Mateso Yanayoweza Kukufaidi Wewe
“Kwa sababu hii mnafurahi sana, ingawa sasa kwa muda mfupi, ikiwa lazima, mmehuzunishwa na majaribu mbalimbali, ili kwamba ubora uliojaribiwa wa imani yenu, iliyo na thamani kubwa kuliko dhahabu inayojaribiwa na moto, uonekane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima katika ufunuo wa Yesu Kristo.”—1 Pet. 1:6, 7, NW.
1. Ni ubaya gani waliotendewa Wakristo katika siku za mwanzo-mwanzo wa kundi?
WALIDHIHAKIWA, wakapigwa na kufungwa gerezani. Nyumba zao zilivamiwa na mali zao zikanyakuliwa kwa nguvu. Wengine wa rafiki zao washikamanifu na washiriki wa jamaa waliuawa na makundi ya watu wenye ghasia au walihukumiwa kifo na amri za baraza za hukumu. Hawakuwa wamevunja sheria yo yote kustahilisha watendwe vibaya namna hiyo. Waliishi maisha mema sana yaliyo mfano kwa wengine nao waliwapenda wanadamu wenzao kikweli. Walakini walichukiwa na wengi. Kwa sababu gani? Kwa sababu walikuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.—Matendo 8:1-3; Ebr. 10:32-34.
NAMNA YA ADHABU YENYE KUFAIDI
2, 3. (a) Wengine wa Wayahudi waliokuwa wamegeuka kuwa Wakristo walikuwa wakichoshwa na mbio za uzima kwa sababu gani? (b) Walikuwa wamesahau nini?
2 Je! mateso makali waliyoyapata Wakristo yalikuwa na faida yo yote? Huenda mtu akajibu kwa haraka, Hapana. Walakini, Biblia inaonyesha kwamba mtu kulazimika kuvumilia mateso ni jambo lenye faida kubwa. Wayahudi waliogeuka kuwa Wakristo katika karne ya kwanza waliambiwa hivi: “Maana katika kupambana na dhambi, ninyi hamjapigana mpaka kumwaga damu yenu. Je, mmesahau yale maneno ya kutia moyo ambayo Mungu anawataja ninyi kuwa wanawe? ‘Mwanangu usidharau adhabu ya Mungu, wala usife moyo anapokukanya. Maana [Yehova] humwadhibu kila anayempenda, humpinga kila anayekubali kuwa mwanawe.’”—Ebr. 12:4-6, Habari Njema kwa Watu Wote.
3 Upinzani ulioelekezwa kwa Wayahudi waliogeuka kuwa Wakristo ulikuwa mkali kweli kweli. Walakini kushindana kwao na ile dhambi ituzingayo kwa upesi—kupoteza imani—hakukuwa kumefikia hatua ya kumwaga damu yao. Labda wengi wao walikuwa wenye moyo-nusu katika kufanya mbio za uzima na kwa hiyo hawakuwa wakishindana na dhambi hii katika njia ambayo ingewahitaji kuipinga ‘mpaka kumwaga damu yao.’ Walikuwa wameanza kuchoshwa na mashutumu ya watu wasiomwogopa Mungu waliyokuwa wakipata. (Ebr. 12:3) Walishindwa kufahamu kwamba mateso waliyoyapata kutoka kwa wapinzani wao yalitumika kama mafundisho kutoka kwa Yehova nayo yalithibitisha kwamba yeye aliwapenda sana wakiwa wanawe. Walikuwa wamesahau maneno ya kuwatia moyo ya Maandiko yanayopatikana katika Mithali 3:11, 12. Ikiendelea kutumia maneno hayo barua waliyoandikiwa Waebrania inasema hivi:
“Vumilieni adhabu kwani ni mafundisho; Mungu huwatendea ninyi kama wanawe. Maana ni mwana gani asiyeadhibiwa na baba yake? Lakini msipoadhibiwa kama wana wengine, basi, ninyi si wanawe, bali ni wana haramu. Zaidi ya hayo sisi tuliwaheshimu wazazi wetu waliotuzaa hata wanapotuadhibu. Basi, tunapaswa kumtii zaidi Baba yetu wa kiroho ili tupate kuishi. Wazazi wetu hapa duniani walituadhibu kwa muda, kama wao wenyewe walivyoona kuwa vema; lakini Mungu anatuadhibu kwa ajili ya faida yetu wenyewe, tupate kuushiriki utakatifu wake. Kuadhibiwa si jambo la kufurahisha bali la kuhuzunisha. Lakini wale waliofunzwa kuwa na nidhamu watavuna mwishowe tuzo la amani kutoka katika maisha [ya] adili.”—Ebr. 12:7-11, Habari Njema Watu Wote.
4. Tunapaswa kuyaonaje mateso makali ambayo huenda tukayapata kutokana na wanadamu?
4 Kulingana na shauri hili lililoongozwa na Mungu, Wakristo wanapaswa kuyaonaje mateso ambayo Yehova Mungu anaruhusu yawapate? Tunapaswa kuyaona kuwa namna ya adhabu au mafundisho tunayopewa na Baba anayetupenda sana na anayependezwa na hali yetu njema ya milele. Uhakika wa kwamba tunapata adhabu kama hiyo unathibitisha kabisa kwamba tunatendewa kama wana wala si kama wana haramu wasiotakikana na wasiopendwa. Kwa kuwa Yehova Mungu anaruhusu Wakristo wapatwe na mateso haya makali, inatupasa tujinyenyekeze chini yake kwa kutii. Hili linapatana pia na onyo la upole la mtume Petro: “Mujinyenyekeze basi chini ya mukono wa uwezo wa Mungu, ili awatukuze ninyi katika wakati wake. Wekeni masumbuko yenu yote juu yake, kwa maana yeye anawatunza ninyi.”—1 Pet. 5:6, 7, ZSB.
5. Kwa sababu gani ni jambo linalofaa kukubali adhabu tunayopewa kwa namna ya mateso?
5 Ni jambo linalofaa kabisa kwamba tukubali adhabu hii pasipo kuiasi, pasipo kujaribu kutoka chini ya mkono wa Mungu. Mwanamume anayewapenda na huwahangaikia watoto wake atawaadhibu anapoona inafaa kufanya hivyo. Kwa kuwa yeye, si mkamilifu huenda akaamua mambo kwa makosa. Kwa hiyo, ‘anapoadhibu kama vile anavyoona kuwa vema; huenda asifanye linalofaa sikuzote na linalowafaidi watoto katika “siku chache” za utoto wao. Hata hivyo baba kama huyo anaheshimiwa na watoto wanaompenda. Hili ni jambo linalofaa kweli kweli, kwa kuwa wamepata uhai wao kutoka kwake. Kwa upande mwingine, Yehova Mungu hafanyi makosa hata kidogo, nasi tunapata mengi zaidi ya uhai kutoka kwake. Kulingana na Kigiriki halisi cha Waebrania 12:9, Aliye Juu Zaidi anaitwa “Baba wa maroho,” ikionyesha kwa wazi kwamba uzima wa kiroho pamoja na wa milele wa Wakristo unamtegemea yeye. Hakika, basi, kuna sababu kubwa hata zaidi ya kutii adhabu tunayopewa na Baba yetu wa mbinguni kuliko ile ya kumheshimu baba ya kidunia asiyekamilika.
FAIDA ZINAZOTOKANA NA MATESO
6. Mateso yanaweza kutusaidiaje kuwa washiriki wa utakatifu wa Mungu?
6 Zaidi ya hayo, adhabu inayokuja kwa namna ya mateso sikuzote inawafaidi watumishi wa Mungu. Inaweza kuwa na matokeo ya kuwasafisha, ikifunua makosa fulani katika utu wa mtu ambayo lazima yasahihishwe. Haya huenda yakatia ndani kiburi, ushupavu, kukosa subira, uchoyo, uulimwengu pamoja na kupenda maisha ya raha, au anasa. Mkristo anapofanya maendeleo yanayohitajiwa, anakuwa safi zaidi au mtakatifu zaidi katika mwenendo wake. Kwa ‘kuwa mtakatifu kama Yehova Mungu alivyo mtakatifu,’ anakuwa ‘mshiriki wa utakatifu wa Mungu.’ (1 Pet. 1:14-16) Hivyo, kusudi la kutoa adhabu linatimizwa.
7. Kama inavyoonyeshwa kwa habari ya Yesu Kristo, tunaweza kujifunza jambo gani kutokana na dhiki? (Ebr. 5:8)
7 Kutokana na mateso huenda vilevile mtu akajifunza mambo yatakayomwezesha kufanya utumishi wa Mungu vizuri zaidi. Hii inaonyeshwa katika habari ya Yesu Kristo. Kwa kulazimika kupatwa na mateso makali katika mwili, alipata ujuzi uliohitajiwa ili awe kuhani mkuu mwenye huruma. Hii imetuwezesha kumkaribia Mungu kupitia kwa Kristo tukiwa na uhuru mkubwa zaidi wa kusema, tukiwa na hakika kwamba Yesu anafahamu hali yetu naye atatutetea akiwa kuhani mkuu mwenye rehema.—Ebr. 4:15, 16.
8, 9. Kama inavyoonyeshwa katika Waebrania 12:11, kipindi cha kupata adhabu inayokuja kwa namna ya mateso kinaweza kuwa na matokeo gani kwetu wakati inapoendelea na inapokwisha?
8 Bila shaka, huenda ikawa vigumu sana kuvumilia mateso. Bila shaka hakuwezi kuwa na furaha katika kupatwa na mateso. Linakuwa jambo lenye kuhuzunisha sana. Lakini tukiitii na kuiruhusu ituonyeshe sehemu tunazopaswa kufanya maendeleo, jaribu hilo laweza kuwa mazoezi mazuri kwetu. Matokeo ya mwisho ya mazoezi hayo yatakuwa “tuzo la amani kutoka maisha adili.” Au kama vile Moffatt anavyotafsiri maneno hayo ya Waebrania 12:11: “Sikuzote adhabu inaonekana kuwa kitu chenye uchungu katika wakati wake, si cha furaha; lakini wale wanaozoezwa kwayo wanavuna matunda yake baadaye katika amani ya maisha manyofu.”
9 Huenda ikawa umepata kuthamini matokeo mema yanayoweza kuletwa na adhabu kama hiyo kwa kushirikiana na ndugu na dada Wakristo waaminifu. Huenda wakawa wamepatwa na majaribu kwa muda wa miaka mingi wakiwa chini ya utawala wenye kudhulumu wa wenye mamlaka peke yao au wakiwa katika kambi za mateso na katika gereza. Walakini, mara nyingi ukamilifu wao unaangaza utu wao wote. Mtu anajua kwamba anashirikiana na wale ambao imani yao imetengenezwa na adhabu, nao wonyesho wenye utulivu na wenye furaha wa imani hiyo unaweza kusaidia sana wengine watembee vivyo hivyo katika ukamilifu.
10. Tunapaswa kuwa na maoni gani juu ya kupatwa na jaribu la namna yo yote na kwa hiyo huenda tukauliza ulizo gani?
10 Kwa hiyo, tupatwapo na jaribu la namna yo yote—ugonjwa, kukata tamaa, dhuluma, msiba au mateso—tunapaswa kuliona kuwa adhabu kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni atupendaye nasi tunapaswa tuliruhusu jaribu hilo liwe na matokeo mema kwetu, litufanye kuwa watumishi wake walio bora. Lakini tunawezaje kuendelea kuwa waaminifu tupatwapo na dhiki ili baadaye tufaidike kutokana na mazoezi hayo?
NAMNA YA KUVUMIUA
11. Ni shauri gani la mwanafunzi Yakobo tunalopaswa kufuata tuendeleapo kupatwa na hali zenye kujaribu?
11 Sana sana ni jambo la maana sana kumtegemea Yehova Mungu atupe hekima katika kushughulika na hali zenye kujaribu. Tunapaswa kumwomba msaada, pasipo kuwa na mashaka hata kidogo kwamba yeye atatusaidia kupitia kwa roho yake takatifu. Ebu angalia shauri bora sana tunalopewa na mwanafunzi Yakobo kuhusu jambo hili:
“Mwione kuwa furaha yote, ndugu zangu, mnapopatwa na majaribu ya namna nyingi, mkijua kwamba sifa hii iliyojaribiwa ya imani yenu inatokeza uvumilivu. Lakini acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, mpate kuwa wakamilifu na timamu katika mambo yote, bila kasoro yo yote. Kwa kweli, ikiwa ye yote kati yenu anapungukiwa na hekima, acheni yeye aendelee kumwomba Mungu, kwa kuwa yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kulaumu; naye atapewa hiyo. Lakini acheni yeye aendelee kuomba kwa imani, bila, kushuku hata kidogo, kwa kuwa yeye ashukuye anafanana na wimbi la baharini lipeperushwalo na upepo huku na huku. Kwa kweli, acheni mtu kama huyo asidhani kwamba atapokea kitu cho chote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu anayesita, asiyeimarika katika njia zake zote.”—Yak. 1:2-8, NW.
12. Tunajifunza nini kutokana na Waebrania 5:7?
12 Bila shaka Yesu Kristo aliweka mfano bora sana wa kumtegemea Baba yake wa mbinguni. Ingawa alikuwa mkamilifu, Yesu alikuwa akisali kwa bidii sana alipokuwa akipatwa na mateso. Biblia inaripoti hivi: “Yeye, [katika] siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.” (Ebr. 5:7) Kwa kuwa Yesu alikuwa na woga wa kimungu, Baba yake alisikia kwa kibali kilio chake cha kuomba msaada. Kwa msaada wa roho takatifu, Mwana wa Mungu alishikilia ukamilifu wake, na, kwa hiyo, alikufa akiwa amekubaliwa na Babaye. Kisha aliokolewa kutokana na mauti kwa kufufuliwa.
13. Kulingana na Waebrania 12:2, ni kitu gani kilichomsaidia Yesu Kristo adumishe uaminifu wake chini ya mateso?
13 Jambo jingine lililomsaidia Yesu Kristo adumishe ukamilifu wake lilikuwa kuweka mbele yake thawabu kuu aliyokuwa amewekewa na Baba yake. Katika Waebrania 12:2 (tafsiri ya Habari Njema kwa Watu Wote) kwa wazi thawabu hii ndiyo inayoitwa “furaha.” Tunasoma hivi: “Kwa ajili ya furaha iliyokuwa inamngojea yeye alivumilia kifo msalabani, bila kujali aibu yake, na sasa anaketi upande wa kulia wa kiti cha enzi cha Mungu.” Sisi, pia tunaweza kudumisha uaminifu wetu chini ya majaribu, tukitazamia mbele kwenye thawabu ya uzima wa milele pamoja na baraka zake. Kama zawadi iliyowekwa mbele yetu katika mashindano ya mbio, thawabu hii inaweza kututia nguvu tuzipige mbio za uzima kwa uvumilivu, tukizitupilia mbali tamaa zo zote mbaya zinazoweza kuvunja imani yetu.—Ebr. 12:1.
14. Maneno ya Maombolezo 3:20, 21 yanaweza kututia moyo namna gani tunapokuwa katika hali zenye taabu?
14 Hata hali yetu iwe yenye hatari namna gani, haitupasi hata kidogo kujiachilia tufikiri kwamba Aliye Juu Zaidi hatujali. Tupatwapo na magumu makubwa sana, maneno ya Maombolezo 3:20, 21, NW yaweza kutufariji sana: “Bila shaka nafsi yako [Yehova] itakumbuka na kuinama chini juu yangu. Hili ndilo nitakaloukumbusha moyo wangu. Kwa sababu hiyo nitaonyesha nia ya kungojea.” Yehova Mungu ‘atainama chini’ atuangalie kwa kibali, katika kuonyesha unyenyekevu wake. Atatuinua kutoka katika hali yetu yenye taabu, kama alivyowafanya Wayahudi wenye kutubu katika karne ya sita K.W.K. Walakini, muda wa dhiki unapoendelea, tunapaswa kumngojea Yehova Mungu kwa subira na tukiwa na imani isiyoyumba-yumba achukue hatua kwa ajili yetu.
15. Kulingana na Maombolezo 3:22, 23, ni jambo gani linaloonyeshwa na uhakika wa kwamba tungali hai?
15 Uhakika wa kwamba bado tunaishi ni ushuhuda wa fadhili zisizostahilika za Mungu, hangaiko lake lenye huruma kwetu. Huu ni uhakikisho wa kwamba Aliye Juu Zaidi atawaonyesha rehema watu wake wanaopatwa na dhiki. Katika Maombolezo 3:22, 23, tunasoma hivi: “Ni huruma za [Yehova] kwamba hatuangamii, kwa kuwa rehema zake hazikomi. Ni mpya kila siku asubuhi; uaminifu wako ni mkuu.”
16. Kwa sababu gani tunaweza kuzitegemea rehema za Yehova?
16 Kwa sababu ya uaminifu wa Yehova, kutegemeka kwake, kutumainika kwake, ni kwingi mno, tunaweza kuzitegemea rehema zake. Wonyesho wa rehema au huruma za kimungu kwetu hazitakuwa dhaifu au bila matokeo. Rehema za Yehova ni “mpya kila siku asubuhi,” zikipatikana kila wakati katika nguvu zote kwa watumishi wake washikamanifu. Kwa sababu hii, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mwenye Nguvu Zote anaona dhiki yetu na kwamba kwa rehema yeye atatupa msaada unaohitajiwa.
17. Tunapaswa kufanya nini wakati nira ya adhabu imewekelewa juu yetu?
17 Lakini, akiruhusu nira ya adhabu iwekelewe juu yetu, tunapaswa kuikubali pasipo kunung’unika wala tusizihubiri taabu zetu. Maombolezo 3:28, 29 linapendekeza hivi: “Na akae peke yake na kunyamaza kimya; kwa sababu [Mungu] ameweka hayo juu yake. Na atie kinywa chake mavumbini,” na kulala kifudifudi akionyesha nia ya kutii kabisa.
18. Yehova anakuwa na maoni gani juu ya dhiki ambazo watumishi wake wanalazimika kuvumilia?
18 Wakati ule ule tunaweza kufarijiwa kwa kujua kwamba jaribu hilo ni la muda mfupi tu na kwamba Yehova Mungu hafurahii kuona tukipatwa na dhiki. “Kwa kuwa [Yehova] hatamtupa mtu hata milele,” yasema Biblia. “Maana ajapomhuzunisha atamrehemu, kadiri ya wingi wa huruma zake. Maana moyo wake hapendi kuwatesa wanadamu, wala kuwahuzunisha.” (Omb. 3:31-33) Mahali pake, kusudi la Yehova ni ili mazoezi tunayopata kupitia kwa mateso yatupatie hali njema ya milele.
19. Kwa sababu gani Yehova hawezi kulaumiwa kwa sababu ya kuruhusu udhalimu na mateso yaweko?
19 Hata hivyo, wale wanaoyafanya maisha ya watumishi wa Mungu yawe magumu, mwendo wao wa uadui hauachiliwi na Mungu. Vilevile, Yehova hawezi kulaumiwa kwa sababu ya kuruhusu mateso kama hayo. Kwa sababu gani? Kwa sababu, ijapokuwa anaruhusu watu wake watendewe vibaya hivyo ili wafaidike, yeye hakubaliani na matendo mabaya yanayotendwa juu ya wanadamu na wanadamu wenzao. Neno lake linalaumu matendo hayo mabaya. Biblia inatuambia hivi: “Kumseta chini ya miguu mfungwa ye yote katika nchi, kumnyima mtu haki zake katika kumkaidi Aliye Juu Zaidi, kupotoa hukumu katika baraza za hukumu—mambo kama hayo Bwana hajakubaliana nayo kamwe.” (Omb. 3:34-36, The New English Bible) Wanadamu wanaowatendea vibaya wanadamu wenzao watatoa hesabu yao kwa Yehova Mungu. “Kulipiza kisasi ni shauri langu; mimi nitalipiza, asema Bwana.” (Rom. 12:19, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa hiyo, lazima tujiangalie tusimkasirikie Aliye Juu Zaidi kwa sababu ya ubaya unaofanywa na wanadamu wanaodharau sheria ya Mungu.
20. Hata mateso ya wanadamu yenye kuhuzunisha sana hayapaswi yaturuhusu tufanye nini, na kwa sababu gani?
20 Nyakati nyingine hali zinazowapata watumishi wa Mungu kwa sababu ya magonjwa, misiba ya barabarani au kwa kutendwa vibaya ni zenye kuhuzunisha sana. Huenda tukawahurumia sana mioyoni mwetu watu vipofu, viwete pamoja na vilema. Hili ni jambo linalofaa. Walakini hatupaswi hata kidogo, kuachilia hata mateso makali zaidi ya wanadamu yatufanye tumpe Yehova Mungu kisogo. Yeye peke yake ndiye awezaye kurekebisha madhara ambayo wanadamu wamepata kwa sababu ya dhambi na kutokamilika. Ebu angalia alivyosema Yesu Kristo kwa habari ya mwanamume aliyezaliwa kipofu: “[Ili] kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake.” (Yohana 9:3) Lo! namna Aliye Juu Zaidi atakavyotukuzwa wakati macho ya vipofu yatakapofunguliwa, masikio ya viziwi yatakapozibuliwa na wakati vilema watakapotembea, watakaporuka-ruka na kukimbia! (Ufu. 21:3-5) Kama dhiki kama hizo hazikuwapo, hatungepata hata kidogo kujua mambo ya ajabu sana ambayo Yehova Mungu anaweza kuwafanyia wanadamu. Na, kwa sababu ya thawabu ya uzima wa milele, mateso ya wanadamu katika taratibu hii ya mambo yatakuja kuwa bure. Itakuwa kama kwamba hakujapata kuwa na mateso hata kidogo.
21. (a) Mateso yatatufaidi wakati gani? (b) Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike kutokana na dhiki?
21 Ikiwa mateso ambayo huenda tukapata bado yatatufanya tuwe wenye fadhili zaidi, wenye huruma zaidi kwa wanadamu wenzetu, yatusaidie kukaribia zaidi matakwa ya haki kama yalivyoandikwa katika Biblia, namna hii ya adhabu itakuwa imetimiza kusudi lenye faida kweli kweli. Ili hii iwe hivyo, lazima tumtumaini Baba yetu wa mbinguni kabisa kama vile mtoto mchanga anavyomtumaini baba yake wa kidunia. Tunahitaji kuwa na imani isiyotikisika kwamba cho chote ambacho Yehova Mungu anaruhusu kitupate mwishowe kitatuletea hali njema na furaha yetu ya milele. Kwa hiyo, sikuzote na tuweke maneno ya Warumi 8:28, NW mbele yetu: ‘Mungu hufanya mambo yote yashirikiane kwa faida ya wale wampendao yeye.’—
Kutoka The Watchtower Oct. 15, 1978.
[Picha katika ukurasa wa 20]
“Kuadhibiwa si jambo la kufurahisha.”