Viumbe Vyautangaza Utukufu wa Mungu
“Lakini nasema, Je! wao hawakusikia? Naam, wamesikia, sauti yao imeenea duniani mwote, Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.”—Rum. 10:18.
BILA sauti na bila kusema ama maneno, kazi za Yehova za kuumba zinatangaza utukufu wake. Zaburi 19:1-4 inashuhudia jambo hili hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, Na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa. Hakuna lugha wala maneno, sauti yao haisikilikani. Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.” Ni kweli mbingu zenye nyota zinautangaza utukufu wa Mungu.
Lakini viumbe vyake hapa duniani vinatangaza hekima na uweza wake: “Ee [Yehova] jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako. Bahari iko kule, kubwa na upana, ndimo mlimo viendavyo visivyohesabika, viumbe hai vidogo kwa vikubwa.” (Zab. 104:24, 25) Wanadamu wavumbuzi wanaona hekima hii ya kimungu na wanaiga samaki wanaotoa nguvu za umeme, na namna ya manyingu yanayotengeneza karatasi, kobe wa baharini wanaotoa maji ya kuambatanishia karatasi au wambiso, shakwe wanaoondolea maji ya bahari chumvi, nyuki wanaogeuza hali ya hewa katika makao yao iwe baridi au moto, pweza wanaotumia nguvu za kusukuma mbele, popo wanaovuma sana—na hesabu hiyo inaweza kuendelea sana.
Mtume Paulo alitaja viumbe kama vikitangaza utukufu wa Mungu: “Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru.” (Rum. 1:20) Watu wasioamini kuwako kwa Mungu hawawezi kuwa na udhuru (sababu). Watu wote wanaokataa kukubali kuwako kwa Muumba mwenye nguvu zote, uwezo wote, hawana sababu ya kutoamini. Ushuhuda uko kila mahali kutuzunguka, usiku na mchana. Bila kusema ama kutoa sauti ama kutamka maneno, kuhubiri huku kunaendelea. Walakini Paulo anataja kuhubiri ambako kunatoa usemi na maneno na sauti. Alifananisha kuhubiri huku katika dunia yote na kule kwa ulimwengu wote kunakofanywa na mbingu zenye nyota.
Paulo anataja maneno yaliyoko katika Yoeli 2:32 wakati anapotaja “Kila atakayeliitia Jina la [Yehova] ataokoka,” halafu akaendelea kusema: “Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wahubirije, wasipopelekwa?” (Rum. 10:13-15) Baada ya kukazia uhitaji wa kutumwa kwa wanadamu wahubiri, ili watu waweze kuliitia jina la Yehova na kuokolewa, Paulo anasema: “Lakini nasema, Je! wao hawakusikia? Naam, wamesikia sauti yao imeenea duniani mwote,” Hapa Paulo anataja maneno yaliyo katika Zaburi 19:4, juu ya ushuhuda unaoenea duniani pote wa uumbaji wa Yehova uonekanao katika mbingu zilizo juu.—Rum. 10:18.
Ni kweli kwamba hata bila kuwa na wahubiri wa kibinadamu, jamii ya kibinadamu haijakosa kusikia habari za ukuu wa Yehova Mungu. Kazi zake zionekanazo zinashuhudia jambo hilo. Mtunga zaburi na mtume Paulo wanatujulisha jambo hili. Katika Warumi sura ya 10 inaonekana kwamba Paulo anasema “habari njema” juu ya Kristo zilisikiwa na wengi waliohubiriwa, kama vile mahubiri ya uumbaji unaoonekana yanavyoenea duniani mwote. “Je! wao hawakusikia?” “Je! Waisraeli hawakufahamu?” Musa alisema kwamba Waisraeli wangepatwa na wivu kwa kuona Mataifa wakijiunga nao katika ibada ya Yehova. Isaya naye alitabiri mapema kwamba Mataifa wangemwendea Yeye lakini Waisraeli wakaidi wangekataa mwaliko Wake. (Rum. 10:18-21; Kum. 32:21; Isa. 65:1, 2) Waisraeli wa asili katika siku za Paulo walikuwa wamepelekewa wahubiri wa habari njema za Kristo, si Wayahudi katika Palestina peke yao, lakini pia wale waliokuwa wametawanyika katika sehemu nyingi. Kama vile mbingu zionekanazo zilivyohubiri kwa wale wote waliokuwa duniani, ndivyo wahubiri wanadamu walivyotangaza Habari Njema kwanza kwa Wayahudi na baadaye kwa Mataifa mengine.
Mbingu zenye nyota nyingi, pamoja na uumbaji mwingine wote, unaonyesha hekima ya Yehova kadiri fulani, lakini hekima hiyo peke yake inayoonyeshwa haitoi uzima. Kazi zake zinatangaza uwezo wake mkuu na ukuu wake, ujuzi wake wa kubuni namna nyingi za vitu. Lakini hata kama tungeweza kufahamu vitu vingi vya ajabu alivyoviumba, bado hili halingetupa hekima na uwezo unaohitajiwa kupata uzima wa milele. Kinachohitajiwa ni hekima iliyo tofauti na uwezo ulio tofauti. Linalohitajiwa ni “Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.” Mbingu zisizosema, zisizotoa maneno wala sauti, zote pamoja zinatangaza tu utukufu wa Mungu, “lakini sisi tunamhubiri Kristo [aliyetundikwa juu ya mti].” “Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.” Jinsi Wayahudi na Wagiriki walivyokuona kuhubiri habari njema za “Kristo [aliyetundikwa juu ya mti]” katika siku za Paulo ndilo jambo kuu litakalozungumzwa katika makala mbili zifuatazo.—1 Kor. 1:22-24; Matendo 4:12.
[Blabu katika ukurasa wa 3]
“Lakini Sisi Tunamhubiri Kristo (Aliyetundikwa Juu ya Mti)”