Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 3/15 kur. 12-17
  • “Kesheni”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kesheni”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • PINGA USINGIZI WA KIROHO
  • WALE WAPANDA FARASI WANGALI WAKIWAPANDA
  • USIVUTWE NA MAMBO MENGINE!
  • Wana-Farasi Wanne Katika Mwendo!
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Mpanda Farasi wa Ufalme Aendelea
    “Ufalme Wako Uje”
  • Kazi Tukufu Inayofuata Uendeshaji wa Wapanda-Farasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Wapanda Farasi Wanne​—Jinsi Wanavyokuhusu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 3/15 kur. 12-17

“Kesheni”

“Kesheni na kusali [daima] ili msiingie katika majaribu.”​—⁠Mat. 26:​41, Habari Njema kwa Watu Wote.

1, 2. (a) Kulikuwako matukio gani hata Yesu akawaambia mitume wake, “Kesheni”? (b) Lakini mitume hao waliitikiaje?

YESU aliposema maneno hayo, hali ilikuwa namna gani? Ulikuwa wakati wa hatari iliyo kubwa kuliko zote katika maisha yake ya hapa duniani​—⁠jioni ya kusalitiwa kwake, kukamatwa, kuhukumiwa na kuuawa. Siku hiyo ingekuwa ya maana zaidi katika historia ya wanadamu. Mambo yanayokaribia kutukia yangeongoza kwenye wokovu wa wanadamu wote. Siku hiyo, Yesu angeutoa uhai wake iwe dhabihu. Akiwa Mwana ambaye ametumikia kwa uaminifu mpaka mwisho, angeweza kupiga ripoti kwa Baba yake kwa maneno haya wakati wa kufa kwake: “Yametimia!”​—⁠Yohane 19:​30, Habari Njema kwa Watu Wote.

2 Lakini, mitume wa Yesu walikuwa wakifanya nini? Hapakuwa pamepita muda mrefu tangu waliposhiriki pamoja na Bwana wao katika kuanzisha Ukumbusho wa kifo chake. Ijapokuwa hawakuthamini maana yake, walijua kwamba ulikuwa wakati wenye hatari sana. Hata hivyo, walilala usingizi wakati alipokuwa akisali katika bustani ya Gethsemane! Alikuwa amewaambia hivi: “[Nafsi] yangu ina uchungu mkubwa mno, hata karibu nife. Kaeni hapa mkeshe pamoja nami.” Lakini mara tatu, kila aliporudi aliwakuta wakisinzia. Katika pindi ya tatu, Yesu alipaza sauti hivi: “Je, mngali mmelala na kupumzika? Tazameni! Saa yenyewe imefika.” Na wakati huo adui zake wakawa wamemfikia!​—⁠Mat. 26:​36-47, Habari Njema kwa Watu Wote.

3. (a) Sababu gani huu ndio wakati wa maana kuliko wote wa kuendelea kukesha? (b) Sababu gani ingekuwa hatari sana kushindwa kutii onyo la Ufunuo 16:15?

3 Leo tuko karibu na tukio jingine kubwa katika historia ya wanadamu​—⁠ile “dhiki kubwa,” ambayo mwisho wake utakuwa ni “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–​Magedoni. (Mt. 24:21; Ufu. 7:14; 16:14, 16) Huu ndio wakati wa kukesha kuliko nyakati zote! Hata hivyo unabii wenyewe unaosimulia vita hiyo inayokuja, unaonya juu ya watu ambao huenda wasikeshe. Onyo hilo limetiwa katikati ya mtajo wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” na ule wa “Har–​Magedoni.” Ni Bwana Yesu Kristo mwenyewe anayetoa onyo hili: “Sikiliza! Mimi naja kama mwizi! Heri mtu akeshaye na kuvaa nguo zake ili asije akaenda uchi huku na huko mbele ya watu.” Inawapasa wale walio katika utumishi wa Mungu wa ukuhani leo, na vilevile “umati mkubwa wa watu,” waangalie wasije wakapoteza mavazi yao ya kuwatambulisha. Na ni kitu gani kinachowatambulisha kuwa watumishi wa Mungu leo? Ni kazi zao za bidii, wanapozungumza pamoja na watu nyumbani kwao na mahali pa watu wengi, na kuzoea katika maisha yao kanuni njema zile zile za Kikristo wanazopendekeza kwa wengine. Mtumishi wa Mungu akilala usingizi wa kiroho, angepata aibu (haya) kubwa. Angevuliwa hali ya kujulikana kuwa shahidi wa Mungu wa kweli. Jambo hilo lingekuwa la hatari wakati wa “vita kuu Siku ile ya Mungu Mwenyezi.”​—⁠Ufu. 16:​14-16, Habari Njema kwa Watu Wote.

PINGA USINGIZI WA KIROHO

4. Jambo ambalo ni tisho (ogopesho) kubwa kwa taratibu ya mambo leo ni nini?

4 Zamani, hali duniani hazijapata kuwa zenye hatari zaidi kama zilivyo leo. Viongozi wa siasa wanakubali uhakika huo. Mchafuko katika utawala na jeuri vinaongezeka haraka kuzunguka dunia yote. Hata tukitazama kwa maoni ya kilimwengu, taratibu iliyopo ya mambo inazidi kuwa mbaya sana, nayo iko katika hatari ya kuharibiwa wakati ujao uliotangulia kuonwa. Lakini kulingana na maoni ya Mungu, taratibu hii iko katika hali gani? Yehova anatangaza kwamba ataivunja vipande wakati ingali ikitenda kazi. (Dan. 2:​44, 45) Hiyo itakuwa karibuni sana, kwani mambo yanaharibika haraka katika kizazi hiki cha uvunjaji wa sheria na chenye jeuri.

5. Yesu alikazia nini alipokuwa akisema habari za mwisho wa taratibu ya mambo”?

5 Bwana Yesu Kristo alitoa unabii wazi-wazi juu ya wakati wetu. Katika unabii huo, alikazia mara nyingi lazima ya kukesha. Haya ni maneno yake machache, kama yanavyoripotiwa katika njia mbali-mbali:

“Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.”​—⁠Mt. 24:42.

“Jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”​—⁠Mt. 24:44.

“Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa.”​—⁠Mt. 25:13.

“Bali ninyi jihadharini; nimekwisha kuwaonya yote mbele.”​—⁠Marko 13:23.

“Mwe macho, kesheni, maana hamjui wakati huo utafika lini.”​—⁠Marko 13:​33, Habari Njema kwa Watu Wote.

“Kesheni basi, kwa maana hamjui ajapo bwana.”​—⁠Marko 13:35.

“Na hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.”​—⁠Marko 13:37.

“Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha.”​—⁠Luka 12:37.

“Jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu.”​—⁠Luka 12:40.

“Siku ile [itawajilia] ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni.”​—⁠Luka 21:​34-36.

6. Yesu anakazia nini kwa habari ya “mambo ambayo yanapaswa kutukia karibuni”?

6 Vilevile, katika ufunuo wake wa mwisho juu ya “mambo ambayo yanapaswa kutukia karibuni,” tena Yesu anakazia hali hiyo ya ghafula ya kuja kwake:

“Ninakuja kwako upesi. Linda, basi, ulicho nacho sasa.”​—⁠Ufu. 2:16; 3:​11, Habari Njema kwa Watu Wote.

“Sikiliza! Naja upesi. . . . Naam! Naja upesi.” ​—⁠Ufu. 22:​7, 20, Habari Njema kwa Watu Wote.

Katika kuitikia maneno hayo ya mwisho ya Bwana wetu, bila shaka kila mmoja wetu anajiunga na mtume Yohana katika kusema: “Amina. Na iwe hivyo! Njoo Bwana Yesu.”

7. Sababu gani inatupasa tuendelee kuwa macho?

7 Usikosee! Ulimwengu huu unaelekea haraka kwenye mwisho wake. Unapata maumivu ya kifo. Inasemekana waziwazi kwamba miji mingi mikubwa inatoweka. Lakini Yehova ataiondoa katika taabu yayo kabla haijaweza kutoweka yenyewe. Inatupasa tuendelee kuwa macho, tuwe tayari kwa ajili ya siku ile kuu ambayo manabii wengi sana wa Yehova wamesimulia habari zake.​—⁠Isa. 2:​12, 17; Yer. 30:7; Yoeli 2:11; Amosi 5:​18-20.

8. (a) Sababu gani ‘tuzidi kumngojea’ Yehova? (Sef. 2:3) (b) Ni hali gani iliyo katika Umoja wa Mataifa inayotaka tuwe wenye kukesha?

8 Nabii Sefania, aliyekuwa mkuu katika ukoo wa Daudi, alitangaza hivi:

“Ningojeni, asema [Yehova], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”​—⁠Sef. 3:8.

Siku hiyo ya “hasira” kali ya Yehova inakaribia kwa hatari sana. Unabii mkubwa wa Yesu mwenyewe juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo” umetimizwa sasa kiajabu katika karne yetu ya 20 tangu mwaka 1914. Tunaona waziwazi majeshi ya lile “chukizo,” yaani, chama cha Umoja wa Mataifa, yakiwa tayari kuharibu makao ya Jumuiya ya Wakristo. Serikali za kikomunisti zinaonyesha waziwazi chuki yazo juu ya dini, zikiita “afyuni ya watu.” Usikosee! Wakati wa Mungu utakapofika, zile “pembe” za yule mnyama mwekundu sana, yaani, Umoja wa Mataifa, zitaigeukia milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ambayo imekufuru jina la Yehova kwa muda mrefu, ziiharibu kabisa kabisa.​—⁠Mt. 24:15; Ufu. 17:​3-6, 16.

9. Sababu gani ile “dhiki kubwa” itakuwa wakati wenye majaribu kwa watu wa Mungu duniani?

9 Bila shaka, ile “dhiki kubwa” itakuwa wakati wenye kujaribu imani ya watu wa Mungu mwenyewe hapa duniani. Kwa maana zile “pembe kumi” zitapigana vilevile na Bwana Yesu Kristo, aliye “Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme.” (Ufu. 17:14) Serikali hizo za kidunia haziwezi kumfikia kule mbinguni, basi zitashambulia nani wengineo kuliko wajumbe wake waaminifu waliopo hapa duniani, na sana sana mabaki ya mashahidi watiwa mafuta wa Yehova? Lakini hawatashinda! “Mwana-kondoo pamoja na wale aliowaita na kuwachagua, ambao ni waaminifu, atawashinda.” (Habari Njema kwa Watu Wote) Ufunuo 19:​11-21 unaeleza zaidi habari ya kushindwa kwa serikali za dunia za kisiasa na huyo “MFALME WA WAFALME NA BWANA WA MABWANA.”

WALE WAPANDA FARASI WANGALI WAKIWAPANDA

10. Sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu atashinda kwa ajili yetu?

10 Yule mshindi mwenye nguvu katika Har–​Magedoni atapigana akiwa mbinguni. Mtume Yohana alimwona katika maono akipanda farasi mweupe, kufananisha vita ya haki. Alisema hivi: “Nikaona mbingu zimefunguliwa; na huko alikuwako farasi mmoja mweupe, na mpanda farasi wake aliitwa: “Mwaminifu” na “Kweli”. Huyo huhukumu na kupigana kwa ajili ya haki.” Vita hiyo itawatokezea wanaopenda haki baraka. (Ufu. 19:​11, Habari Njema kwa Watu Wote) Hapo mapema katika Ufunuo, Yohana aliandika maono mengine ya mpanda farasi yule yule, katika maneno haya: “Mimi nikatazama, na kumbe palikuwa na farasi mmoja mweupe hapo. Na mpanda farasi wake alikuwa na upinde, akapewa na taji. Basi, akatoka kama mshindi aendelee kushinda.” (Ufu. 6:2, Habari Njema kwa Watu Wote) Katika maono hayo, twamwona Yesu akipokea mamlaka ya Ufalme katika mwaka 1914, akiwa si kama kitoto kichanga kisicho na uwezo katika hori ya kulia ng’ombe, au maiti mtini, bali akiwa shujaa mwenye nguvu wa vita kuliko ye yote ambaye amepata kupigana vita. (Ufu. 11:15; Mt. 25:31) Tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba huyu “Mfalme wa wafalme” atashinda kwa ajili yetu.

11. (a), Sababu gani wale wapanda farasi wengine wa Ufunuo 6 hawawezi kushinda? (b) Yule mpanda ‘farasi mwekundu’ ametimiza nini, na tangu wakati gani?

11 Walakini, wapanda farasi wengine wanaonwa katika maono hayo. Hawatajwi kuwa wanashinda, bali, badala yake, wanatajwa kuwa wakiwatesa wanadamu. Mpanda farasi mweupe ndiye mwenye ushindi peke yake, maana ni haki itakayoshinda pamoja naye. Lakini Yohana alisema nini juu ya wapandaji hao wengine? “Palikuwapo farasi mwingine hapo, mwekundu. Mpanda farasi wake alikabidhiwa jukumu la kuondoa amani duniani, watu wauane; akapewa upanga mkubwa.” (Ufu. 6:​4, Habari Njema kwa Watu Wote) Katika maono hayo, vita yenye damu nyingi ya namna ya pekee, iliyotokea mwaka 1914, inaonyeshwa katika mfano huo. Vita hiyo iliitwa na wanahistoria, “Vita Kuu.” Lakini wakati huo “upanga mkubwa” ulipotumiwa katika Vita ya Pili ya Ulimwengu iliyoleta uharibifu mkubwa tangu mwaka 1939 mpaka 1945, mauaji hayo yalikuwa makubwa mara nne kuliko yale ya vita iliyotangulia. Nayo jeuri inaendelea kutokea katika dunia yote, Tangu mwaka 1914, amani ya kweli imekuwa haipo, kwa sababu farasi huyo mwekundu anazidi kutembea kwa kuogopesha sana. Ijapokuwa Mashahidi wa Yehova hawashiriki vita hivyo, hata wamepatwa moja kwa moja au kwa njia nyingine na jeuri, mateso na taabu inayofuatana na ‘kuondolewa huko kwa amani duniani.’

12. Yule mpanda farasi wa tatu anafananisha nini, na hilo linahusuje watu wa Mungu mwenyewe?

12 Yohana mwenye kukesha alimwona bado mpanda farasi mwingine akiwa anapanda. “Kumbe palikuwapo farasi mmoja hapo, mweusi. Mpanda farasi wake alikuwa na vipimo viwili vya kupimia uzito mkononi mwake. Nikasikia kitu kama sauti . . . ilisema, “Kibaba kimoja cha unga wa ngano kwa kiasi cha fedha dinari moja, na vibaba vitatu vya shayiri kwa dinari moja. Lakini usiharibu mafuta wala divai!” (Ufu. 6:​5, 6, Habari Njema kwa Watu Wote) Mpanda farasi huyo wa tatu anafananisha njaa kuu, na njaa kuu inapotokea watu wanapimiwa chakula, kama vile wakati wa vita ya kutumia vifaa vyote. Hata vitu vya lazima sana, ngano na shayiri, vimekuwa vichache sana. Wale wenye mali wanashtuka sana, visije vitu vyao vya anasa, kama ‘mafuta na divai,’ vikachukuliwa. Mpanda farasi huyo amepanda kwa hasara kubwa katika dunia yote tangu mwaka 1914. Kupunguka kwa thamani ya fedha, kuendelea kupanda kwa bei ya vitu, ukosefu wa imara ya mpango wa fedha na upungufu wa mafuta, yote hayo yanaletwa na mpandaji huyo wa farasi. Hata hivyo, watu wa Yehova wenyewe hawapaswi kuvunjika moyo kwa sababu ya kuwa na chakula chache wala kupungukiwa na fedha wanakopaswa kuvumilia kwa muda. Kumbuka, mpanda farasi mweupe huyo anatangulia, naye atamaliza mambo hayo.

13. Yule mpanda farasi wa nne analeta nini, pamoja na matokeo gani kwa watu wa Yehova?

13 Walakini, bado anatokea mpanda farasi mwingine. Yohana anatoa maelezo haya: “Nami nikatazama, na kumbe alikuwapo farasi mmoja hapo, rangi yake kijivu. Na jina la mpanda farasi wake lilikuwa Kifo, na Kuzimu alimfuata nyuma. Hao walipewa mamlaka juu ya robo moja ya dunia, wawaue watu kwa upanga, njaa, tauni, na kwa wanyama wakali wa dunia.” (Ufu. 6:​8, Habari Njema kwa Watu Wote) Huyu ndiye wa mwisho kati ya wapanda farasi wote; mwenye kuogopesha sana, kwani anailetea dunia magonjwa yenye kuharibu sana. Alianza baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu wakati alipoua watu kama milioni 20 kwa ugonjwa wa homa mbaya ya mafua ya Spania katika miaka ya 1918 mpaka 1919. Na bado mpanda farasi huyo angali akipanda. Ijapokuwa kumekuwako maendeleo katika uvumbuzi wa dawa, jamii ya wanadamu ingali ikisumbuliwa leo na magonjwa ya kipuku (magonjwa mabaya sana ya kuambukia). Matumizi ya dawa za magonjwa yanaongezeka sana. Lakini kuongezeka kwa magonjwa ya moyo, kifafa, donda baya, kaswende na kisonono na masumbuo yasiyohesabika, kunapeleka wengi kaburini. Sana sana katika huu “wakati wa mwisho,” kaburi (katika Kiebrania Sheol) halisemi “Inatosha!” (Mit. 30:​15, 16, NW) Vilevile watu wa Yehova wameumizwa na kupandwa kwa farasi huyo wa rangi kijivu, mwenye kuua, maana wao ni wanadamu wenye kupatwa na magonjwa. Lakini wao wanajua sababu ya magonjwa yao ya mwili, nao wako tayari kuyavumilia wakiwa na furaha, maana wanajua kwamba dhabihu ya Yesu itaondoa karibuni magonjwa hayo yote ya kuambukia​—⁠hata mpanda farasi mwenyewe, yaani, Mauti. Wajapokufa na kuzikwa kaburini, wameahidiwa kufufuliwa katika taratibu mpya yenye haki.​—⁠Yohana 5:​28, 29.

14. Sababu gani imetupasa tushukuru kwa sababu ya maono hayo, nayo?

14 Kupanda kwa hao wapanda farasi kunaonekana wazi hata leo. Wanadamu wote sasa wanapatwa na vita vya kutumia vifaa vyote, upungufu wa chakula, magonjwa ya kipuku na kifo cha kuua watu wengi kama mainzi. Lakini ni wale tu wanaoona kwa macho ya imani, ndio wanaomwona farasi huyo mweupe, pamoja na “Mfalme wa wafalme” ambaye ni mshindi, yaani, yule mtu aliyevikwa taji na mwenye upinde. Jinsi inavyotupasa tushukuru kwa sababu ya maono hayo yenye kutia imani nguvu! Yamepaswa yatuchochee tuwe na bidii sana katika kutoa ushuhuda wa mambo hayo. Katika njia hiyo, tunaweza kuwa washikamanifu kwa agizo lililotoka kwa Yehova kwa kufuata mfano wa Yesu, ambaye akaitwa “Mwaminifu na wa kweli”​—⁠“Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli.”​—⁠Ufu. 3:14; 19:11.

USIVUTWE NA MAMBO MENGINE!

15. Sababu gani tuliamini Neno la Mungu kuliko neno la wanadamu?

15 Ulimwengu hauamini kwamba mwisho wake umekaribia. Ungependa utuvute tusiamini hivyo, vilevile. Lakini wewe utamwamini nani​—⁠maneno yao au Neno la Mungu? Ni Neno la Mungu linaloeleza wazi kwamba tunaishi katika “mwisho wa taratibu ya mambo.” Wala hata silaha za makombora ya atomiki za “mungu wa ngome”​—⁠zinazosifiwa na “mfalme wa kaskazini”​—⁠haziwezi kitu katika kupigana na “Mfalme wa wafalme” aliye mshindi kabisa.​—⁠Dan. 11:​38, 45.

16. Ni shauri gani jema ambalo Paulo anatoa katika Waroma 13:​11, 12, nasi tunaweza kuitikiaje?

16 Mtume Paulo anampa shauri jema ye yote anayeelekea kama amekuwa mwenye kusinzia, akisema:

“Sasa ndio wakati wa kuamka usingizini; naam, wokovu wetu u karibu zaidi sasa kuliko wakati ule tulipoanza kuamini. Usiku unakwisha na mchana unakaribia. Basi, tutupilie mbali mambo yote ya giza, tukajitwalie silaha za mwanga.” (Rom. 13:​11, 12, Habari Njema kwa Watu Wote)

Silaha hizo za mwanga twazijua sana, maana limekuwa pendeleo letu la maana kuzitumia katika kutangaza “habari njema ya ufalme” katika dunia yote kuwa ushuhuda.​—⁠Mt. 24:14; Efe. 6:​11-17.

17. Tunaweza kuepukaje “mambo yote ya giza”?

17 Walakini, namna gani “mambo yote ya giza”? Hayo ni matendo ya ulimwengu, mambo ambayo watu wenye kufikiria mambo ya kimwili wanapenda kufanya pasipo kumfikiria Mungu na njia yake ya nuru. Kwa hiyo imetupasa tuyaepuke. “Mwenendo wetu uwe wa adabu kama inavyostahili wakati wa mwanga; tusiwe na ulafi na ulevi, uchafu na uasherati, ugomvi na wivu.” (Rom. 13:​13, Habari Njema kwa Watu Wote) Hayo ni mambo ya ulimwengu ambayo yangeingia katika maisha yetu ya Kikristo na katika kundi ikiwa tungeyaruhusu. Ni lazima tujihadhari nayo. Katika nchi zenye utajiri zaidi, kwa kawaida watu wanaona kustarehe na kuwa na mali za kimwili ni kwa maana sana. Mahali pengi, ile juma ya kufanya kazi inazidi kuwa fupi sana, kupenda anasa kunazidi kuongezeka, na watu wa Mungu wanakazwa wawe kama ulimwengu ulivyo. Je! tutashinda tatizo hilo katika roho ya Kikristo ya kujinyima?

18. Kukaza fikira zetu juu ya mambo ya kiroho kutakuwa ulinzi wetu namna gani?

18 Tukiwa wenye bidii katika utumishi wa Mungu, tukiwa macho na kukesha ili tufanye utumishi huo, basi hatutakuwa na wakati wa kuvutwa na “ulafi na ulevi,” pamoja na “uchafu na uasherati.” Kumpenda kwetu Yehova na kupenda utumishi wake, na kutanguliza hayo, kutakuwa ulinzi wetu. (Mt. 6:33) Fikira zetu zikiwa juu ya mambo ya kiroho, na juu ya kusitawisha tunda la roho, tutakuwa wanyenyekevu na wenye kufahamu katika uhusiano wetu na jamaa zetu na ndugu zetu. Tutaepuka “ugomvi na wivu.”

19, 20. (a) Ni mfano gani bora ambao Yesu alituachia sisi? (b) Tutapataje faida tukitii shauri katika Waroma 13:14?

19 Mtume Paulo anaendelea kusema: “Bwana Yesu Kristo awe vazi lenu; msishughulikie tena tamaa zenu za maumbile na kuziridhisha.” (Rom. 13:​14, Habari Njema kwa Watu Wote) Lo! Bwana Yesu Kristo ni mfano wetu bora kweli kweli! Katika huduma yake yote ya hapa duniani, yeye alikuwa macho ili afanye mapenzi ya Yehova, lililokuwa pendeleo lake bora. Hakuna hata wakati mmoja alipoepuka utumishi wake wa nafsi yote wa kujulisha wengine jina la Baba yake. Hata siku aliyopaswa kufa, lo! jinsi alivyoonyesha upendo na kujinyima, akitumia kila dakika ya saa zake zilizobaki ili awape wanafunzi wake maagizo yanayofaa! (Yohana sura 13 kufika 17) Yesu alipokuwa akikaribia mwisho wake katika mti wa mateso, alikataa dawa ya kulevya ambayo labda ingepunguza maumivu yake makali. Yeye alitaka atunze kabisa akili zake, awe mwenye kushika ukamilifu mpaka mwisho.​—⁠Mt. 27:34.

20 Sote na tuhesabiwe kuwa pamoja na wale wanaomfanya “Yesu Kristo awe vazi” lao, wakizifuata sana nyayo zake. (1 Pet. 2:21; Mt. 16:​24, 25) Kwa kutangulia kupangia mambo ya kiroho, si ya kimwili, tunaweza kuendelea kukesha sana katika utumishi wa Yehova kama Yesu. Basi na tuendelee kukesha, tukiyajaza maisha yetu utumishi wa Ufalme mpaka ile saa ambayo “Mwana wa Adamu” atakapokuja kutekeleza hukumu. Zawadi yetu itakuwa kubwa! ​—⁠Kutoka The Watchtower, Oct. 1, 1978.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki