Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 3/1 kur. 3-5
  • Ufunguo wa Maisha ya Jamaa Yenye Furaha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufunguo wa Maisha ya Jamaa Yenye Furaha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JAMAA KATIKA SHIDA
  • MWANZILISHI WA JAMAA
  • UONGOZI WA KUPATA MAISHA YA JAMAA YENYE FURAHA WATOLEWA
  • Je, Kuna Siri ya Kupata Furaha ya Familia?
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kuona Njia ya Kupata Furaha ya Jamaa
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Kushiriki na Wengine Siri ya Kupata Furaha ya Familia
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
  • Kujenga Pamoja Kijamaa kwa Ajili ya Wakati Ujao wa Milele
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 3/1 kur. 3-5

Ufunguo wa Maisha ya Jamaa Yenye Furaha

SISI sote tunatamani kuwa na furaha, au sivyo? Hata umri wetu uwe gani, taifa letu liwe gani, au cheo chetu maishani kiwe gani, tunataka tuwe wenye furaha. Na kwa kuwa furaha inaongezeka tunapoishiriki pamoja na wengine, tunafurahia kuona wengine wakiwa na furaha na kuridhika. Sana sana hii inakuwa hivyo kwa habari ya wale tuwapendao. Nayo hali hii njema, ijulikanayo kama furaha, inapokuwamo kati ya washiriki wa jamaa, je! si kweli kwamba inakuwa vyepesi kukabili (kuelekeana na) misiba ambayo lazima itokee katika maisha, na kuivumilia? Hivyo, basi, ni nani anayeweza kukataa kwamba maisha ya jamaa yenye furaha hayahitajiwi?

Kwa kweli, hata katika ulimwengu huu wenye machafuko, maisha ya jamaa yanaweza kuwa yenye furaha sana. Ni kweli, kazi ngumu inahitaji kufanywa, na kunakuwa na masumbufu pamoja na kujinyima. Lakini ni jamaa gani isiyoweza kukubali kwamba furaha inayopatikana inastahili hayo yote?

Hata hivyo, ijapokuwa maisha ya jamaa yanaweza kuwa yenye furaha hivyo, leo ni jamaa chache sana zilizo na furaha hiyo ya kweli. Bila shaka, jamaa ye yote itakuwa na nyakati zake za furaha na za shida; hakuna jamaa isiyopatwa na magumu. Kwa mfano, kutofahamiana kunaweza kuharibu furaha ya jamaa kukiruhusiwa kuendelee. Au mambo kadha kama vile magonjwa au mikazo kazini yanaweza kuleta wasiwasi na kuudhika upesi, kisha kutokeze maneno au vitendo vyenye majuto. Haya nayo, yanaweza kuudhi na kuharibu uhusiano. Kwa hiyo, magumu makubwa, au madogo ni sehemu ya kawaida ya maisha ya jamaa katika ulimwengu huu usiokamilika tunamoishi.

JAMAA KATIKA SHIDA

Namna za maisha katika karne hii ya 20 zimeongeza sana magumu ya jamaa hivi kwamba wengine wana mashaka sana kama mpango wa jamaa utaendelea ambao ndio msingi wa jamii ya kibinadamu. Mashaka hayo yanaletwa na mambo kama talaka zinazoendelea kuongezeka, kutengana, wanaume na wanawake kuishi pamoja bila kuoana pamoja na ngono za wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake.

Kwa kuwa jamaa nyingi sana ulimwenguni pote ziko katika hali za shida, ni jambo la akili kuuliza: Kwa sababu gani? Wajapofaulu katika mambo mengine wanayofanya, sababu gani wengi hivyo wanashindwa kufaulu katika maisha ya nyumbani? Wajapotafuta msaada kwa washauri wa jamaa, madaktari (waganga) wa akili na wengine kama hao, sababu gani hawajafahamu ufunguo wa maisha ya jamaa yenye furaha?

Lijapokuwa si jambo la kuchezewa, jibu linapatikana katika usemi ambao mara nyingi unatumiwa kwa mchezo: “Mengine yote yanaposhindwa, fuata maagizo.” Maagizo yanapofuatwa, kama vile wakati wa kutumia mashine, mara nyingi kuvunjika kwa mashine na kuitumia isivyofaa kunaweza kuepukwa. Kwa hiyo, bila shaka uongozi wa maagizo unapaswa kutafutwa kwanza. Walakini, kwa sababu ya namna hali ya wanadamu ilivyo, uongozi huo unatafutwa kama hatua ya mwisho, “mengine yote yanaposhindwa.” Lakini “maagizo” ni yapi? Yanapatikana wapi?

MWANZILISHI WA JAMAA

Jamaa ni mpango mgumu sana na uliohitaji ujuzi mwingi sana kutengeneza kuliko mashine yo yote iliyopata kutengenezwa na mwanadamu. Kwa hiyo, ni jambo lisilopatana na sayansi kabisa kudhania kwamba ulitokea kwa bahati au kwa tukio lisilotazamiwa, pasipo mbuni na mtengenezaji. Kila tukio lazima liwe na chanzo ,chake. Kwa hiyo, mwandikaji wa karne ya kwanza, alitumia sayansi sahihi aliposema: “Kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu.”​—⁠Ebr. 3:4.

Kwa hiyo maisha ya jamaa si jambo lililojitokeza. Lilitokezwa. Wakati fulani baada ya kumwumba mwanamume wa kwanza, Yule yule aliyemtokeza alisema hivi: “Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.”‏ Kisha, baada ya kuwaunganisha wazazi wetu wa kwanza katika ndoa, na kwa kupatana kabisa na kusudi lake la kuwafanya mwanamume na mwanamke, “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.” (Mwa. 2:18; 1:​27, 28) Hivyo, kwa utimizo wa kusudi la Mungu lililotajwa, mpango wa jamaa ukaanza.

UONGOZI WA KUPATA MAISHA YA JAMAA YENYE FURAHA WATOLEWA

Sasa je! Mwanzilishi wa jamaa alitazamia watoto wake wa kidunia wajifunze juu ya madaraka yao katika maisha kwa kujiamulia wenyewe? Au, je! alitupatia uongozi wa kuonyesha namna mpango wa jamaa ungefanya kazi? Kama vile tungetazamia kutoka kwa Baba mwenye upendo, alitupatia kanuni za kufuata au “maagizo” ya kutuongoza. Ufunguo wa kupata maisha ya jamaa yenye furaha unapatikana ‘tunapofuata maagizo’ juu ya maisha ya jamaa na tunapositawisha uhusiano (urafiki) mwema na Yeye aliyeyabuni, ambaye Ndiye alietuumba.​—⁠Zab. 100:3; 119:​1, 2; 128:​1, 2.

Ili tufaidike, kama miaka 3,500 iliopita, Muumba wetu mwenye upendo alianza kuandikisha uongozi huu katika kitabu kimoja chenye vitabu vingi vidogo kinachotoa mambo mengi sana juu ya jamaa. Kitabu hicho kinachopatikana sasa, kikiwa kizima au sehemu yake, kwa lugha zaidi ya 1,600, jamaa zote za dunia zaweza kukipata. Kwa sababu ya thamani yake isiyoweza kulinganishwa na cho chote kingine, bila shaka ilikuwa kwa uongozi wa Mungu kwamba kitabu hicho ndicho chenye kuenezwa zaidi katika historia yote. Bila shaka, kitabu hicho ni Biblia Takatifu.​—⁠2 Tim. 3:​16, 17.

Tukitaja Biblia Takatifu kuwa chanzo cha habari juu ya maisha, je! msomaji hawezi kuamua kwamba tunazungumza juu ya mafundisho ya makanisa juu ya habari hii? Hapana. Kwani, hata uchunguzi wa juujuu tu unaweza kuonyesha kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamemsingizia Yehova, Mungu wa Biblia, na yamebatilisha (fanya kuwa bure) Neno Lake kwa sababu ya filosofia na mapokeo yao ya wanadamu. (Zab. 83:18; Mt. 15:6) Hivyo, basi, kuvunjika kwa maisha ya jamaa kunakoonekana wazi katika nchi zao si jambo linalotukia bila sababu nzuri. Hata hivyo, matendo yenye lawama ya makanisa hayapunguzi uhakika wa kwamba Biblia ndicho kitabu cha kweli, chenye kutumainika na chenye kuleta matokeo mema tunachohitaji sana kama uongozi ili tupate ufunguo wa maisha ya jamaa yenye furaha.

Biblia ni kitabu kinachozungumza sana juu ya maisha ya jamaa. Kikituambia juu ya ndoa ya kwanza, kinatuambia sababu gani Mungu aliumba watu wakiwa wanaume na wanawake, na kwa hiyo, kusudi la ngono na mahali pake panapofaa katika maisha ya jamaa yenye heshima.

Vilevile, katika Neno la Mungu, tunaweza kusoma juu ya furaha na magumu yaliyowapata jamaa nyingi sana. Habari kama hizo za jamaa zaweza kutufaidi sana sisi sote, vijana kwa wazee. Je! wewe unatafuta mwenzi wa ndoa ambaye atajionyesha kuwa mwenzi mshikamanifu? Basi utataka kutafuta shauri la Biblia juu ya kufanya uchaguzi mzuri na juu ya kujitayarisha wewe mwenyewe kuchukua madaraka ya ndoa. Je! wewe ni mume na kichwa cha jamaa? Ikiwa ndivyo, bila shaka utafaidika kutokana na mifano mingi ya Biblia ya wanaume waliofaulu sana katika madaraka hayo. Je! wewe ni mke na mama watoto? Kwa kweli, kazi zako ni nyingi, sivyo? Hata hivyo, Biblia itakuonyesha namna ya kupata furaha unapozitimiza na namna ya kujipatia sifa kutokana na jamaa inayothamini. Au labda wewe ni mtoto. Unaweza kufanya nini usaidie kuleta hali yenye uchangamfu na upendo nyumbani kwenu? Je! ungetaka kujua? Neno lililoongozwa na Mungu litakujulisha.

Jawabu la mengi ya magumu ya maisha, kutia na magumu ya jamaa utalipata katika Neno la Mungu. Kwa kuwa yeye ni “Mungu wa furaha,” Muumba wako anataka jamaa yako ipate furaha vilevile. (1 Tim. 1:​11, NW; Mit. 2:6; 3:​13, 18) Sikuzote Mashahidi wa Yehova wako tayari kusaidia wengine wapate furaha, pamoja na upendo na amani.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki