Mahubiri ya Mlimani—“Msalipo”
KUFUATA maelezo yake juu ya kuepuka unafiki mtu atoapo zawadi za rehema kwa maskini, Yesu alisema: “Tena msalipo, msiwe kama wanafiki.”—Mt. 6:5a.
Usemi “msalipo” unaonyesha kwamba, kwa wanafunzi wa Yesu, sala ingekuwa sehemu ya kawaida ya ibada ya kweli. Walakini wasingepaswa kuiga “wanafiki,” au Mafarisayo waliojiona kuwa wenye haki, ambao matendo yao ya kidini waliyofanyia mbele ya watu yalikuwa ya kujifanya tu.—Mt. 23:13-32.
Kuhusu wanafiki hao, Yesu alitangaza hivi: “Wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu.”—Mt. 6:5b.
Kufikia karne ya kwanza W.K., ilikuwa imekuwa desturi kwa Wayahudi kuomba kama kundi wakati wa asubuhi na jioni wa kutoa sadaka za kuteketezwa hekaluni katika Yerusalemu, yapata saa 3 asubuhi na saa 9 alasiri. Wakaaji wengi wa mji huo walifanya hivyo wakiwa pamoja na kikundi cha waabudu wenzao katika ua wa hekalu. Nje ya Yerusalemu, Wayahudi watawa walikuwa wameamua kuwa wakisali mara mbili kwa siku “katika masinagogi.” Kwa kawaida walikuwa wakisali hali “wamesimama.”—Angalia pia Luka 18:11, 13.
Kwa kuwa watu wengi hawangekuwa karibu na hekalu au sinagogi wakati wa sala ya asubuhi na jioni, kulikuwa na desturi ya kusali po pote pale alipokuwa mtu. Watu fulani ‘walipendelea’ kupatwa na saa ya kusali walipokuwa wangali “katika Pembe za njia” walivutiwa na wazo la ‘kuonekana na watu’ waliokuwa wakitoka pande zote nne. Katika kuonyesha utakatifu wa uongo, ‘kwa kujifanya walitoa sala ndefu,’ ili wasifiwe na watazamaji.a—Luka. 20:47.
Kuhusu wanafiki hao, Yesu alitangaza hivi: “Amini, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao.” (Mt. 6:5c) Walikuwa wakipata kile walichokuwa wakitamani sana—kutambuliwa na kusifiwa na wanadamu wenzao; na hiyo ndiyo iliyokuwa zawadi yao kamili. Sala zao za kinafiki hazingejibiwa na Mungu.
“Bali wewe,” akaendelea Yesu, “usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, tena ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”—Mt. 6:6.
Maneno haya ya Yesu hayakukataza sala ya kundi, onyo la upole kuomba katika ‘chumba cha ndani baada ya kufunga mlango’ kusudi lake lilikuwa kupunguza sala za hadharani zenye kusudi la kuvuta fikira na kusifiwa na watazamaji waliovutiwa. Linalingana na shauri lile la kutoa misaada kwa ajili ya maskini: “Mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume.” (Mt. 6:3) Yesu aliweka mfano bora katika kuomba bila kuvuta fikira za watu kwake. Kwa mfano, alipokuwa akisali usiku wote kabla ya kuchagua mitume wake kumi na wawili, hakumwomba Mungu mbele ya watazamaji bali “aliondoka akaenda mlimani ili kuomba.”—Luka 6:12.
Akielekeza fikira kwa njia nyingine ambayo wanafiki walitumia vibaya pendeleo la sala, Yesu alisema hivi: “Nanyi mkiwa katika: kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao mengi.”—Mt. 6:7.
Yesu hakuwa akisema kwamba wanafunzi wake walipaswa kuepuka kurudia maombi na misemo ya kushukuru inayotoka moyoni katika kusali. Injili ya Mathayo inasimulia kwamba katika bustani ya Gethsemane Yesu aliomba mpaka wakati wa usiku sana, akirudia “maneno yale yale.”—Mt. 26:36-45.
Hata hivyo ingekuwa makosa kuiga sala za kurudia-rudia za “watu wa mataifa.” Walikuwa na mazoea ya kubwata-bwata maneno yale yale ya semi walizokuwa wamekariri kutia ndani maneno mengi ya kupita kiasi. Biblia ina mfano wa waabudu wa Baali wa nyakati za kale ambao “waliliitia jina la Baali tangu asubuhi hata adhuhuri, wakisema, Ee Baali, utusikie.” (1 Fal. 18:26) Na kuhusu wapinzani wa Mataifa wa Ukristo huko Efeso, tunasoma hivi: “Wakapiga kelele wote pia kwa sauti moja kwa muda wa kama saa mbili, wakisema, Artemi wa Waefeso ni mkuu.” (Matendo 19:34) Katika maandishi ya mtunga mashairi Mrumi Terence (wa karne ya pili K.W.K.), twasoma lalamiko lifuatalo: “Naomba ewe, mke, acha kuduwaza miungu kwa kutoa shukrani, kwa sababu mtoto wako yu salama; ikiwa wewe hukujifanya hakimu wao, wasiweze kufahamu lo lote, ila tu waambiwe mara mia moja.”
Mpaka leo hii, ‘watu wengi wa mataifa hutoa sala za kurudia-rudia kwa miungu wao. Kwa mfano, Wabudha wengine hutumia tasbihi zenye shanga zapata 108 katika kurudia-rudia kusema namu amida butsu (“nafsi yake na ipumzike kwa amani”). Vivyo hivyo, katika makanisa, mengi ya Jumuiya ya Wakristo watu mmoja mmoja husali kwa maneno yale yale kwa kuyakariri, wakidhani kwamba “watasikiwa” kwa kuyarudia-rudia. Walakini matumizi haya ya ‘maneno mengi’ ni bure machoni pa Mungu.
“Basi msifanane na hao,” akaendelea Yesu, “maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba.”—Mt. 6:8.
Ni wazi kwamba viongozi wengi wa kidini Wayahudi walikuwa ‘wamejifanya kama’ watu wa mataifa kwa kutumia maneno mengi katika sala zao. Wonyesho wa maelekeo haya ni masimulizi yafuatayo katika kitabu Babylonian Talmud: ‘[Msomaji] mmoja alipiga magoti mbele ya [Rabi] Hanina na kusema, Ee Mungu, uliye mkubwa, mkuu, mwenye kuogofya, mwenye fahari, mwenye kutisha, mwenye uweza, usiyehofu, mwenye hakika mwenye kuheshimika.’ Rabi huyo alipinga matumizi haya ya maneno mengi yasiyo ya lazima na kusema kwamba ni “kumtukana” Mungu.
Sala ya kawaida ya kutoka moyoni inayotia ndani kusifu, kushukuru na kumwomba Mungu ni sehemu ya muhimu ya ibada ya kweli. (Flp. 4:6) Walakini ingekuwa makosa kuyasema mambo yale yale mara nyingi ukitumaini kwamba Mungu hayajui, hasikilizi na ni msahaulifu. Mtu anapaswa kusali akitambua kabisa kwamba anazungumza na yule anayefahamu ‘tunayohitaji kabla ya kumwomba.’
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu kusali barabarani na mahali pa watu wote, maandishi ya kirabi ya Wayahudi yanatoa mifano kama huu ufuatao: “Rabi Yokanani amesema: ‘Niliona namna Rabi Yanai alivyokuwa akisimama na kutoa sala ya Musaf [nyongeza]:’ “(Palestinian Talmud) “Ikiwa mtu amesimama akiomba barabarani au mahali palipo wazi, husogea kando [apishe punda], mpanda punda au mbeba mzigo pasipo kukatisha sala yake. Kuhusu Rabi Chanina ben Dosa [wapata mwaka 70 W.K.] inasimuliwa kwamba alikuwa amesimama akiomba. Halafu nyoka mwenye sumu akamwuma. Hata hivyo, yeye, hakukatiza sala yake.”—Tosephta (maandishi ya nyongeza ya Mishnah).