Je! Kweli Hizi Ndizo “Siku za Mwisho”?
JE! NYAKATI hizi zenye jeuri zamaanisha kwamba sasa twaishi katika “siku za mwisho”? Wale wanaouliza ulizo hili kwa unyofu watapata jibu lenye kuridhisha. Lakini wengine wanauliza wakiwa na kusudi baya, na kwa habari zao mtume Petro anaandika hivi: “Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake [Bwana Yesu Kristo]? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, [katika mauti], vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.” (2 Pet. 3:3, 4) Katika ulimwengu wa leo usiomwogopa Mungu, wanaolidhihaki Neno la Mungu hivyo ni wengi sana—jambo hilo lenyewe likionyesha kwamba tumeingia katika “siku za mwisho.”
Petro anawakumbusha wenye dhihaka hao namna ulimwengu wa siku za Nuhu ulivyoharibiwa kwa gharika, na kuongeza hivi:
“Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo [la Mungu], zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.”(2 Pet. 3:5-7)
Mamlaka za kiserikali pamoja na jamii za kibinadamu za huu ulimwengu mwovu wanaelekeana na uharibifu kama huo. Lakini je! kweli sisi tunaweza kuwa na hakika kwamba hizi ndizo “siku za mwisho”?
USHUHUDA WA “SIKU ZA MWISHO”
Mtume Paulo anatuambia kwamba “katika siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari,” na kuongeza hivi:
“Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.”
Kisha Paulo anatuambia tujiepushe na watu kama hao. (2 Tim. 3:1-5) Je! sisi hatuoni ukosefu huu wa upendo wa kweli, maoni haya ya ‘kujitanguliza’ yakitiliwa mkazo ulimwenguni pote leo? Yanaongeza sana magumu yenye hatari ya wakati wetu.
Roho hii ya ulimwengu ya kufuatia mambo ya kimwili hata inahatarisha kundi la Kikristo. Ndiyo sababu Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu anawaonya watu matajiri wasiishi maisha ya anasa, au kwa kufuata tamaa za mwili, akiwaambia; “[kitu] kama moto mmejiwekea akiba katika siku za mwisho.” (Yak. 5:1-5) Kwa hiyo, “siku za mwisho” si wakati wa Wakristo wa kweli kufuata njia za kujifurahisha anasa nyingi mno za ulimwengu huu wenye uadui na Mungu.
Tumekwisha jifunza kwamba kipindi cha vita vya ulimwenguni pote pamoja na mambo yenye kuogopesha kilianza duniani katika mwaka 1914. Ni wachache sana wanaoweza kubisha kwamba 1914 ulianza badiliko kubwa lisilo na mfano katika mambo ya wanadamu, “mwanzo wa utungu,” kama alivyoueleza Yesu. Ndiyo, “mwanzo,” nao unabii mkubwa wa Yesu, ulioandikwa katika Mathayo sura ya 24 na 25, Marko 13 na Luka 21, unatoa maelezo mengi juu ya taabu isiyo na mfano ambayo imewapata wanadamu tangu 1914: vita, njaa, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kipuku, matukio yenye kuogopesha, uvunjaji wa sheria, kukosa upendo, woga, dhiki. “Chukizo la uharibifu,” ambalo pia linajulishwa katika Ufunuo 17:3, 8 kuwa “mnyama mwekundu sana,” vilevile limeonekana, kwanza akiwa Ushirika wa Mataifa na baadaye akiwa Umoja wa Mataifa, walakini hakupata kuwapa wanadamu njia ya kutokea.—Mt. 24:15, 16; Dan. 11:31.
Wafuasi wa kweli wa Kristo wamelazimika kuvumilia taabu hizi pamoja na ulimwengu wote kwa jumla. Vilevile Wakristo wamepatwa na magumu mengine ya ziada kama yalivyoelezwa na Yesu katika unabii wake: hukumu mahakmani, kupigwa, chuki na mateso. Katika wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu waliwindwa na kudhulumiwa hata katika nchi za kidemokrasi. Kabla na katika wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu walichukiwa sana na Wanazi, Wafascisti na Washinto. Katika nyakati za karibuni, Mashahidi wamechukiwa sana na nchi za Kikomunisti za Ulaya pamoja na nchi fulani za Afrika zenye kutaka mabadiliko. Walakini, enyi Wakristo, jipeni moyo! Haya yote yamewapata “ili ubora uliojaribiwa wa imani yenu, iliyo na thamani kubwa zaidi sana kuliko dhahabu inayoharibika ijapokuwa inajaribiwa kwa moto, uonekane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima katika ufunuo wa Yesu Kristo.”—1 Pet. 1:7, NW.
USHUHUDA WENYE NGUVU
Ushuhuda wenye kusadikisha wa kwamba sasa tunaishi katika “siku za mwisho” unaonekana katika kazi ambayo Bwana Yesu Kristo amekuwa akiongoza duniani tangu mwaka huo wenye msiba wa 1914. Inatimiza sehemu ile ya unabii wake mkubwa ambayo imeandikwa katika Mathayo 24:14, NW:
“Na habari hizi njema za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”
Mbele kidogo katika unabii huu, Yesu alieleza namna kazi hii ingefanywa duniani chini ya uongozi wake na wa malaika watakatifu wa mbinguni:
“Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.”
Jamii ya “kondoo” wenye haki waingia katika uzima wa milele, bali “mbuzi” wasiothamini wauendea uharibifu wa milele.—Mt. 25:31-46.
Hivyo, katika “siku za mwisho,” ushuhuda mkubwa kuhusu ufalme wa Kristo unaokuja unapaswa kutolewa ulimwenguni pote. Je! ushuhuda huo umeonekana tangu 1914? Bila shaka umeonekana! Wanahistoria wa kisasa wana maandishi yanayoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wameeneza mahubiri yao duniani pote. Kukawa na matokeo gani? Kufikia mwaka 1977 walikuwa wamegawa Biblia na vitabu vyenye kueleza Biblia zenye idadi 4,831,823,111 katika lugha 210 tofauti, na kufanya watu zaidi ya milioni mbili kuwa wanafunzi Wakristo katika nchi na maeneo 216 na kufariji mamilioni wengine kupitia kwa mafunzo ya Biblia ya bure nyumbani mwao. Kazi hii, inayofanywa kwa utimizo wa unabii wa Yesu, ni ushuhuda wenye nguvu kweli kweli kwamba kwa kweli hizi ndizo “siku za mwisho.”
“SIKU ZA MWISHO”
Unabii mwingine wa Biblia, sana sana ule wa Isaya sura ya 2 na Mika sura ya 4, unataja “siku za mwisho.” Ushuhuda wa namna hizi mbili za unabii unakaribia sana kufanana, kwa wazi, ukirudiwa ili kutia mkazo. Ebu angalia vile Mika 4:1, 2, linavyosema:
“Itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”
Hivyo, katika lugha nzuri sana ya mfano, nabii huyo anaeleza namna hekalu la kiroho la Yehova—nyumba yake ya ibada—inavyotukuzwa juu zaidi ya namna nyingine za ibada za kibinadamu, katika siku za mwisho, ndiyo, “juu ya vilima.” Watu wa mataifa yote wanaiendea nyumba ya Yehova ya ibada makundi makundi, ambapo wanapokea mafundisho yake na kujifunza kutembea katika njia zake za haki. Kuna wakati mmoja tu katika historia’ ya kibinadamu ambapo “watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” kuizunguka dunia yote, wameunganishwa katika ibada moja ya Mungu wa kweli. (Ufu. 7:9) Unabii huu unaohusu “siku za mwisho” unatimizwa machoni petu leo, kati ya mashahidi Wakristo wa Yehova.
Walakini, unabii huo una jambo jingine la maana linalotimizwa leo. Jambo gani hilo? Yasikilize maneno haya mengine:
“Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.—Mik. 4:3.
Je! panga zinafuliwa leo na kuwa majembe? Hakika mataifa ya dunia hayafanyi hivyo! Wanaendelea kujipatia silaha, tena silaha zilizo zaidi ya mapanga na mikuki! Wanaendelea kujilundikia silaha zenye kuogopesha zinazoweza kuangamiza watu wengi ajabu kwa mara moja, katika mipango ya kujipatia silaha ambayo inaendelea kwa haraka sana hata haizuiliki. Uwezekano uliopo unaogopesha sana. Kama vile Richard J. Barnet alivyoandika katika gazeti la New York Times la Juni 6, 1978:
“Ama tugeuze kanuni ambazo mataifa yote yenye uwezo yanatumia katika mchezo—kwa kuweka vizuizi vikubwa, visivyo vya mchezo, katika makao ya majeshi, katika usafirishaji wa silaha duniani pote, katika matendo ya siri—au mchezo tunaocheza utamalizikia katika vita ya makombora yenye sumu katika wakati wetu.”
Walakini, kuna jamii ya watu katika wakati wetu ambayo haishiriki katika “mchezo” huo. Kikundi hiki ni kile kinachojulikana kama Mashahidi wa Yehova. Ikiwa ‘wangejifunza vita,’ hii ingewafanya wapigane na ndugu zao Wakristo katika sehemu nyingine za ulimwengu. Wao wanapendelea zaidi kusitawisha upendo kwa Wakristo wenzao, na kwa wanadamu wengine wote, na kwa njia hiyo wanashiriki katika kuutimiza unabii wa Mika. Kutokuwamo kwa Mashahidi kumewafanya waheshimiwe katika sehemu nyingi za Afrika, katika Ireland, katika Lebanoni na katika sehemu nyingine ambako dini imegawanya watu katika vikundi vya watu wenye kupiga vita. Kwa kuendelea ‘kufua panga zao kuwa majembe,’ hata wanapokuwa chini ya mikazo ya mateso, watu wa Yehova wanaonekana wakitimiza unabii huu “katika siku za mwisho.”
Kwa furaha, “katika siku za mwisho” duniani leo kuna jamii moja ya watu waliounganishwa katika vifungo vya upendo ulimwenguni pote, ambayo imeazimia kutembea, si kulingana na “miungu” ya dini zenye mgawanyiko, bali katika jina lenye thamani sana la ‘Yehova Mungu wao,’ milele na milele. (Mik. 4:5) Wanaamini kabisa, kulingana na unabii uliotimizwa, kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” na ya kwamba, kama alivyoeleza Petro, “siku ya [Yehova] itakuja kama mwivi” kuiharibu taratibu mbovu ambayo sasa inaitawala dunia ya Mungu. Kwa hiyo, wao ni wenye bidii katika kulitii onyo hili la upole:
“Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafunuliwa hivyo, yawapasa ninyi mwe watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa, mkingojea na kuhimiza akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.”—2 Pet. 3:10-12, NW.
“Siku” hiyo haitamaliza ‘kutembea kwao katika jina la Yehova Mungu wao,’ kwa kuwa wanatazamia kufanya hivyo milele na milele. Kwa hiyo, wakitazamia kwa shauku sana mpango wa ajabu sana wa Yehova wa taratibu mpya, wanafanya yote wawezayo ili wastahili kuingia wakati huo wenye utukufu sana. Tumaini lao lenye furaha linaonyeshwa katika maneno haya mengine ya Petro:
“Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.” (2 Pet. 3:13, NW)
Hili ni tumaini halisi, tumaini la sasa, kwa kuwa ushuhuda wote unaonyesha kwamba kwa kweli hizi ndizo “siku za mwisho” za taratibu ya ulimwengu iliyopo. Ni jambo la muhimu sana tuzijue kwamba hivyo ndivyo zilivyo.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Watu kutoka katika kila taifa duniani pote hawajapata hata kidogo kuunganishwa hapo mbele katika ibada safi kwa msingi wa Biblia