Uzima wa Wakati Ujao Kupitia kwa Ufufuo
“Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.”—Yohana 6:53.
1, 2. Yesu alisema nini katika Yohana 6:53, 54, nao ni watu wanaoamini fundisho gani wanaoweza kuona ugumu wa kufahamu maneno hayo?
FUNDISHO la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu linaenea pote. Kwa hiyo wale wanaoliamini lazima waone ugumu wa kukubali kwamba maneno ya Yesu Kristo ni ya kweli, kama yalivyoandikwa katika Biblia katika Yohana 6:53, 54:
2 “Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wa Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.”
3. Ni maulizo gani yanayopatana na akili yanayoulizwa na wanaoamini kutokufa kuhusu “uzima ndani yenu” pamoja na ufufuo?
3 Ikiwa nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa, inaendelea kuishi baada ya mwili kufa ambao ndani yake huwa inafungiwa, kama wanavyodai watu wengi, ni kwa sababu gani inakuwa lazima kuula mwili wa Yesu Kristo, “Mwana wa Adamu,” na kuinywa damu yake ili tuwe na ‘uzima ndani yetu’? Ikiwa nafsi inawekwa huru mwili unapokufa inaponyoka ikiwa hai na kuuendea ulimwengu wa roho, sababu gani inakuwa lazima kumfufua mwanadamu ili aishi tena? Bila shaka kila mmoja wetu lazima akubali kwamba huku ni kuwaza kunakopatana na akili.
4. Ni akina nani, kati ya wasikilizaji wa Yesu, walioona ugumu wa kufahamu aliyokuwa akisema Yesu, lakini namna gani leo?
4 Hata wafuasi wa Yesu Kristo waliona ugumu juu ya yale aliyosema, kwa kuwa tunasoma hivi: “Naye Yesu akafahamu nafsini mwake ya kuwa wanafunzi wake wanalinung’unikia neno hilo, akawaambia, Je! neno hili linawakwaza?” (Yohana 6:61) Hata leo wengine wa wasomaji wetu huenda wakashindwa kufahamu maneno ya Yesu. Hata hivyo, Yesu alijua alilokuwa akisema wakati huo, kwa kuwa yeye mwenyewe hakuamini fundisho la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu. Maneno yake mwenyewe yanathibitisha hivyo.
5. Yesu alionyesha kwamba yeye hakuamini katika kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu kwa misemo gani?
5 Pindi moja Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Musiwaogope wale wanaoua mwili lakini hawawezi kuua nafsi; lakini zaidi mwogope anayeweza kuharibu nafsi na mwili vilevile katika Gehena.” (Mt. 10:28, ZSB) Baadaye, kabla hajakamatwa katika bustani ya Gethesemane, aliwaambia wanafunzi wake: “[Nafsi] yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa.” (Mt. 10:28, ZSB) Baadaye, kabla hajakamatwa Yesu alitaja maneno katika unabii wa Isaya naye alikubaliana na yale yaliosemwa juu yake humo: “Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; na pamoja na matajiri katika kufa kwake; . . . alimwaga nafsi yake hata kufa.”—Isa. 53:9, 12.
6. Kulingana na Yohana 6:53, 54, wengine wangefanya nini juu ya dhabihu ya kibinadamu ya Yesu kabla ya “siku ya mwisho,” na kungetukia nini kwao katika siku hiyo?
6 Hiyo ndiyo sababu Yesu alionyesha katika Yohana 6:53, 54, kwamba angekuwa dhabihu ya kibinadamu, na kwamba kungekuwako wale ambao wangeula au kujilisha mwili wake na kunywa damu yake kabla ya “siku ya mwisho.” Hawa wangekufa baada ya muda kupita, walakini, kwa habari ya kila mmoja wao, Yesu alisema hivi: “Nitamfufua siku ya mwisho.” Kulingana na yale aliyoyasema Martha wa Bethania, katika Yohana 11:24, wakati wa kufufuliwa kwa wafu ulidhaniwa kuwa “siku ya mwisho.” Martha aliishi karibu na Yerusalemu. Hapo, muda fulani kabla ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka 31 W.K., Yesu alikuwa amesema juu ya amri aliyokuwa amepewa na Mungu ya kuwafufua wafu. Alikuwa amelaumiwa na viongozi wa kidini kwa sababu alikuwa amemponya mtu mmoja katika siku ya Sabato na kumwambia ainuke achukue godoro lake aende nyumbani kwake. Alipokuwa akijibu lawama hizo Yesu alijibu hivi:
7, 8. (a) Ni nani wanaohuishwa na Yesu Kristo kutoka kwa wafu, naye anastahili kuheshimiwa kama nani, na kwa sababu gani? (b) Ni nani ambao sasa wanatoka katika mauti kuingia uzimani? (c) Waliomo makaburini wataitwa na Mwana wa Adamu kwenye namna gani za ufufuo?
7 “Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana awahuisha wale awatakao. Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote; . . . Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka. Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani.
8 “Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa, ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai. Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu. Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.”—Yohana 5:21-30.
9. Katika maneno hayo ya Yesu yaliyotangulia kutajwa ni jambo gani linalotiliwa mkazo?
9 Katika maneno yaliyo juu tunaona namna habari ya hukumu ilivyotiliwa mkazo, maneno yanayohusiana na neno “hukumu” yakitajwa mara saba. Vilevile, watendao mabaya wanangojea “ufufuo wa hukumu.”
10. Katika wakati wa utawala wa Kristo wa miaka elfu, ni nani anayepewa nafasi ya kuwahukumu wanadamu, na kwa sababu gani hakutakuwa kuomba rufani katika hukumu hiyo?
10 Kwa hiyo, habari ya ufufuo inashirikishwa na hukumu. Kwa kuwa Mwana wa Mungu alikuja kuwa “Mwana wa Adamu” duniani, amepewa mamlaka ya kuhukumu washiriki wote wa jamaa ya kibinadamu. Kwa hiyo Mungu Baba amempa Mwanawe mwaminifu nafasi ya kushiriki katika kuhukumu. Akishiriki katika kuhukumu, Mwana wa Mungu atapewa nafasi ya kwanza ya kuwahukumu wanadamu wote wakati wa utawala wa Yesu Kristo wa miaka elfu. Kwa kuwa hukumu itakayotolewa na Mwana wa Mungu itakuwa kamilifu, hakutakuwa kuomba rufani. Hukumu inayotolewa na Yehova Mungu baada ya Siku ya Hukumu ya miaka elfu haitakuwa kwa sababu ya rufani yo yote itakayofanywa kwake na wanadamu waliokamilishwa akiwa Hakimu aliye Mkuu Zaidi, Hakimu wa Mwisho.—1 Kor. 15:24-28.
KUTOKA MAUTINI KUINGIA UZIMANI SASA
11. Katika Yohana 5:24, 25, Yesu alielezaje sababu wasikilizaji wake‘ walitoka mautini kuingia uzimani’?
11 Alipokuwa duniani Yesu Kristo alitenda kama mnenaji wa Mungu kwa mwanadamu. Kwa hiyo wasikilizaji ambao wangeamini yaliyosemwa na Mwana wa Mungu ingekuwa kama kwamba wanakuwa wakiamini yaliyosemwa na Mungu Baba. Faida ambayo Wayahudi waliomsikia Yesu wangepata kutokana na hili, alionyesha aliposema maneno haya kwa Wayahudi hao: “Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani. Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakaposikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.” (Yohana 5:24, 25) Bila shaka, wafu halisi waliokuwa makaburini hawangeweza kusikia maneno yaliyosemwa na Yesu na kuyatii, wakati wa “saa” hiyo aliyokuwa akisema habari zake. Hivyo, basi, Yesu alikuwa akisema juu ya “wafu” gani?
12, 13. (a) Yesu alimaanisha “wafu” gani alipokuwa akisema juu ya kusikia kwao maneno yake na kuishi kwa sababu hiyo? (b) Kwa sababu ya mpango huo wa kimungu, Paulo angeweza kuwaandikia nini wale waliokuwa “wafu” katika makosa na dhambi kulingana na Waefeso 2:2-7?
12 Kwa kuwa Yesu alisema kwamba “saa” ya jambo hili kutukia “sasa ipo,” lazima awe alimaanisha wanadamu waliokuwa wakitembea duniani lakini waliokuwa chini ya hukumu ya mauti kwa sababu ya kutokamilika na dhambi waliyorithi kutoka kwa Adamu. Wanadamu wote kwa jumla ni “wafu” kulingana na maoni ya Mungu; hawana haki ya uhai nao “mshahara” wa dhambi kwao ni mauti. (Rum. 6:23) Walakini kwa kulisikia na kulitii “neno la Yesu wangetoka chini ya hukumu ya mauti iliyopitishwa kwao na Mungu na kwa njia hiyo, kusema kwa njia ya mfano, ‘watoke mautini waingie uzimani.’
13 Kwa sababu ya mpango kama huo wa kimungu, mtume Paulo angeweza kuwaandikia waamini watakatifu katika Efeso waliokuwa “[katika umoja na] Kristo Yesu” maneno yafuatayo: “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; . . . Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda; hata wakati ule tuliokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, mmeokolewa kwa neema. Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu ili katika [taratibu za mambo] zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake [uliyokuwa umekwisha pita] upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi [tulio] katika [umoja na] Kristo Yesu.”—Efe. 1:1; 2:1, 4-7.
14. Hao waliofanywa hai kiroho hivyo wanakaa wapi nao wanakuwa kikundi cha namna gani nao lazima waendelee kukaa katika umoja na nani?
14 Wale walioondolewa hukumu ya mauti na kufanywa hai kiroho ili waketi pamoja na Kristo Yesu katika “ulimwengu wa roho” walifanywa washiriki wa kundi lililo kama mwili wa Kristo. Vilevile walifanywa kuwa jamii ya “hekalu” ambalo Mungu angekaa kwa roho yake takatifu kama vile katika “hekalu takatifu.” (Efe. 1:22, 23; 2:20-22) Kwa sababu wao ni “mwili” wa Kristo, sana sana wao wako “[katika umoja na] Kristo Yesu.” Wanahitaji kuendelea kuwa katika umoja naye.—Yohana 15:4.
15. Ni maulizo gani yanayojitokeza kwa habari ya Baba kuwa na “uzima nafsini mwake”?
15 Maneno haya ya Yesu yatumika kwao: “Kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana awahuisha wale awatakao.” (Yohana 5:21) Hii inamaanisha kwamba vilevile Mwana ana uwezo wa kuwapa wengine uzima. Yesu alionyesha sababu ya hili aliposema: “Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa Mwana kuwa na uzima nafsini mwake.” (Yohana 5:26) Baba kuwa na “uzima nafsini mwake” kunamaanisha nini hasa? Je! kunamaanisha tu kwamba yeye yu hai akiwa “Mungu aliye hai, wa kweli” peke yake? (1 The. 1:9) Je! kunamaanisha kwamba yeye anajitegemea mwenyewe kwa habari ya uhai, akiwa na uhai unaokaa ndani yake? Yaani, kutokufa? An American Translation ndivyo inavyofahamu mambo kuwa, kwa kuwa inatafsiri Yohana 5:26 hivi: “Kwa maana kama vile Baba alivyo na chemchemi ya uzima ndani yake mwenyewe, ndivyo alivyompa na Mwanawe uwezo wa kuwa na chemchemi hiyo ya uzima ndani yake mwenyewe.” Kulingana na hili, The Holy Bible in Modern English ya Ferrar Fenton inafahamu jina Yehova kumaanisha “Aishiye-Milele,” kwa hiyo inatafsiri Isaya 42:8 hivi: “Mimi ndimi [yule] Aishiye-Milele;—kwa kuwa hilo ndilo jina langu.” Yehova amepata kuitwa “Yeye Anayejitegemea Mwenyewe kwa habari ya Uzima.”
16. Ikiwa kumpa Mwana wa Mungu “uzima nafsini mwake” kulimaanisha kumpa uzima mkamilifu tu, ni kwa sababu gani Mwana hangekuwa wa pekee kuhusiana na jambo hilo?
16 Walakini, kulingana na sababu zinazotolewa kuhusu maneno yanayozunguka, usemi “uzima nafsini mwake” una maana yenye nguvu zaidi ya yeye kuwa tu anajitegemea kwa habari ya uzima. Usemi huo unamaanisha kwamba Baba wa mbinguni ana kisima cha uzima nafsini mwake, hivi kwamba, akiwa kama baba ana uwezo wa kuwapa wengine uzima. Kwa sababu ya uhakika huu, aliweza kumpa Mwanawe uzima kiasi kikubwa hivi kwamba yeye naye angeweza kuwapa wengine uzima. Ikiwa uwezo aliopewa Mwana na Baba wa kuwa na “uzima nafsini mwake” ulimaanisha tu kwamba alimpa uzima mkamilifu, basi Mwana hangekuwa wa pekee. Sababu gani? Kwa kuwa Mungu aliwapa malaika wa mbinguni uzima mkamilifu pia. Wala si hivyo tu, bali aliwapa Adamu na Hawa uzima mkamilifu katika bustani ya Eden. Lakini sababu gani Mwana wa Mungu akapewa “uzima nafsini mwake”?
17. Sababu gani Mwana akapewa “uzima nafsini mwake,” nayo sala yake, katika Yohana 17:1, 2, inapatanaje na jambo hili?
17 Ni kwa sababu Mwana wa Mungu alitoa uzima wake mkamilifu wa kibinadamu uwe dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya wanadamu wote. (Mt. 20:28; 1 Tim. 2:5, 6) Katika njia hiyo angeweza kuwakomboa wanadamu kutokana na mauti ambayo chini yake walikuwa wamehukumiwa kwa sababu ya kutokamilika kulikorithiwa. Akikumbuka hili, Yesu angeweza kufungua sala yake katika usiku wa Sikukuu ya Kupitwa kwa maneno haya: “Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe; kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili wote uliompa awape uzima wa milele.”—Yohana 17:1, 2.
18. Tafsiri ya R. A. Knox ya Yohana 5:26 inaonyeshaje wazi ukweli huu, naye Kristo alipewa mamlaka na uwezo wa kuwapa wengine uzima wakati gani?
18 The New Testament of our Lord and Saviour Jesus Christ ya Ronald A. Knox inashika ukweli huo na kuuonyesha wazi katika tafsiri yake ya Yohana 5:26: Hapo tunasoma hivi: “Kama vile Baba alivyo na zawadi ya uzima ndani yake, vivyo hivyo amempa Mwana ili yeye naye awe na zawadi ya uzima ndani yake.’”a Baada ya kifo chake cha dhabihu, kufufuliwa kwake na kutoa thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa Baba yake wa mbinguni, Yesu Kristo angeweza kupewa mamlaka na uwezo wa kutoa faida zake kwa wale wanaozihitaji—wanadamu wote waliohukumiwa na wanaokufa. Kwa hiyo, twasoma katika Warumi 6:23, ZSB hivi: “Kwa maana mushahara wa zambi ni mauti, lakini zawadi ya Mungu ni uzima wa milele katika Yesu Kristo Bwana yetu.”
19. Kwa sababu gani Yesu Kristo ndiye anayestahili kutumiwa na Mungu kuwahukumu wanadamu?
19 Akiwa mwanadamu mwenye mwili na damu, Yesu “Mwana wa Adamu” angeweza kumtolea Mungu kitu kinacholingana barabara na kile ambacho Adamu alipotezea uzao wake kwa dhambi yake ya kukusudia katika Edeni. (Ebr. 2:9, 14, 15; Yohana 1:14) Kwa kuwa Yehova anamtumia katika kutoa uzima kwa wanadamu waliohukumiwa, na wanaokufa, Yesu Kristo “Mwana wa Adamu” ndiye anayestahili kutumiwa na Yehova katika kuwahukumu wanadamu waliokombolewa.
20. Katika Yohana 5:26, 27, Yesu alisema nini juu ya mamlaka ya kuhukumu, naye mtume Paulo alithibitishaje jambo hilo katika hotuba yake katika Areopago?
20 Kulingana na uhakika huo, Yesu aliendelea hivi: “Vivyo hivyo [Baba] alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu.” (Yohana 5:26, 27) Kwa sababu Yesu Kristo aliyetukuzwa sasa wakati mmoja alikuwa mwanadamu katikati ya taratibu ya mambo ya kilimwengu yenye upotovu, anaweza kuwa hakimu mwenye rehema na mwenye haki kwa wale aliokomboa na mauti. Baraza kuu zaidi ya hukumu iliyokuwako Athene wa kale, Ugiriki, ilijulishwa wazi uhakika huu wakati mtume Paulo aliposimama kati ya mahakimu katika Areopago akasema: “[Yeye Mungu wasiomjua] ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”—Matendo 17:23, 31.
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu Yohana 5:25, 26, tunasoma hivi: “Uzima unaoonyeshwa kwa [neno] hili zésousin [neno la Kigiriki kumaanisha wataishi], kwa kuwa wanaotajwa kwalo walikuwa wafu, lazima liwe jambo analoendelea kupewa,—uzima unaotoka kwa Mwana, anayehuisha. Walakini hangeweza kuwapa ikiwa Yeye mwenyewe hana kisima cha kimungu cha uzima ndani Yake Mwenyewe chenye kujitegemea, kama vile Baba, ambacho Baba, Aliye hai peke yake (vi 57) alimpa Yeye alipomtuma duniani atimize kazi Yake ya kimasihi; Linga. x 36.”—Ukurasa 184, wa Critical and Exegetical Handbook to the Gospel of John cha Heinrich August Wilhelm Meyer, kilichochapwa katika Kingereza katika mwaka 1884.
Tafsiri ya Good News Bible hutafsiri Yohana 5:26 hivi: “Kama vile Baba mwenyewe aliye chemchemi ya uzima, vivyo hivyo yeye amemfanya Mwanawe kuwa chemchemi ya uzima.” (Ilichapwa na American Bible Society katika mwaka 1976)