na taratibu ya kidini ya Kiyahudi. Badala yake, wale waliomsikiliza wakamfuata Yesu wangefurahia maana kubwa ya mafundisho yake bila kujaribu kuyapatanisha na njia za Kifarisayo za viongozi wa Kiyahudi.