Kuishi Pamoja na Ugonjwa
MFALME DAUDI alikuwa mgonjwa sana, na adui zake walikuwa wakitumaini kwamba atakufa. Ingawa walikuwa wakiangalia kwa hamu sana ishara ya kuendelea kuharibika kwa afya ya mfalme, wageni walikuwa wakimtakia vema kwa unafiki. Baadaye walikuwa wakifurahia kuwaambia wengine mambo yasiyofaa waliyoona. Wakawa wakisema, “Ugonjwa unaoelekea kuleta kifo umejaa mwilini mwake. Sasa anapolala yu mgonjwa, hatainuka tena.” Hata rafiki yake wa karibu sana mshauri aliyetumainiwa Ahithofeli, akawa msaliti wake.—Zab. 41:6-10, The New American Bible.
Ni kitu gani kilichomsaidia Daudi avumilie wakati huo wa ugonjwa mbaya sana? Yeye hakupoteza tumaini na kushindwa na woga unaodhoofisha. Tumaini lake kwa Mungu liliendelea kuwa lenye nguvu, kwa sababu alisema hivi: “[Yehova] atamtegemeza [mtumishi wake] alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia [au, “bila shaka kitanda chake chote utakibadilisha wakati wa ugonjwa wake,” NW].” (Zab. 41:3) Mwishowe Daudi alipata nafuu.
Lakini Aliye Juu Zaidi anawategemezaje watumishi wake walio wagonjwa? Kwa njia ya roho yake, Yehova Mungu analeta akilini mwa mgonjwa mawazo ya kufariji na kutia tumaini lao nguvu. Anayofanya Mungu kuhusiana na jambo hili ni ya maana sana katika kupata nafuu.
Inafaa kuona kwamba madaktari (waganga) wa kisasa wamepata kufahamu ubora wa tumaini katika kupata nafuu. Kwa mfano, katika kitabu The Vital Balance, Dakt. Karl Menninger ameandika hivi: “Maarifa yetu ya kisasa ya kisayansi hayatoshi kufahamisha au kutambulisha au kusifu inavyostahili nguvu zote zitendazo kwa ajili ya kuponya kama vile tusivyojua nguvu zote tunazoshindana nazo. Na tunajua hili: Nyakati nyingine tumaini linashindwa, na kifo kinatokea, hali nyakati nyingine tumaini linavumilia, na lisilowezekana linawezekana.”
Kwa habari ya matokeo yenye kudhuru ya kukosa tumaini na woga, kitabu The Encyclopedia Americana kinasema hivi: “Mara nyingi, utendaji wa woga juu ya akili, ikiwa haurekebishwi, unatokeza matokeo yaliyo mabaya zaidi, sana sana ukiwapo ugonjwa au maradhi. Woga unaotokezwa na magonjwa yenye kuambukiza wengi kwa mara moja unakuwa na matokeo yenye kuleta kifo kama vile kuambukizwa ugonjwa kwenyewe—ukipooza mwili na kuunyang’anya hali yake ya asili ya kubadilika kwa nguvu zake za neva, [kunyang’anya] akili uchangamfu wa tumaini, na kuwaua wale ambao, wangekuwa na uwezekano bora zaidi wa kupona, kwa sababu ya umri [wao] na nguvu [zao]. Woga ni sumu ya akili, na ndio wenye nguvu zaidi ya mambo yote yanayoshindana na afya na utabibu.”
Mtu aliye na imani isiyotikisika katika Mungu na katika ahadi za Neno lake analindwa asishindwe na woga huo unaoharibu. Anapata faraja kwa hakikisho la kwamba ugonjwa wo wote ule mwishowe utamalizika. Hata ukimalizikia mautini, yeye hatashindwa kabisa na woga, kwa sababu ahadi ya Mungu ya ufufuo kutoka kwa wafu inamtegemeza. Anapoivumilia hiyo taabu, anamlilia Yehova Mungu ampe msaada apate kuvumilia. Na roho ya Mungu au nguvu ya utendaji inatoa nguvu zinazohitajiwa. Kuongezea hayo, mgonjwa huyo anatazamia kwa uhakika utimizo wa ahadi ya Biblia: ”[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufu. 21:4.
Tumaini la kwamba ahadi hii iliyo kuu itatimizwa linaweza kumsaidia mtu adumishe maoni yenye uchangamfu anapokabiliana (anapoelekeana) na huzuni nyingi inayotokana na ugonjwa au tukio baya lisilotazamiwa. Chukua mfano wa Robert mwenye umri wa miaka 43 ambaye alipatwa na donda baya la uti wa mgongo. Madaktari walimwambia kwamba alikuwa na muda wa juma moja hivi wa kuishi. Lakini miezi minne baadaye, ijapokuwa ugonjwa wake mbaya, alijitayarisha kuhudhuria kusanyiko fulani la Mashahidi wa Yehova. Hali amelala kitandani aliweza kusikiliza vipindi kadha vya kusanyiko hilo. Wataalamu wa utabibu (uganga) hawakuamini kwamba angaliweza kuendeleza hali ya uchangamfu namna hiyo. ‘Tumaini la taratibu mpya ambayo Yehova ameahidi kuleta linanisaidia kuendelea,’ husema Robert. Vilevile alidumu katika sala, akimlilia Aliye Juu Zaidi ampe uwezo wa kuvumilia.
Ahadi iyo hiyo ilibadilisha maisha ya Yuko, mwanamke fulani kijana katika Japan. Alipokuwa na umri wa miaka 31, alipatwa na Kogenbyo, ugonjwa unaokausha ngozi, na kufanya mwili ukauke kama maiti iliyokaushwa, nao unaleta kifo cha pole pole kadiri unavyoenea. Hapo kwanza mkono wake wa kuume ulikauka na vidole vikajikunja. Kwa vile hakuna dawa ijulikanayo ya kuuponya, Yuko alishuka moyo sana, sana sana alipofikiria wakati ujao wa watoto wake watatu. Alipokuwa hospitalini, akapatwa na ugonjwa wa anemia (kupungukiwa sana na damu), nayo minofu ya mdomo na kidevu chake ikakauka hata kwamba asingeweza tena kusema kwa urahisi. Ikawa lazima Yuko ale chakula cha maji-maji.
Lakini ilitukia nini alipoanza kujifunza Biblia? Alifarijiwa sana kujifunza juu ya taratibu ya Yehova ambayo katika hiyo watu hawatapata magonjwa na kifo. Yuko anasimulia hivi: “Kwa mara ya kwanza nilipata tumaini hakika. Mwishowe nikawa na tamaa nyingi ya kutaka kuwaambia niliyoamini wengine walio katika hali iyo hiyo ili wao, nao, wajifunze kuweka mambo yote mikononi mwa Yehova. Akiogopa ugonjwa wangu wa amenia, daktari hakutaka niende nje juani. Lakini nilijisikia inanilazimu kushiriki na wengine niliyojifunza. Matokeo yakawa nini? Ugonjwa huu wa amenia haujanipa matatizo (magumu) zaidi. Kwenda nje kuwaambia wengine habari za Biblia kulinipa tamaa ya chakula hata kwamba nikaongezeka uzito. Vilevile, minofu ya mdomo wangu ikaanza kujiendesha kwa urahisi. Anapofikiria maendeleo ya kimwujiza katika hali yangu ya afya, daktari hutikisa kichwa chake tu kwa mshangao, bila kufahamu kilicholeta badiliko hilo.”
Badiliko linalofanana na hilo lilionwa na mwanamume fulani kijana mwenye ugonjwa wa kukauka sana sehemu za mwili. Nusu ya mwili wake ilikuwa imepooza, na alitumia wakati wake akiwa ameketi katika kiti chake chenye magurudumu katika chumba cha faragha cha nyumba ya kutunzia wagonjwa. Alikuwa akiendesha hiki kiti chenye magurudumu nyuma na mbele, kushoto na kulia kwa mkono mmoja. Akiwa hana tumaini lo lote, alikuwa anatazamia kufa tu. Hata hivyo, baada ya kipindi fulani cha kujifunza Biblia na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mwanamume huyu alianza kupendezwa zaidi na maisha. Alijaribu kutembea-tembea kwa kujishikilia kwenye viti vyake na meza. Muda si muda akawa stadi kabisa katika kutumia bakora. Mahali pa kuendelea kuishi katika nyumba ya kutunzia wagonjwa, alihamia chumba chake mwenyewe, akaanza kujipikia na hata kujisafishia chumba chake. Mahali pa kuendelea kutazamia kufa, mwanamume huyu kijana alianza kutazamia utimizo wa unabii wa Biblia juu ya ulimwengu usio na magonjwa.
Kwa hiyo mpaka siku zetu za leo, ujumbe wa Biblia umeota faraja na kitia-moyo kwa walio wazee, dhaifu na wanaotaabika kwa sababu ya misiba au magonjwa. Kwa kujifunza kumtegemea Yehova Mungu awape nguvu na kufanya tumaini atoalo kuwa lao wenyewe, watu hawa wameweza kuvumilia taabu nyingi. Lo! namna huu ulivyo ushuhuda mzuri kwamba Biblia ni chanzo cha faraja isiyoshindwa!