Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 2/15 kur. 14-20
  • “Nitamfufua Katika Siku ya Mwisho”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nitamfufua Katika Siku ya Mwisho”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MWILI WANGU, KWA AJILI YA UZIMA WA ULIMWENGU”
  • “UZIMA, NDANI YENU”
  • MIPANGO YA MUNGU KWA AJILI YA UZIMA WA ULIMWENGU
  • “Mkate wa Uzima” Upo kwa Watu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Maneno ya Yesu Yawashtua Wengi
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Wanafunzi Wengi Waacha Kufuata Yesu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 2/15 kur. 14-20

“Nitamfufua Katika Siku ya Mwisho”

1. Maneno ya Yesu. “Nitamfufua siku ya mwisho,” hayatumiki kwa jamii gani ya watu leo?

MANENO hayo yenye maana sana yalisemwa na Yesu, katika Yohana 6:54. Hayawezi kutumiwa juu ya “mkutano mkubwa” ulio hai ambao unaiokoka “dhiki ile iliyo kuu” inayokaribia. (Ufu. 7:9-17) Basi, Yesu alikuwa akiwafikiria nani aliposema maneno hayo karne 19 zilizopita?

2. Yesu alisema maneno hayo juu ya ufufuo kwa nani, na wakati huo ulikuwa karibu na sikukuu gani ya Wayahudi iliyompasa yeye?

2 Mistari ya Biblia inayozunguka Yohana 6:54 inaonyesha kwamba Yesu alikuwa akiyasema maneno hayo, si kwa Wayahudi tu, bali pia kwa wengine wa wanafunzi wake Waisraeli, kutia na mitume wake 12. Sikukuu ya Kupitwa yao ya mwaka 32 W.K., “sikukuu ya Wayahudi,” ilikuwa inakaribia. (Yohana 6:4) Katika matayarisho ya karamu hiyo, Wayahudi walichinja mwana-kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa hekaluni katika Yerusalemu na makuhani waliiweka damu katika bakuli na kuinyunyiza kuelekea chini ya madhabahu. (Tazama M’Clintock na Strong’s Cyclopoedia, Kitabu cha 7 chini ya “Sikukuu ya Kupitwa,” ukur. 738, safu 1, fungu la 4, mistari 1-34; pia, The Temple​—Its Ministry and Services As They Were at the Time of Jesus Christ, cha Alfred Edersheim, 1874 W.K., kur. 190, 191.) Yesu alikusudia kuhudhuria karamu hiyo apate kuadhimisha ukumbusho wa Sikukuu ya Kupitwa ya kwanza iliyoadhimishwa huko Misri katika mwaka 1513 K.W.K. Kwa kweli, ndiye aliyekuwa akifananishwa na mwana-kondoo wa Sikukuu ya Kupitwa, “Mwana-kondoo wa Mungu.”​—Yohana 1:29, 36.

3. Sababu gani Wayahudi wakamfuata Yesu baada ya mwujiza wake wa siku iliyotangulia, nao waliliteteaje jambo hilo?

3 Wayahudi, kutia na wanafunzi wake, walikuwa wamemwona akifanya mwujiza wenye kushangaza sana siku iliyotangulia maongezi yale yanayosimuliwa kati yake nao katika Kapernaumu. Alikuwa amezidisha vipande vitano vya mkate na samaki wawili ili kulisha maelfu ya wasikilizaji wake. Basi Wayahudi watukuzaji wa taifa wakataka kumfanya mfalme na Kiongozi wao wa Kimasihi. Kwa kuwa Yesu angekuwa Mfalme wa Kimasihi wa mbinguni, aliwaepa waliotaka kumfanya mfalme. Baadaye, kwa kutembea juu ya maji, alijiunga na mitume wake 12 waliokuwa mashuani katika Bahari ya Galilaya. (Yohana 6:14-21) Walakini kusudi la Wayahudi la kumfuata Masihi aliye mwanadamu wa kidunia halikushindwa vivi hivi tu. Basi walimfuata, wakikumbuka mwujiza wa siku iliyotangulia. Walitaka Mfalme wa Kimasihi ambaye angewapa chakula halisi kama vile Yesu alivyokuwa amejionyesha anaweza kufanya. Katika kutetea jambo hili, walimkumbusha Yesu kwamba katika jangwa la Sinai lililozungukwa na maji, Mungu alikuwa amewapa babu zao “chakula kilichotoka mbinguni” wale na ambacho kilikuwa kwa namna ya mana ya kimwujiza.​—Yohana 6:22-31.

4. Yesu alielezaje kama Musa alikuwa amewapa babu zao “chakula kilichoshuka kutoka mbinguni” cha kweli?

4 Akijibu hili, Yesu aliwaambia kwamba Musa hakuwapa babu zao chakula cha kweli kilichotoka mbinguni. “Chakula cha Mungu,” akasema, “ni kile kilichoshuka kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.”​—Yohana 6:32, 33.

5. Wakati huo Wayahudi walimwomba Yesu nini, naye alisema nini katika kuwaeleza njia ya kupata uzima wa milele?

5 Wayahudi waliposikia hiyo walisema: “Bwana, sikuzote utupe chakula hiki.” Yesu akaonyesha kuwa ndiye chakula hicho akisema: “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe . . . Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.”​—Yohana 6:34-40.

6. Sababu gani wanaomjia Yesu na kuamini ndiye Masihi wakati huu wa taratibu ya mambo iliyopo wanahakikishiwa ufufuo?

6 Kwa hiyo, sana sana wale wanaomjia Yesu na kuamini ndiye Masihi wakati huu wa taratibu ya mambo iliyopo wana taraja la uzima wa milele. Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu Yesu Kristo atawafufua kutoka kwa wafu katika siku ya mwisho. Hii inawahakikishia kwamba watapata ufufuo. Hapa twapaswa kuangalia kwamba Yesu hakusema, katika habari hii, kwamba lazima kwanza mtu apate ufufuo ndipo baadaye amjie katika imani na kumla kisha apate uzima wa milele. Kwa wazi kabisa hapa Yesu hazungumzi juu ya wafu waliomo makaburini ya ukumbusho kama vile Ibrahimu, Isaka, Yakobo na Musa, Daudi na Yohana Mbatizaji. Hapo Yesu alikuwa akizungumza na Wayahudi waliokuwa wakiishi wakati huo, kutia na wengine wa wanafunzi wake, ambao walikuwa katika agano la torati ya Musa.

7. Akijibu manung’uniko ya Wayahudi, Yesu alisema nini juu ya mtu anayevutwa kwake na kupata uzima wa milele?

7 Wasikilizaji Wayahudi walianza kunung’unika wao kwa wao katika kushindana juu ya alikotoka Yesu. Kutokana na aliyosema Yesu juu ya hili tunaweza kuwajua wale hasa ambao kwao anaelekeza mazungumzo yake. “Yesu akajibu, akawaambia, Msinung’unike ninyi kwa ninyi. Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. Imeandikwa katika manabii Na wote watakuwa wamefundishwa na [Yehova]. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba [Aliye Mwalimu] huja kwangu . . . Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele.”​—Yohana 6:41-47.

8. Yesu alikuwa akitaja maneno ya unabii gani, naye alikuwa akiwatolea wasikilizaji wake Wayahudi nafasi gani?

8 Hapo Yesu alikuwa akitaja maneno ya unabii wa Isaya 54:13, ambao unaelekezwa kwa “mwanamke” wa Mungu, Sayuni wa mbinguni, unaosema hivi: “Na watoto wako wote watafundishwa na [Yehova]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” Hawa ndio wana wa kiroho wa Yehova Mungu. Hawa ndio anaowavuta kwa Yesu kwa sababu ya kumwamini wakati huu. Hawa ndio wanaosemwa na Yesu kwamba wanaongia kwenye uzima wa milele kwa kufufuliwa naye katika siku ya mwisho. Uzima wao ungekuwa wa milele katika tengenezo la Yehova la kiroho la kimbinguni. Kwa hiyo Yesu alikuwa anawapa wasikilizaji wake Wayahudi, kutia na wengine wa wanafunzi wake, nafasi ya kuwa wana wa “mwanamke” wa Mungu, Sayuni wa mbinguni.

“MWILI WANGU, KWA AJILI YA UZIMA WA ULIMWENGU”

9-11. (a) Kusema kwa Yesu kwamba kile “chakula” alichotoa ni “mwili” wake na hii ni “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu” kunatokeza ulizo gani? (b) Paulo anajibuje ulizo hilo katika 1 Wakorintho 10:2-11?

9 Baada ya Yesu kusema mara nyingi kwamba ndiye “chakula cha uzima,” aliendelea kusema hivi: “Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu [ye yote wenu wasikilizaji wangu] akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.”​—Yohana 6:51.

10 Kwa hiyo Yesu alikuwa Mana ya kweli kutoka mbinguni itoayo uzima. Alisema kwamba chakula hiki cha mfano, ni mwili wake. Mwili huu, alisema, ulikuwa “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” Kwa kuongeza maneno hayo, je! Yesu alimaanisha kwamba Wayahudi waliokula mana jangwani katika siku za Musa walifananisha “ulimwengu” wa wanadamu wakati wa miaka elfu ya utawala wa Kristo na kundi lake lililotukuzwa?

11 Paulo anajibu hivi: “Wote wakabatizwa katika Musa kupitia kwa wingu na bahari; na wote wakala chakula kile kile cha kiroho [mana] na wote wakanywa kinywaji kile kile cha kiroho. Kwa maana waliunywea mwamba wa kiroho uliowafuata, na mwamba ule ulimaanisha Kristo. . . . Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, [Wakristo] kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani. . . . Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi [Wakristo waliozaliwa kwa roho] tuliofikiliwa na miisho ya zamani.”​—1 Kor. 10:2-11; Kut. 16:1-35; Hes. 11:1-9.

12. Hali ya Waisraeli wa kiroho wakati wa taratibu hii ya mambo inatofautianaje na ile ya ulimwengu wa wanadamu wakati wa ile miaka elfu?

12 Basi Waisraeli hao katika jangwa la Sinai chini ya Musa walifananisha Waisraeli wa kiroho wakati wa taratibu hii ya mambo. Taratibu hii inatokeza kifo, kwa maana ya kiroho. Sasa ndio wakati Waisraeli wa kiroho wanapokula mana ya kisasa ya kimbinguni, Yesu Kristo aliyetolewa dhabihu. Wakati wa miaka 1,000 ya utawala wa Kristo, wanadamu waliofufuliwa hawatakuwa katika hali ya jangwa kama lile la Sinai. Kurudishwa kwa paradiso duniani pote kutakuwa kumeanza kufanywa. Wakati huo Yehova Aliye Mwalimu hatakuwa ‘akiwavuta’ wanadamu kwa Yesu kama anavyofanya sasa kwa Waisraeli wa kiroho. (Yohana 6:44) Mahali pake, Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu atamweka Mwanawe Yesu Kristo kuwa Mfalme juu ya wanadamu, na Mfalme huyu atawaita wafu watoke makaburini.

13. Ili upate kuwa mfano wa kisasa wa mana ya kale, ‘‘mwili” huu wapaswa uwe na namna gani au uwe umefanyizwaje?

13 Chakula kilichotengenezwa kwa nafaka ni kitu kisicho na damu ambacho chaweza kuliwa, kama vile mana ya kale ilivyokuwa. Yesu Kristo alisema kwamba “chakula cha uzima,” kilichofananishwa na mana, kilikuwa mwili wake “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” Ili ufanane na mana ya kale, hapa mtajo “mwili” lazima ufahamike kuwa unamaanisha mwili usio na damu. Kile ambacho Yehova aliwapa Waisraeli jangwani wapate kunywa ni maji, wala si damu.

14. Ni kwa sababu gani wasikilizaje wa Yesu walifahamu mtajo wake ulikuwa juu ya “mwili” ulioondolewa damu, hata mwili wa kibinadamu?

14 Wayahudi waliokuwa wakimsikiza Yesu walifahamu hivyo, kwa kuwa, katika kushindana kwao juu ya alichomaanisha, walisema hivi: “Awezaje [kwa njia gani] mtu huyu kutupa sisi mwili wake tuule?” (Yohana 6:52) Waliijua sheria ya Mungu juu ya damu. Wakati uliofuata gharika ya siku za Nuhu, wakati Mungu alipoongezea wanadamu chakula chao, hakuwapa damu ya wanyama wanywe pamoja na nyama ya wanyama kiwe chakula chao kigumu cha kuendeleza uzima wao. Aliwapa maji wawe wakiyanywa na nyama isiyo na damu wawe wakiila. Alitaka damu iwe yake akiwa Mpaji-Uzima kwa viumbe vyote vyenye mwili na damu. (Mwa. 9:1-4) Chini ya torati ya Musa kama ilivyopewa taifa la Israeli, kuvunja sheria ya Mungu inayohusu damu ya wanyama kulileta adhabu ya kifo kwa mkosaji. (Law. 17:10-12; Kum. 12:16, 22-27) Kula mwili wa kibinadamu, hata ukiwa umeondolewa damu yake, kulichukiza Wayahudi waliokuwa wakimsikiliza Yesu. Hawakutaka kuwa walaji-watu.​—2 Fal. 6:26-31.a

15, 16. (a) Kuula mwili wa Yesu kungefanywa kwa njia gani? (b) Kulingana na Yohana 6:53-59, Yesu alikaziaje zaidi jambo hilo?

15 Yesu alitaka wasikilizaji wake Wayahudi wafahamu kwamba kuula mwili wake kungekuwa kwa njia ya mfano. Basi, ili kukazia zaidi jambo hili, aliendelea kusema jambo ambalo lisingekubalika hata zaidi likichukuliwa kwa njia halisi. Tunasoma hivi:

16 “Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, [ninyi wasikilizaji wangu Wayahudi] Msipoula mwili wake Mwana Wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. [Yeye nyie, wasikilizaji wangu] aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye [nyie, wasikilizaji wangu] mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi. Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa [wenu] walivyokula [mana jangwani,] wakafa; bali akilaye chakula hicho ataishi milele. Maneno hayo aliyasema katika sinagogi [kusanyiko la watu wote, NW], alipokuwa akifundisha, huko Kapernaumu.”​—Yohana 6:53-59.

17. (a) Matokeo ya maneno haya ya Yesu yalikuwa nini katika sinagogi la Wayahudi, na juu ya wengi wa wanafunzi wake? (b) Basi, sana sana maneno ya Yesu katika Yohana 6:53 yalielekezwa kwa nani, nao wakapata kuwa nini?

17 Hapa msemo “katika kusanyiko la watu wote,” kwa maana halisi katika maandishi ya awali ya Kigiriki ni, “katika sinagogi.” Yesu alitumia msemo uu huu katika Yohana 18:20, akisema: “Katika sinagogi na katika hekalu, wakusanyikapo Wayahudi wote.” Basi Yesu alikuwa akihutubia wasikilizaji Wayahudi waliokuwa katika agano la torati ya Musa. Hii ilitia ndani wanafunzi wengi wa Yesu. Tunaweza kuwazia matokeo ya maneno ya Yesu wakati aliposema, si juu ya kuula mwili wake tu, bali pia juu ya kuinywa damu yake. “Basi watu wengi miongoni mwa wanafunzi wake waliposikia, walisema, Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia?” (Yohana 6:60) Maneno haya yanaonyesha kwamba si wanafunzi wote wa Yesu waliochukizwa na aliyosema. Licha ya waliochukizwa, kulikuwako “wanafunzi” zaidi, kutia na wale mitume 12. (Yohana 6:61-66) Basi maneno ya Yesu katika Yohana 6:53 yalielekezwa zaidi kwa wanafunzi wake na, yakipanuliwa kwa wale ambao wangekuwa wanafunzi wake kabla ya “siku ya mwisho.” Walipata kuwa Wayahudi wa kiroho, Waisraeli wa kiroho.​—Rum. 2:28, 29.

18, 19. (a) Damu ya dhabihu zilizotolewa ilikuwa mali ya nani, na kwa hiyo kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake kulimaanisha nini? (b) Kwa sababu ya imani ya akida Mtaifa na vilevile ya Myahudi fulani aliyezungumza walipokuwa wakila chakula, Yesu alitajaje chakula kama hicho?

18 Wayahudi waliokuwa katika agano la torati ya Musa walifahamu kwamba damu pamoja na mafuta ya dhabihu iliyotolewa vilikuwa vya Yehova. (Law. 3:16, 17) Yesu alipopaa mbinguni na kuonekana mbele za Yehova alimtolea Yehova “damu” yake au thamani yake ikiwa bei ya ukombozi. (Ebr. 9:12-16; Yohana 6:61, 62) Kwa kuwa damu ilikuwa ni mali ya Yehova, kuinywa na kuula mwili wa Yesu kungemaanisha kula chakula pamoja na Yehova. Kwa hiyo Mungu angekuwa anashiriki damu ya Mwana-Kondoo wake Yesu Kristo pamoja na wanafunzi wa Mwana-Kondoo huyu. Yesu alizungumza juu ya kula chakula hiki na Yehova akiwa ndiye Ibrahimu Mkuu Zaidi, alipotabiri kwamba waamini wa Mataifa (kama yule “akida” aliyeamini) wangetoka katika sehemu zote za dunia na “[kuketi mezani] pamoja na Ibrahimu [Yehova] na Isaka [Yesu Kristo] na Yakobo [kundi la Kikristo lililozaliwa kwa roho] katika ufalme wa mbinguni.”​—Mt. 8:5-12.

19 Wakati mmoja alipokuwa akizungumza juu ya chakula kilichokuwa na ubora halisi kwa sababu ya wale walioalikwa, alisema hivi: “Utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.” Hii ilileta akilini mwa mtu pendeleo la kula chakula na Yehova Mungu, kwa kuwa twasoma hivi: “Basi aliposikia hayo mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja naye alimwambia, Heri yule atakayekula mkate katika ufalme wa Mungu.” (Luka 14:12-15) Katika kujibu maneno haya ya mshangao Yesu alitoa mfano wa ‘karamu kubwa ya jioni’ iliyotayarishwa na mwenye nyumba fulani. Kwa hili Yesu alionyesha kwamba si wote wangepata furaha ya kuketi chakulani pamoja na Mungu katika Ufalme.—Luka 14:16-24.

“UZIMA, NDANI YENU”

20. Wanaopata ‘uzima ndani’ yao kwa kuula mwili wa Kristo na kuinywa damu yake wana uzima kadiri gani, nao watautumia uwezo wao wapi na wakati gani?

20 Katika Yohana 6:53 Yesu alisema hivi: “Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.” Kwa sababu usemi uo huo unapatikana hapa kama ulivyo katika Yohana 5:​26, An American Translation inatafsiri Yohana 6:53 hivi: “Nawaambieni, ikiwa hamtakula mwili wa Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna [uwezo wa] kujitegemea wenyewe kwa habari ya uzima.” Basi hapa Yesu alimaanisha “uzima” ulio na maana fulani alipoendelea kusema hivi: “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.” (Yohana 6:54) Atakayepata huo uzima wa milele ataufurahia, si duniani, bali katika ufalme wa kimbinguni pamoja na Kristo. Ataingia katika maisha hayo atakapofufuliwa na Yesu Kristo wakati wa “siku ya mwisho.” Wale walio na ‘uzima huu ndani yao’ wakiwa pamoja na Kristo mbinguni, watakuwa na uwezo wa kuwapa wengine faida za dhabihu ya kibinadamu ya Kristo. Watafanya hivyo wakati waliokombolewa kati ya wanadamu watakapoitwa watoke katika makaburi ya ukumbusho wakati wa “siku ya mwisho.”​—⁠Yohana 5:​28, 29.

21, 22. (a) Ni kwa namna gani mwili na damu ya Yesu vilikuwa chakula cha kweli” kwa wanaokila? (b) Wanaokila wana uhusiano gani naye nao wana tegemeo gani kwake?

21 Tunapoufikiria ubora wa “uzima wa milele” utakaopatikana mbinguni, tunafahamu sababu ya Yesu kusema: “Mwili wangu ni chakula cha kweli na damu yangu ni kinywaji cha kweli.” (Yohana 6:55) Baada ya kusema hayo alionyesha ule uhusiano wa pekee ambao wanafunzi wake wangekuwa nao alipoongeza maneno haya: “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi.” (Yohana 6:​56, 57) Hivyo, Yesu alisema kwamba wanafunzi wake hukaa ndani yake au wanakaa katika umoja naye kadhalika naye hukaa ndani yao au anakaa katika umoja nao. Baadaye, alitumia maneno yanayofanana na hayo, aliposema katika mfano hivi:

22 “Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi; akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote.”​—Yohana 15:4, 5.

23. Basi ni kwa sababu gani Yudasi Iskariote alishindwa kupata ‘uzima ndani yake’?

23 Ijapokuwa Yudasi Iskariote aliendelea kushirikiana na Yesu Kristo kwa zaidi ya mwaka mmoja, hakukaa katika umoja na Bwana wake. Kwa hiyo hakula mwili wa Yesu uliotolewa dhabihu na kuinywa damu yake, kuanzia na Pentekoste ya mwaka 33 W.K. na kuendelea. Alishindwa kupata ‘uzima ndani yake.’​—Yohana 6:66-71.

24. (a) Ni kwa njia gani Yesu alikuwa “chakula” kilichoshuka kutoka mbinguni? (b) Ni kwa namna gani Yesu aliishi kwa sababu ya Baba, nao wanaomla wanaishije kwa sababu yake?

24 Hata hivyo, Yesu alimkumbusha Yudasi na wale wasikilizaji wengine Wayahudi katika kusanyiko lile katika Kapernaumu namna mababa zao walivyokula mana jangwani ili waendeleze uhai wao. Katika kumalizia hotuba yake, alisema hivi: “Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; . . . akilaye chakula hicho ataishi milele.” (Yohana 6:58) Yeye alikuwa amekuwa “Neno” la Mungu huko mbinguni, lakini, kwa wakati uliowekwa wa Mungu, ‘akawa mwanadamu.’ (Yohana 1:14) Hivyo, akiwa Mwana mkamilifu wa kibinadamu wa Mungu akawa “chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni,” mana iliyofananishwa. Mwili wake, uliotumika kama mana ya mfano kwa Waisraeli wa kiroho,b unatumika pia “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Leo Yesu Kristo anaishi tena mbinguni, akiwa na uzima usioweza kufa, kwa sababu ya Baba yake wa kimbinguni, kwa kuwa huyu “Baba aliye hai” alimfufua kutoka kwa wafu kwenye uzima wa roho. Vivyo hivyo, mwanafunzi yule ‘anayekula’ mana iliyofananishwa (“mwili” wa Kristo) kabla ya kufika kwa “siku ya mwisho,” “ataishi kwa sababu yangu,” kama alivyosema Yesu, kwa maana Yesu aliye hai atamfufua katika “siku ya mwisho.”​—Yohana 6:54, 57, 58.

25. (a) Wanaoila dhabihu ya Kristo duniani wataendelea kufanya hivyo mbinguni? (b) Watatumikia katika cheo gani kitakatifu, kukiwa na faida gani kwa wanadamu?

25 Kule mbinguni watakapokuwa na ‘uzima ndani yao wenyewe,’ Waisraeli wa kiroho waliofufuliwa hawatapaswa wale mwili wa Yesu na kuinywa damu yake tena. (Yohana 6:53) Watapendelewa watumikie wakiwa “makuhani wa Mungu na wa Kristo” hivyo watakuwa na uwezo wa kuwapa wanadamu faida zenye kudumu za dhabihu ya Kristo iondoayo dhambi. (Ufu. 20:6) Kwa maana mbinguni wataishi milele, hawatahitaji warithi katika cheo chao cha kikuhani. Kama Kuhani Mkuu, Yesu Kristo, watatumikia wakiwa makuhani wadogo wa kudumu kwa miaka hiyo elfu. Kwa njia hii watashiriki pamoja na Kristo katika kuinua wanadamu kwenye ukamilifu wa kibinadamu duniani.

MIPANGO YA MUNGU KWA AJILI YA UZIMA WA ULIMWENGU

26. “Mkutano mkubwa” umekuwa ukikusanywa tangu wakati gani, nao wanaona uhitaji gani kwa damu ya Mwana-Kondoo Yesu Kristo?

26 Kama tujuavyo, kuanzia karibu na mwaka wa 1935, “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Kristo umekuwa ukikusanywa. (Ufu. 7:9, 10; Yohana 10:16) Wao nao watafaidika kutokana na ukuhani huu wa miaka elfu. Mtume Yohana, ambaye aliona njozi ya ufunuo ya huu “mkutano mkubwa,” alikumbushwa kwamba hata wao wanathamini damu iliyomwagwa ya Mwana-Kondoo Yesu Kristo. Wanaithamini kuwa ndiyo inayosafisha, kwa maana Yohana aliambiwa hivi: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufu. 7:14) Wanafahamu kwamba hawawezi kumtumikia Mungu kwa kukubaliwa katika hekalu lake takatifu ikiwa wanaendelea kuvaa mavazi machafu.​—Linganisha Zekaria 3:3-10.

27. Ijapokuwa hawatahitaji ufufuo, watahitaji faida za utumishi gani wakati wa ile miaka elfu?

27 “Mkutano mkubwa” wanawahesabia Mungu na Mwana-Kondoo Yesu Kristo, si ufufuo kutoka makaburini ya ukumbusho, bali “wokovu” kutoka katika “dhiki ile iliyo kuu.” Kwa hiyo hawahitaji ‘kufufuliwa katika siku ya mwisho, kama wale wanaotajwa katika Yohana 6:54. Hata hivyo, watahitaji faida za utumishi wa Kuhani Mkuu Yesu Kristo pamoja na makuhani wake wadogo 144,000 wakati wa ile miaka elfu.

28. Ni “saa” ipi inayokaribia kuhusiana na wanadamu wafu waliokombolewa, na ni nafasi gani itakayowekwa mbele yao?

28 Sasa “saa” ya ajabu inakaribia. Ni “saa” ambayo katika hiyo Yesu Kristo akiwa hakimu mshirika wa Yehova atakapowaita “wote waliomo makaburini” watoke wakiwa wakombolewa wake. Watake wasitake wote watafanywa raia za kidunia za ufalme wake wa kimbinguni. Mbele yao wote watawekewa nafasi ya kuufikia uzima mkamilifu wa kibinadamu katika dunia ya paradiso.​—Yohana 5:28, 29.

29. Wakati huo “mkutano mkubwa” na wanadamu waliofufuliwa watakunywa na kula nini, nao “mkutano mkubwa” utapata nafasi gani ya pekee?

29 Basi raia za Kristo watapaswa kunywa nini wakati huo? Watakula nini? Ufufuo uliopewa mtume Yohana unaonyesha kwamba wakati huo “mto wa maji ya uzima” utakuwa ukitiririka kutoka chini ya kiti cha enzi cha Yehova Mungu na cha Mwana-Kondoo Yesu Kristo. Pande zote za “mto” kulikuwa “miti ya uzima,” izaayo matunda kila mwezi. Majani yake yalikuwa ya kuponya mataifa. “Mkutano mkubwa” na wafu waliofufuliwa, watakunywa na kula mipango ya Mungu. (Ufu. 22:1-3) Kwa kutumia kabisa fadhili zisizostahilika za Yehova Mungu kupitia kwa Yesu Kristo wale wanaothamini na kutii ufufuo wao utakuwa “ufufuo wa uzima.” Wale ambao hawakufufuliwa wa “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Kristo watapata nafasi ya kuendelea kuishi bila kufa hata kidogo na kuyarudia mavumbi ya ardhi!​

—Kutoka The Watchtower Sept. 1, 1978.

[Maelezo ya Chini]

a Katika Kiebrania, neno linalolingana na “mlaji-watu” ni okhelʹ adamʹ, linalomaanisha “mlaji wanadamu;” au, okhelʹ ben minoʹ, “mlaji mwana wa aina yake.”‏ Kwa ogofyo la mfano wa namna hii katika Yerusalemu katika” mwaka wa 70 W.K., tazama kitabu cha Yosefo “Wars of the Jews,” sura ya 3, kitabu cha 6.

b Angalia kwamba, kulingana na Ufunuo 2:​9, 17, “ile mana iliyofichwa” imewekewa Waisraeli wa kiroho wanaoshinda.​—Linganisha Waebrania 9:4.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama vile mana ilivyoendeleza uzima wa Waisraeli jangwani, ndivyo Yesu, “chakula cha uzima,” anavyoendeleza uzima wa Waisraeli wa kiroho sasa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki