“Wahudumu wa Mungu Wetu” Wapainia Katika Kazi ya Maana Sana ya Kutengeneza Upya
“Na wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu. Bali ninyi mtaitwa makuhani wa [Yehova]; watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu.”—Isa. 61:5, 6.
1. Wahudumu wa Serikali wanajitahidi sana leo wafanye nini, wakiwa na hali gani akilini mwao?
WAHUDUMU wa Serikali walishiriki katika kazi kubwa sana ya kutengeneza upya iliyosababishwa na Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Mengi ya mambo waliyoshiriki kuyatengeneza yaliharibiwa tena na vita iliyokuwa yenye kuleta msiba zaidi ya 1939-1945. Kukawa na lazima tena ya kufanya kazi ya kutengeneza upya, lakini iliyokuwa kubwa hata zaidi. Leo wahudumu wa watu wote wanajitahidi sana ili wazuie mambo yasikae katika hali ya kuharibika. Wahudumu wa serikali wanaona wasiwasi sana.
2, 3. (a) Ni kazi gani ya kutengeneza upya ya maana zaidi ya namna nyingine ambayo imepata maendeleo hata kuweko Vita ya Pili ya Ulimwengu? (b) Ilitabiriwa katika lugha gani yenye kueleza katika Isaya 61:4-6?
2 Walakini, kazi ya kutengeneza upya yenye maana zaidi ya namna nyingine ilianza katika mwaka uliofuata kumalizika kwa vita, 1919. Hata kukiwa na uharibifu mkubwa wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, kazi hiyo iliendelea mbele bila kushindwa. Ilikuwa kazi ya kutengeneza upya ya namna ya kiroho, iliyosaidiwa na nguvu ambayo idara za serikali za kibinadamu hazikuwa nayo. Ni kweli kwamba, kulingana na yaliyoandikwa katika Warumi 13:4, mamlaka zilizo kuu za ulimwengu huu zinatumikia kama watumishi wa Mungu kwa watu wote hata kuwafaidi Wakristo. Lakini hao waliopainia katika kazi ya kutengeneza upya ya namna ya kiroho wamekuwa watumishi wa Mungu kwa watu wote wenye cheo cha juu zaidi. Kazi ya painia iliyofanywa na wahudumu hawa ilitabiriwa na Isaya, nabii aliyeongozwa na Mungu kama inavyofuata:
3 “Nao watajenga mahali pa kale palipoharibiwa, watapainua mahali palipokuwa ukiwa zamani, watatengeneza miji iliyoharibiwa, mahali palipoachwa kizazi baada ya kizazi. Na wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu. Bali ninyi mtaitwa makuhani wa [Yehova]; watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu; mtakula utajiri wa mataifa.”—Isa. 61:4-6.
4. Unabii wa Isaya ungetimia katika wakati gani wa mabadiliko, naye Yesu Kristo alionyesha hili namna gani na wapi?
4 Yesu Kristo mfanya kazi ya kutengeneza upya wa karne ya kwanza alionyesha ni wakati gani maneno hayo yangeanza kutimizwa. Wakati huo ungekuwa wakati ambapo taifa lililokuwapo kwa muda wa karne nyingi lingekuwa likivunjika-vunjika na taifa jingine jipya na bora lingekuwa linakaribia kuanzishwa. Taifa hilo jipya lingekuwa na washiriki ambao wangekuwa wanafunzi wa Yesu Kristo, waliozaliwa kwa roho ya Mungu. Lingekuwa taifa la Israeli wa kiroho. Lakini Yesu alionyeshaje wakati wa kutimizwa kwa unabii huo wa Isaya unaotajwa hapo juu? Alifanya hivyo alipotaja maneno yanayotangulia unabii huu akayatumia juu yake mwenyewe. Wakati huo Yesu alikuwa akitembelea sinagogi katika mji wa kwao, Nazareti, wakati fulani baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 30 W.K. Alisimama asome. Alikunjua kitabu cha kukunja cha unabii wa Isaya mahali sasa inapopatikana sura ya 61 akasoma sehemu ya maneno ambayo sasa ni mstari wa kwanza na wa pili. Ndipo alipowaambia wasikilizaji wake: “Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu.”—Luka 4:16-21.
5, 6. (a) Mwanahistoria Luka aliyeandika katika Kigiriki aliandika maneno ya Yesu kutoka Isaya yasomeke kulingana na tafsiri gani? (b) Isaya 61:1-3 yanasomwaje katika maandishi ya kale ya Kiebrania?
5 Luka, mwanahistoria aliyeandika habari hii, aliandika maneno yaliyotajwa na Yesu kutoka katika unabii wa Isaya yasomeke kama yalivyoandikwa katika tafsiri ya Kigiriki inayojulikana kama Septuagint Version. Lakini unabii huo unasomwaje katika maandishi ya Kiebrania cha asili, ambayo bila shaka ndiyo Yesu akiwa Myahudi wa Palestina aliyosoma? Hivi:
6 “Roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Yote i juu yangu, kwa sababu Yehova amenitia mafuta nisimulie habari njema kwa wapole. Yeye amenituma mimi kuganga waliovunjika moyo, kutangaza uhuru kwa wale waliochukuliwa mateka na kufunguliwa wazi kwa macho hata kwa wafungwa; kutangaza mwaka wa nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu; kufariji wote waombolezao; na kuwapa migawo wale wanaoombolezea Sayuni, na kuwapa vazi la kichwa badala ya majivu, mafuta ya shangwe badala ya kuomboleza, vazi la sifa badala ya roho ya kushuka moyo; nao wataitwa miti mikubwa ya haki, iliyopandwa na Yehova, ili [yeye] apate uzuri.”—Isa. 61:1-3, NW.
7. Ni maneno gani ya kazi ya kutengeneza upya yanayofuata?
7 Ndipo yanapofuata maneno kuhusu kazi ya kutengeneza upya: “Nao watajenga mahali pa kale palipoharibiwa, watapainua mahali palipokuwa ukiwa zamani, watatengeneza miji iliyoharibiwa, mahali palipoachwa kizazi baada ya kizazi.”—Isa. 61:4.
8. Katika wakati wa kutimizwa kwa unabii huu, kungekuwa na watu wenye hali za moyoni za namna gani, na ni kwa sababu gani kuwaangalia kungekuwa jambo la muhimu sana?
8 Na tuangalie kwamba katika wakati wa kutimizwa kwa unabii wa Isaya kungekuwako “wapole,” “waliovunjika moyo,” “wale waliochukuliwa mateka,” na “wafungwa” pia na “wale wanaoombolezea Sayuni.” Hawa wangehitaji kuangaliwa inavyofaa kwa haraka sana. Wakati ungekuwa umefika wa jambo hili, kwa kuwa kilikuwa kipindi cha wakati kinachoitwa “mwaka wa nia njema upande wa Yehova.” Kufika kwake yule aliyetiwa mafuta kwa “roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Yote” kungeanzisha mwaka huo wa nia njema Yake. “Mwaka” huo wa mfano ungefuatwa na “siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.” Hii ilifanya kazi ya Yesu mtangazaji wa ukombozi na uhuru aliyetiwa mafuta kwa roho iwe kazi ya haraka sana.
9. Wasikilizaji wa Nazareti walitangaziwa badiliko gani na Yesu, nao walijionyeshaje kwamba hawakuwa “wapole” vya kutosha kuzikubali “habari njema”?
9 Yesu alikuwa amebadili kazi yake ya kidunia. Mpaka alipofikia umri wa miaka 30 alikuwa amekuwa seremala katika Nazareti, Galilaya. Ndipo palipokuwa na sinagogi ambalo katika hilo Yesu alisoma maneno ya maana sana ya unabii wa Isaya. Kubadilika huku kwa kazi yake alikutangazia wasikilizaji wake Wanazareti alipomaliza kusoma Isaya 61:1, 2 akasema: “Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu.” Ndipo alipoonyesha uhakika huu kwa kutoa hotuba kutoka kwa Biblia ambayo wananchi wenzake hawakudhani kwamba mtu huyu aliyekuwa seremala hapo kwanza angeweza kuitoa. Walikuwa wamesikia kwamba Yesu alikuwa amekuwa tatibu (mganga). Kwa hiyo, walitaka ‘ajiponye’ kwa kuponya katika ‘nchi yake mwenyewe’ aponye watu wa mji wa kwao. Kwa kutumia mifano ya Biblia Yesu alieleza sababu hangefanya hivyo. Walikasirika sana kwa kusikia hayo wakajaribu kumwua. Walijionyesha kwa nguvu sana kwamba wao hawakuwa watu “wapole” kiasi cha kukubali “habari njema.”—Luka 16:21-30.
10. Yesu alikuwa ametiwa mafuta kwa roho takatifu wakati gani?
10 Ajapotendwa hivyo katika mji wake mwenyewe, Yesu alisonga mbele atimize kusudi la kutiwa kwake mafuta kwa “roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Yote.” Katika vuli wa mwaka 29 W.K., alikuwa ametoka Nazareti kwenda katika Mto Yordani akabatizwe na Yohana mwana wa kuhani Zekaria. Baada tu ya Yesu kutoka katika maji ya ubatizo Yohana Mbatizaji aliiona roho takatifu ikishuka juu yake ikiwa katika mfano wa hua. Wakati uo huo alisikia sauti ya Yehova kutoka mbinguni ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mt. 3:13-17; Luka 3:21, 22; Yohana 1:29-34) Roho iyo hiyo ilimsukuma Yesu akakae katika jangwa la Uyahudi kwa muda wa siku 40.
11. Ni kwa sababu gani bado Yesu alikuwa na roho aliyokuwa ametiwa mafuta kwayo alipotoa hotuba yake katika sinagogi katika Nazareti?
11 Baada ya siku hizo 40 za kufunga kula na kuzungumza na Baba yake Yehova, Shetani Ibilisi aliweka mbele ya Yesu majaribu matatu. Kama Yesu angeshindwa na majaribu hayo matatu, angalipoteza roho aliyokuwa ametiwa mafuta kwayo. Lakini, kwa kumpinga Mjaribu huyo, yeye aliendelea kuwa aliyetiwa mafuta kwa roho. Kwa hiyo, alipotoa hotuba yake katika sinagogi la Nazareti bado alikuwa nayo.—Mt. 4:1-13; Luka 4:1-21.
12. Kwa sababu ya yale yaliyotukia katika nchi ya Wayahudi katika mwaka 537 K.W.K., ni maswali gani yanayotokea kuhusu Wayahudi katika wakati wa Yesu kutiwa mafuta?
12 Yesu alipotiwa mafuta kwa roho takatifu katika mwaka 29 W.K., ilikuwa imepita miaka 565 tangu watu wa Yesu wafunguliwe kutoka utumwa wa Babeli katika mwaka wa 537 K.W.K. wakarejea katika nchi yao iliyokuwa imeachwa ukiwa, mkoa wa Uyahudi. Walikuwa ‘wametengeneza upya miji iliyoharibiwa’ ya nchi hiyo, kutia na Yerusalemu, ambao hekalu lake walijenga upya. Walikuwa ‘wameinua mahali palipoharibiwa’ wakati wa miaka 70 iliyotangulia ya kuachwa ukiwa wakaigeuza nchi ikawa kama paradiso. Katika sikukuu tatu za kila mwaka katika Sayuni ya Wayahudi, au Yerusalemu, ulijaa waabudu milioni nyingi. Kwa sababu gani, basi, kuwe na Wayahudi au Waisraeli waliovunjika moyo wakati Yesu alipotiwa mafuta? Sababu gani kuwe “waliochukuliwa mateka”? Sababu gani kuwe “wafungwa”? Sababu gani kuwe “wanaoombolezea Sayuni”? Sababu gani kuwe maskini wanyenyekevu, “wapole” wanaohitaji “habari njema”? Kwa sababu gani kuwe na watu wa namna hiyo katika mwaka 29 W.K.?
WALE WANAOHITAJI “HABARI NJEMA,” KUWEKWA HURU NA FARAJA
13. “Wafungwa” Wayahudi walikuja chini ya utumwa wa namna gani waliporudi kwao baada ya kufunguliwa kutoka Babeli?
13 Sababu ilikuwa hali ya kiroho ambayo ilikuwa imelipata taifa la Israeli. Ni kweli kwamba Yehova alikuwa ameleta “siku ya kisasi” juu ya Milki ya Kibabeli, ambayo watawala wake walikuwa wamekataa ‘kufungulia wafungwa njia waende kwao.’ (Isa. 14:17; Yer. 50:15, 28; 51:6, 11, 36) Waliporudishwa katika nchi yao baada ya hapo, “wafungwa” hao Wayahudi hawakuja chini ya utumwa wa ibada ya sanamu wakiabudu sanamu halisi za kuchongwa. Hata hivyo walikuja chini ya utumwa mkubwa hata zaidi, ule wa taratibu ya kidini ya Kiyahudi. Hii ilikuwa taratibu iliyoongozwa na mawazo na mapokeo ya wanadamu, mambo yaliyoihalifu Torati pamoja na amri za Yehova Mungu. Waandishi wa serikali na Mafarisayo wakawa wakuu katika taratibu hii ya kidini. Waliwapofusha watu wasiione kweli kwa kuondoa “ufunguo wa maarifa,” na kuwazuia wasiingie katika ufalme wa Mungu, wakiwawekelea watu wa kawaida mizigo mizito ambayo wao wenyewe hawangegusa.—Luka 11:52.
14. Ni kwa sababu gani kulikuwa na sababu ya mabaki Wayahudi “kuombolezea Sayuni” katika siku za Yesu?
14 Zaidi ya hayo, wakuu hao wa dini ya Kiyahudi, wakiwa viongozi vipofu, waliwaongoza Wayahudi waliopofushwa katika njia inayomalizikia katika kuharibiwa kwa taifa. Waliongoza Sayuni, au Yerusalemu, umkatae Masihi wa kweli, Yesu, na kumfanya auawe juu ya mti wa mateso kana kwamba alikuwa Kristo wa uongo. Viongozi hao wa kidini waliufanya Yerusalemu uendelee kuwa mwuaji wa manabii na mpiga mawe wale wanaotumwa kwake na Mungu. (Mt. 23:1-37) Kwa hiyo, je! wale “wapole” wa taifa kama hilo hawakuhitaji kuelezwa “habari njema”? Je! kulikuwako wale “waliochukuliwa mateka” waliohitaji kutangaziwa uhuru? Je! kulikuwako “wafungwa” waliohitaji “kufunguliwa wazi kwa macho” yao kwa kuwatoa katika giza la kidini? Je! Sayuni, au Yerusalemu, uliokuwa mahali pa kati pa ibada ya Yehova ulikuwa katika hali iliyoharibika sana ya kidini hivi kwamba kulikuwa na sababu ya kweli ya kuuombolezea? Ndiyo, hakika! Naye Yesu aliyetiwa mafuta alipata kuona kwamba kulikuwako na mabaki ya hao waliokuwa “wakiomboleza” kati ya Wayahudi.
15. Yohana Mbatizaji alitumikia kama painia katika njia gani, naye alikuwaje painia wa uzima na wokovu?
15 Yesu alitosheleza mahitaji ya hao waliokuwa wakiomboleza, hao “waliochukuliwa mateka,” hao “wafungwa,” hao maskini “wapole.” Aliwafariji hao waliokuwa wakiomboleza kwa kuhubiri habari njema za “ufalme wa mbinguni,” licha ya kuwaponya wagonjwa na hata kuwafufua wafu. (Mt. 4:17; 11:4-6) Walakini hata faraja na uhuru zaidi ulikuwa mbele ya hao waliokuwa wakiombolezea Sayuni. Uliletwa na kifo na kufufuka kwake Yesu na kupaa mbinguni akamtolee Mungu ubora wa dhabihu yake yenye kufunika dhambi. Kwa kutimiza hivyo unabii wa Biblia uliomhusu yeye, Yesu Kristo akawa painia wa uzima na wokovu kwa wale waliokubali huduma yake yenye kutoa uzima. Yohana Mbatizaji alikuwa amemtangulia Masihi wa Yehova na alikuwa ametayarisha njia, kwa hiyo Yohana pia angeweza kuitwa painia. (Luka 1:76, Tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya New World, 1950) Walakini, Yesu alifanya mengi zaidi ya Yohana ili apainie (atangulize) njia ya uzima na wokovu.
16. Kulingana na tafsiri ya Moffat ya Matendo 3:15, Petro alimwitaje Yesu katika hekalu katika Yerusalemu?
16 Ilikuwa kama Petro alivyowaambia Wayahudi kwa ujasiri katika hekalu la Yerusalemu majuma machache baada ya Yesu kupaa mbinguni: “Ninyi mlimwua painia [“wakili,” UV] wa Uzima. Lakini Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, kama sisi [Petro na Yohana] tunavyoweza kushuhudia.”—Matendo 3:15, Moffat.
17. Kulingana na Matendo 5:31 wale mitume 12 walimwitaje Yesu wakiwa mbele ya Mahakama Kuu ya Yerusalemu?
17 Baadaye, wale mitume 12 wa Yesu Kristo walishuhudia hivi mbele ya Mahakama Kuu yenye hatia ya damu katika Yerusalemu, ambayo wakati huo washiriki wake walikuwa Masadukayo, Mafarisayo na waandishi: “Mungu alimpandisha katika mkono wake wa kuume awe painia [Kigiriki: arkhegos] na mwokozi wetu, ili awape Israeli toba na msamaha wa dhambi.”—Matendo 5:31, Mo.
18, 19. Mtume Paulo alimwitaje Yesu katika Waebrania 2:10 na 12:2?
18 Alipokuwa akiwaandikia mabaki Waebrania (Wayahudi) waliomkubali Yesu kuwa Masihi, au Kristo, wakawa wana wa Mungu wa kiroho, mtume Mwebrania Paulo alisema hivi: “Kwa kuwa ilifaa kwamba yeye, ambaye kwa ajili yake na kwa njia yake vitu vyote viko, katika kuwaleta wana wengi katika utukufu, ilimpasa kumkamilisha painia [arkhegos] wa wokovu wao kwa njia ya mateso.”—Ebr. 2:10, Revised Standard Version; pia Moffat.
19 Pia: “Tukimtazama Yesu, painia [arkhegos] na mkamilishaji wa imani yetu, ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba, na kuidharau aibu, naye ameketi katika mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu.”—Ebr. 12:2, RS; Mo.
20. Ni katika njia gani Yesu akawa “painia . . . wa imani yetu?” na mwenye kuikamilisha?
20 Hivyo Yesu ametangazwa kuwa “painia” kwa ajili ya wanafunzi wake, painia wa uzima, painia wa wokovu, painia wa imani yetu. Alitimiza mamia mengi ya unabii wa Biblia uliohusu Masihi, au Kristo. Katika njia hii alianzisha jambo jipya na lenye maana sana katika imani yetu katika Yehova Mungu. Kwa hiyo akawa painia (mwanzilishi) wa imani iliyo kamili ambayo Wakristo wa kweli wanayo sasa. Hivyo, basi, anaitwa kwa kufaa “painia . . . wa imani yetu.” (Ebr. 12:2, RS; Gal. 3:24, 25) Wakati uo huo imani yetu kuhusu Masihi wa Yehova inatimizwa katika Yesu Kristo. Imani ya Wayahudi waliomkataa Yesu Kristo wakaendelea kuishika torati ya Musa ndiyo peke yake iliyoachwa bila kukamilika.
“MITI MIKUBWA YA HAKI”
21. Kama matokeo ya Yesu kuwatokea wanafunzi wake baada ya kufufuka kwake na kuwafariji, wangepata ukuzi wa kiroho kadiri gani?
21 Katika muda wa siku 40 baada ya kufufuka kwake Yesu Kristo aliwatokea wanafunzi wake mara nyingi ili aijenge imani yao. Alifariji wale waliokuwa wakiombolezea Masihi aliyetumainiwa. Ilikuwaje kwa wale waliofarijiwa na Yesu Kristo aliyefufuliwa? Kulingana na unabii wa Isaya 61:1-3, NW, Yesu aliyetiwa mafuta alipaswa “kuwapa vazi la kichwa badala ya majivu, mafuta ya shangwe badala ya kuomboleza, vazi la sifa badala ya roho ya kushuka moyo.” Kwa sababu hii wangepata ukuzi wa kiroho hivi kwamba wangeitwa “miti mikubwa ya haki, iliyopandwa na Yehova, ili yeye apate uzuri.”
22. Maneno haya “vazi la kichwa,” “majivu,” “mafuta,” na ‘“vazi” katika unabii wa Isaya yalipaswa kufahamikaje, na yalilinganaje na hali ya wanafunzi kuanzia na Pentekoste na kuendelea?
22 Kwamba ye yote wa mitume au wanafunzi wa Yesu alikuwa amejipaka majivu katika kichwa chake na kuvaa magunia hatuambiwi. Kwa wazi usemi wa kinabii “vazi la kichwa,” “majivu,” “mafuta,” na “vazi” ulikuwa unatumiwa kwa mfano. Bila shaka kuonekana kwake Yesu baada ya kufufuka kwake kulibadili maoni ya wanafunzi wake juu ya jambo hilo. Ah, ndiyo, walakini katika siku ya Pentekoste iliyofuata, Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu alimtumia Mwanawe Yesu Kristo aimimine roho takatifu juu ya wanafunzi waliokuwa wakingojea katika Yerusalemu. Ndimi za moto za mwujiza zilikaa juu ya vichwa vyao, katika kuonyesha roho hiyo iliyomwagwa. Wonyesho huo ulikuwa wa muda tu, wala haukuwa “vazi la kichwa” la kudumu (kuendelea) lililotabiriwa katika unabii wa Isaya. Mahali pake, vichwa vyao vilivalishwa taji ya furaha ya kuwa na kibali ya Mungu, kama furaha ya bwana-arusi kuhani katika siku ya arusi yake. (Isa. 61:10) Ilikuwa kama kwamba vichwa vyao vilikuwa vimepakwa mafuta yenye kutuliza, yakiwaburudisha mpaka wakashangilia. Roho ya moyo uliovunjika ilitoweka, nazo sifa za Yehova Mungu zikawatambulisha kama kwamba zilikuwa “vazi la sifa.” Watazamaji wa jambo hilo lenye kutokeza la siku ya Pentekoste walisema: “Twawasikia hawa wote wakisema kwa lugha zetu matendo makuu ya Mungu.”—Matendo 2:11.
23. (a) Yesu alipainia katika kazi ya namna gani kwa ajili ya wanafunzi wake? (b) Kwa kutiwa mafuta kupitia kwake, wanafunzi waliagizwa kufanya nini?
23 Sisi leo tunaona nini kutokana na haya yote? Uhakika huu, kwamba kulingana na kutiwa mafuta kwake, Yesu Kristo alipainia katika kazi ya kutengeneza upya wale wakawa wanafunzi wake. Yehova alimtumia amimine roho takatifu juu ya wanafunzi wake waliobatizwa, ili kwamba hao walioipokea roho takatifu walikuwa watu waliotiwa mafuta kwa roho ya Bwana Yehova Mungu Mwenye Enzi Kuu. (2 Kor. 1:21; 1 Yohana 2:20, 27) Sasa wao vilevile waliagizwa wahubiri “habari njema” kwa “wapole” katika taifa la Israeli, kutangaza uhuru kwa wale waliochukuliwa mateka na kufunguliwa kwa wafungwa, na kufariji wale wote waliokuwa wakiombolezea Sayuni. Katika njia hii wangewasaidia wale waliokuwa wakifariji na kutangazia uhuru washangilie “mwaka wa nia njema upande wa Yehova” na kumsifu kwa kuwarudisha katika kibali yake na katika utumishi wake kupitia kwa watiwa mafuta wake.
24. Kuanzia Pentekoste na kuendelea, hali ya kiroho ya wanafunzi wa Yesu ilikuwa imepambwaje ‘kama vile Paradiso ilivyokuwa imepambwa, nani apate uzuri?
24 Roho hiyo iliyomiminwa ilifanya mabadiliko makubwa sana katika wale waliotiwa mafuta kwayo. Mahali pa kuwa mimea dhaifu inayofifia kwa kukosa chakula kizuri cha kuitia nguvu, wakawa kama “miti mikubwa ya haki” ambayo ni Yehova peke yake angeweza kuipanda na kuifanya ikue kupitia kwake Kristo. “Paradiso ya Furaha” ya kwanza ya wanadamu ilikuwa imepambwa kwa miti ya namna nyingi. (Mwa. 2:7-9) Walakini kuanzia na Pentekoste na kuendelea Yehova alipanda “miti mikubwa” katika nchi ya kiroho ya watu wake walio wakf ambayo ilikuwa imeharibiwa na kuachwa ukiwa na adui zao. “Miti mikubwa” hiyo ya mfano walikuwa ni wale Wakristo imara, wenye nguvu, wasiotikisika waliojiinua juu kwa ajili ya haki ya Yehova Mungu. Yeye, ambaye Ndiye aliyewapanda, alipata uzuri kwa sababu ya kuwako kwao katika kundi la Kikristo.
25. Hao waliobatizwa katika Pentekoste walikuja chini ya wajibu gani, na ni katika kazi gani walipaswa watumikie kama mapainia?
25 Katika siku ya Pentekoste, licha ya lile kundi la wanafunzi kama 120, wengine elfu nyingi wakawa watiwa mafuta baada ya kutubu, kumkubali Masihi na kubatizwa katika maji na wale mitume 12. (Matendo 2:37-42) Hawa vilevile walikuja chini ya wajibu wa kutiwa mafuta na roho ya Yehova kupitia kwa Kristo. Kiongozi wao, Yesu, alikuwa amepainia (atangulize) njia kwa ajili yao ili wapate imani iliyokamilishwa pamoja na uzima na wokovu. Wakawa “wahudumu wa Mungu wetu.” (Isa. 61:6) Wakiwa hivyo, sasa lazima nao wapainie (watangulie) njia kwa ajili ya wengine waliokuwa wakitafuta uhusiano (urafiki) na Mungu ili wapatanishwe naye kupitia kwa Kristo. (2 Kor. 5:20) Kwa njia hiyo wangekuwa na furaha ya kushiriki katika kazi ya Mungu ya kutengeneza upya.