Yehova Hubariki Wale Wanaojitahidi Wenyewe kwa Nguvu
“Jitahidini wenyewe kwa nguvu kuingia kupitia ule mlango mwembamba, kwa sababu wengi . . . watatafuta kuingia lakini hawataweza.”—Luka 13:24, NW.
MAELEKEO ya wanadamu wasiokamilika ni kufuata mwendo ulio rahisi zaidi. Mara nyingi watu wanataka mambo mengi zaidi katika maisha lakini hawapati kamwe wanayotamani kwa sababu ya kutokuwa na nia ya kufanya jitihada inayotakiwa. Wengine wanatosheka tu na kuwazia-wazia mambo na pengine kutafuta bahati yao mara kwa mara kwa kucheza kamari, wakitumaini kupata fedha za kutimiza wanayowazia-wazia. Wafanya kazi wengi wanadai mshahara mkubwa na siku chache zaidi za kufanya kazi katika juma. Fedha nyingi zaidi kwa jitihada kidogo tu ndilo wazo linalofaa zaidi kwa watu wengi leo. Walakini watu wengine wanatambua kwamba kuna jambo lililo la maana zaidi kuliko utajiri wa mambo ya kimwili. Ni jambo gani hilo?
Ni jambo gani linaloweza kuwa lenye thamani zaidi kwa ye yote wetu kuliko kibali ya Mungu ikiongoza kwenye kupata wokovu? Na je! twaweza kutumaini kuupata pasipo kujitahidi ko kote? Ijapokuwa Mungu amefanya yote yanayohitajiwa katika kuokoa wanadamu, je! hilo lamaanisha kwamba wanadamu watapata wokovu vivi hivi tu, bila jitihada yo yote kwa upande wao? (Tito 3:4-7) Yesu Kristo alitoa jibu alipokuwa akijibu ulizo hili: “Wale wanaookolewa ni wachache?” Alisema hivi: “Jitahidini wenyewe kwa nguvu kuingia kupitia ule mlango mwembamba, kwa sababu wengi, nawaambia ninyi, watatafuta kuingia lakini hawataweza.’—Luka 13:23, 24, NW.
Je! wewe una nia ya kujitahidi mwenyewe hivyo upate kuishi katika taratibu mpya ya Mungu? Watu wengi wangefurahia kuishi katika dunia isiyo na kifo. Walakini wakati watu ao hao wanapotiwa moyo wajifunze Biblia, mara nyingi wanatoa visababu visivyofaa kitu. Nako kukataa kwao kutia jitihada ya kweli wapate kumjua Mungu, kukiendelea, kunaweza kuwazuia wasipate kibali ya kimungu. Wote wanaotaka kukubaliwa na Yehova Mungu wanapaswa kuwa na nia ya ‘kujitahidi wenyewe kwa nguvu’ katika kufanya maendeleo wakiwa watumishi wake, wapate kumjua Muumba vizuri zaidi na kuishi kulingana na maarifa yao ya kumjua yeye. Yeye, bila shaka, atawasaidia kupitia kwa roho yake, mradi tu wanatafuta kuongozwa nayo.
Kwa kweli, katika hali nyingi za maisha, nafasi zaweza kupotezwa ikiwa mtu hajitahidi mwenyewe. Mithali 26:15 hutupa mfano wenye kupita kiasi wa jambo hilo, ikisema: “Mtu mvivu hutia mkono wake sahanini; kwamchosha kuupeleka tena kinywani pake.” Kwa habari ya chakula cha kiroho, mara nyingi hali inakuwa sana kama vile inavyoonyeshwa na mithali hiyo. Watu wengi walio na Biblia nyumbani wanakufa njaa kiroho kwa sababu tu hawajitahidi kuichukua kutoka kwenye rafu za kuwekea vitabu na kuisoma.
Licha ya maelekeo ya uvivu, lazima mtu apigane na mawazo yasiyofaa ili aweze kujitahidi mwenyewe. Kwa mfano, akiona kwamba kuwatembelea watu nyumbani kwao ashiriki ujumbe wa Biblia pamoja nao ni jambo gumu sana, hilo litamzuia hata asijaribu. Hata hivyo, mara nyingi, ikiwa angejaribu, angeona kwamba anaweza kutimiza kazi hiyo ngumu kwa msaada wa roho ya Mungu.
Kwa upande mwingine, nyakati nyingine urahisi wa jambo lililopendekezwa ndilo hufanya watu waone shaka juu ya kufaa kwalo. Huenda ikawa kwamba hawaoni maana yo yote katika jambo hilo. Naamani alikuwa mmoja aliyekaribia sana kuangukia kwenye mtego huo. Alikuwa amesafiri kwenda Israeli, akitumaini kuponywa ukoma. Akiwa mtu mashuhuri, yeye alitazamia kwamba angetendewa kipekee na nabii Elisha. Walakini Elisha hata hakumwona yeye binafsi, akimwagiza tu mtumishi wake amwambie Naamani aoge mara saba katika Mto Yordani. Naamani aliona kwamba ni jambo lisilostahili heshima yake kuoga katika mto wa Yordani wenye matope. Yeye alikuwa ametazamia kuponywa katika njia yenye kutokeza. Kama hakusikiliza shauri la watumishi wake, Naamani angerudi Dameski akiwa na hali yake yenye ukoma. Lakini alitii maagizo mepesi ya Elisha naye akaponywa.—2 Fal. 5:9-14.
Kisha, tena, inaweza kuwa kwamba kuogopa kumwudhi mtu fulani au kuogopa kupata jibu lisilofaa ndiko kunakozuia watu wasichukue tendo linalofaa. Nehemia wa karne ya tano K.W.K. ni mfano mzuri wa mtu ambaye hakuruhusu woga huo umzuie. Ijapokuwa alikuwa na cheo cha mnyweshaji mwenye kutumainiwa katika ua wa Mfalme Artashasta, Nehemia hakuruhusu mawazo ya kukataa au kuudhika kwa mfalme huyo kumnyamazishe. Nafasi ilipojitokeza, Nehemia alimwomba Yehova kisha kwa heshima akajulisha ombi lake. Si kwamba tu mfalme huyo alimpa ombi lake, bali pia alimpa Nehemia barua zilizompa mamlaka ya kurudi Yerusalemu pamoja na kutumia mbao kutoka katika msitu wa kifalme ili ajenge kuta na malango ya Yerusalemu.—Neh. 2:1-8.
Namna gani sisi? Wakristo wengine huenda wakaogopa kuomba ruhusa kazini ili wahudhurie kusanyiko pamoja na waamini wenzao. Ijapokuwa huenda wangepewa ruhusa kama wangeomba, kuogopa kukataliwa kunawafanya wakose mafundisho bora sana ya kiroho. Wanawake fulani Wakristo nyakati nyingine wanafurahia nusu tu ya mikutano ya kundi kwa sababu wao wanafikiri kwamba waume zao wasioamini hawawezi kuwapa kibali ya kuhudhuria zaidi. Walakini, huenda ikawa kwamba wengine wao hawajapata kamwe kuuliza waume zao. Hata hivyo, wengine walio katika hali moja na hiyo waweza kueleza mambo mengi yenye kujenga waliyoyaona kwa sababu walipata kuuliza. Kwa kweli, katika mambo mbalimbali, tusipoomba, hatutapata.—Linganisha Mathayo 7:7-11.
Naam, ikiwa tunataka baraka ya Yehova, tunahitaji kujitahidi wenyewe kwa nguvu. Kwa sababu hiyo, yapinge maelekeo ya uvivu, usijiruhusu uvunjwe moyo na ukubwa wa kazi wala na namna inavyoelekea kuwa nyepesi, nawe usikose kuomba kwa kuogopa kupata jibu lisilofaa.
Inapokuwa ni utendaji unaohusiana na ibada ya kweli, waweza kufaulu kwa msaada wa roho ya Mungu.